Sir John Roberts

JF-Expert Member
Mar 1, 2017
9,614
15,942
Kamati Kuu ya Halmashauri Kuu ya Chama Cha Mapinduzi Taifa imemteua Ndg. Emmanuel Nchimbi kuwa Katibu Mkuu wa Chama Cha Mapinduzi (CCM).

Nchimbi anachukua nafasi iliyoachwa wazi na Daniel Chongolo ambaye alijiuzulu.

Katibu Mkuu Dkt. Nchimbi ametanguliza shukrani zake za dhati kwa Mwenyekiti wa CCM Taifa na Rais Dkt. Samia Suluhu Hassan pamoja na Wajumbe wote wa Halmashauri Kuu ya CCM Taifa kwa kumuamini na kumpotisha kuwa katika kuhudumu nafasi ya Ukatibu Mkuu wa Chama Cha Mapinduzi - Taifa.

1705333212492.png

Picha: Rais Samia kushoto akipeana mkono na Dkt. Nchimbi baada ya kuteuliwa
WASIFU WA DKT. EMMANUEL NCHIMBI
Dkt. Emmanuel Nchimbi alizaliwa Desemba 24, 1971 mkoani Mbeya, (atafikisha miaka 54 Desemba mwaka huu). Elimu yake ya Msingi aliianzia jijini Dar es Salaam katika Shule ya Msingi Oysterbay kati ya mwaka 1980 – 1986.

Baba yake mzazi, Mzee John Nchimbi kutoka wilayani Songea ni askari mstaafu wa Jeshi la Polisi na wakati anastaafu alikuwa Kamishna Msaidizi wa Polisi (ACP) na Kamanda wa Polisi Mkoa wa Mtwara. Mzee Nchimbi pia amewahi kuwa Mjumbe wa Halmashauri Kuu ya CCM (NEC) kwa vipindi viwili kupitia kundi la majeshi na baadaye katibu wa CCM wa mkoa, alikoma kushiriki masuala ya kisiasa mfumo wa vyama vingi ulipoanzishwa.

Dk Nchimbi alijiunga na elimu ya sekondari kwenye Shule ya Sekondari Uru kati ya mwaka 1987 – 1989 (kidato cha I – III) halafu akahamia Shule ya Sekondari Sangu na kukamilisha kidato cha nne mwaka 1989 – 1990.

Nchimbi alisoma Shule ya Sekondari ya Forest Hill, Mbeya masomo ya kidato cha V na VI mwaka 1991 – 1993. Alijiunga katika Chuo cha IDM Mzumbe (Morogoro) na kuhitimu Stashahada ya Juu ya Utawala (mwaka 1994 – 1997).

Wakati anahitimu IDM, pia alichaguliwa kuwa Mjumbe wa Halmashauri Kuu ya CCM (NEC) na mwaka uliofuatia (1998), alichaguliwa kuwa Mwenyekiti wa Umoja wa Vijana wa Chama cha Mapinduzi (UVCCM).

Dk Nchimbi amewahi kuajiriwa na Baraza la Taifa la Usimamizi wa Mazingira (NEMC) kati ya mwaka 1998 – 2003.

Alisoma shahada ya uzamili ya usimamizi wa biashara Chuo Kikuu cha Mzumbe mwaka 2001 – 2003 akibobea kwenye maeneo ya (benki na fedha).

Dk Nchimbi aliteuliwa kuwa Mkuu wa Wilaya ya Bunda (mwaka 2003 – 2005) na (mwaka 2008 – 2011) alisoma na kufanikiwa kuhitimu shahada ya uzamivu (PhD) katika Chuo Kikuu cha Mzumbe.

Dk Nchimbi amemuoa Jane na wana watoto watatu.

Mbio za Ubunge
Dkt. Nchimbi alirudi nyumbani kwao (Songea Mjini) kuanza harakati za ubunge tangu alipokuwa anaongoza UVCCM. Ilipotimu mwaka 2005, aliingia kwenye kinyang’anyiro cha uchaguzi akakutana na Edson Mbogoro wa Chadema aliyekuwa mpinzani wake mkuu. Dk Nchimbi alisaidiwa na mtandao mkubwa wa CCM na kupata ushindi wa asilimia 67.6 dhidi ya asilimia 30.5 za Mbogoro.

Mara tu baada ya kuwa mbunge, Rais Kikwete alimteua kuwa Naibu Waziri wa Habari, Utamaduni na Michezo, hii ilikuwa Januari 2006, alidumu kwenye wizara hiyo hadi Oktoba 2006 alipohamishiwa kwenye Wizara ya Kazi, Ajira na Vijana – hapa pia alikuwa Naibu Waziri tangu Oktoba 2006 hadi Februari 2008 kisha Wizara ya Ulinzi na Kujenga Taifa ambako pia alikuwa Naibu Waziri hadi Novemba 2010.

Katika Uchaguzi Mkuu wa mwaka 2010, Dk Nchimbi alijitosa tena Jimbo la Songea Mjini. Kampeni za 2010 zilimnyima usingizi pamoja na kuwa chama chake kilikuwa kimechukua asilimia zaidi ya 90 ya vijiji, vitongoji na mitaa mwaka 2009.

Kama kawaida, alipambana tena na Mbogoro wa CHADEMA na kumshinda kwa mara ya pili, japo safari hii Dk Nchimbi akipoteza takriban ushindi wa asilimia 10 ukilinganisha na mwaka 2005. Katika uchaguzi huo, alipata asilimia 59.9 dhidi ya 37.48 za Mbogoro.

Upandaji vyeo wa Nchimbi uliendelea, Rais Kikwete alimpa Wizara ya Habari, Utamaduni na Michezo akiwa Waziri kamili, alidumu hapo hadi Mei 2012 alipohamishiwa Wizara ya Mambo ya Ndani kabla ya kujiuzulu Desemba 2013.

Mbio za Urais
Dkt. Nchimbi alianza mbio za urais tangu alipokuwa naibu waziri kwenye awamu ya kwanza ya uongozi wa Rais Kikwete lakini nimeambiwa kuwa alikuwa anajipanga kistratejia kwa kuzingatia kuwa mbio hizo ndani ya CCM huhitaji fedha nyingi, ambazo hana.

Lakini kwa sababu amekulia ndani ya CCM amekuwa akifahamu kuwa fedha peke yake si kila kitu na kwamba mtu anayejipanga na kuwa chaguo muhimu hufika mbali.

Ndiyo maana ameendelea kuwa mtiifu kwa chama chake hata alipoondoka katika uwaziri kwani anajua kuwa safari za siasa ndani ya CCM huhitaji utulivu ili ufanikiwe.

Kuteuliwa kuwa Balozi
Desemba 3, 2016, Nchimbi aliteuliwa na Rais Dkt. John Pombe Magufuli kuwa Balozi, baadaye alipangiwa kituo cha kazi Nchini Misri na kisha Agost 11, 2023 Rais Samia alimrejesha nyumbani.

Leo Januari 15, 2024, Dkt. Nchimbi ameteuliwa kuwa Katibu Mkuu wa Chama Cha Mapinduzi akichukua nafasi ya Chongolo aliyejiuzulu nafasi hiyo.

Pia soma: Emmanuel Nchimbi anafaa kuwa Katibu Mkuu wa CCM, anaweza kujenga chama, kudhibiti nidhamu ya chama, akiwemo yule bwana mdogo
 
Back
Top Bottom