Wakuu Mpo!
Mwaka 2013 mwezi march tarehe kapuni ilikuwa ndio siku yangu kuu ya harusi yangu na Mke wangu kipenzi, niliyesota naye miaka mitano kwenye uchumba.
Ilikuwa sikukuu na yenye furaha kwa sababu; Nilioa mwanamke mzuri sana. Yaani wakiambiwa wanaume watoke waliooa wanawake wazuri basi nami nami nitakuwa mmoja wao. Lakini jambo la pili na kubwa ni kuwa Nilitimiza ndoto na msimamo wangu wa kuoa mwanamke mwenye bikra yake. Rafiki zangu chuoni nilikuwa nawaambia mimi kamwe siwezi kuoa mwanamke asiye na bikra wakawa wanasema nisiseme hivyo kwani siwezi kujua Mungu kapanga nini, nikawa nawajibu kuwa Mungu sio anayeoa bali mimi ndiye ninayeoa. Wakasema wataona, na sasa siku ya wao kuona ilikuwa imefika. Hakika nilijivunia sana. Sababu ya tatu, mke wangu alikuwa ni ndoto ya kila mwanaume sio kwa uzuri wake tuu bali akili yake iliyochagizwa na elimu yake ya MD.
Muda wa Bwana harusi kutoa neno walau la shukrani ulifika, na hapa ndipo watu wakajua Jokajeusi ni mwendawazimu, niliongea maneno mazito sana lakini ndio ulikuwa ukweli wenyewe hata kama haukuwa unanihusu lakini ulihusu watu wanaume wenye akili timamu pekee. Nilisema;
" Mama(mkwe) kama ni kuzaa wengi wamezaa watoto wazuri kama mwanao, kama ni kusomesha wengi wamesomesha kama ulivyomsomesha mwanao. Hivyo kwangu mambo hayo ni sifa ndogo sana ambazo siwezi kuzitaja hapa kama sababu ya kukushukuru Mama yangu. Jambo moja kuu ninalokusifu Mama(mkwe) ni kumtunza binti huyu(hapa nilimuangalia mke wangu aliyekuwa kaangalia chini kwa aibu kwani alijua naenda kusema nini), sio kila mzazi amewatunza binti zake kama ulivyo wewe. Wewe ni Mama wa mfano na kuigwa. Mama(mkwe) kama nisingekuta bikra kwa binti yako ni hakika siku ya leo isingekuwepo kama Mungu aishivyo. Wala nisingekuja uchagani kutoa mahari na kujihangaisha. Lakini natangaza rasmi ndani ya Ukumbi huu mbele ya wakwe zangu, mbele za wazazi wangu, ndugu, jamaa na rafiki. Binti huyu nilimkuta akiwa msafi, akiwa kajitunza, anastahili kuvaa vazi hili la Bibi harusi, vazi jeupe kama alivyo yeye"
" Na kwa maana hiyo, binti huyu ni mke wangu kweli dunia ikishuhudia na mbingu zikitazama. Sio mke wa jamii kwani nilimkuta akiwa bikra. Nitamtunza kwa gharama kama alivyotunzwa na kuitunza bikra yake kwa ajili yangu, pengine maneno haya yakawa ya aibu miongoni mwenu lakini nimeona niyaseme tuu"
Nilimeza mate, wakati huo ukumbi mzima upo kimya, wengine wakiona nimeongea maneno yenye kuumiza wengine hasa wale ambao hawajaoa wakiniona kama mfano wao.
Nikamaliza kwa kusema;
" Mimi kama mwanaume, ambaye kwa sasa ni mume wa binti huyu(nikataja jina lake) naomba nieleze kuwa binti huyu nitaachana naye kwa sababu kuu tatu; Mosi, uchawi na ushirikina kama nitamkuta nao, pili, Kama atajifunza umalaya, na mwisho kabisa, kifo kikitutenganisha. Hivyo Mama mke siku utakayomuona binti yako karudi nyumbani usijiulize sababu ya jambo hilo, jua sababu ni moja kati ya hizo. Sina haja ya kukaa vikao yatakapofanyika makosa hayo, na ninyi kama mashuhuda katika sherehe hii maneno haya mmeyasikia kwa masikio yenu na kwa macho yenu mliniona nikisema haya. Niwashukuru wote kwa kushirikiana nami mpaka kufanikisha harusi hii. Ahsanteni sana"
Hayo ndiyo maneno ambayo niliyasema, ingawaje baadaye kama siku kumi hivi Wazazi wangu waliniambia kuwa sikuwa na sababu ya kusema mambo yale. Nikawajibu, kikao changu cha ndoa cha kwanza ndio ile harusi yangu na hicho hicho ndio kikao cha mwisho. Sitakaa kikao chochote kwa ajili ya ndoa yangu na ndio maana nikayasema yote palepale.
Wazazi wangu hawakuwa na chakusema kwani wananijua jinsi nilivyo na ndivyo walivyo nilea hivyo hivyo.
Jokajeusi