Mwita Maranya
JF-Expert Member
- Jul 1, 2008
- 10,565
- 7,988
Asema CHADEMA ipo tayari kwa uamuzi wowote
na Tamali Vullu = Tanzania Daima
CHAMA cha Demokrasia na Maendeleo (CHADEMA) kimesema kipo tayari kupokea maamuzi yoyote yatakayotolewa na Naibu Katibu Mkuu wa chama hicho, Zitto Kabwe, ya kuamua kujiuzulu nyadhifa zote katika chama hicho ama la.
Kauli hiyo ilitolewa jana na Katibu Mkuu wa chama hicho, Dk. Willibrod Slaa, siku moja baada ya Zitto kukaririwa na vyombo vya habari jana kuwa amekuwa akiandaa barua ya kujiuzulu nyadhifa zote ndani ya chama hicho, ikiwamo na ya ubunge. Zitto pia alituma nakala ya maelezo hayo kwa gazeti hili.
Akizungumza na Tanzania Daima jana, Dk. Slaa alisema tangu Zitto aanze kunukuliwa katika baadhi ya vyombo vya habari kuwa anamuunga mkono aliyekuwa Ofisa Habari wa chama hicho, David Kafulula, amekuwa kimya licha ya kumtumia barua pepe kutaka kufahamu ukweli juu ya suala hilo.
"Zilipotolewa taarifa hizo kwenye vyombo vya habari mama yake Zitto, Shida Salum, alieleza kuwa mwanawe hausiki kwa kuwa e-mail yake imekuwa ikiingiliwa na watu na kutuma ujumbe huo," alisema.
Mama huyo pia aliwasilisha madai hayo katika kamati kuu iliyokutana Desemba 2 na kwamba kutokana na hali hiyo alilazimika kumtumia taarifa kwa barua pepe (e-mail) Zitto ili ampe ukweli wa suala hilo, lakini tangu wakati huo amekuwa kimya.
"Baada ya kutolewa kwa madai hayo na kuwasilishwa katika kamati kuu, Desemba 2, nilimtumia e-mail Zitto, lakini mpaka leo (jana) hajanijibu," alisema Dk. Slaa.
Alisema kutokana na hali hiyo, ameanza kupata wasiwasi kuwa huenda mama huyo anadanganywa na mtoto wake huyo (Zitto).
Hata hivyo, alisema asipopata majibu kutoka kwa Zitto atajua kuwa maelezo hayo yana ukweli na kusema kwamba CHADEMA ni taasisi, haitayumba kwa kuondoka kwa mtu yeyote.
"Wakati ule aliondoka Kabourou (Amani Walid Kabourou) na CHADEMA imeendelea kuwapo…anaweza kuondoka Freeman Mbowe na Dk. Slaa, lakini CHADEMA itabaki," alisema.
Aidha, alisema suala hilo linakuzwa ili chama hicho kiachane na ajenda ya kupigania ufisadi nchini na kujikita katika mizozo ya aina hiyo.
"CHADEMA haitaacha kupiga vita ufisadi na ndiyo maana hivi karibuni tumetoa tamko la kuitaka serikali ijibu hoja kuhusu ripoti ya Umoja wa Mataifa (UN) kuichafua Tanzania kuhusu kupeleka silaha kwa kundi la waaasi katika nchi ya Jamhuri ya Kidemokrasia ya Kongo (DRC)," alisema Dk. Slaa.
Jana, Zitto alikaririwa na gazeti moja (si Tanzania Daima) kupita barua pepe akieleza kuchukizwa na siasa chafu zinazoendelea ndani ya chama hicho na kwamba yupo tayari kujivua nyadhifa zote ndani ya chama hicho ikiwamo ubunge.
Mbunge huyo kijana, alikaririwa akieleza kuwa uamuzi wa kumfukuza Kafulila haukuwa wa haki na kwamba ataendelea kumuunga mkono kama atagombea ubunge katika Jimbo la Kigoma Kusini kwa tiketi ya NCCR - Mageuzi na si mgombea wa CHADEMA.
Hivi karibuni, chama hicho kilimtimua Kafulila na Danda Juju, ambao walikuwa wapambe wakuu wa Zitto katika uchaguzi mkuu wa chama hicho, akiwania nafasi ya uenyekiti wa taifa kabla ya kuamua kujitoa badaa ya vikao mbalimbali vya wazee wa chama hicho vilivyomsihi asigombee ili kutokigawa chama katika kipindi hiki kuelekea uchaguzi mkuu mwakani.
Hapo ndipo busara za wazee wa chama zinapohitajika.
Nadhani mzee mtei na waasisi wenzake hawatoachia hali hii iendelee kama kweli wanajali maslahi ya chadema.
lakini vile vile hali hii inatukumbusha kwamba busara walizotumia kumshauri zitto ajitoe kugombea uenyekiti huenda hazikukubaliwa na zitto isipokuwa alishinikizwa.
lakini yote kwa yote wazee wasipoingilia kati mapema sakata hili chadema kutatimka vumbi hivi karibuni.
Mungu awanusuru na kimbunga kinachowanyemelea.