Habari za leo Ndugu wana Forum, Leo nimekuja na hii habari kutoka gazeti la wapinzani wetu kuhusu bwana Lipumba katika hili sakata la rada. Japokuwa linawasema viongozi wangu vibaya lakini duh!!
THATS THE TRUTH
Lipumba afichua siri mpya ya rada
Ibrahim Lipumba
Kutoka gazeti la 'wapinzani wetu' Tanzania Daima,
na Asha Bani
SIKU chache, baada ya Rais Jakaya Kikwete kumkingia kifua Rais mstaafu Benjamin Mkapa, kwa kuwataka Watanzania waache kumhusisha katika sakata la ununuzi wa rada, Mwenyekiti wa Chama cha Wananchi (CUF), Profesa Ibrahim Lipumba, ameibuka na tuhuma nzito dhidi ya serikali.
Lipumba, mmoja wa viongozi wa mwanzo kabisa wa kisiasa kuonya kuhusu kashfa hiyo ya rada iliyoligharimu taifa dola za Marekani bilioni 40, aliilaumu serikali kwa kumficha mhusika mkuu wa sakata hilo, ambalo katika miezi ya hivi karibuni limezusha mjadala mkali ndani ya Bunge la Uingereza na miongoni mwa Watanzania wadadisi.
Akizungumza na waandishi wa habari, ofisini kwake Buguruni, Dar es Salaam, Lipumba bila ya kumtaja kwa jina, alisema mhusika mkuu aliyeliingiza taifa katika kashfa hiyo ya rushwa ni kijana Mtanzania anayeishi nchini Uingereza, akiwa na pasi ya nchi hiyo hiyo.
Lipumba alieleza kushangazwa kwake na hatua hiyo ya serikali kufumbia macho ukweli huo, na kumwacha Mtanzania huyo aliyesema ndiye aliyevuna pato liliso halali linalofikia dola bilioni 12.
Alisema, uchunguzi uliofanywa na makachero wa Uingereza, umebaini kuwa aliyekula rushwa ya dola za Marekani mil. 12 kutokana na ununuzi wa rada hiyo, ni kijana wa Kitanzania na viongozi wa serikali wanamfahamu, lakini wameamua kufumba macho na wala hawataki kulijadili suala hilo.
Serikali inamjua kijana aliyefanya udanganyifu huo wa kula rushwa, ni kijana wa Kitanzania mwenye kitambulisho cha uraia wa Uingereza. Wananyamaza, hawataki kumtaja ili achukuliwe hatua. Hii inaonyesha kuwa, Tanzania ni nchi iliyojaa rushwa, alisema Prof. Lipumba.
Alisema hivi sasa Uingereza inamchunguza mtu huyo aliyeshirikiana na maofisa wa Kampuni ya BAE System waliouzia Tanzania rada hiyo kwa njia za rushwa.
Mwanasiasa huyo, aliyepata kuwa mshauri wa kiuchumi wa Rais wa Awamu ya Pili, Ali Hassan Mwinyi na Rais Yoweri Museveni wa Uganda, alisema jeuri ya viongozi ndiyo iliyosababisha wakatae kusikiliza ushauri aliotoa mapema mwaka 2000 na 2001 kuhusu ununuzi huo wa rada.
Alisema mwaka 2000, serikali ilipoamua kununua rada hiyo, alimwandikia barua Rais mstaafu Benjamin Mkapa na aliyekuwa Waziri Mkuu wake, Frederick Sumaye, akiwatahadharisha kuhusu uamuzi huo.
Lipumba alisema, pamoja na nakala ya barua hiyo kuiwasilisha kwa aliyekuwa Spika wa Bunge wakati huo, Pius Msekwa, bado serikali iliendelea na mipango yake ya kununua rada hiyo, ambayo sasa imegeuka na kuwa kashfa ya kimataifa.
Alisema katika barua yake hiyo, alieleza wazi msimamo wake na wa chama cha CUF, kupinga uamuzi wa kununua rada kwa bei kubwa ya dola bil. 40 za Kimarekani wakati nchi ikiwa katika lindi zito la umaskini.
Prof. Lipumba alisema mwaka 2002 aliandika barua nyingine kwa Mkapa na nakala akaipeleka tena kwa Sumaye, akiionya serikali kuhusu suala hilo hilo, na akaonya kuhusu kuwapo kwa vitendo vya rushwa katika ununuzi wake.
Nilishangaa kuona Tanzania, kama nchi chepe kama Abunuasi, lakini imepata wapi uwezo wa kununua rada ya dola bilioni 40? alihoji Prof. Lipumba.
Alisema pamoja na Serikali ya Mkapa kupuuza ushauri wake, hakuishia hapo, na hivi karibuni tena, wakati wa kikao cha Bunge kilichomalizika, aliandika barua ya tatu kwa wabunge wa chama chake na akampelekea nakala Spika Samuel Sitta, akiwataka waliwasilishe suala hilo bungeni.
Hata hivyo, kwa sababu ambazo hakuzitaja, barua yake hiyo pia iliwekwa kapuni, na Bunge likamaliza kikao chake bila ya ajenda hiyo kujadiliwa.
Alisema, Serikali ya Tanzania inapaswa kulaumiwa kwa kulea rushwa, na ili ijisafishe, ni lazima ichukue hatua dhidi ya kijana huyo wa Kitanzania, ambaye alichukua rushwa.
Akizungumzia hali ya uchumi wa taifa, Prof. Lipumba alisema, inazidi kuwa ngumu na mfumuko wa bei unazidi kuongezeka.
Alisema, mfumuko wa bei kwa bidhaa muhimu unaathiri kwa kiwango kikubwa maisha ya Watanzania, yanayoendelea kuwa magumu kiasi cha kuwafanya wazeeke zaidi wakati muda wa kuzeeka bado.
Alisema, bei ya mafuta nchini inazidi kupanda, bei ya bidhaa mbalimbali zinapanda pia wakati serikali iliahidi kupunguza bei ya mafuta.
Katika soko la dunia, alisema bei ya mafuta imepungua kutoka dola 75 hadi 60, lakini katika nchi ya Tanzania bei ya mafuta bado iko juu.
Prof. Lipumba alisema, wakulima wanapatwa na wakati mgumu kutokana na bei za bidhaa zao kuwa chini na kuwafanya kunyonyeka, huku serikali ikishindwa kuwatetea.
Wakulima wa korosho walitangaziwa na serikali kuzidishiwa bei ya kilo ya korosho kutoka sh 300 hadi 600, lakini kwa sasa hali inazidi kuwa ngumu kwao, kwa kuwa wanauza korosho hizo kwa kilo sh 200 hadi 300 ambapo kwa mkulima anakuwa amekandamizwa, alisema Prof. Lipumba.
Alisema, utafiti alioufanya amegundua wakulima wengi wa korosho wamezirundika korosho zao ndani wakisubiri bei mpya kutangazwa.
Prof. Lipumba, alisema kampuni za madini nyingi nchini zimeingia katika kutapeli uchumi wa Tanzania kutokana na kupata faida kubwa, lakini serikali haipati faida yeyote.
Akizungumzia suala la uchaguzi wa Jimbo la Tunduru, alisema chama chake kiko katika mazingira mazuri ya kushinda, hasa baada ya mgombea wake kuungwa mkono hata na baadhi ya wanachama wa chama tawala, CCM.