Fikra dhaifu huweza kutawala kwa muda wote ule ambao fikra hizo zinaonekana na hudhaniwa kuwa zina nguvu. (M. M. Original quote). Watu wenye kukubali fikra dhaifu wakidhania zina nguvu, huweza kuzitetea fikra hizo hata kwa kumwaga damu. Hata hivyo fikra zenye nguvu zinapotokea lazima zigongane na fikra zile zinazoonekana zina nguvu na kumbe ni dhaifu. Mgongano huo ni wa lazima na usioepukika.
Unapotokea mgongano huo njia mojawapo ya fikra dhaifu kujitutumia ni kudai kuwa hizo fikra mpya na zenye nguvu ni fikra zile zile za awali isipokuwa zimebadilishwa tu na watu na hivyo kuziuza tena kwa lugha nyingine. Zinapozidi kutishiwa fikra dhaifu badala ya kushambulia zile fikra zenye nguvu na kujaribu kuzishinda huanza kushambulia wabeba fikra zenye nguvu na kuwafanya wawe duni!
Hapa ndipo tunavuka kutoka mgongano wa kifikra na kuwa mgongano wa watu, vyombo na taasisi. Yote hata hivyo ni sehemu ya mapambano yale yale ya fikra. Ni jukumu la wale wanaoamini kuwa fikra zao zina nguvu kusimama kidete na kutosalimu amri, au kupiga magoti ya msamaha, au kurudi nyuma kwa woga!
a. Upinzani hakuna Tanzania?
Mtoa mada katangaza kwa ujasiri kuwa "Upinzani hakuna Tanzania ni Uwongo mtupu".
Naomba niangalia kwanza kichwa cha habari mkinikubalia, ili niweze kuonesha japo kwa wenye uwezo wa kuona kuwa kauli hiyo ndani yake inapingana yenyewe (has internal contradition).
= upinzani hakuna Tanzani = Sasa kama hakuna upinzani hakuna cha kujadili. Unaweza vipi kujadili kitu ambacho hakipo kihalisia au kinadharia? Mtu akija nyumbani kwako na kusema "hakuna mlango" aidha anasema kweli au anadangaya. Kwa sababu ni rahisi kumuonesha mlango ulipo au mahali ambapo mlango haupo.
= Ni uongo mtupu = Sasa kama upinzani haupo unawezaje kuwa uongo? Aidha upinzani upo na ni "uongo" au haupo na siyo uongo kwa sababu uongo hauwezi kuwa hewani! Sasa kama mtu anasema "mlango haupo, ni matundu tu kwenye mlango" hawezi kuwa anasema kweli kwa sababu aidha mlango ni mbovu, unaning'inia kwenye kona, umevunjika, au una matatizo fulani.
b. Upinzani upo au vyama vya upinzani havipo?
Mtoa hoja alipoanza kuzungumza akaanza kuonesha anachozungumzia hasa. Lakini anajichanganya kwa sababu aidha anazungumzia Upinzani, baadhi ya viongozi wa upinzani, au vyama vya upinzani. Hebu tuangalia mkanganyo huu dhahiri na wa wazi.
Vyama vyoooote vya upinzani Tanzania
Sasa, ndugu yetu zomba anasema "vyama vyoote vya upinzani Tanzania". Sasa kwa kudai kwanza kuna vyama vya upinzani, anadai mambo mawili kwamba vipi, na ni vya upinzani. Hivyo, kwa kukiri kwake mwenyewe anasema "upinzani" upo na ushahidi ni wake ni kuwepo kwa vyama vyake. Hilo peke yake linafuta sehemu ya kwanza ya kichwa chake cha habari kisemacho "upinzani hakuna".
"vilianzishwa na system",
Hata hili nalo linajibu swali lake, kuwa kama vyama vya upinzani vipo na vilianzishwa na system, anachosema kuwa system ndiyo ilianzisha upinzani. Sasa kauli yake hii ina ukweli mkubwa kuliko anavyodhania. Na tuungalie:
Ni kweli kuwa tume iliyokuwa inakusanya mawazo kuhusu mfumo wa vyama vingi ilitokana na CCM na maamuzi ya CCM. Mmojawapo wa wajumbe wake alikuwa ni Philip Marmo na nakumbuka tulivyofanya mazungumzo kuhusu ili mwaka 1990 kule Mbulu.
Matokeo yake tukaambiwa kuwa asilimia 80 ya Watanzania walitaka tuendelee na mfumo wa chama kimoja na ni asilimia 20 tu waliotaka tubadilishe. Kwenye "wengi wape" Tanzania tungeendelea kuwa na mfumo wa chama kimoja kwani miaka kumi na tano baadaye asilimia 80 ya wapiga kura waliichagua CCM na hivyo kwa namna moja kuakisi mawazo ya wakati ule japo kwa sababu tofauti.
Hivyo, kitendo cha serikali ya chama kimoja iliyokuwa na labda ambayo bado inakubalika na wananchi wengi kuamua kubadili mfumo wa kisiasa hata kama ni kutokana na nguvu zilizokuwa nje ya uwezo wake, na kukubali upinzani urudi tena nchini kilikuwa ni kitendo cha wao kuanzisha upinzani. So factually, yuko sawa ni mfumo (system) ya CCM iliyoanzisha upinzani.
Lakini kuna jambo jingine ambalo Mtoa hoja ameshindwa kutuonesha. Je mawazo ya upinzani yaani yaliyo kinyume na CCM tunayoyashuhudia leo hii na ambayo yametufikisha hapa leo ni mazao ya CCM? Je ni CCM waliotuambia tuibua maswala ya rada, Buzwagi, Richmond, ufisadi BoT n.k Kama CCM wamefanya haya basi wamerukwa na akili na kwa hakika akili zao hazina akili!
Mawazo ya upinzani hayapandikizwi na hayawezi kuanzishwa na mtu yeyote, yanatokea ndani ya mtu huyo au jamii hiyo. Kwa hilo tunaweza pia kuwapa sifa CCM. Ni kweli ni wao wamewapa watu sababu ya kuwa na mawazo ya upinzani.
Kama CCM ingekuwa inatawala vizuri, inasimamia fedha zetu vizuri, inashughulikia matatizo ya wananchi, haielei mafisadi, inatoa nafasi sawa kwa wote n.k kusingekuwa na mtu mwenye mawazo ya kipinzani. Lakini kwa vile wao (CCM) wako kinyume na maadili mema na bora ya uongozi wamesababisha watu kuwa na mawazo ya upinzani.
Hivyo kwa hilo pia mtoa hoja yuko sawa.
Lakini ndugu yetu sidhani kama tatizo lake ni upinzani per se, bali ni viongozi waupinzani. Kama hilo ndilo tatizo lake, basi naomba kutoa hoja kuwa mada ibadilishwe na iwe juu ya "viongozi wa upinzani wako kwenye System" au "Hakuna viongozi wa upinzani wasiokuwa kwenye system" kwani mada ilivyo sasa siyo tu imepotoka bali pia haina ukweli wa kimantiki, kihistoria na kihalisia.
Upinzani Tanzania upo, na si uongo kwani hilo ni kweli. Kama anataka tuzungumzie viongozi na jinsi walivyopatikana na walivyo sasa tunaweza kuendelea na mjadala huo!!!!
peace!