•
CCM yatamba kwenye udiwani
*CHADEMA yafurukuta Songea, TLP Arusha
Na John Daniel, Dodoma
KATIBU Mkuu wa CCM Bw. Yusuph Makamba, ameubeza Muungano wa vyama vinne vya Upinzani, akisema ni sawa na wagonjwa dhidi yakwani utasambaratika wakati wa Uchaguzi Mkuu mwaka 2010.
Amesema Muungano huo pia ni sawa na paka watatu ambao wakiwekewa panya mbele kila mmoja atataka kumla bila kujali kuwa ni kitu kimoja hivyo kuishia kugombana wao kwa wao.
Bw. Makamba alisema hayo jana mjini hapa wakati akizungumza na waandishi wa habari kuhusu matokeo ya uchaguzi wa udiwani katika kata 14 ambazo alitamba kuwa CCM imeuaibisha muungano huo kwa kunyakua kata 11.
"Kuna Muungano wa Vyama vinne vya Upinzani vya CUF, CHADEMA, TLP na NCCR-Mageuzi, lengo la Muungano huo ni kuing'oa CCM madarakani na juzi wamefanya majaribio ya kuachiana kata katika uchaguzi wa kata 14, lakini awali katika kata 16 walikuwa na viti sita lakini sasa wameambulia viti vitatu tu kati ya kata 14, tumewashinda sana," alitamba.
Katibu huyo ambaye aliainisha kata zote 11 ambazo CCM imeshinda na zile tatu zilizochukuliwa na wapinzani alisema
Watanzania bado wanakipenda chama chake tawala na kwamba kama mtu ana matatizo ni mtu na wala si chama na kutamba kuwa kitaendelea kutawala kwa kuwa kina sera zinazotekelezeka. Kuhusu tuhuma zinazotolewa na wapinzani dhidi ya viongozi mbalimbali wa Serikali na chama chake, alikebehi akisema hayo ni maneno yanayotokana na kukosa sera baada ya kuona kuwa za CCM zinatekelezeka na kugusa mahitaji muhimu ya Watanzania na kuwataka kwanza wao wajisafishe kabla ya kukinyooshea kidole chama chake.
"
Wapinzani walisema sera za CCM hazitekelezi, sasa shule tunajenga, walimu wanajifunza, barabara tunatengeneza na mwakani tunaanza kila kijiji kuwa na zahanati, wamekosa cha kusema sasa wamebaki na kusema uongo na kashfa dhidi ya viongozi wa Serikali na CCM, rushwa, mara mafisadi. "Hata mwongo uwe na akiba ya uwongo wa kusema kesho, usimalize uwongo wote kwa siku moja, nawatahadharisha wapinzani, kuwa wamewachosha Watanzania kwa uongo, hata siku watakaposema ukweli hawataeleweka," alisema Bw. Makamba na kuongeza:
"Wanasema CCM inachota fedha za Serikali wakati wao wanaiba fedha za ruzuku zinazotolewa na Serikali na kununua majumba yao binafsi, wanapokuwa jukwaani hawasemi hayo, wanasema tu mawaziri wa CCM, kila chama kinapata ruzuku ya Serikali, CCM inatumia vizuri kwa kazi za chama si kununua nyumba za watu binafsi kwa sh. milioni 40," alisema Bw. Makamba.
Kuhusu Uchaguzi Mkuu wa CCM alisema maandalizi yote yamekamilika na kwamba kinachosubiriwa sasa ni wajumbe kuwasili na kwamba jumla ya wajumbe 1,969 (sasa ni 1,968 baada ya Bibi Salome Mbatia, kufariki dunia hivi karibuni) wa mkutano pamoja wageni waalikwa 550 wamealikwa wakiwamo 60 kutoka nje ya nchi, viongozi wa vyama vyote vya siasa, waasisi wa CCM, viongozi waastafu na wageni wengine.
"Mwaka huu tumejiandaa vya kutosha, kila mjumbe atapata mashati mawili sawa na muda wa kikao cha siku mbili, hoteli zote tulishalipia tangu mwezi wa nane, nyumba tatu mpya zimejengwa kwa ajili ya viongozi wakuu, wastaafu na waasisi na viongozi waalikwa, hata wajumbe wakifika leo, mkutano unafanyika," alitamba Bw. Makamba.
Alipoulizwa kama Taasisi ya Kuzuia na Kupambana na Rushwa (TAKUKURU) wamealikwa kushughulikia tatizo hilo katika Mkutano huo alisema "wewe (Mwandishi) kazi yako nini...na wale kazi yao ni kushughulikia rushwa popote wanapohisi kuna rushwa wanakwenda si lazima waalikwe".
Kuhusu malalamiko yaliotolewa na baadhi ya wana CCM ya kuwapa vyeo wanaohamia chama hicho kutoka kambi ya upinzani alisema hilo si tatizo na kwamba hata Mwislamu akiokoka na kuingia Ukristo, anaweza kuwa Mzee wa Kanisa ili mradi awe na uwezo.
Naye Cresensia Kapinga anaripoti kutoka Songea, kuwa mgombea udiwani katika Kata ya Majengo mjini hapa kwa tiketi ya CCM, Bw. Alfani Kigwenembe, amebwagwa na mgombea wa CHADEMA, Bw. Iddi Ibrahim Abdalah, aliyeibuka kidedea kwenye uchaguzi mdogo.
Akitangaza matokeo ya uchaguzi huo juzi saa 5 usiku huku mamia ya wakazi wa manispaa ya Songea wakiwa wamelizunguka jengo la SACCOS ya wafanyakazi wa halmashauri ya manispaa ya Songea ambamo shughuli za kuhesabu kura, zilikuwa zikifanyika, msimamizi wa uchaguzi, Bw. Edgar Belege, alisema wapiga kura waliotarajiwa walikuwa 3,754 kati yao wanawake wakiwa 1,948 na vituo vilivyopangwa kupigia kura vikiwa 10.
Bw. Belege ambaye pia ni Mkurugenzi wa Halmashauri ya Manispaa ya Songea, alisema katika uchaguzi ambao ulianza saa 12 asubuhi, ulifanyika vizuri na kwamba matokeo ni Kwamba Bw. Kigwenembe alipata kura 554 na Bw. Abdalah kura 1,015 na hivyo kutangazwa kuwa mshindi.
Alisema pamoja na ushindi huo, Bw. Abdalah hatua ya kwanza atakula kiapo cha kuingia kwenye Baraza la Madiwani ambalo linatalajiwa kufanyika hivi karibuni na kuwa mpaka mchakato wa uchaguzi unamalizika hakukuwa pingamizi kutoka kwa mgombea aliyeshindwa.
Akizungumza na waandishi wa habari baada ya kutangazwa mshindi, Bw. alisema ushindi alioupata ni matokeo ya udhaifu wa CCM kwani awali aliomba kugombea udiwani kwa tiketi ya CCM kwenye kura za maoni, wakambwaga na kudai kwamba yeye ni 'bata' asiyeuzika lakini CHADEMA wakaridhika naye na kumteua kugombea.
Alieleza kukubali kuwa mwakilishi wa wananchi wa Majengo kwenye Baraza ambako atakuwa mtetezi katika kuchochea maendeleo ya kata hiyo na si kukimbilia kutafuta maslahi binafsi ambayo hayanufaishi wananchi ambao ni wapiga kura wa kata ya Majengo.
Mwenyekiti wa CHADEMA, Bw. Joseph Fuime, alisema ushindi wa udiwani wa kata ya Majengo, ni mvua za rasharasha na kwamba kwa sasa CHADEMA inajipanga kuchukua nafasi nyingine za udiwani wa kata zingine ikiwa ni pamoja na ubunge wa jimbo la Songea Mjini.
Aidha, matokeo ya awali ya uchaguzi mdogo wa udiwani katika kata za Muwesi na Malumba wilayani Tunduru, CCM iliibuka kidedea, ambapo katika kata ya Muwesi, Bw. Nurdini Nolela alipata kura 1,140 na kata ya Malumba Bw. Msenga Saidi alipata kura 1,557.
Naye Glory Mhiliwa, anaripoti kutoka Arusha, kwamba CCM katika manispaa ya Arusha kimebwagwa na Tanzania Labour Party (TLP), katika uchaguzi mdogo wa udiwani katika kata ya Sombetini uliofanyika juzi.
Kabla ya kutangazwa matokeo ya jumla ya uchaguzi huo, TLP tayari ilishabaini kuwa mgombea wao amenyakua kiti cha udiwani wa kata hiyo, hivyo kuanza shamrashamra kushangilia kuibwaga CCM.
Shamrashamra hizo zilisababisha vurugu kubwa baada ya aliyekuwa mgombea ubunge wa TLP, Arusha, Bw. Godbless Lema kupigwa na Polisi.
Pia wafuasi wa TLP katika vurugu hizo, walipigwa na mabomu ya machozi na Polisi kwenye kituo cha kupigia kura cha shule ya msingi Sombetini, ambako kulikuwa na vurugu.
Vurugu hizo zilianza saa 12 jioni, kutokana na wafuasi wa TLP na CCM kuanza kurushiana maneno ya kejeli na polisi kufika katika kituo hicho na kutumia mabomu ya kutoa machozi kutuliza vurugu.
Hata hivyo, licha ya tambo na shamrashamra za wana CCM kujihakikishia kuchukua kata hiyo kwa madai kuwa ni chama tawala kisicho na upinzani,TLP iliibuka kidedea kwa kura 42.
Akitangaza matokeo hayo jana jijini hapa, Msimamizi wa Uchaguzi wa manispaa ya Arusha, Dkt. Job Laizer, alisema Bw. Chemu Mawazo wa TLP aliibuka mshindi baada ya kupata kura 1,515 na mpinzani wake kutoka CCM Bw. Fabian Muhindi kupata kura 1,473.
Dkt. Laizer alisema katika uchaguzi huo, kura 2,988 zilipigwa sawa na asilimia 13 ya watu waliojiandikisha ambao walikuwa ni 22,149.
Alieleza kuwa katika uchaguzi huo, kura 49 zilikataliwa na wapiga kura waliojitokeza.
Upinzani katika kampeni zake ulitumia silaha za kashfa kuhusiana na mkataba wa Buzwagi na tuhuma za ufisadi dhidi ya viongozi wa Serikali.
Hata hivyo, baadhi wa wana CCM wa wilaya ya Arusha, waliwatupia lawama viongozi wa CCM ngazi ya wilaya, kwa kukaidi maoni yao ambao tangu awali waliutaka uongozi huo kuwa makini katika uteuzi wa wagombea.
http://www.majira.co.tz/kurasa.php?soma=tanzania&habariNamba=4371
sasa hili la kuiba pesa za ruzuku si ufisadi eeh?
haya tuchambue ripoti ya mkuuu makamba.
mwaka huu utaisha kwa kilio kwa ndugu zetu hawa.