Siri ya mabilioni ya Chenge Jersey
na Mwandishi Wetu
Tanzania Daima~Sauti ya Watu
MBUNGE wa Bariadi Magharibi, Andrew Chenge, ameanza kufanya juhudi mahususi za kujinusuru na mkono wa sheria unaoweza kumnasa kutokana na akaunti yake moja iliyoko Jersey, Uingereza kukutwa na zaidi ya dola za Marekani milioni moja, ambazo zinahofiwa kuwa na uhusiano na rushwa iliyotolewa kwa maofisa wa serikali wakati Tanzania iliponunua rada kutoka nchini Uingereza mwaka 2002.
Habari za uhakika ambazo Tanzania Daima imezipata kutoka kwa watu walio karibu na mwanasiasa huyo ambaye jina lake limekuwa likitawala vichwa vingi vya magazeti kwa takriban wiki mbili sasa zinaeleza kwamba, tayari ujumbe maalumu umeshatumwa nchini Finland ili kujaribu kumuokoa Chenge katika kadhia hiyo ambayo ilisababisha alazimike kujiuzulu uwaziri hivi karibuni.
Chanzo cha habari cha kuaminika kimeieleza Tanzania Daima kwamba, uamuzi huo wa Chenge na wanasheria wake umechukuliwa kama jitihada za kujaribu kuhakikisha fedha hizo hazihusishwi kwa namna yoyote ile na zile zinazoaminika kuwa zilitolewa na Kampuni ya BAE ya nchini Uingereza inayolalamikiwa kuiuzia Tanzania rada kwa bei kubwa kuliko ilivyostahili.
Kwa mujibu wa chanzo hicho cha habari, uamuzi huo wa kutuma ujumbe wa mtu mmoja mzito kwenda nchini Finland umefanywa kwa siri kubwa na pasipo kuwahusisha maofisa wa Taasisi ya Uchunguzi wa Makosa Makubwa ya Jinai ya SFO, ambao wanatarajia kuanza kufanya uchunguzi mkali katika kipindi kifupi kijacho.
Kikubwa ambacho kimesababisha kufikiwa kwa uamuzi huo ni ukweli kwamba, fedha hizo ambazo ni sawa na shilingi bilioni 1.2 za Tanzania, ziliingia katika akaunti hiyo mwaka 2002, wakati ule ule uliposainiwa mkataba wa BAE Systems kuiuzia Tanzania rada hiyo.
Ni kweli amelazimika (Chenge) kutuma ujumbe maalumu kwenda Finland ili kumuomba ...aliyeziweka fedha zile katika ile akaunti awe tayari kujitokeza na kueleza sababu ya kuziingiza na malengo yake. Mjumbe anasubiriwa kwa hamu Dar kwani bado hajarudi, alisema mtoa habari huyo ambaye hakuwa tayari kutajwa jina lake gazetini.
Chanzo hicho cha habari kimeieleza Tanzania Daima kwamba, fedha hizo zilizowekwa katika Kisiwa cha Jersey zilikuwa zimetengwa kwa ajili ya mradi mahususi aliokataa kuutaja, ambao hata hivyo alidai ulikuwa hauna mahusiano yoyote na rada.
Ninaweza kukuhakikishia kwamba, fedha zile zina maelezo yake ambayo hayana uhusiano wowote na ununuzi wa rada, alisema mtoa habari wetu ambaye hata hivyo alishindwa kueleza iwapo zilipatikana kihalali na kwa nini basi zilihifadhiwa katika Kisiwa cha Jersey na si hapa nchini.
Mwanasiasa mwingine aliye karibu na Chenge aliyezungumza na gazeti hili mwanzoni mwa wiki hii, alithibitisha kuhusu kutumwa kwa ujumbe huo nchini Finland.
Hata hivyo, pamoja na kukiri kuzifahamu taarifa hizi, mwanasiasa huyo alikataa kuingia katika undani wa suala hilo akimtaka mwandishi kuwasiliana ama na Chenge mwenyewe moja kwa moja au mwanasheria wake.
Ni kweli kuna mtu mmoja mzito (anamtaja kwa wadhifa), ametumwa huko nje kwa kazi hiyo ya kuonana na mwenzake anayehusishwa na fedha hizo...mkitaka taarifa zaidi mtafuteni Chenge mwenyewe au mwanasheria wake, alisema mwanasiasa huyo.
Tanzania Daima ilipowasiliana kwa simu na Chenge mwenyewe kuhusu jambo hilo, ikimuuliza kuhusu kutumwa kwa mtu huyo Finland, hakuwa tayari kusema lolote zaidi ya kumtaka mwandishi asubiri matokeo kamili ya uchunguzi dhidi yake.
Mimi nimeshasema kwamba sina lolote la kusema kuhusu jambo hili kwa sasa. Tuache uchunguzi ukamilike ndipo nitajua nini cha kusema, alisema mwanasiasa huyo kwa ufupi.
Chenge aliendelea kushikilia msimamo wake huo wa kutokuwa tayari kueleza lolote kwa hivi sasa, kila mara mwandishi alipojaribu kutaka maelezo zaidi kuhusu taarifa hizo zinazomhusu.
Habari hizo zinakuja zaidi ya wiki moja tangu Chenge mwenyewe alipozungumzia fedha hizo na kuziita vijisenti, kauli ambayo ilizua manunguniko mengi kutoka kwa wananchi wa kada mbalimbali, ambao waliichukulia kauli hiyo kuwa yenye dharau.
Chenge alilazimika kuzungumzia suala hilo muda mfupi baada ya kutua katika Uwanja wa Kimataifa wa Julius Nyerere (JNIA) jijini Dar es Salaam kwa ndege ya Shirika la Qatar akitokea China alikokuwa ameongozana na Rais Jakaya Kikwete katika ziara ya kiserikali.
Tusubiri uchunguzi ukamilike... kama uthabiti ukithibitisha hata hivyo vijisenti, itajulikana vilipatikanaje, alisema Chenge siku hiyo na kusababisha mshangao kwa wanahabari waliokuwa wakizungumza naye nje ya chumba cha wageni mashuhuri uwanjani hapo (VIP).
Alipoulizwa iwapo kwake yeye kiasi hicho cha zaidi ya dola milioni moja anachohusishwa nacho anaziita vijisenti, Chenge alijibu swali hilo kwa kusema; kila mtu ana viwango vyake.
Chenge alikiri kwamba tuhuma hizo dhidi yake ambazo kwa mara ya kwanza ziliandikwa katika gazeti maarufu na linaloheshimika la nchini Uingereza la The Guardian ni nzito na zilizomshtua.
Pamoja na kujaribu kujibu takriban kila swali aliloulizwa, Chenge alikataa kuelezea chochote kwa undani kuhusu kuwa na fedha hizo au njia alizozipata au iwapo kulikuwa na uhusiano wowote kati ya tuhuma hizo na kashfa ya ununuzi wa rada ya kijeshi mwaka 2002, akisema kufanya hivyo kwa wakati huu, kunaweza kuingilia uchunguzi unaofanywa na taasisi mbalimbali za dola ambazo hata hivyo hakuzitaja.
Hata hivyo alisema amekuwa kiongozi serikalini kwa muda mrefu, akishika nyadhifa tofauti, akiwa ameshika nafasi ya Uanasheria Mkuu wa Serikali kwa miaka 10, hivyo fedha alizokuwa akilipwa zilikuwa halali.
Tuhuma za ufisadi dhidi yangu ni nzito mno
inabidi nipate muda wa kukaa na kutafakari kwanza, na ukweli wa mambo utajulikana baada ya vyombo vya dola vilivyopewa kazi ya kunichunguza kumaliza kazi yake na hapo nitakuwa na muda wa kujibu, alisema Chenge.
Siku kadhaa baada ya kutoa kauli hiyo, Chenge alizungumza na gazeti hili na akaomba radhi kwa matamshi yake ya vijisenti, akisema aliyatoa kwa nia njema na pasipo kuwa na kusudio la kumkejeli mtu yeyote.
Mzozo huu kwa mara ya kwanza uliripotiwa na gazeti la The Guardian la Uingereza likinukuu vyanzo kutoka SFO iliyokuwa ikikaribia kuanzisha uchunguzi wake.
Kwa mujibu wa gazeti hilo, SFO ilikuwa ikitarajia kuanza upya kufanya uchunguzi kuhusu fedha hizo ili kuangalia iwapo zina uhusiano wowote na zile zinazoaminika kutolewa kwa njia ya rushwa wakati Tanzania iliponunua rada ya kijeshi kutoka nchini humo kwa paundi milioni 28 ambazo ni sawa na shilingi bilioni 70.
The Guardian katika habari yake hiyo iliyowekwa katika mtandao wa intaneti, liliripoti kuwa, taarifa hizo zinakuja ikiwa ni miaka mitatu sasa tangu Taasisi ya Kuzuia na Kupambana na Rushwa nchini (Takukuru) kwa kushirikiana na SFO na taasisi za uchunguzi za Uswisi na Jersey zilipoanza kufuatilia kashfa nzima ya ununuzi wa rada.
Gazeti hilo lilimkariri Waziri Chenge akikiri kwamba, fedha hizo ni zake na akatumia fursa hiyo kukanusha kuwapo kwa uhusiano wowote kati ya fedha hizo na kashfa nzima ya ununuzi wa rada, uliofanywa wakati yeye akiwa Mwanasheria Mkuu wa Serikali.
"Jambo la wazi linalotaka kuonekana hapa ni kwamba mimi nilipokea kwa lengo la kujinufaisha mwenyewe fedha za rushwa kutoka BAE. Huu ni uongo, Chenge alikaririwa akilieleza gazeti hilo la Uingereza.
Aidha, gazeti hilo lilimkariri Chenge akisema kuwa, wakati rada hiyo ilipokuwa ikinunuliwa yeye alihusika kwa kiwango kidogo sana katika mchakato mzima, kwani jambo hilo lilishughulikiwa na wizara nyingine na uamuzi ukaidhinishwa na Baraza la Mawaziri.
Mbali ya hilo, gazeti hilo lilimkariri Mwanasheria wa Chenge anayeishi Cleveland, Ohio, nchini Marekani, J Lewis Madorsky, akikanusha kwa niaba ya mteja wake huyo, kuwapo kwa uhusiano wowote kati ya fedha zake na tuhuma zozote.
"Wakati tukitambua kuwa masuala hayo yalitokea muda mrefu uliopita, tunaweza tu tukathibitisha kuwa, tuhuma zozote za ukiukwaji wa sheria, ukiukwaji wa maadili, kutenda isivyo sawa na mambo mengine ya hivyo dhidi ya mteja wetu ni mambo ambayo kimsingi tunayakanusha kwa nguvu kubwa, alisema mwanasheria huyo wa Chenge.
Hata hivyo, gazeti hilo liliandika kwamba, uchunguzi huo dhidi ya Chenge unamfanya yeye kuwa shahidi muhimu, kwani wanaielenga zaidi BAE ambayo inadaiwa ilimlipa wakala mmoja wa Tanzania mamilioni ya fedha ili kujenga ushawishi wa rada iliyokuwa ikiiuza kununuliwa.
Wakala huyo ambaye amekuwa akitajwa kwa muda mrefu na ambaye sasa anaaminika kukimbia nchini na kutafutwa na polisi wa kimataifa ni, Shailesh Vithlani.