The Radar Scandal: Investigation & Progress

The Radar Scandal: Investigation & Progress

Chenge: Nimezushiwa




na Jane Kajoki, Bariadi



MBUNGE wa Bariadi Magharibi aliyejiuzulu uwaziri hivi karibuni kwa kashfa ya kukutwa na fedha zinazohusishwa na ufisadi, Andrew Chenge amewataka wananchi wa jimbo lake kuendelea kumwamini kwa kuwa yeye ni mtu safi na asiye na hatia yoyote kwani tuhuma dhidi yake ni za kuzushwa.

Mbali ya hilo, Chenge alisema alifikia uamuzi wa kujiuzulu wadhifa wa Waziri wa Miundombinu zaidi ya wiki mbili zilizopita si kwa sababu ya kukiri makosa, bali ili kutoa fursa kwa taasisi zinazochunguza kashfa yake kufanya kazi yake kwa uwazi.

Chenge ambaye jana alihutubia mikutano ya hadhara katika maeneo ya Bariadi Mjini, Ramadi, Nyakabimbi na Kapiwi, alisema wakazi wa Dar es Salaam ndio ambao wamekuwa wakimuona kuwa mtu asiyefaa kutokana na kubebeshwa tuhuma zisizo za ukweli, ikiwa ni pamoja na kuzushiwa kifo.

“Dar es Salaam wanasema sifai labda kwa sababu ya sura yangu...Pamoja na watu wa Dar es Salaam kupiga kelele kuwa sifai, naamini sina hatia yoyote, na ndiyo maana nilijiuzulu. Ninyi wakazi wa jimboni kwangu ndio mnajua kama sifai au nafaa.

“Haya mambo yaliyotokea ni ajali ya kisiasa. Ni mambo ya kupikwa na watu, lakini kwa tuhuma hizi wacha tuwape nafasi waendelee na uchunguzi. Sitakiwi kuzungumzia hilo kwa sasa, nimekuja nyumbani kuhimiza shughuli za maendeleo katika jimbo letu katika nyanja zote za barabara, elimu, afya na maji,” alisema Chenge ambaye alivuta umati mkubwa wa wananchi waliokuwa wakimshangilia kila alipokuwa akihutubia.

Alisema pamoja na kujiuzulu uwaziri, aliahidi kuendelea kuwatumikia wananchi wa jimbo lake na akasema anaamini ifikapo mwaka 2010 atakuwa ametekeleza Ilani ya Uchaguzi ya CCM ya mwaka 2005-2010.

“Walio na ndoto za ubunge tukutane kwenye hoja za utekelezaji wa ilani mwaka 2010. Mmeona tulivyojenga shule za sekondari, barabara, mabwawa, visima, vituo vya afya vyote hivyo ni katika jimbo letu. Pamoja na habari ya kuzushiwa kifo, nawaomba mtulie, tushirikiane kwa kutembea kifua mbele kufanya kazi na kujiletea maendeleo,” alisema Chenge ambaye anatembelea jimbo lake kwa mara ya kwanza tangu ajiuzulu.

Akiwa katika Kijiji cha Dutwa alisema alitaja vijisenti si kwa nia ya kukejeli bali akiwa na mtazamo wa Kisukuma ambao wao wanapoongelea ng’ombe 100 kwa mfano wanasema ‘vijing’ombe’.

Hii ni mara ya pili kwa Chenge kuzungumzia kauli yake ya vijisenti ambayo kwa kiwango kikubwa ndiyo inayoonekana kuwa iliyokuza tuhuma alizokuwa akihusishwa nazo.

Kwa mara ya kwanza, Chenge alizungumzia kauli yake hiyo jijini Dar es Salaam wakati alipofanya mahojiano kwa njia ya simu na gazeti hili, ambapo aliwaomba radhi Watanzania ambao walikwazika au kuumizwa na kauli yake hiyo ya vijisenti.

Alisema halikuwa lengo lake kuwakera wananchi kwa kauli hiyo iliyozua mjadala kiasi cha baadhi ya makundi ya watu wa kada tofauti kutoa maoni yao wakimtaka Rais Jakaya Kikwete amwajibishe.

“Mimi siyo Mzaramo. Hiki ni Kiswahili. Sisi wengine kule Usukumani kusema vijimambo, au vijisenti, vijitoto hivi ni kawaida kwa desturi zetu...ndiyo maana napenda kusema wazi kwamba iwapo kuna Watanzania niliwaumiza kwa kauli ile niliyoitoa kwa nia njema kabisa na wala si kwa lengo la kuwakejeli, naomba radhi kwa hilo,” alisema Chenge wakati huo.

Tuhuma dhidi ya Chenge ziliandikwa kwa mara ya kwanza katika gazeti la The Guardian la nchini Uingereza likikariri taarifa kutoka Taasisi ya Uchunguzi wa Makosa Makubwa ya Jinai ya nchini humo (SFO).

Gazeti hilo liliandika kuwa, uchunguzi wa SFO uligundua akaunti moja inayohusishwa na Chenge ikiwa na zaidi ya dola za Marekani milioni moja iliyopo kwenye kisiwa cha Jersey.

Gazeti hilo liliandika kwamba, SFO ilikuwa ikitarajia kuanza upya kufanya uchunguzi kuhusu fedha hizo ili kuangalia iwapo zilikuwa na uhusiano na zile zinazoaminika kuwa zilitolewa kwa njia ya rushwa wakati Tanzania iliponunua rada ya kijeshi kutoka nchini humo kwa paundi milioni 28 ambazo ni sawa na shilingi bilioni 70, mwaka 2002.

The Guardian katika habari yake hiyo liliripoti kuwa, taarifa hizo zinakuja ikiwa ni miaka mitatu sasa tangu Taasisi ya Kuzuia na Kupambana na Rushwa nchini (Takukuru) kwa kushirikiana na SFO na taasisi za uchunguzi za Uswisi na Jersey zilipoanza kuchunguza kuhusu kashfa nzima ya ununuzi wa rada.

Gazeti hilo lilimkariri Waziri Chenge akikiri kwamba fedha hizo ni zake na akatumia fursa hiyo kukanusha kuwapo kwa uhusiano wowote kati ya fedha hizo na kashfa nzima ya ununuzi wa rada, uliofanywa wakati yeye akiwa Mwanasheria Mkuu wa Serikali.

“Jambo la wazi linalotaka kuonekana hapa ni kwamba mimi nilipokea kwa lengo la kujinufaisha mwenyewe fedha za rushwa kutoka BAE. Huu ni uongo,” alisema Chenge.

Aidha, gazeti hilo lilimkariri Chenge akisema kuwa, wakati rada hiyo ilipokuwa ikinunuliwa yeye alihusika kwa kiwango kidogo sana katika mchakato mzima, kwani jambo hilo lilishughulikiwa na wizara nyingine na uamuzi ukaidhinishwa na Baraza la Mawaziri.

Mbali ya hilo, gazeti hilo lilimkariri mwanasheria wa Chenge anayeishi Cleveland, Ohio, nchini Marekani, J Lewis Madorsky, akikanusha kwa niaba ya mteja wake huyo, kuwapo kwa uhusiano wowote kati ya fedha zake na tuhuma zozote.

“Wakati tukitambua kuwa masuala hayo yalitokea muda mrefu uliopita, tunaweza tu tukathibitisha kuwa, tuhuma zozote za ukiukwaji wa sheria, ukiukwaji wa maadili, kutenda isivyo sawa na mambo mengine ya hivyo dhidi ya mteja wetu ni mambo ambayo kimsingi tunayakanusha kwa nguvu kubwa,” alisema mwanasheria huyo wa Chenge.

Hata hivyo, gazeti hilo liliandika uchunguzi huo dhidi ya Chenge unamfanya yeye kuwa tu shahidi muhimu, kwani wanaielenga zaidi BAE ambayo inadaiwa ilimlipa wakala mmoja wa Tanzania mamilioni ya fedha ili kujenga ushawishi wa rada iliyokuwa ikiiuza kununuliwa.

Wakala huyo ambaye amekuwa akitajwa kwa muda mrefu, na ambaye sasa anaaminika kukimbia nchini na kutafutwa na polisi wa kimataifa ni, Shailesh Vithlani.


Hivi amezushiwa kuwa amesaini mikataba ya kifisadi au kuna mtu amegushi saini yake? Au ndio ile hekaya ya wanasheria ya "This document is not mine'?

Wakati ukifika hata mawe yatasema ukweli

JJ
 
Kama yaliyompata Chenge ni ajali ya kisiasa basi namwomba Mungu hizi ajali ziongezeke mpaqka tutakapokuwa na Tanzania yenye uongozi safi.
 
Nimegundua kuwa Mawaziri ambao wamebainika na wale ambao wataibainika kuwa na makosa ya ufisadi au kuhusishwa na dili chafu za wizi wa fedha za umma wataandaa maandamano ya ufisadi kama ya Lowasa na Chenge.


Kitambo atafuatia Mramba naye kuandaa maandamano kwenda Rombo baada ya mambo yake kuwekwa hadharani.


Kamwe, haitakaa itokee.
Siyo Kilimanjaro, na hususani siyo Rombo, na hata kama ni Rombo si kwa ajili ya Mramba.
Ki-siasa Mramba hana ubavu Rombo au Kilimanjaro. Kelele zake ni huko huko Dar, Dodoma.
 
HATERS.jpg
 
Viongozi wa CCM wa Mwanza na Shinyanga walioandaa mapokezi hayo ni vema wakapimwe akili nadhani kuna walakini.
Kiongozi mwenye akili timamu kwa wakati huu na hali ilivyo hawezi kukubali kutumika kuandaa upuuzi kama huu.CCM ingekuwa chama makini,pamoja na kuwapima akili kule Mirembe ingewaita kujieleza makusudio yao yalikuwa nini?
 
these kind of things only happens in Tanzania.

viongozi wanajua kuwa wanaowaongoza hamna kitu, ndo maana wanafanya kila aina ya upuuzi.

taifa letu haliwezi kuwa safi mpaka pale watu wengi zaidi watakapopata elimu ya zaidi ya form 6. na hilo lina long way kufikiwa.
 
ALL THE BEST CHENGE (change) Lakini UKUMBUKE KUWA SIKIO LA KUFA HALISIKII DAWA.....it is good that you have learnt that the people who took you to the way up, are the ones that you need the most now on your way down!
 
"Small nations are like indecently dressed women. They tempt the evil-minded." - JK Nyerere

UMENIACHA HOI!!!
hIVI HUYU NYRERE ALIWA VIPI MBONA VITU ALIVYOVIONGEA ZAMANI MPAKA LEO VIKO APPLICABLE?
Anyway, Chenge anatumia pesa, kuvuta watu, ngechinja ngombe hapa daa uone kama mamilioni ya watu na mashati yao ya kijani wasingejaa kwake, hata wangepiga makofi hotuba zake.
 
Kujisafisha! Nadhani kuna watu wanatuona kuwa sisi wapiga kura hatuna akili kabisa na tunaweza kununuliwa kwa chakula cha siku moja. Kawaida hii ikiendelea itafikia wakati mtu anaua na anaandaliwa mapokezi kwa kuwa tu anakuja kujisafisha.

Nimeshangazwa sana na kitendo hiki cha kujisafisha kwa huyu fisadi, ktendo kingine ni kile kilichofanywa na viongozi wakuu wa chama mkoani, wilayani na katika majimbo, yaani ianfikia wakati hata kiongozi wa wilaya (mkuu wa wilaya) naye anashiriki katika upumbavu huu. Kweli CCM chama cha mafisadi.

Sijashangazwa na umati uliojitokeza kwani najua hawa wote walinunuliwa kwa ng'ombe na wali, kwani la mahalialipokuwa anapita huyu fisi kulikangushwa bonge la ''sherehe'. Mafisadi wananunua watu ili wawapokee, unakumbuka suala la bwana Sauper na mapanki ya mwanza ambako JK alikanunusha na chama kununua watu kumuunga mkono. Bahati mbaya sana kwao kwani ukweli ulidhihirika na kweli watu wanakula mapanki.


Ikifika saa, wanaokushangilia watakutandika viboko vyo moto
 
Ina maana hawa waandishi wa Habari waliamua kuyakuza maandamano hayo??Huu ukaribu wa waandishi wa Habari na wanasiasa utatupeleka kubaya.

Sio waandishi wote.

Kuna ile type ya kina Balile ambao watafanya chochote for a buck!
 
Huyu kwanza analeta Elementi za ukabila.Huyu ni mtu hatari sana.Inatakiwa akemewe kwani hizo statement zake anajitetea nazo kwamba ni za kisukuma.Sasa tumegundua dhambi yake nyingine zaidi ya ufisani na MKABILA
 
Kwani Kuna Ng'ombe Alibaki?
Nadhani Chakula Chote Kililiwa, Na Bajeti Yote Ya Kamisheni Ilitumika. That Is The Point To Me.
Lakini Kwanini Wavae Nguo Za Kijani, Ina Maana Wanadhalilisha Ccm? Au Ndio Imewatuma?
ITS TIME CCM WAKATAE NGUO ZAKE KUVALIWA KATIKA MAMBO KAMA HAYA, INATIA KICHEFUCHEFU,
HIZI NGUO KWA SASA NIKIZIONA TU NAPATA PICHA YA WATU WAONGO, SELFISH, WABABAISHAJI, CROOKS, WEZI, MAJAMBAZI, MACHO JUU JUU, MALAYA ETC
 
Kampuni iliyomzulia balaa Chenge yabanwa

Habari Zinazoshabihiana
• Serikali yatoa mabilioni kukarabati barabara zote nchini 06.03.2007 [Soma]
• Chenge: Wabaya wangu wamenizulia 08.05.2008 [Soma]
• Maoni kujinga EAC kugharimu milioni 700/- 22.03.2006 [Soma]

Na Mwandishi Wetu

KAMPUNI ya BAE Systems ya Uingereza inayotuhumiwa kutumia vitendo vya rushwa katika kupata masoko nje ya nchi ikiwemo Tanzania ilikouza rada ya kijeshi, wiki hii imepata pigo jingine katika utendaji wake.

Kampuni hiyo ambayo ndiyo iliyomzulia balaa aliyekuwa Waziri wa Miundomibinu nchini, Bw. Andrew Chenge ikidaiwa kuwa pauni 507,000 alizoziweka kwenye ukaunti ya ughaibuni visiwani Jersey huenda ni sehemu ya fedha za rushwa zinazodaiwa kutolewa kwa waandamizi kadhaa hapa nchini katika ununuzi wa rada hiyo, sasa 'imetiwa hatiani' kuwa haina maadili.

Kutiwa huko hatiani kwa kampuni hiyo kunazidi kuongeza nguvu katika nadharia ya vitendo vichafu zaidi vya BAE katika shughuli zake za kibiashara na linaweza kuwa pia ni pigo kwa watuhumiwa waliojihusisha nayo.

Kwa mujibu wa ripoti ya ukaguzi wa ndani wa kampuni hiyo iliyofanywa na Jaji Woolf, Mwanasheria Mwandamizi na mkongwe nchini Uingereza, BAE katika ripoti hiyo ambayo gazeti hili limefanikiwa kuiona nakala yake, imelaumiwa kwa kutozingatia maadili katika utendaji wake au kutokuwa kabisa na kanuni za kimaadili hali iliyoifanya iandamwe na tuhuma za ufisadi ambazo zimeiathiri kibiashara.

"Kwa kina,Mwenyekiti na Ofisa Mtendaji Mkuu (wa BAE), katika majadiliano na Kamati, wamekiri kuwa huko nyuma kampuni ilikosa kutilia maanani maadili ya utendaji kazi.

"Haya yote yalichangia kwa kiasi kikubwa katika kuifanya kampuni ijiingize katika tuhuma za kufanya vitendo visivyokubalika na hayo yote yameathiri taswira yake."

Ingawa Kamati hiyo haikuangalia moja kwa moja matukio mahsusi kama ya BAE kutoa kamisheni kubwa kwa wakala wa rada nchini Tanzania, Bw. Vithlani Shailes ili awape viongozi kadhaa wa kisiasa kuchagiza ununuzi huo, ripoti inakiri kuwa kampuni hiyo inapaswa kuzingatia maadili kama inataka kujenga hadhi yake kwa siku za usoni.

Hata hivyo pamoja na kuiumbua kwa kiwango hicho kampuni ya BAE, ripoti ya Jaji Wolf imepingwa kutokana na ukweli kuwa alikuwa akilipwa na kampuni hiyo pauni 6,000 (zaidi ya sh. milioni moja) kwa siku kuiandaa ripoti hiyo iliyolenga kusaidia kusafisha taswira ya kampuni hiyo.Ripoti hiyo ilichukua miezi tisa kuandaliwa.

Taarifa rasmi ya BAE nayo iliunga mkono changamoto hiyo ikisema: "Ripoti ya Kamati hii ni changmoto muhimu kwa BAE katika kuelekea kujijengea uwajibikaji imara wa ndani katika shughuli zake za kila siku.

“Tutaangalia kwa makini mapendekezo ya ripoti hiyo na tunathibitisha kuwa tunajituma kuhakikisha tunatekeleza yale yaliyopendekezwa," alisema Ofisa Mtendaji Mkuu wa BAE, Bw. Mike Turner.

Wanaoipinga zaidi ripoti hiyo wanasema haikujibu maswali mengi kama ilivyotarajiwa awali.

Maswali kama Je, BAE iliunda kampuni ya siri ughaibuni iitwayo Red Diamond kwa ajili ya kupitishia fedha za rushwa kwenda nchi mbalimbali na iwapo kampuni hiyo iliweka kwenye akaunti moja nchini Uswisi kiasi cha fedha kinachofikia asilimia 31 ya fedha iliyotumika kuuza rada ya kijeshi nchini Tanzania, hayajajibika.

Pia maswali kama kampuni hiyo iliwahi kumuajiri Bw. lfons Mensdorff-Pouilly, ambaye aliwahi kukamatwa kwa rushwa, kuwa wakala wake wa siri kwa ajili ya nchi za Ulaya ya Kati? Na pia iwapo kampuni hiyo iliwaalika makahaba kwa ajili ya kuwaburudhisha viongozi wa Serikali yaSaudi Arabia nchini Marekani ikiwa ni 'takrima' kwa ajili ya kupata mikataba ya kuiuzia nchi hiyo silaha.

Alipoulizwa kuhusu hayo yote wakati akitangaza ripoti yake Jaji Wolf alijibu kwa kifupi tu: "Kazi yetu haikuwa kuangalia hayo yaliyotokea huko nyuma."

BAE imekuwa ikichunguzwa katika miji ya London, Washington, Dar es Salaam, Bucharest, Prague, Berne, Budapest na Johannesburg kote kwa tuhuma za kutoa rushwa kuchagiza biashara jambo ambalo limewaudhi wabunge wengi wa nchi hiyo.

Baadhi ya Waingereza pia wameidhihaki ripoti ya Jaji Wolf kwa kutoeleza undani wa tuhuma hizo na kushindwa kutoa majibu ya maswali ya msingi na kuiita 'tamko tamu la kitaalauma.'

Wakati BAE ikijisafisha kwa kutumia staili hiyo, mmoja wa watuhumiwa wa kufaidika na rushwa zinazodaiwa kutolewa na kampuni hiyo, Bw. Andrew Chenge yeye wiki hii ametumia staili ya kukutana na wananchi wa jimbo lake Bariadi, Shinyanga, ambako pamoja na mambo mengine alieleza kuskamwa kwake kuwa ni 'matatizo ya watu wa Dar es Salaam.'

Chenge pia anaelezwa 'kumwaga' pilau na ng'ombe karibu katika kila sehemu alikopita huku pia akijinadi kuwa yeye ni mtu safi, anayechafuliwa tu na baadhi ya maadui zake kisiasa.Hakuwataja.

Kitu kimoja kilicho dhahiri kwa Chenge na BAE, wote kwa sasa wakiwa chini ya uchunguzi mzito wa Taasisi ya Kupambana na Makosa ya Ufisadi ya Uingereza (SFO), wote wawili, kwa mkakati unaowezwa kuonekana kuwa wa pamoja, wameamua kutumia fedha ili 'kusafisha' taswira zao.
 
Wazito PPF wachota ‘vijisenti’

Mwandishi Wetu Mei 14, 2008

Walipwa kama wastaafu, kisha warudi kazini

WAKURUGENZI kadhaa wa Mfuko wa Pesheni ya Mashirika ya Umma (PPF), wamejilipa mamilioni ya fedha, ikiwa ni mafao yao ya kustaafu kazi, lakini imebainika kuwa wanaendelea na nyadhifa zao licha ya kujilipa.

Habari ambazo Raia Mwema imezipata wiki hii zinasema kuwa mafao ya wakurugenzi hao yanafikia kati ya Sh. milioni 130 na 220 kwa kila mmoja, kiwango ambacho kinafikia jumla ya Sh. bilioni 1.2, kilichotolewa na PPF kwa ‘wastaafu’ hao.

Raia Mwema imearifiwa kuwa malipo hayo yamefanyika kwa kufuata utaratibu uitwao Group Endowment Scheme, ambao unahusu mafao ya wafanyakazi yanayopaswa kutolewa kwa mtumishi anapostaafu kazi katika PPF.

Kwa mujibu wa habari hizo, chini ya mpango wa Group Endowment Scheme, wafanyakazi hukubaliana na mwajiri kabla ya kuanza kazi, ambapo shirika linakuwa linachangia kiasi fulani cha fedha kama akiba ya mfanyakazi, ambayo hupewa mara anapostaafu.

“Mnakubaliana wewe mfanyakazi na mwajiri. Ni kama mkataba wa aina fulani. Shirika linatoa fungu, linakuchangia…Unapoondoka kazini wakati unastaafu, unapewa fedha zako ili zikusaidie kwenye maisha yako mengine.

“Ukipewa fedha chini ya utaratibu wa Group Endowment Scheme, hatutarajii kuona mhusika anabaki kazini. Kama kuna watu wanafanya hivyo, basi wanauhujumu utaratibu huu,” alisema Mkurugenzi Mkuu wa zamani wa PPF, Naftali Nsemwa, ambaye aliombwa na Raia Mwema kutoa ufafanuzi wa jinsi mpango huo unavyofanya kazi.

Lakini Raia Mwema imeambiwa kwamba katika jambo ambalo linashangaza, wakurugenzi hao sita wa PPF wamejilipa mafao hayo ya Sh. bilioni 1.2, kwa maana ya kustaafu, lakini hadi jana Jumanne walikuwa wakiendelea na kazi, wakiwa tayari wameweka mafao yao vibindoni.

Kaimu Mkurugenzi Mkuu wa PPF, Badru Msangi, alipoulizwa kuhusu suala hilo, alikiri kuwapo kwa utaratibu wa Group Endowment Scheme, lakini akakataa kuzungumza zaidi kwa maelezo kuwa yeye si msemaji wa PPF, bali Mkurugenzi Mkuu mwenyewe, William Erio ambaye yuko safarini Afrika Kusini.

Hata baada ya kumsihi azungumze, Msangi alisema: “Msubiri Msemaji wa Shirika, ambaye ni Mkurugenzi Mkuu. Atakuwepo ofisini wiki ijayo. Unapotaka sisi ndio tuzungumze, hututakii mema, unataka tufukuzwe kazi.”

Mwenyekiti wa Bodi ya PPF, Gray Mgonja hakupatikana jana kuzungumzia suala hilo, na hata pale Raia Mwema ilipojaribu kuwasiliana naye, simu yake ilikuwa ikiita mfululizo na baadaye ikafungwa.

Raia Mwema ina majina ya wakurugenzi hao lakini kwa kuwa haikufanikiwa kuzungumza nao kuoata maelezo ya upande wao kwa sasa hawatatajwa.

Habari zaidi zilizopatikana zinasema kulipana huko kumehojiwa na mmoja wa wajumbe wa Bodi ya PPF, Monica Mbega akitaka kujua ni nani aliyeyaidhinisha.

Mbega alihoji suala hilo katika mkutano wa Jumamosi iliyopita wa timu ya ukaguzi ya Bodi ya PPF ambayo yeye ndiye Mwenyekiti wake. Yeye na Erio, na baadhi ya wakurugenzi ambao ni wajumbe wa timu hiyo, wako safarini Afrika Kusini.

Mikataba ya Group Endowment Scheme katika PPF imekuwa ikifanyika kila baada ya miaka mitatu, na mwenye kufaidika na mpango huo anapaswa kuwa awe anastaafu na kuondoka kabisa katika ajira ya PPF.
 
•
Chenge asakamwa jimboni ajitoe siasa

Habari Zinazoshabihiana
• Kikwete mfukuze Chenge -Wasomi 18.04.2008 [Soma]
• Chenge: Wabaya wangu wamenizulia 08.05.2008 [Soma]
• Wapinzani wapinga uteuzi wa Chenge 13.02.2008 [Soma]

Na George Boniphace, Bariadi

ZIARA ya aliyekuwa Waziri wa Miundombinu, Bw. Andrew Chenge, jimboni mwake Bariadi Magharibi iliyoanza juzi, imeleta hisia tofauti miongoni mwa wananchi jimboni humo hivi sasa.

Baadhi ya wananchi waliozungumza na gazeti hili juzi, walisema kitendo cha Bw. Chenge kutembelea jimboni humo akiwa na umati mkubwa wa watu ambao ni wafuasi wake, haumaanishi kwamba anakubalika katika jamii ya wananchi wengi wilayani Bariadi bali nguvu za vijisenti vyake.

Ziara hiyo ya Bw. Chenge jimboni mwake, ilikuwa na nia ya kujisafisha na kuwaelezea wananchi sababu za kujiuzulu kwake uwaziri, baada ya tuhuma za kukutwa na fedha nyingi kwenye akaunti yake katika visiwa vya Jersey, Uingereza.

Wananchi hao kwa nyakati tofauti walisema tangu awali Bw. Chenge alipata wadhifa huo wa ubunge, akiwa hakubaliki na wengi ingawa kwa mshangao alishinda katika uchaguzi wa mwaka 2005 Bariadi Magharibi.

Walieleza kuwa akiwa Mwanasheria Mkuu wa Serikali katika Serikali ya Awamu ya Tatu, Bw. Chenge wananchi alichangia kwa kiasi kikubwa kuiingiza nchi katika mikataba ya kifisadi na yenye utata, kwani alikuwa ndiye Mshauri wa Serikali wa masuala ya kisheria.

Pia wananchi hao walisema sababu zingine ambazo zinawafanya wakazi wa jimbo hilo kumwona kuwa hafai ni tabia yake ya kujisikia yenye majigambo iliyosababisha kutoa kauli chafu ya kuyaita mabilioni ya fedha kuwa vijisenti, huku wananchi wengi jimboni humo wakilazimika kula mlo mmoja kwa siku kutokana na ukosefu wa chakula.

Hali hiyo ilichangiwa na ukosefu wa mvua miaka miwili iliyopita 2006/2007 na wengine kushindwa kulipa karo za watoto wao na huduma duni katika vituo vya afya kutokana na uchakavu wa vifaa.

Mmoja wa wananchi katika mkutano huo wa Bw. Chenge uliofanyika hivi karibuni mjini hapa ambaye alijitambulisha kwa jina la Bw. Busulu Budoto, mkazi wa kijiji cha Igegu wilayani hapa, alisema licha ya kitendo hicho cha mbunge wao kudharau kiasi hicho cha fedha kwenye akaunti yake ya nje na kuwaumiza wananchi wengi nchini kutokana na kauli hiyo, jimboni humo wameonesha kukerwa zaidi.

“Mtu yeyote anayeshabikia ziara hii ya Bw. Chenge kuja kuwadanganya wananchi kwa maneno matamu hana nia njema kwa wakazi wa jimbo hili. Ni ushabiki wa kiini macho,” alisema mmoja wa wananchi hao na mkereketwa wa UDP mjini hapa.

Baadhi ya wananchi ambao walifanya mahojiano na gazeti hili walisema umati wa wananchi ambao walijitokeza katika shamrashamra hizo wengi wao walikuwa wanavutiwa na mlo wa pilau, kwani kila kijiji wilayani hapa kilikuwa kimetengewa sh.300,000 kwa ajili ya mapokezi hayo.

Aidha, wananchi hao waliitupia lawama CCM na viongozi wake ambao walikuwa mstari wa mbele katika kuhakikisha kuwa sherehe hizo za makaribisho zinafana na mtu anayemtupia mwenziwe mchanga jichoni.

Hata hivyo, baadhi ya wananchi katika mkutano huo walijitokeza waziwazi kumshauri mbunge huyo aachane na siasa mwaka 2010 ili kulinda heshima yake katika jimbo hilo na kuwa mfanyabiashara wa kawaida.

Walitoa msimamo wao kuwa endapo Bw. Chenge atalazimisha kuingia katika mchakato huo wa kugombea tena wadhifa huo wa Ubunge wa jimbo hilo, wananchi watalazimika kuandamana kupinga ushindi ambao utakuwa hauna baraka kwa wakazi wa Bariadi na vitongoji vyake.

“Ni heri tubaki kuwa hatuna mwakilishi bungeni kama Chenge atagombea jimbo hili, labda apeleke uozo huo katika jimbo lingine,” alieleza Bw. Budoto.

Bw. Chenge alijiuzulu uwaziri wa Miondombinu hivi karibuni baada ya kutuhumiwa kumiliki kiasi kikubwa cha fedha katika benki ya Jersey, Uingereza na anachunguzwa.

Baada ya kujiuzulu nafasi hiyo ambayo hivi sasa inashikiliwa na Dkt. Shukuru Kawambwa, Bw. Chenge alikwenda jimboni na kufanyiwa sherehe kubwa na wapiga kura wake.
 
Back
Top Bottom