Rostam azua gumzo
na Martin Malera
Tanzania Daima~Sauti ya watu
HATUA ya Mbunge wa Igunga, Rostam Aziz (CCM), kutinga kanisani na kutoa kauli nzito za kujisafisha kutokana na tuhuma za ufisadi zinazomwandama huku akiwasuta wabaya wake kisiasa, imezua maswali mengi kuliko majibu.
Mhadhiri Mwandamizi wa Chuo Kikuu cha Dar es Salaam, Profesa Mwisiga Baregu, alisema jana kuwa anamshangaa mbunge huyo kuamua kulitumia kanisa kujisafisha.
Alisema hali hiyo imelichafua kanisa hilo kubwa na lenye heshima kubwa nchini.
Mimi namshangaa Rostam, lakini pia nalishangaa kanisa lenyewe. KKKT ni kanisa kubwa sana nchini na maaskofu wake kwa nyakati tofauti walishatoa kauli kadha wa kadha za kukemea ufisadi, lakini leo kanisa hilo hilo liko mbele kupokea fedha za ufisadi, hiyo mimi imenishangaza sana, alisema mwanazuoni huyo ambaye pia ni mjumbe wa Kamati Kuu na Halmashauri Kuu ya Chama cha Demokrasia na Maendeleo (CHADEMA).
Rostam anachotakiwa kufanya ni kujibu tuhuma zake ni kwa namna gani amehusika ama hakuhusika kabisa na Richmond au Dowans, lakini kwa stahili hii hawezi kujibu tuhuma, sana sana ataendelea kuibua maswali mengi yasiyo na majibu, na binafsi nashangaa sijui nani mshauri wake aliyemtuma kufanya hivyo, alisisitiza Profesa. Baregu.
Kwa mujibu wa Baregu, Rostam anapaswa kujibu tuhuma zake ama kwa kutumia vyombo vya habari au mahala pengine popote au ndani ya Bunge, lakini si kutumia mimbari ya kanisa kujisafisha.
Kwa upande wa kanisa, Profesa. Baregu alishauri litoe taarifa ni namna gani limekubali kutumika kama kichaka cha kumsafisha Rostam ambaye kwa imani ni muumini wa dini ya Kiislamu.
Profesa Baregu aliwaasa Watanzania na vyombo vya habari kuwa makini na mbinu zinazotumiwa na watuhumiwa wa ufisadi kujisafisha, kwa madai kuwa wana mbinu nyingi mbaya na chafu kwa jamii kutokana na uwezo wao kifedha.
Naye Mwenyekiti wa Chama cha Tanzania Labour (TLP), Augustine Mrema alieleza kushangazwa kwake na hatua ya Rostam kutumia kanisa kujisafisha.
Alisema mbunge huyo ni mjanja kutokana na staili yake aliyotumia kujisafisha na tuhuma zinazomwandama.
Kwa upande wa kanisa, Mrema alilishangaa na kuyataka makanisa yote kuiga mfano na kauli ya Askofu Mkuu wa Jimbo Kuu la Dar es Salaam, Mwadhama Polycarp Kardinali Pengo aliyewahi kuyatahadharisha kujiepusha na fedha za mafisadi.
Hilo kanisa limejidhalilisha, na linaweza kupoteza heshima yake lisipoangalia. Rostam na kanisa wapi na wapi? Halafu kwa nini hakuzungumzia kilichompeleka pale? Kwa nini ameruhusiwa kutumia kanisa kujisafisha? alihoji Mrema na kuongeza kuwa Rostam ameibua maswali mengi kuliko majibu.
Mbali ya viongozi hao, baadhi ya wananchi waliopiga simu katika chumba chetu cha habari, walielezea kushangazwa kwao na hatua ya Rostam kuamua kuuwasha moto unaoonekana kufifia wa ufisadi wa Richmond.
Juzi, Rostam aliibuka Kanisa la Kiinjili la Kilutheri Tanzania Usharika wa Kinondoni, Dar es Salaam, ambako alisema taifa liko kwenye wakati mgumu kisiasa na kijamii, hivyo kuwataka wananchi watumie makanisa kulirejesha katika mstari ulio sahihi.
Mbunge huyo anayeandamwa na jinamizi la ufisadi, alisema waumini wa dini hawamtuhumu mtu, hawamshutumu, hawapendi wenye wivu na wenye chuki bali wanapenda haki.
Alisema hivi sasa nchini, watu wameanzisha tabia ya kuchukiana mpaka kuzushiana uchawi na kuombeana vifo, na kusisitiza kuwa wananchi watumie makanisa kukemea vitu hivyo.
Ingawa katika kauli hiyo hakutaja mtu, lakini mbunge huyo ambaye hajawahi kupata mpinzani katika jimbo lake, alikuwa akizungumzia tukio la hivi karibuni bungeni, ambako Mbunge wa Bariadi Mashariki, Andrew Chenge (CCM) na ofisa mmoja mwandamizi wa Bunge, walituhumiwa kuweka vitu aina fulani ya uchawi au sumu ya kisasa ndani ya Ukumbi wa Bunge.
Alisema ana watoto watatu ambao aliahidi kanisani hapo kwamba anataka awalee katika misingi ya dini ili wawe wananchi bora na waadilifu hapo baadaye.
Nawashukuru kwa kuamua kunialika kuwa mgeni rasmi leo, hii ni ishara kwamba mmeamua kupuuza viji-maneno na upuuzi wa vijiweni. Nafurahi kuwa miongoni mwenu
hamtuhumu, hamshutumu, hampendi wenye wivu na wenye chuki, mnapenda haki. Ninao watoto watatu na nataka niwalee katika misingi hii, alisema Rostam huku akishangiliwa na umati wa watu walioshiriki hafla hiyo.
Rostam alialikwa kanisani hapo katika hafla ya uzinduzi wa albamu ya kwaya ya Amkeni ya kanisa hilo, ambako alitoa mchango wa sh milioni tano kuchangia seti za vyombo vya muziki kwa kwaya hiyo pamoja na jenereta yenye thamani ya sh milioni 2.6.
Katika siku za hivi karibuni, Rostam amekuwa akiandamwa na jinamizi la ufisadi kiasi cha baadhi ya wabunge na wananchi kutaka achukuliwe hatua za kisheria.
Amekuwa akitajwa kuwa na uhusiano na Kampuni ya Dowans iliyokuwa inaendesha shughuli za Richmond kabla ya serikali hivi karibuni kuamua kuvunja mkataba wake. Hata hivyo Rostam alikanusha tuhuma hizo kupitia gazeti hili