CHADEMA yanunua kesi ya Mengi, Masha
Mbowe ashtuka Masha kumtisha Mengi
na Edward Kinabo
CHAMA cha Demokrasia na Maendeleo (CHADEMA), kimeinunua kesi ya Waziri wa Mambo ya Ndani, Lawrence Masha, dhidi ya Mwenyekiti wa IPP, Reginald Mengi, kwa kusisitiza kuwa kina ushahidi kutoka kwenye vikao nyeti vya serikali kuwa waziri huyo kijana ndiye aliyepeleka hoja ya kutaka mfanyabiashara huyo afilisiwe.
Hali hiyo ilibainishwa jana na mwenyekiti wa chama hicho, Freeman Mbowe, katika mahojiano maalumu na Tanzania Daima jana ofisini kwake jijini Dar es Salaam.
Mbowe aliithibitishia Tanzania Daima kwamba chama chake kina ushahidi wa kuaminika kutoka kwenye vikao nyeti vya serikali kwamba Waziri Masha ndiye aliyeishauri serikali ipange mkakati wa kumfilisi Mengi kwa lengo la kuvidhoofisha vyombo vyake vya habari visiendelee kuibua na kuandika habari zinazohusu ufisadi.
Alisema mwelekeo wa suala hili unamnyima Waziri Masha haki ya kuzungumza na hapaswi kujitetea wala kusema chochote zaidi ya kuviachia vyombo vya ulinzi na usalama vifanye kazi yake kwa uhuru.
Kitendo cha Waziri Masha kumpa Mzee Mengi amri ya kuwasilisha ushahidi ndani ya siku saba kinashangaza, kwani Waziri huyo hana mamlaka kisheria ya kudai ushahidi na badala yake chombo chenye mamlaka ya kudai ushahidi ni mahakama, alisema Mbowe. Mwenyekiti huyo alisema kama serikali inaona imeonewa au imechafuliwa katika suala hilo, iende ikashitaki mahakamani na si vinginevyo.
Waziri hana mamlaka ya kisheria ya kudai kupelekewa ushahidi. Chombo chenye mamlaka hayo ni mahakama. Kama wao (serikali) wanaona wameonewa au wamechafuliwa waende mahakamani, kama ni uongo waende wakashtaki kama walivyokimbilia mahakamani kwenye sakata la mgomo wa walimu, alisisitiza Mbowe.
Kwa mujibu wa Mbowe, Waziri Masha ameendeleza rekodi ya mawaziri wengine wa Serikali ya Awamu ya Nne ya kupenda kukurupuka na kupayuka hovyo bila kutafakari kwa makini na matokeo yake ni kuvuka mipaka ya mamlaka waliyonayo.
Na hii imekuwa ni tabia ya Mawaziri wa Kikwete ya kukurupuka na kupayuka hovyo bila kutafakari kwa umakini hadi wanavuka mipaka ya mamlaka yao. Waziri hana mamlaka ya kudai apelekewe ushahidi
hiyo ni kazi ya mahakama, alisema Mbowe.
Alisema mtu au chombo chochote kinachopinga ufisadi kinahitaji kulindwa kwa gharama yoyote badala ya kutishwa na serikali.
Aliitaka serikali kutumia vyombo vyake kufanya mambo ya maana na yenye maslahi kwa taifa . Serikali itumie vyombo vyake kufanya mambo ya maana na yenye maslahi kwa taifa. Jambo hili la kumfilisi Mengi halina tija. Serikali inataka kuwawajibisha wananchi badala ya wananchi kuiwajibisha serikali. Serikali iache mchezo wa kutisha raia wake, iache kuwahujumu raia wa nchi. Jukumu la serikali ni kupambana na uhalifu si kufanya uhalifu dhidi ya raia wake wema, alisema Mbowe.
Alisema inasikitisha kuona serikali inataka kumshughulikia Mengi kwa kumfilisi bila kujali mchango mkubwa wa vyombo vyake vya habari na biashara katika kupambana na ufisadi na kuwawezesha wananchi kiuchumi.
Alionya kuwa iwapo serikali itamfilisi Mengi kama alivyopendekeza Waziri Masha, uchumi utaathirika kwa pato la taifa kushuka kwa sababu itapoteza mapato ya kodi zinazotozwa kwenye makampuni ya mfanyabiashara huyo.
Kumfilisi Mengi ni kuathiri ajira
.hata uchumi wa nchi unaweza kuathirika. Ni wananchi wangapi wameajiriwa kwenye makampuni yaliyo chini ya Mengi
.Watanzania wengi watapoteza ajira. Pato la taifa linaweza kushuka
..serikali itapoteza mapato ya kodi inayopata kutoka kwenye makampuni anayoyamiliki Mengi. Serikali iache mchezo wa kushugulikia raia wake na kudai kuwa inawalinda, alitahadhalisha Mbowe.
Juzi Naibu Katibu Mkuu wa CHADEMA, Zitto Kabwe, alisema ana ushahidi kuwa Waziri Masha, ndiye aliyepeleka hoja ya kumhujumu Mengi katika vikao vya juu vya serikali.
Zitto alisema yeye hana sababu ya kumtetea Mengi ila hawezi kunyamaza kuona Mtanzania anayeipenda nchi yake na kulazimika kupinga ufisadi, anafanyiwa hujuma. Naye Katibu Mkuu wa chama hicho, Dk. Wilbrod Slaa, jana alinukuliwa na vyombo kadhaa vya habari akimtaka Waziri Masha kuviacha vyombo vya upelelezi vifanye uchunguzi wake.
Kuibuka kwa sakata hilo kunatokana na Mengi kumtuhumu Waziri mmoja kuwa ameagiza abambikiwe kodi bandia ya kiasi kikubwa atakachoshindwa kulipa ili hatimaye afilisiwe.
Mengi akizungumza na vyombo vya habari wiki iliyopita, alimtuhumu waziri huyo ambaye hakumtaja jina, kuwa amekuwa akitumiwa ujumbe wa vitisho kutokana na vyombo vyake vya habari kuwa mstari wa mbele katika kupinga ufisadi.
Kutokana na hatua hiyo, Waziri wa Mambo ya Ndani ya Nchi, Lawrence Masha, kupitia mkutano wake na waandishi wa habari, alimpa Mengi siku 7 awe amekwisha wasilisha vielelezo vya kuthibitisha madai yake kwake yeye (Masha), vinginevyo atamchukulia hatua za kisheria.
Akijibu amri ya Masha, Mengi alisema yupo tayari kutupwa jela ikithibitishwa kuwa amedanganya na kumwomba Masha pia aseme kama atakuwa tayari kujiuzulu iwapo ukweli utathibitika.
Hata hivyo juzi jumapili, Masha alinukuliwa na vyombo vya habari akisema kuwa hayuko tayari kujiuzulu kwa sababu nia yake ya kuwaagiza polisi kufanya uchunguzi inalenga kumlinda Mengi.
Alisema kutokana na taarifa ambayo Mengi aliipeleka kituo cha polisi cha Oysterbay, polisi wameamua kuifanyia uchunguzi ili kuhakikisha maisha yake yanakuwa salama.
Alisema, hata kama hawamuamini, basi waupeleke huo ushahidi kwa Rais au Waziri Mkuu kuuonyesha na kama ikibainika kama ni kweli yeye ndiye anayemhujumu Mengi, basi atajiuzulu.
Alidai kuwa yeye hakusema kuwa atamshughulikia Mengi kama alivyonukuliwa kwenye baadhi ya magazeti ila alisema kuwa sheria itachukua mkondo wake kama ikibainika kuwa tuhuma zilizotolewa ni za kweli.