SAKATA LA NDESAMBURO
CHADEMA yaamua kumgeukia Lowassa
.Yamtaka atoe tamko la kukubali au la
.Serikali yakaa kimya, yamsubiri Mengi
Na Tamali Vulu, Tanzania Daima
Chama cha Demokrasia na Maendeleo (CHADEMA), kimemwandikia barua Waziri Mkuu, Edward Lowassa , kikimtaka atoe tamko kuhusu kuhusishwa kwenye tuhuma za rushwa kwa wajumbe wa Kamati ya Haki, Maadili na Madaraka ya Bunge zilizotolewa na Mbunge wa Moshi Mjini, Philemon Ndesamburo.
Barua ya Katibu Mkuu wa chama hicho, Wilbroad Slaa ya Januari 15,2006, kwenda kwa Lowassa, inaeleza kushangazwa na ukimya wake pamoja na tuhuma hizo nzito zilizotolewa na Ndesamburo.
Taarifa ya uhakika ambazo gazeti hili limezipata kutoka Ofisi ya Waziri Mkuu zinaeleza kwamba , barua hiyo imeshafika katika meza ya kiongozi huyo wa tatu kimamlaka serikalini, baada ya Rais na Makamu wa Rais.
Hata hivyo jitihada za gazeti hili kuwasiliana ama na Lowassa mwenyewe au mwandishi wake wa habari, Said Nguba ili kupata maoni yake kuhusu swala hili, zimekuwa zikigonga ukuta kwa takribani wiki moja sasa tangu Ndesamburo alipotoa tuhuma nzito wiki iliyopita, sambamba na Kutangaza kujiuzulu ujumbe wa Kamati ya Haki, Maadili na Madaraka ya Bunge.
Ofisa mmoja wa juu serikalini aliyezungumuza na Tanzania Daima kwa sharti la kutotajwa jina, alisema Waziri Mkuu amekaririwa akiyaeleza maneno hayo ya Ndesamburo kuwa yasiyo na ukweli wowote.
Alipotakiwa na Tanzania Daima aeleze hatua ambazo Lowassa amepanga kuzichukua dhidi ya suala hilo ambalo kauli yake inahusishwa, ofisa huyo alisema, vyombo vinavyohusika vitalishughulikia.
Sisi tunajua ni kwa nini Ndesamburo kasema maneno hayo, Tunajua kila kitu kinachoendelea kuhusu jambo hili. Ni vyema tukanyamaza. Waziri Mkuu anajua anachofanya, hawezi akasema maneno ya namna hiyo. Ipo siku ukweli utabainika, alisema ofisa huyo wa serikali.
Baada yake, ofisa huyo wa Serikali alieleza pia kushangazwa kwake na ukimya wa Mengi ambaye ndiye aliyetajwa na Ndesamburo kumwimbia maneno hayo kuendelea kukaa kimya pasipo kutamka hadharani, iwapo ni kweli alifikisha maneno hayo au la.
Ninyi mnamtafuta Waziri Mkuu atoe tamko, mbona hatujasikia Mengi akisema hadharani ni kweli kuwa alimwambia Ndesamburo meneno haya? Si yuko na anapatikana mbona amekaa kimya? alihoji ofisa huyo.
Slaa katika barua aliyomwandikia Lowasa anasema: Pamoja na uzito wa tuhuma hizi na hasa ukizingatia uzito wa nafasi yako ya Uwaziri Mkuu mpaka sasa hujajitokeza wewe mwenyewe kukanusha au kukubali taarifa hii.
Kwa vyovyote ukimya wako katika suala hili kadiri unayoendelea unaweza kuwafanya wananchi kupoteza imani kuhusu msimamo wako katika vita dhidi ya rushwa na jitihada za kuleta utawala bora nchini.
Kama kweli wewe ulifahamu kuwa kuna mtu ametoa rushwa kwa wabunge na hukuchua hatua zinazostahili, kwa vyovyote ni kinyume cha sheria, maadili ya uongozi, na dhamira ya Mheshimiwa Rais Jakaya Kikwete ya kupambana na rushwa bila kumfumbia macho mtu.
Kwa upande mwingine, tuhuma kwamba mhimili wa serikali unaingilia mhimili wa Bunge zinakuelekea wewe (Waziri Mkuu) moja kwa moja kama kiongozi wa shughuli za serikali bungeni. Suala hili ni kinyume na utawala bora na mgawanyiko wa madaraka uliomo katika sheria na katika ya nchi ambayo umeapa kuilinda, ilieleza sehemu ya barua hiyo ambayo nakala yake imepelekwa kwa Rais Jakaya Kikwete na Spika wa Bunge, Samwel Sitta.
Tayari Spika amemwandikia barua Ndesamburo akimtaka kumwandikia kwa maandishi tuhuma za rushwa alizozitoa dhidi ya kamati hiyo.
Wiki iliyopita, Ndesamburo alitangaza kujiuzulu ujumbe katika kamati hiyo ya madai kuwa alielezwa na Mwenyekiti wa Kampuni ya IPP, Reginald Mengi, kuwa aliambiwa na kiongozi mwandamizi wa serikalini kwamba, wajumbe wa kamati hiyo wamepewa rushwa kutoka kwa mfanyabiashara, Yusuf Manji, ili asitendewe haki kwenye kezi yake na Mbunge wa Mkuranga, Adam Malima.
Ndesamburo alieleza kuwa anahofia usalama wa maisha yake na hataki kuhusika na maamuzi ambayo yanagubikwa na tuhuma za rushwa, huku akitaka kuitwa na Mengi na Mengi na kiongozi huyo ili kuthibitisha madai hayo.
Akichangia bajeti ya Wizara ya Habari, Utamaduni na Michezo, Malima alimtuhumu Mengi kuwa kujipa muda mwingi kujitangaza kwenye matukio yanayomhusu huku akitoa muda mfupo katika matukio yanayomhusu Rais na Waziri Mkuu.
Kutokana na tuhuma hizo, Mengi alilalamika kwa Spika kuwa Malima hakumtendea haki kumtuhumu sehemu ambako hawezi kujitetea.
Baada ya malalamiko hayo , Spika alilipeleka mashauri hayo kujadiliwa kwenye kamati hiyo , hatua iliyozusha malalamiko kutoka kwa baadhi ya wabunge kuwa haikuwa haki.
Tayari Manji ameshatoa tamko kukanusha kuhusika kwa namna yoyote kuwapa rushwa wabunge na ametaka Ndesamburo aeleze kile ambacho alidai kinafichwa katika suala hilo zima.