Inakuwaje katika nchi ya kidemokrasia au ile inayojaribu kujenga jamii ya kidemokrasia kwamba kuna mtu au taasisi fulani inayodai haki isiyokuwa nazo? Ripoti ya Kamati ya Bunge ya Haki, Maadili na Madaraka kuhusu kesi ya Mengi dhidi ya Mhe Malima inawasilishwa baadaye leo. Mhe. Spika Bw. Samuel Sitta hata hivyo amesema hiyo "Ni ripoti ya Spika" na haitawekwa hadharani. Kwa mara nyingine tena Bw. Sitta anatumia nafasi yake ya Uspika kujitwalia madaraka na uwezo asiokuwa nao!! Tumelikataa kwa Rais kuwa Mungu Mtu, tumekataa kwa Wabunge kuwa Miungu watu, na kwa hakika tunakataa kwa Spika wa Bunge la Jamhuri ya Muungano kujiona yeye ni Mungu Mtu!! Mheshimwa Spika, hapo umepotoka! naungana na Watanzania wengine kutaka ripoti hiyo iwekwe hadharani mara tu baada ya kuwasilishwa Bungeni!
Kamati ya Bunge ya Haki, Maadili, na Madaraka imepewa majukumu matatu:
1. Kuchunguza masuala yote yahusuyo haki, kinga, na madaraka ya Bunge yanayopelekwa kwake na spika.
2. Kushughulikia masuala ya maadili yanayohusu Wabunge
3. Kufikiria jambo jingine lolote litakalopelekwa kwake na Spika.
Hakuna mahala hata pamoja panaposema kuwa Ripoti za Kamati za Bunge ni "Za Spika". Hadi hivi sasa kuna ripoti kadhaa kutoka Kamati nyingine za Bunge ambazo ziko hadharani na hazikudaiwa kuwa ni za siri. Miongoni mwa ripoti hizo ni hizi:
http://www.parliament.go.tz/bunge/Docs/Report/Committee/0506/Ujenzi.pdf
http://www.parliament.go.tz/bunge/Docs/Report/Committee/0506/Kilimo.pdf
Lazima tuelewe kuwa ripoti hii hahihusu madai ya Mbunge wa Moshi Mjini Bw. Ndesamburo bali kwa mujibu wa maagizo waliyopewa ilikuwa inachunguza madai ya Mbunge wa Mkuranga Mhe. Adam Kighoma Ali Malima kuwa mmiliki wa vyombo mbalimbali vya habari Bw. Reginald Mengi anatumia vyombo vyake kujitangaza zaidi na kutotoa nafasi ya kutosha kwa viongozi wa serikali hususan matukio yanayomhusu Rais. Ni hapo Bwana Mengi alipoamua kujibu madai hayo ya Bw. Malima kwenye vyombo vya habari na pia kuamua kuleta malalamiko yake Bungeni.
Hapo mwanzo, baadhi ya Wabunge walipinga kabisa kitendo cha Spika kukubali kupokea malalamiko ya Bw. Mengi na wengine walidai kuwa amevunja Katiba! Wengi walidai kuwa wanachosema Bungeni kina kinga! Bw. Sitta aliwajibu wabunge hao na kuwaambia kuwa "hawako juu ya sheria" na pia kuwa wabunge hawawezi kutoa kashfa bungeni, au kumtukana mtu bungeni wakijidhania kuwa wana kinga kwa vile tu wao ni wabunge!
Hata hivyo hatujui kama ripoti hii imekamilika vipi wakati mmoja wa wajumbe wake amejiengua? Je, inakuwaje ripoti hii ikamilike wakati tuhuma nzito dhidi ya wajumbe wa kamati hiyo zimetolewa na hazijajibiwa? Mmoja wa Wabunge wa Bunge la Jamhuri ya Muungano amedai kuwa Waziri Mkuu wa jamhuri ya Muungano amemwambia Bw. Mengi kuwa tume hiyo kuwa imepokea rushwa toka mpinzani wa kibiashara wa Bw. Mengi aitwaye bw. Yusuph Manji ili tume imkute Bw. Mengi na hatia ya kutumia vyombo vyake vya habari vibaya?
Ni wazi kuwa ripoti hii haiwezi kuwa kamili na ili kutafuta haki, mambo kadhaa lazima yafanyike.
a. Madai ya Mbunge wa Moshi vijijini ni mazito na kama yana ukweli basi ni lazima uchunguzi huru ufanyike. Bunge haliwezi kujichunguza lenyewe!! Hivyo, Rais Kikwete ateue tume huru itakayoongozwa na jaji wa mahakama kuu ili ifuatilie madai ya Bw. Ndesamburo na kuwaita wale wote wanaotajwa katika madai hayo! Je Bw. Mengi aliambiwa na Waziri Mkuu kuwa Manji ameihonga tume ya Maadili? Je, Waziri Mkuu alimwambia Bw. Mengi juu ya hongo hiyo ya Bw. Manji, na yeye alipata wapi habari hizo? Njia pekee ya kufahamu ukweli wa jambo hilo ni kuwaita Bw. Ndesamburo, Bw. Mengi, na Bw. Edward Lowassa ili kutafuta ukweli. Tume iwe na uwezo wa kuitisha mashahidi (subpoena power)
b. Kama Bw. Sitta hataki ripoti hiyo iwekwe hadharani, basi ripoti hiyo isiletwe Bungeni kabisa na aikatae kwani mchakato wa upatikanaji wake umevurugika kutokana na tuhuma nzito.
c. Kamati ya Maadili ivunjwe na Kamati mpya iundwe ili kuchunguza suala la Mengi na Malima. Ama sivyo, Kamati Maalum ya Bunge iundwe kufanya hivyo. Kwa vyovyote vile Kamati iliyopo sasa kutokana na unyeti wa majukumu yake haiwezi kumtendea haki Mbunge mmoja wa upinzani ambaye wanamuaona ana matata! Kamati maalum itakayoundwa iwe na uwiano sawa wa wajumbe. Maazimio ya kamati hiyo lazima yawe ya wingi, na ikitokea kura kufungana basi suala hilo linapelekwa kwenye Bunge zima!
d. Serikali ihakikishe kuwa Mbunge wa Moshi Mjini anapatiwa ulinzi na hakuna mtu yeyote anayetumia madaraka yake kumuonea au kumuadhibu kwa namna yoyote ile. Endapo Bw. Ndesamburo atapatwa na madhara yoyote, wananchi watapoteza imani na viongozi wao.
Tuhuma za rushwa dhidi ya chombo cha Bunge ni tuhuma nzito na lazima zipewe uzito unaostahili. Kujaribu kuzidharau tuhuma hizo kisa tu kuwa zimetolewa na Mbunge wa upinzani ambaye huko nyuma aliwahi kutoa kauli zisizothibitika ni kutokomaa kisiasa. Kila hoja na madai lazima yasimame peke yake na tusimhukumu Bw. Ndesamburo kwa makosa yake ya nyuma.
Watanzania wanataka kujua. Waziri Mkuu wa Jamhuri ya Muungano Bw. Edward Lowassa alimwambia Bw. Mengi kuwa Kamati ya Bunge ya Maadili imepewa Hongo na Bw. Manji? Je, Bw. Mengi anakumbuka kuambiwa maneno hayo na Waziri Mkuu? Waziri Mkuu alipata wapi taarifa hizo za rushwa na hatua gani alichukua!? Kama Bw. Mengi na Bw. Lowassa watakanusha chini ya kiapo kuwa hakukuwa na mazungumzo ya namna hiyo, Bw. Ndesamburo yuko tayari kuomba radhi Bunge la Tanzania na wajumbe wenzake na wananchi wenzake ambao wameshtushwa na kuumizwa na tuhuma hizo nzito dhidi ya chombo chetu cha kutunga sheria? Kama tutapa majibu sijui, lakini kuuliza tutaendelea kuuliza!!