Shutuma za Ndesamburo zatikisa Bunge, viongozi
Shadrack Sagati
HabariLeo; Friday,January 12, 2007
Adaiwa kukiuka kanuni zake
Foka asema lazima ukweli ubainike
TUHUMA za rushwa dhidi ya baadhi ya wabunge zilizotolewa na Mbunge wa Chadema wa Moshi Mjini, Phillemon Ndesamburo zimeelezwa kuwa ni nzito na zimewashitua wabunge na viongozi wa chombo hicho.
Kutokana na hali hiyo uongozi wa Bunge unatafakari hatua za kuchukua dhidi ya tuhuma hizo za kuhongwa na mmoja wa wafanyabiashara ili wabunge wapindishe haki katika shauri la Reginald Mengi na Adam Malima, Mbunge wa Mkuranga. Viongozi wa Bunge ambao walizungumza na gazeti hili jana, walisema tuhuma hizo zimewashitua na ni lazima ukweli uweze kubainika na utangazwe mbele ya wananchi.
Naibu Spika wa Bunge, Anne Makinda aliliambia HabariLeo kuwa Ndesamburo ametoa shutuma nzito dhidi ya wabunge wenzake na hatua yake ya kuzitangaza kwenye vyombo vya habari ni kuvunja kanuni za Bunge. Anne alisema Ndesamburo alishajadiliana na Spika Samwel Sitta na kueleweshwa hatua za kuchukua, hivyo hakustahili kujiuzulu wala kutangaza mambo hayo kwenye vyombo vya habari.
Spika baada ya kujadiliana naye alimshauri vizuri tu kwamba asijiuzulu na badala yake kingeundwa chombo kingine cha kuwahoji wajumbe wa kamati hiyo pamoja na watu wengine ambao Ndesamburo alitaka wahojiwe, alisema Anne.
Naibu spika alisema Ndesamburo alikuwa anataka Mengi na Waziri Mkuu, Edward Lowassa wahojiwe, jambo ambalo Spika alimshauri avute subira iundwe kamati nyingine ya kuchunguza tuhuma hizo.
Wewe uliona wapi watuhumiwa waanze tena kuwahoji watuhumiwa wenzao, isingewezekana. Ndiyo maana Spika akashauri kiundwe chombo kingine cha kuchunguza tuhuma hizo, alisema.
Alisema katika suala hilo Spika alishauri wajumbe wa kamati ya maadili, haki na madaraka ya bunge wangeandika ripoti kuonyesha kama wameshindwa kuendelea na shauri hilo kuhusiana na tuhuma hizo. Naibu Spika alisema kuwa licha ya ushauri huo mzuri, Ndesamburo alingangania Mengi na Waziri Mkuu waitwe. Baadaye akaleta barua yake ya kujiuzulu, alisema.
Alisema Ndesamburo hakupaswa kuzungumzia suala hilo kwenye kamati tu bali pia alitakiwa aende kuzitoa tuhuma hizo kwenye Taasisi ya Kuzuia Rushwa (PCB) ambayo ndiyo yenye uwezo wa kuchunguza tuhuma hizo.
Naye Katibu wa Bunge, Damian Foka alisema Ndesamburo alipaswa kupeleka malalamiko yake kimya kimya kwa Spika yaweze kufanyiwa uchunguzi badala ya kwenda kutangaza kwenye vyombo vya habari.
Tunajifunza nini kweye sakata hili??