Ndesamburo azushia wabunge rushwa
Ni kuhusu shauri la Mengi na Malima
Ajiuzulu ujumbe kamati ya bunge
Akaidi ushauri wa spika
Na Mwandishi Wetu
MBUNGE wa Moshi Mjini kwa tiketi ya CHADEMA, Philemon Ndesamburo, ameibuka na madai kwamba wajumbe wenzake wa Kamati ya Haki, Maadili na Madaraka ya Bunge, wamehongwa na mfanyabishara Yusuf Manji, ili wasitende haki.
Ndesamburo alisema kuwa hongo hiyo imetolewa ili kamati impendelee Mbunge wa Mkuranga, Adam Malima, aliyelalamikiwa na mfanyabiashara Reginald Mengi, kwamba alimkashifu katika hoja yake bungeni.Ndesamburo aliwambia waandishi wa habari jana katika ofisi za Bunge kuwa, alitaarifiwa habari hizo na Mengi, aliyedai aliambiwa na Waziri Mkuu Edward Lowassa, katika mazungumzo yao binafsi.Ndesamburo aliongeza: "Mwaka jana, Waziri Mkuu alimuita Mengi na kumwambia, usipoliondoa shauri utashindwa, Manji amewahonga wabunge wengi."
Kutokana na sababu hizo, Ndesamburo jana alitangaza kujiuzulu ujumbe wa Kamati ya Haki, Maadili na Madaraka ya Bunge, akidai anajiengua kutokana na kashfa ya rushwa iliyoighubika.
Mengi analalamika kukashifiwa na Malima kwamba katika kikao cha Bunge lililopita, alidai matangazo ya tevisheni ya ITV humpa mmiliki wake (Mengi) muda mrefu kuliko viongozi wa kitatifa.
Kwa mujibu wa Ndesamburo, licha ya Mengi kuarifiwa kupitia mazungumzo binafsi, aliona 'halivumiliki' na kuamua kumtaarifu yeye (Ndesamburo), jambo ambalo alilifikisha kamati husika, ambayo yeye pia ni mjumbe.
Aliendelea kudai baada ya kupewa taarifa hiyo kutoka kwa Mengi, alilifikisha kwenye kamati ambako hakuridhika na hatua inayochukuliwa.
Ndesamburo aliendelea kumkariri Mengi kwamba, kwa mara ya pili baada ya Waziri Mkuu Lowassa kupata taarifa kwamba suala hilo limefikishwa kwenye kamati, alimuita Mengi kwa mara nyingine ili amkane yeye, jambo ambalo Mengi alilikataa.
Hata hivyo, licha ya kumtambua Lowassa kama rafiki yake, hakueleza ni sababu zipi zilizomfanya asimfuate kumuona binafsi kuhoji ni kwa nini amechukua hatua hiyo.
Suala la Mbunge Malima na Mengi, sasa linajadiliwa kwa kipindi cha zaidi ya mwezi mmoja kwenye kamati husika.Alisema, viongozi wa bunge wakiongozwa na Spika Samuel Sitta, wamemsihi kwa muda mrefu hadi jana asubuhi asiendelee kulikuza suala hilo na aachane na azma yake ya kujiuzulu, lakini hakukubaliana nao.Katika hatua ya kutatanisha, Ndesamburo aliamua kuita mkutano wa waandishi wa habari, kuliweka hadharani suala hilo, kwani alidai anahofu "maisha yake yako hatarini,"
Alipotakiwa kufafanua, alidai "Waziri Mkuu ni mtu mkubwa" na aliongeza hata binafsi asipokuwa na nia hiyo wapo wafuasi wake wanaoweza kumdhuru, japo alikiri hana ushahidi wowote wa madai hayo yanayomtia hofu. Katika barua yake ya Kujiuzulu ya tarehe ya jana (Gazeti hili lina nakala yake), kwa sehemu inasomeka:
"Kwa masikitiko makubwa, naomba kukutaarifu sitoweza kuendelea kuwa mjumbe wa kamati kuanzia leo (jana) kutokana na kutoridhishwa na mtiririko wa kesi ya mheshimiwa Malima na Mengi." Barua hiyo iliorodhesha sababu hizo kuwa ni: "kuwepo kwa madai kwamba wabunge wamepewa rushwa na Manji na kamati kutolifuatilia suala hili kujua ukweli wa mambo kabla ya kesi ya msingi kuamuliwa." Sababu ya pili ni: "Kuwepo kwa mazingira ya mhimili wa utawala kuingilia mhimili wa Bunge ambayo ni kinyume na utawala bora na mgawanyo wa madaraka. "Dhamira yangu inanisukuma kuamini kwamba mambo haya ni kikwazo cha ukweli na haki hivyo sitawatendea haki Watanzania walionichagua kuwawakilisha bungeni kama nitaendelea kushiriki katika kamati husika."
Source:JANUARI- 11,2007