Labda hii ni update
Aliyeingia bungeni usiku atajwa
na Martin Malera, Dodoma
KATIBU wa Itikadi na Uenezi wa Chama Cha Mapinduzi (CCM), Kapteni John Chiligati, jana alimtaja mbele ya waandishi wa habari mbunge ambaye aliingia katika ukumbi wa Bunge jioni ya Jumatatu.
Tukio hilo linahusishwa na ushirikina kwa mujibu wa taarifa zisizo rasmi, ambazo zimekuwa zikisambaa kwa muda wa siku tatu zilizopita.
Ingawa hakumtaja kwa jina, Chiligati alisema kuwa mbunge huyo alikuwa waziri lakini sasa hana tena wadhifa huo.
Akifafanua, Chiligati alikiri kuwa mbunge huyo aliomba na kupewa ruhusa kuingia ndani ya ukumbi huo wa Bunge, ili kukagua na kuangalia nafasi atakayokuwa anaketi.
Alisema kuwa mbunge huyo alilazimika kufanya hivyo kutokana na kutokuwa na kiti maalumu cha kukalia ndani ya Bunge kutokana na kuondoka kwake kutoka katika wadhifa wa uwaziri.
Chiligati alisema kwamba, kwa kuwa Bunge lilikuwa linaanza vikao vyake siku inayofuata, mbunge huyo aliona ni busara kutafuta mahali pa kukaa jioni hiyo, ili asisumbuke asubuhi.
Alikiri kuwa ni kweli aliingia ndani ya ukumbi wa Bunge na kupita katika kila kiti, akiangalia majina kwa lengo la kutafuta kiti kilichokuwa wazi.
Alisema wakati akifanya hivyo, hakuweka uchawi wowote kama ambavyo inadaiwa na watu hivi sasa.
Kwa taratibu za Bunge, kila kundi ndani ya Bunge hilo lina mahali pake maalumu pa kukaa kwa mpangilio unaoeleweka. Makundi hayo ni pamoja na mawaziri, ambao huketi upande wa kuume kwa Spika, wapinzani, ambao huketi upande wa kushoto wa Spika na wabunge wengine ambao hukaa katika nafasi zilizosalia.
Chini ya utaratibu huo, mpangilio wa kukaa hupangwa mwanzoni mwa Bunge, ambapo kila mbunge hupangiwa kiti chake cha kukaa. Hata hivyo, wabunge wanaruhusiwa kuhama kwa muda kwenda eneo jingine na wanapomaliza dharura hiyo hurejea kwenye viti vyao.
Spika Samuel Sitta, naye alishathibitisha kuwa, zipo picha zinazomuonyesha mbunge huyo akiwa ameandamana na mtumishi mmoja wa Bunge, akipita katika viti kadhaa ndani ya ukumbi huo wakati ukiwa umefungwa.
Ingawa Sitta na Chiligati waliepuka kumtaja mbunge huyo kwa jina, lakini kiongozi ambaye alikuwa waziri na kujiuzulu katika siku za hivi karibuni ni Mbunge wa Bariadi Magharibi, Andrew Chenge.
Chenge alijiuzulu kutokana na kuhusishwa kwake kwenye uchunguzi unaoendeshwa na Taasisi ya Kuchunguza makosa ya rushwa ya Uingereza (SFO).
Makachero wa SFO walivutika kumchunguza Chenge katika uchunguzi wao dhidi ya Kampuni ya Bae Systems ya Uingereza iliyoiuzia Tanzania rada kwa bei ya juu.
Licha ya kuwa Mwanasheria Mkuu wa Serikali wakati mkataba wa mauzo hayo unafikiwa, makachero wa SFO walimkuta Chenge akiwa na akiba ya takriban dola za Marekani milioni moja kwenye akaunti iliyo katika benki moja katika visiwa vya Jersey.
Tangu ajiuzulu nafasi hiyo, Chenge hajawahi kuhudhuria vikao vya Bunge, na ni kweli hivi sasa anawajibika kutafuta nafasi ya kukaa kwa kuwa hataweza tena kukaa katika nafasi ya mawaziri aliyokuwa akikaa zamani.
Tukio hilo limewaweka wabunge roho juu, hasa baada ya Mbunge wa Kyela, Dk. Harrison Mwakyembe, kuugua ghafla katikati ya wiki iliyopita na kulazimika kukimbizwa katika kliniki ya Bunge ili kupata huduma za kiafya.
Wabunge kadhaa sasa wanaonekana kuogopa kuusogelea ukumbi wa Bunge, kutokana na taarifa hizo za kuwepo kwa vitendo vya kishirikina.
Hili tukio limetutia hofu, tunadhani kuna kila sababu ya kukamilisha uchunguzi wa tukio hili mapema. Spika ameeleza kuwa tukio hili linachunguzwa, tunaomba lichunguzwe kweli, tena kwa haraka, ili kutuondolea hofu tuliyonayo sasa, alisema mmoja wa wabunge kutoka Mkoa wa Mwanza.
Mbunge mwingine ambaye pia hakutaka jina lake liandikwe gazetini, alilieleza gazeti hili kuwa Spika anapaswa kutoa taarifa ya tukio hili bungeni na kulitolea ufafanuzi badala ya kuendelea kulizungumza kwenye vyombo vya habari.
Hizi taarifa zipo, wabunge wengi wanazijua, lakini Spika analizungumzia kwenye vyombo vya habari. Mimi nadhani suala hili linagusa maisha yetu, ni bora akalieleza Bunge nini kilitokea, alisema mbunge huyo.
Akizungumza na waandishi juzi, Sitta alisema kuwa, ofisi yake imekabidhi picha za video zilizomnasa mbunge huyo akiwa ameambatana na Ofisa Mwandamizi wa Bunge kwa siri, waliokuwa wakiweka vitu vinavyoaminika kuwa vya kishirikina au aina fulani ya sumu kwenye kila kiti cha mbunge.
Kwa mujibu wa Sitta, picha za mkanda huo zilizonaswa na kamera za usalama zilizomo ndani ya jengo hilo la kisasa, zimefifia kiasi cha kushindwa kubaini kwa haraka watu wanaoonekana ndani ya mkanda huo.
Kutokana na hali hiyo, Sitta alisema ofisi yake imeamua kuukabidhi mkanda wa picha hizo kwa maofisa usalama wa taifa na kwa Kamanda wa Polisi wa Mkoa wa Dodoma, kwa ajili ya kuzifanyia uchunguzi zaidi