Josephat Isango
NITASEMA ukweli daima, ili taifa la Tanzania, linufaike liendelee kudumu. Ni tendo la ukatili sana, ambalo hufanywa na wale tu wenye dhamiri za pekee, ambao kwa kawaida tunaweza tukawaita kwa jina moja tu la ukatili.
Nahitaji ujasiri wa pekee sana, usio na dalili ya hofu kuwadhulumu watu pesa ya kununulia sanda siku ya msiba, hapo kutakuwa na maswali mengi sana kwa sisi wanafalsafa.
Ina maana huyu mtu hajui unyeti wa jambo hili? Na kama anajua kwanini anafanya hivi? Aidha, amekusudia au hajui analolitenda.
Kama anajua anafanya nini mbona anaendelea?
Mateso makubwa yaliyopo kwa Watanzania kwa miongo mingi sasa, yanahitaji wanasiasa makini, wasiotaka kutekeleza matakwa yao binafsi ila matakwa ya Watanzania.
Tumeteseka sana, tunazidi kuteseka, huku kila mmoja akijaribu kuonyesha kuwa kuna ombwe la uongozi katika nchi yetu.
Lakini kwa busara tu hatuwezi kukaa bila uongozi, sasa inapokuwa wale waliotuhadaa tukawaamini tukawapa dhamana wanatusaliti katika wakati muhimu tuwaeleweje?
Akili ya Zitto Kabwe imehasiwa sasa, inatazama kwa macho ya makengeza. Au kama haijahasiwa na kuona kwa macho ya makengeza basi kuna mkakati maalumu wa makusudi wa kuharibu harakati za ukombozi wa Watanzania zinazofanywa na mwanasiasa huyu kijana.
Zitto, Mbunge kijana na mwanasiasa machachari aliyeibukia CHADEMA anawachanganya Watanzania. Aliwahadaa Watanzania wakamwamini, wakajua ni kijana mpiganaji, asiyehongwa na yupo kwa ajili ya wanaoteswa, au wanaokandamizwa. Na kweli ni mzalendo anayepigania ukombozi wa nchi yetu kutoka kwa mafisadi.
Tupo msibani katika safari ya ukombozi, tumechanga pesa ya kununua sanda, Zitto anataka kutudhulumu kwa kuwa kabla ya msiba tulimwamini kuwa ni mwaminifu, ni wa nyumbani, na pesa kiduchu ya kununua sanda isingeweza kumtia kiwewe apate tamaa ya kutusaliti.
Zitto anajua alivyokuwa kivutio kwa Watanzania kwa kukubali kusimaishwa ubunge kwa kusimamia ukweli. Zitto anajua wazi umaarufu wake ulivyoporomoka baada ya kutetea Dowans, kampuni dada ya Richmond iliyo kampuni ya kitapeli.
Zitto hana shaka kuwa umaarufu wake ndani ya chama ulivyoporomoka baada ya kuhusishwa na njama za kuharibu kwa makusudi uchaguzi wa Baraza la Vijana wa CHADEMA (BAVICHA) ili ahakikishe kuwa kipenzi chake David Kafulila anashinda uchaguzi hata kwa njia zisizo halali?
Vijana wakajiuliza, tutalaani vipi vitendo vibaya vya CCM ikiwa vitaota mizizi katika chama makini? Wakapiga kelele, msimamizi wa uchaguzi akafuta matokeo, na Zitto akatoka ukumbini kwa aibu.
Sasa mjadala umeanzia tena kwa Kafulila huyu huyu, ambaye ametenguliwa kuwa Ofisa Habari wa chama, imekuwa gumzo, tena uongozi wenyewe ni wa kuteuliwa.
Hivi iliandikwa wapi kuwa Kafulila ni lazima awe kiongozi tu katika CHADEMA, na kuwa akiondolewa uongozi itakuwa dhambi?
Hatuwezi kufikiri kuwa yule aliyekuwa amemteua ndiye aliyekuwa na uwezo wa kutengua uteuzi? Kwani Kafulila alikuwa kiongozi kwa kupigiwa kura? Na hata kama angekuwa kiongozi wa kupigiwa kura, je, anapotenda kinyume cha utaratibu asingeonywa?
Imefikia hatua tuhoji sasa, je, Zitto anataka tuamini kipi? Yeye ndiye aliyefundisha na kuwasadikisha Watanzania kuwa CHADEMA ni chama safi, na ni yeye huyo huyo anaibuka na mikakati mibovu kuibomoa.
Haihitaji mwekezaji kutoka nje ya Tanzania kuelewa kuwa Zitto anasaliti Watanzania katika safari ya ukombozi.
Kila mara Zitto anasema yupo pamoja na wanyonge na wanaoonewa.
Ifike mahali tujiulize, yupo pamoja nao lini? Yupo pamoja nao wapi? Yupo pamoja nao kwanini?
Na yupo pamoja nao yeye na nani? Na je, yupo pamoja nao kwa kujitegemea au anategemezwa?
Zitto yupo pamoja na Watanzania katika kukomboa nchi kwa kuwa yupo na Kafulila tu?
Watanzania wameipenda CHADEMA, Zitto ni shahidi kuwa siku alipoonyesha kutofautiana na Mbowe, siku walipopatana baada ya uchaguzi kuna mama mmoja pale Dar es Salaam alipowaona katika msafara alishuka katika gari lake la kifahari akibubujikwa machozi na kuwakumbatia huku akiwabariki na kuwatakia mema katika safari ya ukombozi.
Ilikuwa ni mojawapo ya ishara, kati ya ishara nyingi za Watanzania kuamini kuwa CHADEMA sasa ni mkombozi wao, wala hakuna anayesema mkombozi wao ni Freeman Mbowe, wala Arfi, wala Dk. Slaaa, wala Zitto Kabwe, wala Kafulila, wala Tundu Lissu.
Ila tumaini lao ni CHADEMA, maana CHADEMA bila Mbowe, Dk. Slaa, na wengine bado inawezekana na itaendelea kuwepo. Hii ni taasisi.
Wananchi wamewekeza katika sera nzuri za chama, hawajawekeza kwa watu moja moja. Watu wanapita, wanazeeka, wanafariki, wanajiondoa uanachama n.k. hivi ilikuwaje Zitto akawekeza akili zake kuwa mafanikio katika CHADEMA ni mpaka kafulila awe ofisa habari wa chama pale makao makuu, na kuwa akiondolewa inabidi yeye aandike barua ya kuacha madaraka yote, yakiwamo ya ubunge? Kama Zitto haamini haya, apite sasa katika maeneo alipokuwa maarufu anone kama hatazomewa.
Ifike mahali Zitto aache tabia ya uvuguvugu. Awaambie Watanzania anataka nini? Yupo pamoja nao katika safari ya ukombozi au amewaacha. Na kama amewaacha aeleze kwa nini anaacha wakati huu uchaguzi mkuu unapokaribia?
Ifike mahali Watanzania tujiulize, kijana huyu amegeukaje haraka hivi? Inawezekena hakuwa mpiganaji makini na mzalendo, au amenunuliwa na CCM, na kama hajanunuliwa basi anataka anunuliwe muda huu na CHADEMA kwa lengo la kuwalingishia wana CHADEMA umaarufu ambao wamempatia, kwa ushirikiano wao alipokuwa kabla na wakati akiwa mbunge ndani ya chama.
Hivi Zitto angeweza kufundisha mambo ambayo yeye mwenyewe hayasadiki? Kama hakuyasadiki kwa nini alifundisha? Ni mfano wa wachezaji fulani maarufu ambao wanaweza kuringa kucheza siku ya mechi kwa visingizio kibao ili wabembelezwe, wanunuliwe, na wapewe peremende na maji ili kuwaomba waingie uwanjani. Hawachezi kwa uzalendo, wanacheza kwa kuwa wamepewa pipi, hivyo siku tukikosa pipi hawatashirikiana nasi. Si wachezaji wa kutumainiwa.
Ilikuwaje Zitto ashindwe kuamini kuwa nguvu kazi ya vijana wenye ushirikiano ndani ya CHADEMA waliokuwa wakifanikisha kumpatia yeye ushindi katika mambo muhimu apeleke bungeni, ndio wale wale wanaofanikisha kutafuta mawasiliano kutoka kwa marafiki zake wanaoandaa njama za kuiangamiza CHADEMA kwa kuwa wamelipwa ili kuzorotesha nguvu ya ukombozi?
Zitto inafaa ajulikane sasa, kama ni wa moto au baridi, lakini vinginevyo kwa uvuguvugu alionao, si muda mrefu Watanzania watamtapika katika siasa za ukombozi.
Safari ya ukombozi ni ndefu, Watanzania wamechoka, na hawatahofia mawimbi yoyote, kwani ndiyo safari ya ngalawa yetu ya umma.
Umaskini wa Watanzania, na haja ya ukombozi wao vitakuhukumu. Tafakari chukua hatua, kama upo tayari kutudhulumu pesa ya kununulia sanda katikati ya msiba ili tukuelewe.
Tutakuelewa tu upo upande gani na kwa nini.
Wala haihitaji mwekezaji kujua kuwa ama umehongwa, ama unataka kuhongwa!
Ni dhambi gani kubwa unayotaka kuitaja kuwa ndiyo chanzo cha kupoteza uzalendo wako, ili uwaache Watanzania katika safari yao ya ukombozi?
Kusingizia kuacha siasa ni kutuambia kuwa ulichokuwa unakitafuta umekipata, na hauna haja tena na ukombozi wa Tanzania. Hata hivyo wanafalsafa tunakutakia kila jema katika maamuzi, na tunakuomba radhi kwa kukuambia ukweli. Maana ni heri ya ukweli unaouma kuliko uongo unaofurahisha. Tulaumiane katika ukweli, kuliko kupendana katika fedheha.