na Irene Mark
DAVID Kafulila, mwanachama mpya wa NCCR-Mageuzi, ambaye amekuwa akitumia uhusiano wake binafsi na Mbunge wa Kigoma Kaskazini, Kabwe Zitto, kama kete ya kisiasa katika ugomvi wake na uongozi wa Chama cha Demokrasia na Maendeleo (CHADEMA), amesema Zitto ni mzushi.
Kafulila, ambaye alikuwa Ofisa Habari wa CHADEMA kabla hajavuliwa cheo hicho na kukimbilia NCCR-Mageuzi, alisema hayo jana Dar es Salaam, wakati akijibu taarifa kuwa mbunge huyo amekanusha kumsaidia magari matatu ya kufanyia harakati za kujijenga kisiasa mkoani Kigoma baada ya kujiunga na NCCR-Mageuzi.
Msukumo wa Kafulila kumshutumu Zitto umetokana na tetesi kwamba amekuwa anatumia barua pepe ya mbunge huyo kusambaza taarifa zinazoleta chokochoko katika CHADEMA, kwa kuwa anajua neno siri la anuani ya barua pepe ya mbunge huyo ambaye amekuwa anamtumia kama msaidizi wake katika masuala mengi walipokuwa CHADEMA.
Taarifa hizo zilitokana na mawasiliano ya Zitto na watu walio karibu naye ambao juzi waliliambia gazeti hili wanachokiita ukweli wa madai ya mbunge huyo kumuunga mkono Kafulila katika harakati zake mpya akiwa NCCR-Mageuzi, kiasi cha kumpatia magari matatu kwa ajili ya kuzunguka maeneo kadhaa ya Jimbo la Kigoma Kusini katika siku chache zijazo.
Jana Kafulila aliiambia Tanzania Daima kuwa kama ni hivyo, Zitto ni mzushi, kwani hajawahi kumpa neno la siri la kufungua anuani ya barua pepe yake, wala hafahamu lolote kuhusu anuani hiyo.
Katika toleo la jana, gazeti hili lilkuwa na habari kuwa Zitto alimkana Kafulila, na kwamba mbunge huyo amekiandikia barua chama chake (CHADEMA) kukijulisha msimamo wake binafsi, kwa maelezo kuwa wanaomhusisha na kauli za Kafulila wana nia ya kumchonganisha (Zitto) na uongozi wa CHADEMA.
Kauli kama hii ilitolewa na Shida Salum, mama mzazi wa Zitto, katika mahojiano yake na gazeti la MwanaHALISI wiki mbili zilizopita, akisema mwanawe anatumiwa na watu wenye lengo la kuvuruga chama na kumgombanisha mwanawe na uongozi wa chama chao.
Katika kauli yake ya juzi, Zitto alinukuliwa akiwaeleza watu walio karibu naye kuwa hata taarifa zinazoandikwa na vyombo vya habari kuhusu yeye kumbeba Kafulila zinamnukuu bila kumhoji yeye.
Lakini jana Kafulila alisema: Huo ni uzushi unaotengenezwa
password (neno siri) ni kitu muhimu, tena ni siri ya mhusika, sasa iweje Zitto anipe password yake? Hayo ni maneno ya uzushi. Wakati huo huo, aliyevuliwa cheo cha Ofisa Mwandamizi wa Sera na Utafiti wa CHADEMA, Juju Danda, jana alitangaza rasmi kujiunga NCCR-Mageuzi kama Kafulila.
Nimefukuzwa bila kufuata sheria. Sijaridhishwa kabisa na maamuzi yale, ndiyo maana nikaona nitafute tumaini jingine ambalo ni NCCR-Mageuzi, alisema.