View attachment 3521148
Na. M. M. Mwanakijiji
Sijui ni 'genius' gani huyo ambaye ameanzisha hili la kuwa "tunataka amani kwanza". Kwa wiki hasa baada ya Oktoba 29 kumekuwa na jitihada kubwa ya kujaribu kugeuza mambo kinyumenyume. Sasa tunaambiwa "amani kwanza" ndio mambo ya "haki" yaje baadaye. Hili sijui limeanzaje na limeanzishwaje hadi kufikia watu wenye akili timamu wakaanza kulikumbatia.
Ninachoogopa ni kuwa tunatakiwa tuamini kabisa kuwa "utulivu, na kutokuwepo na vurugu" ndiyo "amani" yenyewe. Kwamba, wenzetu hawa wanatafsiri amani ni "hali ya utulivu, bila ugomvi, mabishano, mapigano, au kujibishana na watawala". Kwa wenzetu hawa "amani" kwao ni ile hali ya kuwa na utulivu. Yaani, Ukiwakuta watu wawili wanagombana ukiwaamulia basi umeleta "amani". Yaani, kama hawapigani basi "kuna utulivu". Kwa muda mrefu Watanzania tumeaminishwa kuwa nchi yetu ni "nchi ya amani" kwa maana ya kwamba hakuna "ugomvi, mapigano, vurugu n.k". Na kwa sababu hiyo tumeaminishwa kuwa lengo letu kama taifa ni kuwa katika hali ya utulivu.
Kwenye zizi la ng'ombe chui anaweza kuwa mhubiri mkubwa wa 'amani na utulivu'? Yaani, ukimuuliza chui atakuambia kwa kirefu ni kwanini ni muhimu kwa ng'ombe, mbuzi, na kondoo zizini kuwa katika hali ya utulivu ili kudumisha "umoja, na mshikamano" wa wanyama wote zizini. Kwenye mahojiano na Televisheni ya "Zizini TV" Bw. Chui alipoulizwa kwanini walitumia nguvu kubwa kuua wanyama zizini hasa walipoleta vurugu zizini Bw. Chui alisema kuwa hakuelewa kwanini wanyama wanadai haki zizini wakati wanapewa vyakula kila siku na maji ya kunywa na kuwa vurugu zizini ni kukosa shukrani!
Chui ana kila sababu ya msingi ya kutaka utulivu zizini. Bahati mbaya katika wanyama walioko zizini kuna wengine wanapenda kuwe na utulivu kwa sababu wanaamini wakifanya hivyo chui hatawageuza msosi wa jioni! Wale wenye kufurahia utawala wa chui wanaamini kabisa na watajaribu kuwashawishi wengine waamini kuwa ni bora kuwa na "amani" kuliko kuwa na 'haki'.
Sasa haki kwa maneno ya kawaida ni "kile ambacho mtu anastahili bila kudhulumiwa". Yaani, haki ni kila mtu anachodai kuwa ni mali yake iwe ni hadhi, maisha, ujira, utu n.k Vitu ambavyo mtu ni vya kwake na asidhulumiwe hivyo ndiyo haki yake. Msemo wa "mnyonge mnyongeni haki yake mpeni" una maana kubwa sana. Kwamba, hata kama mtu ni mnyonge lakini anachake anachostahili basi mpeni hata kama mmeshaamua kumnyonga!
Hakuna humu duniani watu wanaoitwa "wapigania amani" Dunia imetetewa na "wapigania uhuru" na 'wapigania haki". Hata hivyo wapo watu wanaosimamia "amani' lakini wanafanya hivyo kwa kupigania 'uhuru na haki' na si vinginevyo. Msemo wa wahenga kuwa "amani haiji ila kwa ncha ya upanga" una maana ya kuwa wakati mwingine ili kuwe na amani ni lazima dhulma iondolewe hata kama ni kwa vita. Ndiyo maana Vita ya Pili ya Dunia ilipiganwa ili kuleta amani Ulaya kwa kuondoa dhulma ya Manazi!
Kupinga dhulma na kutaka haki ni miongoni mwa matakwa makubwa ya dini zetu hizi. Ni kwa sababu hiyo tunaposikia watu wenye imani wanapuuzia "haki" na wanaishusha haki chini ati kwa kisingizio cha "amani" ni lazima tuwakatalie. Amani ni zao la haki na si vinginevyo. Unaweza ukawa na "amani" lakini kukawa na dhulma katika jamii lakini watu wanaimba "amani amani". Matukio ya hivi karibuni yanatudokeza kuwa hata sasa watu wanalalamikia 'dhulma" japo kunaonekana kuna "amani na utulivu".
Tusikubali kudanganyika kwa kulazimishwa kutulia ili tutawaliwe kwa kwa amani. Tukumbuke kuwa wakoloni walitaka kuwe na "amani na utulivu" katika makoloni yao ili watawale wapendavyo. Walipotokea watu kama kina Mandela, Nyerere, na wengine walionekana ni 'wavuruga amani' na walishtakiwa kwa kufanya "uchochezi'. Tanzania ya sasa chini ya CCM hii hii tumeanza kuona geresha hii kubwa ikirudiwa; tuwaache watawale wapendavyo ili tuwe na "amani'. Tusiwapinge, tusiwakatalie, na tusiwaonyeshee mikono. Na jambo kubwa ambalo hawataki tulifanye ni kuwafanya wengine wawachukie na wawakatae.
Lakini kama nilivyosema mbuzi, kondoo na ng'ombe ambao kila siku wanaona wenzao wanaenda kutolewa msosi, wanakamatwa, wanaenda kuchinjwa wana haki ya kugoma, kuhoji, na kupinga? Au kwa vile zizini kunaakiwa kuwe na amani wakubali tu wakae kimya ili kuwe na amani? Au ndiyo yale yaliyoandikwa kwenye kitabu cha "Animal Farm"?
Haki ndiyo msingi wa amani na si kinyume chake. Hakuna AMANI BILA HAKI. Hakuna Amani mahali penye "dhulma".
Kama Quran inavyosema katika Sura 4:135 Enyi mlio amini! Kuweni wenye kusimamisha uadilifu (haki), mtowao ushahidi kwa ajili ya Mwenyezi Mungu, ijapo kuwa ni juu ya nafsi zenu, au wazazi wawili na jamaa zenu. Akiwa tajiri au masikini Mwenyezi Mungu anawastahikia zaidi. Basi msifuate matamanio, mkaacha kufanya uadilifu(haki). Na mkiupotoa au mkajitenga nao basi Mwenyezi Mungu anajua vyema mnayo yatenda
Ni wito huo tunaona kwenye Isaya 1:17 jifunzeni kutenda mema! Tafuteni haki, watieni moyo walioonewa.
Teteeni shauri la yatima, wateteeni wajane.
Amani haiwezi kusimama penye dhulma; na dhulma ni kukosekana kwa haki. Lakini tukimuuliza chui atatuambia "ni lazima kuwe na amani kwanza kabla sijawapa haki yenu". Na wapo watakaokubali na kukumbatia hili. Wengine bado watakataa.