Siasa za vitisho
na Charles Mullinda (Tanzania Daima)
UPEPO wa kisiasa ndani ya Chama Cha Mapinduzi (CCM), unazidi kuchafuka baada ya kusambaa kwa tetesi kuwa Spika wa Bunge, Samuel Sitta, pamoja na wabunge kadhaa wa chama hicho wanaodaiwa kuwa wanamuunga mkono katika kupambana na ufisadi serikalini, kutishiwa kuuawa kwa sumu kali.
Habari zinazodai kuwepo kwa mpango madhubuti wa kumuua Spika Sitta na baadhi ya wabunge zilianza kusambazwa mapema wiki iliyopita katika mitandao ya intaneti na kupitia ujumbe mfupi wa simu za mikononi.
Jumatano wiki hii, habari hizo ziliripotiwa kwa mara ya kwanza na gazeti moja linalochapishwa mara moja kwa wiki, likiwa limemkariri Sitta akieleza kuwa taarifa hizo zimekwisha kumfikia na amekwishatoa taarifa polisi.
Ujumbe huo unaodai kuwa Sitta anawindwa kuuawa, unawataja vigogo wa chama hicho, wakiwemo baadhi ambao walijiuzulu nyadhifa zao mapema mwaka huu.
Akizungumza jana na Tanzania Daima Jumapili kupitia simu yake ya kiganjani, Spika Sitta alisema ujumbe wa kuwapo mpango wa kumuua umekwisha kumfikia na ametoa taarifa polisi ili iwapo atadhurika, polisi wawe na taarifa ya hali halisi ya matukio yaliyokuwa yakimuandama.
Katika hali ya kawaida, naona kama ni upuuzi, lakini si vizuri kupuuza mambo kama haya. Sasa yanaonekana kwa vile yanaandikwa, lakini vinginevyo
inawezekana ni kunitisha ili niache harakati za kupambana na ufisadi uliotanda kila mahali nchini mwetu, lakini hata kama ni kunitisha, sheria zinasema ni lazima utoe taarifa, na ndicho nilichofanya.
Taarifa nilizopeleka polisi ni mbili. Ya kwanza ni ile inayohusu vitisho vya kuuawa dhidi yangu na Dk. Mwakyembe, na ya pili ni ile inayowajumuisha pia katika mpango huo wa kuuawa kina Anne Kilango, Reginald Mengi, Mbunge wa Mbozi na wenzetu wengine kadhaa.
Lakini hata kama tukiuawa, sidhani kama itasaidia kumaliza vita dhidi ya ufisadi. Binafsi ninaumia kwa sababu ninawindwa kila mahali, nyumbani hadi jimboni kwangu, nina sms za matusi zinazowatukana pia mke na watoto wangu ambazo ni za kusikitisha sana.
Jimboni kwangu nako tayari kuna mabilioni ya fedha yamepelekwa, ili kuniangusha katika uchaguzi mkuu ujao, basi tu
wanatumia kila mbinu kutukatisha tamaa. Lakini naamini hawatafanikiwa, alisema Spika Sitta.
Sitta alisema ameamua kusimamia mapambano ya rushwa bungeni kwa sababu hakuna nchi maskini duniani iliyopata mafanikio ya uchumi bila kupiga vita rushwa, akibainisha kuwa Tanzania sasa ina bidhaa feki asilimia 40, jambo ambalo ni moja ya misingi ya nchi kutopata maendeleo.
Alisema yeye na baadhi ya wabunge wameshindwa kuendelea kuangalia jinsi uchumi wa taifa unavyovuja, lakini wapo baadhi wanaochukizwa na hali hiyo, ambao wanatumia kila mbinu kuhakikisha kuwa hawafanikiwi katika azima yao ya kuhakikisha uchumi wa Tanzania unasimama.
Akieleza kusikitishwa kwake na mikataba mingi ambayo taifa linaingia na wawekezaji, alisema mikataba mingi aliyoiona ilimsikitisha, licha ya kuandaliwa na wataalamu waliobobea, kwa sababu ina upungufu ambao unaligharimu taifa, na kwamba katika hali ya kawaida haipaswi kuachwa ikaendelea kutumika.
Kuna mambo yanasikitisha kweli, katika baadhi ya mikataba ambayo taifa limeingia na baadhi ya wawekezaji, mingi ni mibovu, ukiisoma utashangaa, hata mtu wa kawaida akisoma mkataba wa aina hiyo lazima atajiuliza, huyu kiongozi aliyeingia mkataba huu na mwekezaji ni wa aina gani? Sasa wapo wenzetu ambao hawataki mikataba hii irekebishwe.
Tumeamua kulipigania taifa letu, hivyo kuandamwa hakutakwisha, kwa baadhi ya hawa wanaotuandama hawawezi kubadilika, hivyo ni lazima watuandame. Na sisi tutazidisha mapambano, alisema Sitta kwa sauti thabiti.
Akieleza zaidi kuhusu taarifa alizozipata zinazolenga kumwangusha kisiasa, alisema baadhi ya wanasiasa, bila kuwataja majina, lakini akisema wanatokea ndani ya chama chake, wamepeleka mabilioni ya fedha jimboni kwa ajili ya kuwahonga wapiga kura wake, ili wamkatae kuwa mbunge wao katika uchaguzi mkuu ujao.
Alisema taarifa za uhakika alizonazo zinaeleza kuwa yeye pamoja na wabunge 23 wa CCM ambao wamekuwa mstari wa mbele katika kupambana na ufisadi serikalini, mipango imeandaliwa ili kuhakikisha hawarudi bungeni, jambo aliloeleza kuwa baada ya muda litabainika kwa kila Mtanzania.
Mmoja wa viongozi aliyejiuzulu miezi kadhaa iliyopita, ambaye anatajwa katika ujumbe unaosambazwa sasa kuwa mmoja wa vigogo waliosuka mpango wa kuwaangamiza wanasiasa wanaoonekana kumuandama, alipoulizwa na gazeti hili kupitia simu ya kiganjani kuhusu yeye kuhusishwa na njama hizo, alikataa kuzungumza lolote.
Sina taarifa hizo, sitaki
sitaki ku-comment chochote kuhusu jambo hili, samahani sana, naomba uniache, kwaheri, alisema kisha akakata simu.
Msemaji wa Jeshi la Polisi nchini, Abdallah Msika, alipoulizwa kama Jeshi la Polisi limekwisha kuanza kufuatilia kuhusu ukweli wa taarifa hizo, hasa baada ya Spika Sitta kutoa taarifa za vitisho kwa jeshi hilo, alisema hana taarifa za kiongozi huyo kutishwa.
Sina taarifa hizo, labda kama aliripoti Polisi Kanda Maalumu ya Dar es Salaam, lakini mimi sina taarifa. Nashukuru kusikia taarifa hizo, ngoja sasa nianze kufuatilia, alisema Msika.
Jitihada za kuwapata vigogo wengine wanaodaiwa kuhusika katika mtandao huo wa kuwaangamiza baadhi ya wanasiasa na wale wanaodaiwa kulengwa kuangamizwa hazikufanikiwa hadi tunakwenda mitamboni.
Taarifa ya kuwepo mpango wa kumuangamiza Spika na baadhi ya wabunge zinaeleza kuwa walengwa watakuwa wakiuawa kwa sumu kali ambayo watakuwa wakipakwa na mtu aliyevaa glovu yenye sumu, ambaye atakuwa akimgusa mlengwa aliyemkusudia kumuua.
Inadaiwa kuwa sumu hiyo hatari imeingizwa nchini na mmoja wa viongozi wa kisiasa ndani ya chama tawala kutoka moja ya mataifa ya Kiarabu.