Na Leon Bahati, Dodoma (Mwananchi)
SERIKALI imetoa msimamo wake kwamba, Tanzania haitaunda Mahakama ya Kadhi na badala yake itatafsiri sheria za Kiislamu na kuzijumuisha kwenye sheria za nchi, ili zitumike kwenye mahakama za kawaida hapa nchini.
Uamuzi huo wa serikali unatokana na mapendekezo yaliyowasilishwa kwa Mwanasheria Mkuu wa Serikali na Tume ya wataalamu waliochambua mapendekezo ya utafiti uliofanywa na Kamati ya Kurekebisha Sheria.
Hata hivyo, uamuzi huo wa serikali ulipingwa vikali na Mbunge wa Kigoma Kusini, Manju Msambya (CCM), ambaye alisisitiza kuwa haoni kosa kwa Waislamu kuundiwa mahakama hiyo.
Msimamo wa serikali ulitolewa bungeni jana na Waziri wa Katiba na Sheria, Mathias Chikawe wakati akiwasilisha makadirio na matumizi ya wizara yake kwa mwaka wa fedha 2009/10.
Hata hivyo, Chikawe alisema mchakato wa kufikia hatua ya kuzijumuisha sheria hizo za Kiislamu kwenye sheria za nchi lazima upate maoni kutoka kwa madhehebu yote ya Kiislamu nchini.
''Hivi sasa Ofisi ya Mwanasheria Mkuu wa Serikali imeanzisha mchakato wa kukusanya mawazo na maoni kutoka kwa viongozi wa madhehebu yote ya dini ya Kiislamu kwa nia ya kuorodhesha misingi ya dini ya Kiislamu, hususan ile inayohusu sheria binafsi kwa madhumuni ya kuihuisha misingi hiyo katika sheria za nchi, kwa kuzingatia sheria ya The Islamic Law Act, sura ya 375 ya mwaka 1964,'' alifafanua Chikawe na kuongeza:
''Kimsingi baada ya viongozi hawa wa dini kukubaliana kuhusu misingi hii, basi Waziri wa Sheria atatoa tamko kuhusu misingi hiyo na baada ya hapo kwa mujibu wa Ibara ya tatu ya sheria hii, matamko haya yatakuwa ni sheria zitakzotambuliwa na mahakama zetu zote hapa nchini.''
Alisema lengo la serikali la kutumia mfumo huo ni kuweka utaratibu utakaolinda haki za waumini wa Kiislamu bila kuathiri misingi ya Katiba ya nchi.
Chikawe alisema utaratibu kama huo umekuwa ukitumika nchini Afrika Kusini ambako kuna waumini wengi wa Kiislamu na imeonyesha mafanikio.
Akichangia hotuba hiyo, Msambya alipinga utaratibu huo wa serikali na kutaka serikali iunde moja kwa moja mahakama za kadhi ili kutatua matatizo yahusuyo waumini wa Kiislamu.
Vilevile, Msambya alitaka Tanzania ijiunge na Jumuiya ya Uislamu Duniani (OIC), kwa kile alichoeleza, nchi itafaidika kwa mambo mengi kama ilivyo Uganda na Msumbiji.
Katika hatua nyingine, Msambya alilishutumu Kanisa Katoliki nchini kwa kutoa waraka ambao unawafundisha waumini wake kuhusu namna ya kuchagua viongozi bora.
Waraka huo wa Kanisa Katoliki ulikuwa unawaasa waumini wake wasiwachague viongozi ambao wana tabia ya kubadilika badilika kama kinyonga.
Msambya ambaye hakutaja moja kwa moja dhehebu la dini lililotoa waraka, alisema unapingana na kanuni kwamba watu wasichanganye dini na siasa.
Akizungumza kwa jazba, Msambya alisema alichukizwa na kitendo cha waziri ambaye hakumtaja, kwamba alipoulizwa na waandishi wa habari kuhusiana na waraka huo, aliusifu akisema ni mzuri kwa sababu ni moja ya elimu ya kupiga kura.
Hoja ya kuwepo kwa Mahakama ya Kadhi ilianzishwa wakati wa serikali ya awamu ya tatu lakini ilizimwa, kisha ikafufuliwa tena miaka mitatu iliyopita na kuwagawa wanasiasa na wananchi katika makundi mawili. Wako waliounga mkono na wengine waliipinga kwa maelezo kwamba itasababisha vurugu na mgawanyiko katika jamii.
Maswali:
- Kwa kuingiza baadhi ya sheria za dini ya Kiislamu katika sheria za nchi kunaondoa haja ya kuwepo mahakama ya kadhi? Yaani, mahakama za kawaida zitumikee kufanya kazi ya mahakama za Kadhi?
- Je, mahakama za kawaida za nchi zinapotoa hukumu kwa mujibu wa kufuata sheria za Kiislamu je Muislamu analazimika kutii hukumu hizo kana kwamba ni za mahakama ya kidini?
- Je adhabu zitakazotolewa kwa mtu anayevunja sheria hizo mpya zitaendana na adhabu zinazotolewa kama ingekuwa ni mahakama ya Kiislamu?
- Kwa vile sheria hizo zitaingizwa kwenye sheria za kawaida za nchi, je zitawahusu vipi wananchi wengine? Kama zitawekwa kwa ajili ya waislamu tu je hicho si kinyume na Katiba ambapo mamlaka ya nchi inapitisha sheria za kibaguzi (moja za wananchi wote na nyingine za waislamu tu)?
- Kwanini serikali isiamue kuweka mazingira ambapo Mahakama ya Kadhi inaundwa na Waislamu wenyewe kwa misingi ambayo wao wanaikubali na pale ambapo kunahitajika msaada wa serikali basi ijulikane ni kwa vipi na kwa namna gani?