Kwa mtu anayefuatilia kitimu timu cha kashfa ya Richmond, hakuna shaka kuwa ameishaona kuwa dalili zote zinaielekea serikali ya Jakaya Kikwete maarufu kama kasi mpya, nguvu na ari mpya.
Hakuna ubishi kuwa sasa kasi mpya,nguvu mpya na ari mpya tuliyoahidiwa haina maana nyingine bali kuelekea kuzimu. Pia hakuna shaka kuwa kwa taarifa iliyotoka mwezi jana kwenye gazeti la Rai linalomilkiwa na mshirika mkuu wa Kikwete na Lowassa, mbunge wa Igunga, Rostam Aziz, inaonyesha wazi Lowassa alivyo Richmond yenyewe.
Nilisoma makala moja kwenye gazeti la Tanzania Daima ambalo kwa sasa limekuwa adui namba moja ya ujambazi unaoendeshwa nchini mwetu. Makala ya mtu ajiitayo Mpayukaji, ilinivutia kuandika makala hii pamoja na kukaa kimya kwa muda mrefu.
Huyu Bwana ni mpayukaji kweli kweli. Yeye na Mbowe wamesababisha serikali ilione gazeti la Tanzania Daima mwiba kama ilivyokuwa mwaka jana kwa Habari Tanzania.
Sasa tukirejea kwenye taarifa ya kwenye gazeti B la CCM la Rai, kuna maswali yanajitokeza. Kwa mfano, ofisi ya waziri mkuu ilitoa tangazo la kupotosha kuwa kwa vile suala la Richmond liko mikononi mwa TAKURU haliwezi kujadiliwa na bunge. Kwanza ni mpumbavu gani anaweza kuiheshimu na kuiamini TAKURU ambayo inasifika kwa kuwasaka vidagaa wa rushwa huku ikiwakingia kifua mipapa?
Rejea kisa cha Mchungaji Christopher Mtikila alipomtuhumu waziri mkuu wa zamani Fredrick Sumaye kuwa ni mla rushwa nambari wani nchini.
Badala ya TAKURU kumhoji Sumaye ilimhoji Mtikila. Pia ukiachana na hilo ukaangalia wafanyakazi wa TAKURU, wana kila dalili za kuwa walarushwa sawa na waliwaajiri.
Hiyo tisa. Kumi ni pale ilipotoka barua nyingine toka kwa Waziri Mkuu kwenda kwa waziri wa zamani wa nishati Ibrahim Msabaha eti ikionyesha kuwa waziri mkuu, Lowassa alikuwa akimuonya Msabaha kuwa makini na dili la Richmond.
Ni utoto na kutapatapa kiasi gani! Kama waziri mkuu Lowassa kama anavyotaka tumuone mkweli, anashindwa nini kuonyesha nia hiyo ya kumtahadhalisha Msabaha ambapo imeishajulikana kuwa Richmond ni bomu na rushwa tupu? Je kwanini serikali inahangaikia Richmond hata kuliko wajibu wake mwingine? Inachoficha ni nini?
Hawa watawala majambazi wanataka kutufanya sisi mafala. Hawajui kuwa licha ya kuleta Richmond ambayo kimsingi haina lolote la maana zaidi ya kuwa uchochoro wa akina Lowassa kuibia pesa zetu, tunajua kuwa hata wakati wa mgao wa umeme mtoto wa Lowassa aliagiza majenereta toka Uchina akayapitisha bandarini bila kulipia ushuru na kuwalangua watanzania.
Pia hakuna ubishi kuwa jinsi bunge letu chovu la CCM na upinzani dhaifu ambao nao unaonekana kuanza kunogewa mashangingi,serikali imekuwa ikitoa majibu yenye mashaka na kuonyesha kuishiwa.
Akijibu swali la Mbunge wa Bububu, Cosmas Masolwa, waziri mdogo wa Uchumi, Mipango na Uwezeshaji, Gaudence Kayombo, kwa hila na jeuri alilidanganya bunge kuwa halina mamlaka kisheria kuangalia mikataba inayoingiwa na serikali.
Hii ni baada ya Masolwa alipotaka wabunge waletewe mikataba waangalie kulikoni.
Mwongo huyu anayeonekana kihiyo na chitalilo eti alisingizia dhana ya mgawanyo wa mamlaka (Separation of Powers).!
Dhana hii ilianzishwa ili kuzifanya nguzo tatu za dola yaani Utawala,Bunge na Mahakama kukaguana na kuheshimiana kimamlaka bila mmoja kumtumikisha mwenzake,kumdharau au kumuingilia. Hakuna anayeruhusiwa kujiona bora kuliko mwenzake wala mmoja kufanya kazi ya mwenzake.
Lakini chini ya utawala wa sheria ambao ndiyo mzizi wa dhana hii lazima vyombo hivi vitatu vikaguane.
Kwa ufupi ukiangalia waziri mdogo alivyojibu,unajua kabisa kuwa alitumwa na bosi wake.
Sasa Lowassa anaingiaje? Kwa taarifa za magazeti mengi ya Tanzania,kuna kila dalili kuwa kama Richmond si Lowassa ni Kikwete au wote. Kwa sababu jinsi wananchi walivyoshupalia uchafu huu, hakuna shaka wawili hawa wasingekuwa na ubia kwenye kampuni hili wangekuwa wameishachukua hatua.
Hapa ndipo maneno ya Baba wa taifa alipoonya kumtahadhali Lowassa yanatimia.
Hapa ndipo kukataliwa kwa Kikwete na Mwalimu kunaanza kuonyesha maana yake.
Hakuna ubishi kuwa Kikwete ameanza kuwa bomu kuliko hata Benjamin Mkapa ambaye wameunda urafiki wa kulindana na kufichiana madhambi. Rejea magazeti kutaka Mkapa ajieleze kuhusu dili la rada.
Kikwete akiwa Stokhlom alimkingia kifua kuwa Mkapa aachwe. Hiyo tisa. Sasa limefumka bomu la TANESCO. Nalo nyuma yake kuna Mkapa maana kwa wanaokumbuka Net Solution iliyoletwa na shemeji zake ilivyokingiwa kifua naye hawana wasi wasi kuwa alikuwa nyuma ya wizi huu.
Je tutakapomtaka Mkapa kwa mara ya pili atueleze ukweli, Jakaya ataruka na kusema tusimguse?
Kinachoendelea ni kuondoka kibaka mmoja na kuingia kibaka mwingine. Hapa ndipo hata siri ya mawaziri wezi na wachafu walioingia mikataba ya wizi kuteuliwa inapofichuka. Kimsingi kinachoendelea ni kiini macho kinachofanywa na bwana mazingaombwe wale wale.
Tuhitimishe. Jakaya na Lowassa hawawezi kuikomboa nchi yetu. Badala yake wanaizamisha kwenye Richmond na mambo mengine yatakayoibuka baadaye.
Leo uchumi wetu unaanza kuporomoka utadhani unaharisha. Matumizi yasiyo na nidhamu ndiyo hayo yamekuwa fasheni.
Rushwa inazidi kuongezeka. Au ndiyo kurejesha pesa walizotumia kwenye takrima.
Nchi yetu kwa sasa imevamiwa na genge sawa na lile la Marekani ambapo George Bush anaendeshwa na Dick Cheney nyuma ya pazia kama ambavyo Kikwete naye anaendeshwa na Lowassa na Mkapa nyuma ya pazi. Ni hatari kuwa na rais katuni.
Swali la leo. Je Lowassa na Rostam Aziz waliomfaidi Jakaya ndiyo wanaipiga mnada nchi yetu kurejesha takrima waliyowahonga wapiga kura wetu. Yangu macho.
Msisitizo. Kama Richmond siyo Lowassa basi ni Kikwete au Rostam Aziz au tuseme ndiyo utatu mtakakitu? Nuru tuliyoambiwa kumbe siyo bali kiza!
Kama Malecela, laana ya Mwalimu Nyerere na imtafune Lowassa milele na milele.
Source: HabariTanzania.com
http://www.habaritanzania.com/articles/3558/1