Nimetaarifiwa na ndugu yangu wa huko Gongolamboto ambaye anasema ameshuhudia mabomu mengi yakipita juu ya nyumba yake. Moja lilipiga nyumba ya jirani yake na kusambaratisha kabisa, bahati nzuri walikuwa wamekwishakimbia. Mabaki ya bomu hilo yamechukuliwa asubuhi. Bomu moja kubwa lilipiga sehemu ya nyumba yake na kwenda kuanguka kwenye choo chake cha nje, hilo halikulipuka. Askari wamekuja mara mbili asubuhi hii lakini wameshindwa kulichukua maana ni kubwa sana, na halijalipuka.
Familia yake yote ilitawanyika usiku, ni yeye pekee yake alibaki hapo nyumbani, akisali usiku kucha. Mmoja wa wanafamilia alikuwa mgonjwa, alikutwa na wasamaria wema njiani akijikongoja wakamsafirisha kwa ndugu zetu huko Mikocheni. MMoja wa wanafamilia kabla ya kukimbia alikuwa ameumia mkono lakini haukukatika. Namshukuru Mungu kwa kuwanusuru, na ninawapa pole sana wale waliopoteza ndugu, kuumia na kuharibiwa mali na nyumba zao.