Bunge lashtukia Dowans
na Edward Kinabo
KAMATI ya Kudumu ya Nishati na Madini ya Bunge la Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, imefichua siri ya serikali kuanza mchakato wa kununua mitambo chakavu ya kuzalisha umeme kutoka kwenye Kampuni ya Dowans, kwa gharama ya sh bilioni 70.
Kutokana na kugundua nia hiyo ya serikali, kamati hiyo imekataa kuunga mkono uamuzi huo kwa kuwa utakiuka utekelezaji wa maazimio yaliyopitishwa na Bunge Februari 2008, kuhusu Kampuni ya Richmond na Dowans.
Akizungumza kwenye mkutano na waandishi wa habari jana katika ofisi ndogo za Bunge jijini Dar es Salaam, Mwenyekiti wa kamati hiyo, William Shellukindo, alisema juzi Desemba 14, 2008, Waziri wa Nishati na Madini, William Ngeleja, aliitisha kikao cha dharura na kamati hiyo, kwa lengo la kutoa taarifa ya hali ya dharura kuhusu tatizo la umeme nchini.
Shellukindo ambaye pia ni Mbunge wa Bumbuli, alisema Ngeleja alitoa maelezo juu ya uamuzi wa serikali kushiriki zabuni ya ununuzi wa mitambo ya Kampuni ya Dowans ili kukabiliana na changamoto ya upungufu wa megawati 10 za umeme, na kuomba kamati hiyo ibariki uamuzi huo.
Akiwa na mjumbe mmoja wa kamati hiyo, Chritopher ole Sendeka (Mbunge wa Simanjiro), Shellukindo alisema kamati yake imeshtushwa kupewa taarifa hiyo ikiwa ni siku mbili tu kabla ya zabuni hiyo kufungwa, Desemba 16, 2008.
"Kamati imeshtushwa kupewa taarifa ya maamuzi mazito ya serikali kama hayo ya kushiriki zabuni ya ununuzi wa mitambo ya Dowans siku ya Jumapili Desemba 14, 2008, ikiwa ni siku mbili tu kabla ya zabuni hiyo kufungwa (Desemba 16, 2008)," alisema Shellukindo.
Alisema kamati hiyo ilipata taarifa juu ya ununuzi wa mitambo ya Dowans mwanzoni mwa Oktoba 2008, ilipotembelea TANESCO lakini taarifa hiyo ilikanushwa na TANESCO.
"Kamati inashangazwa kuona suala hili la ununuzi wa mitambo ya Dowans likiibuka tena baada ya kamati kumshauri Waziri wa Nishati na Madini Novemba 7, 2008 mjini Dodoma, kuwa hatua yoyote ya kununua mitambo hiyo itakuwa batili na inakiuka maamuzi ya Bunge," alisema Shellukindo.
Alitoa msimamo kuwa, kamati yake haitapenda kujihusisha na uamuzi huo wa serikali kwani unavunja kanuni ya 53 (8) na 54 (4) za kanuni za kudumu za Bunge (toleo la 2007), ambazo zote zinakataza kurudiwa kwa mjadala wa jambo ambalo tayari lilishatolewa uamuzi na Bunge.
Alisisitiza kuwa, kamati yake haiwezi kubariki uamuzi huo wa serikali kwani kufanya hivyo ni kwenda kinyume cha Bunge ambalo lilishaagiza mkataba kati ya Richmond na serikali ambayo ilirithiwa na Dowans uvunjwe.
Alipoulizwa kamati yake itafanya nini ikiwa serikali bado itaendelea na azima ya kununua mitambo hiyo ya Dowans alisema: "Wakifanya hivyo tutakutana bungeni."
Alipoulizwa iwapo serikali ilikuwa haijui kama ni makosa kununua mitambo hiyo alisema:
"Kusema hawajui si sawa, wana kumbukumbu zote. Wana ripoti zote, ile ya Richmond na maazimio ya Bunge ambayo Waziri Mkuu alikuja akatueleza utekelezaji wa awali wa maamuzi hayo. Wakati mwingine unaweza kuficha utendaji mbovu kwa kufanya kila kitu kionekana kama kinatokea kwa dharura. Walikuwa wapi tangu Januari wasitafute njia nyingine mbadala?" alihoji Shellukindo.
Aliishauri serikali kuendelea kutafuta namna bora ya kushughulikia dharura hiyo ya umeme kwa mujibu wa sheria zilizopo ili kuiepusha nchi na maamuzi ya zimamoto ambayo uzoefu unaonyesha huliingizia taifa hasara kubwa kama ilivyoelezwa kwenye azimio namba 19 la kamati teule ya Mwakyembe.
"Kwa mfano sisi tuliwaambia kama mnataka megawati 10, tuna IPTL. IPTL inazalisha megawati 100. Wakatuambia kuna kesi mahakamani, nasi tukawaambia serikali iombe kibali mahakamani cha kutumia IPTL, kutokana na hiyo dharura wanayosema imetokea," alisema Shellukindo.
Aliikumbusha serikali kutekeleza maazimio yaliyopitishwa na Bunge Februari 2008 kuhusu Richmond na Dowans kama alivyoahidi Waziri Mkuu, Mizengo Pinda, kwenye hotuba yake ya utekelezaji wa awali wa maazimio ya Bunge ya Agosti 28, 2008, hasa azimio namba 18 lililotaka wamiliki wa Richmond Development Company LLC na Richmond Development Company (T) Ltd, wafunguliwe kesi ya jinai mara moja kwa udanganyifu na ujanja wa kuiibia serikali.
"Kwa kuwa suala hili bado linashughulikiwa na serikali na hatujui hatima na mipaka ya utekelezaji wake katika mahusiano ya Richmond na Dowans; kamati bado inaendelea na msimamo wake iliyokupatia waziri Novemba 7, 2008.
"Hali hii inaweza kusababisha mgongano mkubwa kati ya serikali na Bunge linalowakilisha wananchi na hivyo kuwafanya wananchi kukosa imani na serikali yao," ilisema taarifa ya maoni ya kamati hiyo kwenda kwa Waziri wa Nishati na Madini.
Naye mjumbe wa kamati hiyo, Ole Sendeka, alisema uamuzi huo wa serikali pia unakwenda kinyume cha Sheria ya Manunuzi ya Umma ambayo hairuhusu serikali kununua mitambo chakavu na kusisitiza kuwa mitambo ambayo serikali imeamua kuinunua ni chakavu.
Uamuzi huo wa Wizara ya Nishati na Madini wa kushiriki kwenye zabuni ya ununuzi wa mitambo chakavu ya Kampuni ya Dowans, umefichuka siku chache tu tangu Rais Jakaya Kikwete, awasifie Waziri wa wizara hiyo, William Ngeleja na Naibu wake, Adam Malima, kwa kazi nzuri wanayofanya kwenye wizara hiyo.