Kundustan mpo?
JENGO LA ABIRIA UWANJA WA NDEGE SONGEA LAZINDULIWA
Waziri wa Uchukuzi, Profesa Makame Mnyaa Mbarawa, leo Julai 10, 2026, amezindua rasmi jengo jipya la abiria katika Uwanja wa Ndege wa Songea. Mradi ambao umegharimu shilingi milioni 842 na umekamilika kwa asilimia 100, ukiwa na uwezo wa kuhudumia abiria 300 kwa wakati mmoja.
Akizungumza katika uzinduzi huo, Prof. Mbarawa amesema serikali inaendelea kuboresha viwanja vya ndege nchini ili kuendana na ongezeko la mahitaji ya usafiri wa anga kote nchini.
Amesisitiza kuwa kiwanja hiko ni mali ya Watanzania wote, hivyo ni wajibu wa wananchi kukilinda na kuhakikisha miundombinu yake inalindwa dhidi ya vitendo vinavyoweza kuhatarisha usalama wa huduma.
Prof. Mbarawa ametoa wito kwa mashirika ya ndege kutumia kikamilifu fursa ya uwanja wa Songea, ili kuongeza safari za ndege mkoani Ruvuma.
Kwa upande wake, Mkuu wa Mkoa wa Ruvuma, Brigedia Jenerali Ahmed Abbas Ahmed, ameiomba serikali kupitia Waziri wa Uchukuzi kujenga jengo lingine la kisasa zaidi katika Uwanja huo. Amesema hatua hiyo ni muhimu itakayosaidia kuendana na kasi ya ukuaji wa sekta ya usafiri wa anga na mahitaji ya wananchi wa mkoa huo.
Amesisitiza kuwa jengo lililozinduliwa litumike kwa muda pekee, huku serikali ikiendeleza maandalizi ya ujenzi wa jengo jipya la kudumu, litakaloongeza uwezo wa kiwanja na kuchochea maendeleo ya kiuchumi katika Ruvuma.