Kigogo anaswa na PCB
2007-05-01 17:33:00
Na Janneth Kiure, Kibaha
Kigogo mmoja wa Serikali mkoani Pwani amejikuta akinaswa juujuu na askari wa Kikosi cha Kuzuia Rushwa nchini, PCB baada ya kudaiwa akipokea mlungula wa maelfu kibao ya pesa za Kibongo.
Kigogo huyo aliyekumbwa na zali baya na linaloweza kumharibia kila kitu kazini kwake, ni Lucius Mulokozi, Ofisa wa Mifugo wa Kituo cha Kwala mkoani Pwani.
Anadaiwa kigogo huyo kuwa amebambwa `laivu` katika baa moja maarufu pale Mlandizi mkoani Pwani, akipokea mlungula wa Sh.600,000 kutoka kwa mfanyabiashara wa ng`ombe.
Hatahivyo, soo la ofisa huyo limeshatua kortini ambapo hivi karibuni, liliunguruma pale kwenye Mahakama ya Wilaya ya Kibaha.
Ikadaiwa mbele ya Hakimu Victoria Nongwa wa korti ya wilaya kuwa Ofisa huyo wa Mifugo, amepokea rushwa kutoka kwa mfanyabiashara mmoja wa ng`ombe.
Akisoma hati ya Mashtaka, Mwendesha mashtaka wa PCB mkoani Pwani, Thuwaiba, alidai kuwa mnamo Aprili 8 mwaka huu, mshtakiwa alidai na kupokea pesa hizo za rushwa kutoka kwa mfanyabiashara Abdallah Hemed, kupitia kwa mwenzake aitwaye Lukumano Mulungu.
``Mheshimiwa hakimu... nia yao ilikuwa awarudishie ng`ombe zaidi ya 200, aliokuwa amewafukuza katika kituo cha Kwala kilichopo chini ya Wizara ya Mifugo,`` akadai Mwendesha Mashtaka huyo.
Hati ya mashtaka ikaendelea kudai kuwa, katika baa moja maarufu pale Mlandizi, mshtakiwa alipokea rushwa bila kujua kuwa maafisa wa PCB walikuwa tayari wamemuwekea mtego maalumu na hatimaye kufanikiwa kumnasa.
Ikadaiwa kuwa mtuhumiwa aliomba pesa hizo kutoka kwa mfanyabiashara Hemed ili amrudishie ng`ombe wake katika kituo cha Kwala ambacho ng`ombe huhifadhiwa kwa muda kwa ajili ya chanjo kabla ya kupelekwa Jijini Dar es Salam kwa kuchinjwa.
Hata hivyo, ilidaiwa kuwa mtuhumiwa alifukuza ng`ombe hao akiwa na vijana wa mfanyabiashara Hemed na kutaka kiasi hicho cha fedha ndipo awarudishe kituoni hapo.
Mshtakiwa amekana shtaka lake kwa nguvu zote, hadi Mei 8, mwaka huu na kuswekwa lupango baada ya kukosa wadhamini.
SOURCE: Alasiri