TAZAMA TANZANIA TOLEO Na. 356 JUMANNE SEPTEMBA 8-15, 2009
DK. MWAKYEMBE AANDAMWA NA MAFISADI
Na mwandishi wetu- KYELA.
Nguvu ya kisiasa ya Mbunge wa Kyela wa chama cha mapinduzi (CCM) Dk. Harrison Mwakyembe ameanza kupungua baada kubainika kuwa tukio la kutaka kumchoma kisu mbunge huyo ni la kupangwa.
Uchunguzi uliofanywa na gazeti hili, umebaini kuwa Dk. Mwakyembe na washirika wake, wameonekana kujiandalia tukio hilo ili ionekane kuwa mbunge huyo anaandamwa na mafisadi hewa;
Baadhi ya watu waliohojiwa na mwandishi wa habari hizi, walisema hakuna ushahidi wa moja kwa moja unaoonyesha uwepo wa tukio hilo, isipokuwa limetengenezwa ili kuonyesha umma kuwa mbunge huyo anawindwa na watu anaowaita maadui wake kisiasa.
Awali lilifanyika tukio linalofanana na hilo, lililohusisha na ajali ya gari la mbunge huyo lililodaiwa kugongwa na roli la mizigo, lakini uchunguzi wa polisi ulipofanyika ulibaini kuwa ajali hiyo ilisababishwa na uzembe wa dereva wa Dk. Mwakyembe.
Tukio hilo la Dk. Mwakyembe kupata ajali lilitafsiriwa kuwa liliandaliwa na kundi aliloliita la maadui zake kutaka kuumaliza kwa lengo la kufifisha juhudi zake za kupambana na ufisadi na mafisadi.
Kuibuka kwa tukio la kutaka kushambuliwa kwa kuchomwa kisu na watu wasiojulikana ni muendelezo wa mbunge huyo kutaka umaarufu hususani katika kipindi hiki cha kuelekea uchanguzi mkuu mwakani (2010).
Martha Mwakasole (45) mkazi wa kata ya Kajunjumele alidai aamini kama tukio hilo lilitokea kutokana na ukweli kuwa alihudhuria mikutano karibu yote inayofanywa na mbunge huyo katika jimbo hilo, lakini hakusikia wala kuona kufanyika kwa tukio hilo.
Mwana mama huyo alidai uenda vijana hao wanaodaiwa kutaka kumdhuru Dk. Mwakyembe waliandaliwa na wapambe wa mbunge huyo ili kunogesha mambo katika ziara hiyo.
Unajua Dk. Mwakyembe amekuwa akizungumza maneno yale yale ya kila siku ya ufisadi, ufisadi tu, lakini hakuna kipya ambacho anakiibua katika kuleta maendeleo ya jimbo. Kwa hali hii wananchi wengi hawahudhurii mikutano yake, sasa inatengenezwa tukio hilo ili kuamsha ari ya wananchi kumshabikia alidai.
Lucas Mwakatobe ambaye pia ni mkazi wa kata ya Kajunjumele alidai hata kama tukio hilo lilitokea basi hizo ni dalili za wazi kuwa Dk. Mwakyembe ameanza kuchokwa kisiasa. Hakuna anayemwinda Dk. Mwakyembe kwa lipi hasa?
Alidai hatua yake ya kuwaambia wakazi Kyela kukaa mkao wa kuhongwa na mafisadi kumewachukiza wananchi kwani kauli hiyo inaonyesha kuwadhalilisha wao na viongozi wao wa dini.
Kauli hiyo ya Mwakatobe inafuatia maneno ya Dk. Mwakyembe aliyoyatoa katika mkutano hadhara uliofanyika Jumamosi ya Agosti 29 katika daraja la Lufilyo kata ya Lusungo ambapo alidai mafisadi wametenga fedha chafu shilling milioni 400 kuwahonga wananchi ili wamchukie.
Mbunge huyo alidai fedha hizo zimeandaliwa mahususi ili kuwatengeneza watu waliojitokeza katika uchaguzi mkuu ujao.
Mwakyembe akawataka wakazi wa jimbo lake kutoogopa kuzitwaa fedha hizo ambazo alidai kuwa zimepitishwa kupitia madhehebu ya dini.
Mbunge anapotoa madai mazito kama hayo kwa viongozi wetu wa madhehebu ya dini na kuwatisha watu wengine wasijitokeze kuchuana naye katika ubunge anamanisha nini si kama kuleta mgawanyo miongoni mwa jamii na wanachama wa Chama Cha Mapinduzi? Alihoji Mwakatobe.
Akaongeza kudai kuwa miundombinu ya jimbo letu imechoka, mbunge wetu ameshindwa kutafuta wafadhili kutusaidia badala yake amekuwa akihubiri wimbo wa ufisadi na mafisadi wasioonekana, wimbo huo utatusaidia nini katika mazingira magumu kama haya?
Tumekuwa tukitembea umbali mrefu kutafuta maji, zahanati hazina dawa, sasa leo mbunge anapokuja na ajenda ya kutukutaza tusichangie maendeleo yetu anataka tumkomoe nani maana hatujawahi mkumuona Mwakyembe akitibiwa katika zahanati hizi za vijijini, mara nyingi yupo Dar es Salaam ambako huko kuna hospitali kubwa kubwa, alidai.
Daminan Mwakibinga mkazi wa Lusungo alidai Dk. Mwakyembe akiulizwa ni fisadi gani ambaye anamjua kwamba baado yumo ndani ya CCM na akitoka huyo basi CCM ndipo itabaki haina fisadi? Mbona hatutajii? Sijui Mwakyembe anaweza kumtaja nani? Lakini kinachoonekana ni namna Fulani ya kampeni za kutaka kutushawishi tumpigie kura za huruma.
Kinachoonekana kwa Dk. Mwakyembe badala ya kuwahubiria watu maandiko ya CCM kwamba rushwa ni adui wa haki, yeye anaifagilia kwa kututaka wananchi tuchangamkie pesa hizo, alidai Mwakibinga.
Akaongeza kudai kuwa mbunge wetu anawataka mafisadi watoke ndani ya CCM, lakini wakati huo huo mpinga rushwa na mchukia hongo ameshikamana na wapiga kura ambao wamelengwa kuhongwa milioni 400, ili kumngoa kwenye ubunge kwa hili tutashindwa kumuelewa.
Naye mmoja wa wachungaji wa kanisa la Pentekoste, ambaye hakupenda jina lake liandikwe gazetini, alimtaka Dk. Mwakyembe kuthibitisha tuhuma zake dhidi ya madhehebu ya dini.
Mchungaji huyo alisema kuwa ipo sababu ya Dk. Mwakyembe kuthibitisha hizo shilingi 400 na nani na wapi. Akishindwa kuthibitisha madai yake basi tutaamini kuwa hizo ni propaganda za kutaka kujikweza kisiasa na kutuhadaa ihali pesa hizo zimetolewa na wapambe kutoka kwenye kundi lake, alidai mchungaji huyo.
Pia Mchungaji huyo aliwataka wananchi wenye sifa za kutaka kugombea jimboni humo wajitokeze bila kuhofia propaganda za Dk. Mwakyembe kwa sababu ni haki ya kila raia kuchangua na kuchaguliwa kwa mujibu wa katiba ya nchi.
Hakuna mwenye hati miliki ya jimbo la Kyela wala hakuna mwenye mamlaka ya kuwazuia wengine wasijitokeze kuwania ubunge kutokana na hira ya choyo, hivyo yeyote mwenye sifa na aje kugombea Kyela bila wasiwasi wowote kwani hili ni jimbo la wote, alibainisha.
Akasema tumechoshwa na ngonjera na mashaihiri ya kupambana na ufisadi barabarani, kama wanaona wana ushahidi na wale wanaowatuhumu kuwa ni mafisadi milango ipo wazi kwenda mahakamani au kupeleka suala hilo kwenye vyombo vya dola. Hatuwezi kukubali kuona katiba ikipindishwa na wachache kwa kuwazuia wengine wasiwanie uongozi, kwa madai kwamba wakithubutu kuwania madaraka basi ionekane wametumwa na mafisadi.
Naye Christina Masangula (89) alihoji kwa nini CCM hivi sasa vikao vyake vingi vya ngazi ya juu vinapofanyika maamuzi mengi yayotolewa na kwa kipindi cha muda mfupi yanakuwa yameisha samba mitaani tofauti na miaka ya nyuma hali inayotia mashaka uadilifu wa viongozi wa chama hicho.
Haiwezekani kikao cha kamati kuu ya Halmashauri kuu ya CCM kinaazimia mambo ya msingi kwa chama hicho lakini cha ajabu na chakushangaza utakuta kwa kipindi kifupi maneno hayo yameenea kwenye vilabu vya pombe. Hali hii inawafanya wananchi kutafsiri kuwa CCM imekuwa sasa kama sawa vyama vya upinzani, mbona enzi za mwalimu Nyerere mambo hayo hayakuwepo? Masangula alihoji huku akionekana mwenye kukereka.