Sihusiki na suala la Kadhi - JK
2007-11-12 08:38:01
Na Simon Mhina
Rais Jakaya Kikwete, `amenawa mikono` kuhusu sakata la uanzishwaji wa Mahakama ya Kadhi Mkuu na kukumbusha kuwa suala hilo halikuanzishwa na serikali yake au yeye binafsi bali liliibuliwa na Mwenyekiti wa TLP, Mbunge wa Temeke Bw. Augustine Mrema.
Rais Kikwete ameyasema hayo jana wakati wa ibada maalum ya kusimika Mkuu mpya wa Kanisa la Kiinjili la Kilutheri Tanzania (KKKT) iliyofanyika katika Kanisa Kuu la Azania Front jijini Dar es Salaam.
Aidha alisema licha ya suala hilo (la Kadhi) kuonekana katika Ilani ya uchaguzi ya CCM iliyomwingiza madarakani kwa kishindo mwaka 2005, bado yeye hahusiki.
Alisema kwa mujibu wa taratibu za CCM mgombea hahusiki wala hashirikishwi katika kuandaa Ilani.
Alisema ilani ya uchaguzi huandaliwa mwaka mmoja kabla ya uchaguzi.
`Hii ina maana kwamba mgombea hashirikishwi kwenye kutunga ilani, ili asije akatunga mambo rahisi na kuyatekeleza, kisha akajipatia umaarufu wa bure.
Ilani ninayoitumikia sasa sio mimi niliyoiandaa, bali iliandaliwa na tume maalum,` alisema na kuongeza: `Mimi pale Jangwani wakati wa kuzindua kampeni, nilikabidhiwa na Mwenyekiti wa Taifa wakati ule mzee wetu Mkapa. Nasisitiza Ilani yetu hutungwa kabla ya mgombea hajajulikana.`
Akizungumzia historia ya sakata la kadhi, Rais Kikwete alisema chanzo chake ni wanasiasa.
`Hivi karibuni naziona dalili zinazoashiria kuwa tusipokuwa waangalifu upendo na mshikamano baina ya Waislam na Wakristo hapa nchini utaharibika.
Kiini cha hali hiyo ni matendo na kelele za baadhi ya wanasiasa na baadhi ya viongozi wa dini wa pande zote mbili kuhusu suala la mahakama ya kadhi.
Chimbuko la kinachoendelea ni bunge na muasisi wake alipokuwa Mbunge wa Temeke, wakati huo Bw. Lyatonga Mrema.` alisema.
Alisema baada ya Bw. Mrema kuliwasilisha Bungeni kama hoja binafsi, Spika alilitafakari kwa hekima.
Alisema hata baada ya Mrema kutoka bungeni, Mbunge kupitia chama chake cha TLP, Bw. Thomas Ngawaiya aliliendeleza.
`Spika wa wakati ule, Pius Msekwa, kwa busara zake akaona kwamba iwapo angeruhusu mjadala juu ya suala hilo bungeni, angebomoa badala ya kujenga. Akaamua kulipeleka kwenye kamati husika ile ya Katiba na sheria iliyokuwa inaongozwa na Athuman Janguo,` alisema.
Rais Kikwete alisema kwa niaba ya Bunge, Kamati ilifanya utafiti wa kina kwa kuzitembelea nchi kadhaa zenye wakristo na waislam ambazo zina mahakama hizo na kujionea jinsi zinavyofanya kazi na kwamba masuala yanayohusu waislam yanashughulikiwa vipi.
Alizitaja nchi hizo kuwa ni Kenya, Uganda na Afrika Kusini.
Alifafanua kwamba nchini Kenya Mahakama ya Kadhi ipo, hasa kwenye maeneo yenye waislam wengi, ilianzishwa enzi za ukoloni na inaendelea.
Alisema Uganda mahakama hiyo ipo kwenye |Katiba lakini haijaanzishwa.
Wakati Afrika kusini hakuna mahakama hiyo, lakini masuala ya waislam yamo katika sheria za nchi.
Alisema baada ya Kamati kwa niaba ya Bunge kukamilisha kazi yake, Spika aliwasilisha taarifa kwa serikali kwa ajili ya kuchukua hatua.
`Lakini na sisi serikali hatuwezi kuchukua suala hili hivi hivi tu, kwa vile tuna chombo chetu cha kujadili, kuhakiki na kutoa maamuzi kwa mambo ya kitaam kama hayo. Kwa hiyo suala hilo tukalikabidhi katika Tume ya kurekebisha sheria,` alisema.
Aliwataka watanzania hasa waumini wa dini za Kikristo na uislam kuwa watulivu ili kusubiri maelekezo na ushauri wa tume ya kurekebisha sheria juu ya suala hilo.
Alisema Tume hiyo itatoa hatima ya suala hilo kabla ya mwezi Februari mwakani.
Rais Kikwete alisema lengo la kuwataka wawe watulivi ni ili kuifanya tume hiyo itoe mapendekezo huru juu ya sakata la mahakama ya kadhi, bila kushinikizwa na upande wowote.
Hata hivyo alisisitiza kwamba uamuzi wowote utakaotolewa na Tume hiyo ni ule utakaokuwa na maslahi kwa taifa zima.
`Nasisitiza hili si jambo langu binafsi, mchakato wake niliukuta na sasa nauacha uendelee,` alisema.
Alisisitiza kwamba hakuna sababu ya watu kutokuwa na subira, kwa vile uamuzi wa suala hilo hautakuwa wa siri, wala wasiweke shinikizo katika hili bali waiache tume iendelee na kazi yake.
Rais Kikwete aliwaomba waumini wa madhehebu yote kuhakikisha amani na utulivu vinaendelea kuimarika nchini.
`Ni jambo lililo wazi kuwa amani na utulivu tulionao hapa nchini umetokana kwa kiwango fulani na juhudi zinazofanywa na Kanisa,` alisema
Jana, gazeti moja la kila siku (si Nipashe) lilidai kuwa Rais Kikwete, wakati huo akiwa mgombea, `inawezekana aliliweka suala hilo katika ilani yake ili kuhakikisha kuwa anapata kura nyingi kutoka kwa waumini wa dini ya Kiislamu..`
Rais Kikwete alimweleza Mkuu mpya wa KKKT, Askofu Alex Gehaz Malasusa, kwamba ni matumaini yake kwamba ataendelea kuliimarisha kanisa hilo na kuendeleza mema aliyoachiwa na mtangulizi wake, Askofu Samson Mushemba ambaye amestaafu.
Alisema serikali yake itaendelea kushirikiana na KKKT hasa katika kudumisha huduma za afya na elimu.
Akijibu hutuba hiyo, Akofu Mkuu Malasusa alisema: `Mheshimiwa Rais, suala la kadhi ni gumu sana, ni jambo nyeti ni uamuzi mgumu mno, lakini Kanisa litakuombea katika kipindi hiki.`
Hata hivyo, Askofu Malasusa alitaka umakini uwepo katika suala hilo na kuonya kwamba lisije likawa chanzo cha kufanya Tanzania kuzalisha wakimbizi. Alisisitiza kwamba mifano juu ya maafa ya migogoro ya kidini ipo.
SOURCE: Nipashe
JAMANI INAKUWAJE MKUU WA NCHI ASEME HAUSIKI? INAMAANA KAMA WANAO KAANZISHA KITU KATIKA FAMILIA BABA UTASEMA SIHUSIKI KWASABABU MWANAO ALIANZISHA?