16. MAISHA MAPYA na UHURU - Ω
“Nakuusieni na kuihusia nafsi yangu juu ya kumcha Mwenyezi Mungu, amesema Mwenyezi Mungu (aliye takasika), … hiki (Qur’an) ni kitabu kisichokuwa na shaka ndani yake na muongozo kwa wale wamchao …”
“Sisi waislamu, tuna miongozo miwili, Qur’an na Sunna. Qur’an ni maneo ya Mwenyezi Mungu na Sunna ni matendo na mafundisho ya Mtume Muhammad (Rehema na Amani zimwendee).”
“Tushikamana na Kitabu cha Mwenyezi Mungu na Hadithi za Mtume, hatuwezi kupotea.”
Hayo yalikuwa maneno ya Walii (kipenzi) wa Mwenyezi Mungu wa Utete Rufiji (kama wenyeji walivyokuwa wakimwita) wakati akinukuu aya kutoka Qur’an akiwa anatujenga kiimani.
“Katika hii Qur’an Mwenyezi Mungu ameweka elimu ya toka watu wa mwanzo mpaka watu wa mwisho, elimu zote zimo ndani ya Qur’an, historia imo, mawaidha yamo, mifano imo, visa vimo, hesabu zimo, utaratibu wa kuendesha Dunia umo ndani ya Qur’an na hiki kitabu huhifadhi waumini kwa fitina iliyomo humu duniani…” aliendelea
“Ndani ya Qur’an kuna habari za watu waliokuwepo kabla yetu, kuna habari za watu baada ya sisi kuondoka, ni hakimu baina yetu na ni upambanuzi juu ya mambo mbalimbali. Haifai kuiacha.”
“Hii Qur’an ajabu zake hazimaliziki, wana zuoni hawashibi, kila siku wanatoa faida na hata majini walipoisikia Qur’an inasomwa, wakasema hakika sisi tumesikia Qur’an ya ajabu, … inaongoza kwenye uongofu kwa hiyo tumeiamini na wala hatutofanya ushirikina…, na kwa hakika utukufu wa Mola wetu mlezi umetukuka kabisa,… hana mke wa mwana…, … na kwa hakika wapumbavu miongoni mwetu walikuwa wakisema uongo uliopindukia juu ya Mwenyezi Mungu… nasi tulidhani kuwa watu na majini hawamsingizii uongo Mwenyezi Mungu…,”
Aliendelea yule mcha Mungu tutupatia mawaidha kupitia kitabu kitukufu Qur’an na kutusimulia habari za majini jinsi baadhi walivyo mrejea Mwenyezi Mungu na wengine waliendelea kukengeuka.
“Eee umesema mmetoka Bagamoyo!” aliuliza yule Walii,
“Rudini huko, kuna Sheikh Mkubwa Zawiani, utapata muongozo na elimu kadha wa kadha, kikubwa shikamaneni na hiki kitabu wala msikiache.” Alimaliza yule Walii na tukaagana na kuanza safari ya kurudi.
Nilikuwa mimi na mke wangu Behat, tulilala Rujiji Ikwiriri na siku ya pili tulifika Dar na moja kwa moja kwenda Bagamoyo.
Bagamoyo pale Zawian tukaambiwa tuende Lushoto kumtafuta Shariff Badowo ili atufanyia maombezi makubwa kabla ya kurudi Zawiani kwa ajili ya kumalizia elimu nasihi.
Tulienda Tanga, tukafika nymbani kwake lakini tukaambiwa amesafiri kwenda Mombasa, tukaambiwa tumtafute kijana mmoja pale Horohoro atatusaidia kufika kwake.
Yule kijana alikuwa ni mfanyakazi wa mabasi ya Modern (Mombasa – Tz – Zambia nk), alikuwa anaitwa Sarojo, alitusaidia sana hadi tukafika kwa Shariff Badowo na kufanya dua kubwa kubwa sijapata kuona na tulivyorudi Zawiani tulikuwa na utulivu mkubwa.
*********
Tukiwa Zawiani – Bagamoyo
“Tatizo lenu mlivyokuja mara ya kwanza hamkutaka kunisikiliza kwa kituo, wewe na kaka yako wote mlikuwa na haraka haraka kiasi cha kutopata yote ambyo nilitaka kuwaambieni.” Alikuwa anaongea Sheikh Mohamed kwa sauti yake nzito iliyojaa umwinyi mwinyi hivi kwa kutulaumu kiaina…
“Sasa ulivyorudi na kuniambia kuwa umepona, nikadhani labda umejuwa asili ya shida yako na kutatuliwa ipasavyo…” aliendelea…
“Kumbe bado kwa maoni yangu, ulikuwa kwenye safari ya kujijuwa na kujitambua… na sasa kwa vile umefikia hatua hii basi ukae kitako nikuelimishe…” alisema.
“Mwenyezi Mungu alituumba ili tumuabudu yeye, tena yeye tu na wala tusimshirikishe na miungu mingine, hayo ndiyo malengo hasa ya sisi kuumbwa, hata maumbile yetu yamewekwa kurahisisha zoezi hilo la kumuabudu yeye”
“Tukimuabudu yeye hatumuongezei chochote, na tusipomwabudu hatumpunguzii chochote, YEYE ambaye hakuna Mola apasaye kuabudiwa kwa haki ile YEYE, Yu hai na ni wa kudumu, halali wala kupatwa na usingizi. NDIYE Mola wa Mbingu na Ardhi na vilivyomo baina yake…”
“Anajuwa yaliyochificha mbele na nyuma, na katika sisi viumbe hatuna tujuwalo ama hatuwezi kujifunza (kupata elimu) ila kwa kuridhia kwake, na utukufu wake umeenea Mbinguni na ardhini na wala hawezi kushindwa kuvilinda viumbe vyake maana yeye ametukuka (aliye juu) na NDIYE MKUU.” Alisema Sheikh kisha akasoma aya katika mpangilio wake.
Alivyoanza kusoma nami nikakumbuka kile kikaratasi nilichopewa Kikokwe niwe nasoma mara kwa mara, maneno hayo yalikuwa sehemu ya dua ile niliyopewa huko.
Sheikh aliendelea na risala…
“Katika uumbaji wake (Mwenyezi Mungu) aliumba viumbe mbalimbali, na kila kiumbe kina mamlaka yake na mipaka yake katika kuyaendea mambo…”
Akatoa mifano mbali mbali jinsi viumbe wengi wanavyoishi humu duniani ikiwemo wadudu, hayawani na hatimaye majini na binadamu.
“Binadamu ndio tumepewa uhalifa (uongozi) katika dunia hii, yani tunatakiwa tuweze kuitawala dunia ipasavyo…”
“Majini nao wana tawala zao, wana mataifa yao, wana makabila yao, wana koo zao, wana mila zao na desturi zao, na wamepewa uwezo mbalimbali lakini pia wamewekewa mipaka…”
“Haifai kwa Majini kuingia kwenye tawala za kibinadamu na kuwasumbua watu kwa kuwapagawisha, kuwatia maradhi ama eti kujifanya wanawalinda…”
“Wao wana ‘ulimwengu’ wao na sisi binadamu tuna ‘ulimwengu’ wetu…”
“Hivyo ni makossa makubwa kwa Jinni kumuingia mwanadamu kwa namna yoyote ile kwa visingizio mbalimbali…”
“Idadi ya majini ni kubwa mara nyingi sana kuliko wanadamu, na kwa kuzingatia kuwa wao wanaishi muda mrefu kuliko wanadamu basi wingi wao huongezeka mara kwa mara kiasi cha kutapakaa duniani kote… kwa wingi wao huo hata kila mwanadamu aliye hai muda huu akikusanya majini sabini kila mmoja, basi binadamu wote watakusanya na wengi sana bado watabaki hawajakusanywa”
“Kuna elimu mbalimbali za kuweza kuwamiliki hawa majini, lakini ni moja ya elimu zilizokatazwa kwa kuwa hatimaye huleta hasara badala ya faida…”
“Lakini kwa kuwa Duniani humu kuna fitina mbalimbali ikiwemo fitna ya afya, mali, wake, waume, watoto nk basi baadhi ya watu hupatwa na husda, chuki na vijicho ambavyo huwadhuru wenzao, na kazi zote hizo hufanywa na hao majini ambao wameasi kwa kushirikiana na binadamu kwa namna mbalimbali za elimu ya kichawi”
“Elimu ya kukabiliana na matatizo hayo pia ipo, ipo kwa njia nyeusi na kwa njia nyeupe…”
“Hivyo tiba zipo, lakini kuna tiba kwa njia sahihi na zipo tiba za kwa njia ya kishirikina”
“Kufanya ushirikina na moja ya dhambi ambayo kama ikitokea umekufa bila ya kutubu basi ni dhambi isiyo sameheka labda kwa rehma zake Mola wetu maana yeye ndiye mjuzi zaidi”
“Hivyo basi ushirikina HAUFAI mbele za Mwenyezi Mungu”
“Kwakuwa tiba sahihi zipo, basi yatupasa kufuata tiba kwa njia zilizoelekezwa kwa miongozo ya dini yetu”
“Tiba isiyo sahihi utaijuwa kwa masharti yake ambayo hatimaye yanakupelekea katika kumuasi Mwenyezi Mungu kwa namna zote nne, kuwaza, kunena, kutenda na kutotimiza wajibu…”
“Sasa kwa kuwa ninyi mliamua kuishi kama binadamu…”
Tukawa tunaangaliana na Behat…
“…yafaa muendelee kuishi hivyo na kufuata maamrisho na makatazo yote ambayo yapo katika muongozo wa Qur’an na Sunna…”
“Pazi…!” aliniita Sheikh
“Mwenzako ana kiumbe tumboni…”
Nikawa manuangalia Behat tumboni sioni kitu zaidi ya ‘flat screen’ (hakuwa na hata kijitambi kidogo)
“Atazaliwa kiumbe ambaye sasa atakuwa mwanadamu kamili, wanenu hawatokuwa na passport ya kuingia Ujinini kama ilivyo kwenu hivi sasa ingawaje bado mpo nusu jinni.., wewe Pazi ni nusu binadamu nusu jinni na huyo mwenzako ni nusu jinni na nusu binadamu…”
Moja kwa moja nikaelewa tofauti yake kwa mmoja wetu alilala kwenye tumbo la uzazi binadamu ilhali mwingine alila kwenye tumbo la uzazi jinni.
Aliendelea kutupa risala pale weeee mwisho akasema…
“Tafuteni njia halali za kupata rizki zenu, hata kama itakuwa ni kutibu watu basi uifanye tiba iliyo sahihi kwa njia za kisunna (yaani kwa njia ya mafundisho ya Mtume Muhammad, Rehema na Amani zimwendee)
“Kitu kingine muhimu sana ni kwamba haifai kubeza dini nyingine, mfano hawa wenzetu wakristo tunaishi nao humu mjini, majumbani na kupeana heshima za kibinadamu, Kuna Kanisa kubwa kule Mantep (Sikuhizi wanaita ADEM), kuna Kanisa dogo kule miembe safa (jirani na kushukia MSALABANI) na kuna Kanisa kule Mwanakalenge. Hawa ni binadamu wenzetu na wana Imani yao thabiti katika kumwabungu Mungu wao kwa mujibu wa mafundisho yao, ukumbuke kuwa hawa pia kiongozi wao alipewa Kitabu kama ilivyo Qur’an kwa sisi. Usiwabeze wala kudharau Imani zao maana kuna wengine huenda wakawa bora mbele ya mwenyezi Mungu kuliko baadhi yetu, lakini haikatazwi kuwalingania ili waje katika uislam, tena kwa lugha iliyo nzuri na staha.”
“Kumbuka hata Nabii Mussa (Rehema na Amani zimfikie) alipoambiwa akamlinganie Firauni (Farao) aliambiwa akazungumze naye kwa upole licha ya kufuru kubwa aliyokuwa akiifanya. Kazi yetu ni kufikisha ujumbe lakini kumuongoa mja siyo kazi yetu, Allah mwingi wa Rehema sisi sote ni viumbe vyake, tusijitie ukiburi, YEYE Allah huamua atakavyo.”
Aliendelea…
“Vitabu cha elimu hiyo ya tiba zipo, vitafute ujifunze kwa walimu ukihitimu uendelee na tiba halali, kama hutoweza basi rejea kwenye kazi ya baba yako, ameshazeeka sasa afaa kusaidiwa sana…”
Alimalizia risala yake kwa kutusihi kuwa sisi bado ni nusu watu nusu majini, hivyo kiasili tuna nguvu za kijinni basi tuwe makini na maneno tuyasemayo na kujitahidi kujizuia hasira zetu maana huenda zikawa na athari kwa binadamu wa kawaida.
Tulirudi nyumbani na kumkuta mama akitusubiri kwa hamu.
“Enhe, mmeambiwaje huko?...” Mama aliuliza kwa shauku
Tukamwelezea yote na hatimaye mimi na mke wangu tukaamua kumtumikia Mwenyezi Mungu kwa kuwalingania watu katika dini huku nikiendeleza kazi ya Baba.
“Nadhiri yako sasa Mama inaenda kutimia…” nilisema.
Baada ya siku tatu, tuliaga kurudi Dar es Salaam kuendelea na maisha.
Leo hii tuna watoto watatu, tunaendeleza kazi ya uvuvi na uchuuzi kwa njia za kisasa, Baba na mama walishafariki, mama mkubwa pia alishafariki.
Tukapata Chakula cha mchana pamoja, kisha akanisindikiza nami nikachukuwa njia ya kurudi kwangu Upanga.
Jumamosi ile ilikuwa tulivu lakini nyumbani kwangu hapakuwa hivyo, nilikuta mke wangu amenuna, lakini nikamwambia hebu baada ya kula uje chumbani nimsimulie kisa chote nilichosimuliwa….
*******
Hakutaka nilale bali nimmalizie kisa chote maana muda tayari ulikuwa umeshaenda sana na siku Jumapili ilikuwa ndio inaingia (kwa mujibu was aa za na kalenda ya Gregori)…
Nilimkidhia haja yake baada ya kuona amevutiwa pia na kushangazwa japo kwa kuifupisha.
Mwishowe tuliendeleza ‘libeneke’ la mume na mke.
**************** MWISHO*************
Update!
Sheikh Mohamed alishafariki, Mzee Zahiri naye, Mwalimu Mwaloki, Mzee wa tiba Mlingotini, Mzee Njembi, Mcha Mungu wa Rufiji, Shariff Badowo, Shariff wa Kikokwe wote wametangulia mbele za haki.
Watu wengine ambao wametajwa katika simulizi hii sina update zao.
Imenibidi nifupishe ili niende na muda-huru niliokuwa nao maana ni mchache.
Niliamua kushea nanyi kisa hiki kama kumbukumbu ya kukumbuka uwepo wa Pazi na familia yake hapa Duniani kwa maana ya kwamba ile familia yote ilifariki kwa kuzama baharini miaka kumi na moja na siku arobaini na nane hivi ziliyopita walipokuwa wakitokea Unguja kuelekea matembezini Pemba kwenye MV. Spice Islander.
**********
Hakika sisi sote ni wa Mwenyezi Mungu na kwa hakika kwake tutarejea.
Ω