7. KUVUKA ZIWA TANGANYIKA
Alfajiri tulikisia vishindo vishindo vya mtu kurudi, lakini hatukuamka hadi palivyokucha kabisa. Tulivyopata staftahi tuliendelea na mazungumzo ya kawaida na mke wa Ustadhi wakati tukisubiri Ustadhi mwenyewe aamke maana alikesha safarini.
Majira ya saa tano na nusu hivi asubuhi Ustadhi alitoka nje na kuja kutusabahi.
“Assalaam aleikum, habari za huko mtokako, poleni kwa safari na karibuni sana Kabwe” alitusalimia salamu ndefu.
Tuliitikia kwa pamoja na kisha akaomba aletewe chai pale nje huku akianza sasa kuongeza na sisi kwa kutusikiliza.
Kama kawaida Shangazi alianza kumuelezea sababu ya safari yetu kwake, kwamba atusaidie ili tuweze kufika huko upande wa pili na wala hatupajui wapi hasa tunapotakiwa kwenda. Alimpa salamu kutoka kwa mzee Njembi…
“Alituambia tukikuona wewe basi safari yetu itakuwa salama na tutafika tuendako” alimalizia Shangazi.
“Sawa karibuni, wa aleikum salaam wa rahmatullah wa barakatu” aliitikia salam ya kutoka kwa mzee Njembi.
“Aaah ni kweli mimi nina chombo changu ambacho nakiendesha mwenyewe, na kazi yangu kubwa ni kupeleka matufa ya wateja wangu upande wa pili. Napeleka petroli, dizeli na wakati mwingine mafuta ya kula na ya kujipaka”
“Ni kazi ambayo nimeifanya kwa muda mrefu tangia kijana mdogo nilipokuja huku kutafuta maisha kutokea Irangi Kondoa”
“Kwa uzoefu nilionao ndiyo maana mzee Njembi ameniamini sana hata katika kumsaidia katika mambo yake mengine binafsi. Nilifahamiana na mzee Njembi siku chache tu baada ya kukabidhiwa chombo niwe nahodha kamili”
“kabla ya hapo nilikuwa nahodha msaidizi lakini kwa bahati nzuri tajiri mwenye chombo alinunua boti nyingine ya kisasa hivyo yule nahodha akapewa chombo kipya nami nikapewa chombo cha zamani”
“Sasa kumbe nisijuwe kuna baadhi ya watu wenyeji wa hapa hawakupenda mimi nipewe kile chombo badala yake wapewe watoto wao. Kwa sababu hiyo nilisumbuliwa sana na mauzauza ya kienyeji hapa, japokuwa nami niliaga kwetu Kondoa lakini haikufua dafu, ikabidi nianze kutafuta msaada”
“Katika kuhangaika kwangu ndipo nikakutana na Mzee Njembi kule Ujiji, hakika alinisaidia sana kiasi kwamba nilivyorudi nilifanya kazi vizuri tena kwa ufanisi na bila bughuza zozote kama za mwanzo licha ya majaribio yao kadhaa ambapo matokeo yalikuwa yanarudi kwao”
“Watu wakaanza kuniita ustadhi ustadhi, kumbe walisemezana wao kwa wao kuwa wamemchezea ustadhi sasa mambo yao hayaendi, na uaslama wao ukawa baada ya kuacha kunisumbua” Alisema kwa kirefu Ustadhi.
“Jina langu halisi ni Muharami bin Said ibn Kassim Chavai, lakini ukiulizia Muharami mji huu huwezi kunipata, we sema ustadhi tu, kila mtu hapa ananijuwa”
“Hebu fikiria, usiku mnalala asubuhi mnajikuta mpo nje barazani mmelala! Siku nyingine mnajikuta ufukweni kabisa mwa ziwa miguu ikiwa inagusa maji kidogo! Siku nyingine wote mkiamka mnakuta mmechanjwa mchirizi mmoja mgongni au kifuani, mchirizi mrefu lazima uuone au mwenzako auone! Siku nyingine unapotea tu ziwani hufika bandarini hadi unaishiwa mafuta uliyopanga kutumia! Siku nyingine unakutana na dhoruba isiyo na kichwa wala miguu yani unashangaa ghafla tu wimbi hili hapa tena mengine yanakuja dabodabo (double double)” Alituambia na kuendelea…
“Hebu niambie, wewe ungefanyeje!” aliuliza. Sisi hatukujibu kitu.
“Nilijaribu kutumia njia ninazozijuwa weee lakini haikuwezekana, nimezunguka Rukwa ya Mpanda, Rukwa ya Upimbwe, Rukwa ya Sumbawanga, Rukwa ya Unyika (siyo Unyiha), Rukwa ya Laela hadi sehemu iitwayo Mkutano jirani na Kijiji cha wachawi sikufanikiwa, maana ilikuwa inaoneka kama wote ni timu moja tu ndipo nikaanza kuhangaika kutafuta msaada nje ya mkoa huu wa Rukwa.” Alimalizizia chai yake kisha akaendelea…; wakati huo sisi tupo kimya tu tunasikiliza na kujifunza kumbe siye Pazi tu anayehangaika kutafuta kwa tabu.
“Nikaenda Kusini Mtwara jirani na Msumbiji, kule yule bibi akaniambia nimepata tabu bure kwenda huko, nigeuze niende Kigoma Ujiji pale wanapawezea Rukwa” Alisema.
Hapa sasa nikaendelea kujifunza kumbe mambo haya ya nguvu za giza zina madaraja, mipaka, mamlaka na utimu. Ama kweli unaweza ukaishi duniani na usijuwe chochote kinachoendelea katika mambo ya nguvu za giza. Vitu vinatisha sana. Nikakumbuka jinsi nilivyo pelekwa mzimuni kule Handeni na kuzungumza na viumbe visivyoonekana lakini kwa kupitia vinywa wa watoto! Sita kaa nisahau.
“Kwa mzee Njembi nilipikwa kwenye chungu cha maji moto yasiyounguza na kutengenezewa ulinzi kwa kadri mahitaji yangu yalivyokuwa na kushida majaribu ya kutisha kutoka kwa ulinzi huo, hatimaye nikawa salama na hadi leo wananiita ustadhi, siyo kwa mazuri bali kwa shughuli waipatayo pindi wakiazimia kunifanyia ubaya.” Alisema.
“Kazi zangu zilienda vizuri hadi miaka michache iliyopita nikanunua chombo changu binafsi na ndipo mzee Njembi akaanza kunitumia kumchukulia miti shamba (dawa) kutoka Zaire. Bahati mbaya ng’ambo huko kuna hatari sana ya usalama, hakuna usalama kabisa, ukienda ukirudi unamshukuru Mungu, maana unaweza kutekwa njiani na waasi wa jeshi lao huko, unaweza kutekwa na maharamia tu humuhumu na kudhulumu mali yote ili mradi usalama siyo wa uhakika huko hata njiani (ziwani)” alisema.
“Kuna siku wakati nafanya kazi zangu za usaidizi wa nahodha, niliwahi kupakia abiria kutoka ng’ambo na kuwapeleka Kigoma, walikuwa wageni kabisa, nikawafanyia ukarimu wa kuwasaidia katika mambo waliyoijia na kuhakikishia usalama wa mizigo yao njiani ziwani, baada ya kufika na wakati wa kurudi na sikuwadai ujira wowote wa ziada kwa usaidizi niliowafanyia.”
“Kumbe wale jamaa walikuwa wanajeshi waasi huko ng’ambo, mimi sikujuwa hadi siku moja chombo chetu kilipotekwa njiani na kupelekwa ng’ambo, wakachukuwa mali zote, mimi na nahodha wangu tukapelekwa kambini”
“Sasa alipokuja yule mkubwa wapo pale akaniangaliaaa, kisha akasema tupelekwe ofisini kwake, nikashangaa tunahudumiwa chakula kizuri na kupewa sehemu ya kulala pazuri. Pazuri kwa maana ya kwamba kuna hema na blangeti lililotandikwa kama kitanda. Katikati ya usiku akaja yule mkubwa wao bado akiwa amevalia magwanda yao ya jeshi na minyota nyota yake iliyo kaa vibaya, akaniita na kuniambia…”
“Mmesalimika kwa kuwa nimekutambua, wewe ni kijana mwema sana, kuna siku ulinisaidia sana. Akajitambulisha vizuri nikamkumbuka. Akaniambia atakuja kunitorosha, ameshawatuma wafuasi wake wakaniwekee pipa moja la dizeli kwenye boti na magunia, alituambia ikifika usiku wa manane atatuma askari aje atuongoze hadi kwenye boti yetu”
“Kweli usiku ule ule alikuja askari akatupa ishara ya kuwa tumfuate, tulitembea kwa kunyata hadi tulipofika ilipoegeshwa boti, akayaloweka yale magunia na kufunika injini ya boti ili isitoe mlio mkubwa ili tutoroke. Pia alituambia tupitie njia nyingine maana ile ya kawaida bado wanajeshi wanafanya doria zao za kuteka mali ili wapate kuishi huko msituni”
“Tuliwasha boti na kuondoka kwa kuelekea kaskazini kwa muda kadhaa kisha ndio tukafuata njia ya kenda uelekeo wa bandari ya Kigoma. Lakini kwa kuwa ilikuwa usiku wa giza totolo na pasipo mwezi wala nyota maana ilikuwa msimu ya mvua tukajikuta tumepotea palipo pambazuka na kuona tupo uelekeo wa hifadhi ya Jeshi letu (JW).”
“Mara tukasikia milio ya risasi na sauti kwenye spika ikituamuru tusalimu amri, tulizima injini na kusimama na kunyoosha mikono juu, kuna boti mbizi za jeshi za doria (fibre boats) zilituzingira wakiwa na silaha nzito huku mwanjeshi mmoja akiongea na simu ya upepo.”
“Sauti ya amri ikatoka kwenye boti moja” “Jitambulisheni, ninyi ni akina nani na mnatoka wapi na mnaelekea wapi?!”
“Sisi ni watanzania, sisi ni watanzania…” tulijitetea,
“Watanzania! Mbona mna boti ya waasi!” alisikika mmoja wa wale wanajeshi. Kuangalia hivi kwenye jina la boti yetu nikaona kumeandikwa BANA SUDI KIVU kwa maandishi mekundu. Kumbe tayari kule wale waasi walishajimilikisha, isingekuwa yule mkuu wao, sijui tungekuwa na hali gani”
“Sisi ni watanzania, mimi ni mfipa na mwenzangu ni mrangi” alijitetea nahodha wangu.
“Bahati nzuri kule kwenye boti ya JW kulikuwa na Msandawe, hivyo alikuwa anakijuwa kwa kubabaisha kirangi na pia alikuwepo Mpimbwe ambaye pia alikuwa anaelewa kifipa”
“Abari ja mutondo!” alisema yule mjeshi huku akituangalia, haraka haraka nikajibu “jaboa”,
“Akasema tena ikiana!”
Nikajibu fasta “anga!” hii ilikuwa kisandawe.
Urangi na Usandawe ni jirani hivyo kwa kiasi fulani unaweza kujuwa baadhi ya maneno ya lugha nyingine. Mara akadakia mjeshi mwingine “Mwalalauli” yule mwenzangu akajibu “Eenditaa!”, japo alichapia lakini ilieleweka kuwa kweli kwa hatua ya kwanza inawezekana kuwa sisi ni watanzania.”
“Tukaelekezwa kuongoza hadi nchi kavu ambako kila tulivyokuwa tunakaribia tukawa tunawaona wanajeshi wakiwa wamekaa tayari kwa mashambulizi kutushambulia”
“Tukafika nchi kavu, tukapelekwa msobe msobe hadi sehemu kavu na kuamriwa kukaa chini”
“Baada ya mahojiano pale kweli wakathibitisha kuwa sisi ni watanzania na tulitekwa, tukapewa usindikizwaji hadi tulivyotoka nje ya eneo leo, lakini walifuta yale maadishi kwa rangi nyeusi”
“Tulifika Kabwe tukiwa hatuamini macho yetu”
“Sasa katika safari zetu zilizofuata za kawaida, kuna siku tukakuta na yule mkuu wa waasi akiwa kiraia pale bandarini ng’ambo kwao, akaifuata boti yetu na kuja kutusalimia kirafiki. Akaniambia, siku nyingine nikienda niseme maneno (ambayo alinitajia) kwa mtu yoyote anayeonekana kama askari nitakuwa salama na nitafikishwa kwake”
“Kwa kupitia huyo mkuu wa waasi, nikapata uchochoro sasa wa kufanya biashara kwa uhuru maeneo hayo na kuanza kupata mafanikio hadi bosi wetu akanunua boti nyingine mpya nami nikaachiwa ya zamani hadi nikanunua boti yangu ambayo ninayo hadi leo”
“Ni boti yangu tu inaweza kutembea mwambao wote wa ng’ambo bila matatizo, ndiyo maana Mzee Njembi alikuambieni mnitafute mimi. Na hata huko msituni kwa mbirikimo nitakupelekeni maana huko ndiyo safari ya huyu kijana ilipo” akaniangalia kisha akawaangalia wenzangu.
“Lakini nasikitika, ninyi safari yetu itaishia hapa, hamuwezi kwenda kule, mtakaa hapa hadi nirudi nije nikupeni habari za ndugu yenu” alimaliza na kutulia.
Tukabaki tunatizamana pale kwa mshangao!
“Sasa ikakuwaje huyo kwenda peke yake wakati hali yake inabadilika badilika, nani atamsaidia?” mama alihoji.
“Mama wala usiwe na wasiwasi, kule mambo ni mengi, mkienda wote kutakuwa na uzito sana wa safari, niaminini mimi, muaminini mzee Njembi” alimaliza na kuingia ndani akatuacha kujidaliana.
Tulijadiliana weee na tukakubaliana akija tumwambie kaka anisindikize, Shangazi na Mama wanisubiri. Basi baada ya muda kupita alirudi na kutuuliza tumefikia muafaka gani.
Ustadhi alikuwa ni mtu wa makamo, ni mmoja wa wale warangi wenye ngozi nyeusi, mwembamba mrefu na mchapa kazi. Baadaye nilikuja kujuwa kuwa alianza shughuli za uvuvi katika bonde la Rukwa kwenye Ziwa Rukwa na hali ya mavuno ilipokuwa ngumu ndipo akaenda Ziwa Tanganyika na kuanza kazi za ubaharia, unahodha usaidizi hadi sasa amekuwa nahodha mahiri.
“Tumeamua kaka yake amsindikize” alijibu shangazi.
“Hapana, haitowezekana, najuwa kwanza hapo ninyi hayupo mwenye makarasi ya kuvukia (passport) wala kadi ya homa ya manjano, sasa huyu atasumbuliwa sana na askari wa kule na wanapenda rushwa balaa, wenyewe wanaita ‘makuta’, chukueni ushauri wangu, huyu kijana niachieni mimi, atarudi salama in shaa Allah” alisema.
Wote pale tukaangaliana, na kisha kaka akasema, “duu tulisahau kuwa tunataka kwenda nchi nyingine, maana pia kuna ishu ya visa na kulipia kwa dola (dollar), vyote hivyo hatuna”
“Kuhusu viza (visa) kama ungekuwa na passport hata ile ya karatasi tungeweza kugonga wakati wa kuingia, lakini ni vyema ninyi mkabaki hapa nami nitarudi na mwanenu salama.” Alijibu Ustadhi.
Siku ikaishia hivyo na tukapanga kesho yake usiku safari ianze. Boti ilipakiwa mapipa ya dizeli na petrol kutoka kwa wateja tayari kwa safari. Kwa kuwa sikuwa mgeni wa safari za kwenye maji sikuwa na hofu.
Baada ya chakula cha jioni, nikachukuwa rasket (kibegi kidogo kilaini cha kufaa mgongoni au begani) yangu, na suruali yangu moja tu ya savco jeans, na nilivaa mtumba wa jeans ya levi’s straus na tshirt ya mtumba ya rangirangi, kwenye rasket kulikuwa na tshirts mbili za ziada, hivyo sikuwa na mzigo mzito, tukaenda kwenye boti na nikapanda, nikakaa jirani na anapokaa nahodha.
Tulikuwa watu watano tu kwenye boti ambapo wawili walikuwa ni wateja wenye mafuta na mmoja ni msaidizi wa Ustadhi. Safari ikaanza kwa msaidizi wa nahodha kuongoza chombo.
“Tuna safari ya kilomita mia moja na ishirini hivi hadi tufike tutakapoanzia safari ya nchi kavu mimi na wewe” alisema Ustadhi.
Safari iliendelea kwa kupiga stori za hapa na pale hadi hali ya ziwa ilipobadilika na kuwa na upepo mkali na mawimbi makubwa, Ustadhi akachukuwa unahodha. Safari iliendelea, kukiwa kimya na nahodha aliyakata mawimbi kwa kuyafuata, hali iliyofanya tutumia muda mwingi kutembea umbali mfupi. Hali ilitulia baada ya kama saa moja hivi ya dhoruba. Nilishangaa sana kuona kumbe hata ziwani kuna mawimbi makubwa sana. Stori zikaanza tena na nahodha msaidizi akachukuwa unahodha kuongoza chombo.
“Unajuwa Pazi, tunapoenda sasa kushusha mzigo ni kama kilomita hamisini tu kutoka kule Kabwe, lakini, siyo hapo tutakapoanzia safari, itabidi mimi na wewe tuelekee kwingine, lakini tutatembea kando kando ya mwambao hadi tutakapofika hapo tutakapo anzia safari…” aliniambia, mie nikawa naitikia tu maana naona napelekwa kama taahira, sijui hata hatma yangu itakuwa nini maana kila sehemu naambiwa uende huku, mara uende huku ili mradi sipati suluhu ya maradhi yangu. Hata hivyo nilijipa moyo kwa historia ya Ustadhi aliyotuhadithia.
“Tutashusha mizigo sehemu panapoitwa Zongwe, kisha tutaelekea bandari ya Moba…” alisema.
Safari ya kufika bandari ya kushusha mizigo ilituchukuwa kama saa sita hivi na mizigo yote ikashushwa hapo na saa kumi na moja tukaanza safari ya kwenda huko Kaskazini kwenye hiyo bandari ya Moba ambapo napo ilituchukuwa masaa manne hivi maana chombo kilikuwa chepesi licha ya ka umbali kidogo.
“Sasa dogo!” alisema Ustadhi huku akimuelekea yule msaidizi wake
“Leo ndio mtihani wako wako wa mwisho kufudhu unahodha, itabidi urudi kule Zongwe, upakie mapipa tupu na abiria utakao wapata urudi Kabwe, na uchukuwe mizigo ya Kabwe ulete huku” aliendelea.
“Uendelee kufanya hivyo hadi siku utakaponiona bandari ya Zongwe, haya, kila la heri” alimaliza na kumuamuru aondoshe chombo kuwahi Zongwe.
**********
Itaendelea