Hatimaye nipo huru

Hatimaye nipo huru

12. KUPANDA NDEGE KWA MARA YA KWANZA

"Mrudi Ujiji safari nyingine lakini siyo kwa kutafuta tiba bali kwa kunitembelea na kubadilishana mawazo." Hii ilikuwa kauli ya Mzee Njembi wakati tunaagana pale Ujiji.

Kila mara sauti hii ilikuwa inajirudia kichwani mwangu.

Jioni ile pale restaurant ya Kigoma Hotel wakati tukisubiri chakula chetu kiandaliwe, nilijaribu tena kupiga simu kwa Baba. Hakukuwa na network kwenye simu ile lakini simu iliita na mimi nikaanza kuongea na baba kiasi cha kuridhika na kisha kumpatia kaka naye akaongea halafu akampatia Shangazi naye akaongea weeee kisha akampatia Mama.

Baada ya mazungumzo na chakula tukaamua tufanye mpango wa kurudi Dar ea Salaam kwa ndege.

Kama kawaida Shangazi akaingia front na kupata taarifa za ndege.

Aliporudi alituambia kuwa kesho mchana kutakuwa na ndege ndogo itakayo waleta watu wa WFP (World Food Program), hivyo saa tano asubuhi tuwe pale uwanja wa ndege.

Tukaagana na kupumzika mimi na kaka chumba kimoja double, Shangazi na Mama chumba kimoja double.

Asubuhi baada ya breakfast ya uongo na kweli waiitayo kontineto, tuli check out na kuchukuwa teksi hadi airport ampapo hapakuwa mbali pia.

Ilipofika saa sita ile ndege ikatua na kushusha wazungu wawili na waafrika watatu, baada ya dakika chache tukafuatwa na kuambiwa tuingie kwenye Ndege maana itaondoka siyo muda mrefu.

Mimi, kaka, na Mama ndio ilikuwa mara yetu ya kwanza kupanda ndege.

Baada ya dakika chache zingine injini ikangurumishwa kwa sauti kubwa kisha ndege ikaanza kutembea kisha kutembea kwa kasi ghafla hiyoo tupo angani.

Nikakumbuka safari za usiku za kupaa na kuangalia ardhi kama mwewe...

Safari hii nilikuwa naona ardhi mchana kweupee na kufurahia mandhari ya nchi yetu na uumbaji wa Mungu.

Kutoka Kigoma tulielekea Arusha ambao rubani alituambia ana makaratasi ya kuchukuwa, kisha ndipo tukapaa tena kuelekea Dar es Salaam.

Ilikuwa safari nzuri yenye utalii wa juu kwa juu ndani yake lakini kutoka Arusha kuja Dar kuna sehemu tulipita kwenye korogesheni (turbulence) kwa sekunde kadhaa lakini tukapapita...

Tulitua DIA saa nne usiku.

Tukashuka na kumshukuru Mwenyezi Mungu na rubani, tukatoka nje ya sehemu za ukaguzi kisha tukaenda upande parking za magari kuchukuwa teksi.

Tukapata moja maridani na kutupeleka hadi Kariakoo ambapo tulikubaliana tufikie pale jirani na nyumbani, hivyo tukalala Al Uruba Hotel.

Asubuhi tukaenda pale nyumbani tulipo pangisha kuwasalimia wapangaji na kuona pakoje na mimi kutaka kujuwa kuhusu mwari Salma na mama yake.

Tukaambiwa kuwa mama Salma alifariki, kisha Salma naye akafariki.

Nikaulizia kuhusu Sinasudi nikaambiwa kuwa alikuja mara moja tu na akaondoka hajaonekana tena.

"Kuna siku alikuja akaomba funguo akaingia ndani akachukuwa nguo zake na kuongoka na begi lako... Tangia siku hiyo hatujamuona tena.. " alisema mmoja wa wapangaji.

"Baba Salma ambaye alikuwa dereva wa malori alihama baada ya misiba, hivyo vyumba vyao amepanga mtu mwingine na hela anakuja kuchukuwaga ndugu yenu. " Alisema

Mara moja tukajuwa ni ndugu yetu yupi aliyekuja kuchukuwa kodi.

Nikaomba funguo nikaingia chumbani kwangu, nikapaangalia kwa muda kisha nikafunga mlango na kumwambia yule mpangaji kiongozi kuwa, na hiki chumba pangisha, hela nitafuata mwenyewe unitunzie.

Tuliendelea kuongea pale wee hadi tukaridhika hivyo tukaamua sasa tuelekee mtaa wa Congo na Mkunguni kuangalia basi liliopo la kwenda Bagamoyo.

Bahati nzuri tukakuta basi moja la Chemsi (Champs Mulji) ambalo lilikuwa zuri sana lilitwa Msala, tukapanda na kusubiri lijae ili safari ianze.

Baada ya kuanza safari, saa mbili baadaye tulifika stendi mpya Bagamoyo palipokuwa pakiitwa "Kwa Kibwana"

Tulishuka na kijana mmoja aiywaye Kurame alitusaidia kubeba begi la Shangazi na mama kwa ujira hadi nyumbani tulipokiwa tunaenda.

Kuanzia tulivyotuwa Dar es Salaam network kwenye simu ya Shangazi ilirudi vizuri na kukawa na mawasiliano ya moja kwa moja hadi tunaingia Bagamoyo na kukuta mapokezi makubwa yameandaliwa.

Watu wa nyumbani kwa mama mkubwa eneo la Chuguuni katikati pia walikuja tukawa wote kwenye nyumba ya Kisima bluu.

Mama mkubwa hakuwa na furaha sana, niliona uso wake lakini dada zetu upande wake wao walionesha furaha kama kawaida.

Tuliongea sana pale muongeaji mkubwa akiwa Shangazi na chumvi chumvi aliongeza ili kunogesha stori.

Zawadi kidogo kutoka Dar ziligawiwa kwa wote, samaki zilizobakia kutoka Kabwe tukawaonesha wakawa wanashangaa samaki wa Ziwani kila mmoja akawa anamega kiasi na kuonja...

"Wamepooza...! Hawana chumvi" alisikika mmoja wa ndugu zetu ambaye alikuwa hodari sana kupika kama mama yake, mama mkubwa.

"Wa maji baridi hao, hawanaga chumvi" kaka alijibu.

Basi ilikuwa ni furaha sana tu kwa wote na tukala chakula saa kumi nanmoja kwa pamoja.

Uliandaliwa wali "shaba" pilau kwa mbuzi.

Baada ya mapumziko ya siku tatu niliamua kwenda Mlingotini kwa ajili ya kumsalimia mzee wa tiba.

Alifurahi sana akataka kujuwa kama nimepona, nikamuambia safari hii nimepona kabisa.

Wakati naingia pale Mlingotini niliona vitu vya ajabu ajabu (kwa macho yangu ya sasa) maana havionekani kwa macho ya kawaida, lakini niliuchuna nakujifanya sioni chochote.

Nikampa zawadi yake ya kiasi kidogo cha fedha na kuaga.

Siku iliyofuata nikaenda kwa Mwalimu Mwaloki, alifurahi na kuniombea dua kwamba, Mwenyezi Mungu azidi kunifungua niifuate iliyo kweli.

Siku hiyo hiyo nikaenda Kwa Sheik Mohamed na kumwambia kuwa alisema ukweli...

"Sheikh, hakika ulisema ukweli kuwa matibabu yangu yataanzia magharibi, lakini nadhani yameishia huko huko magharibi, mimi sasa nimepona... " Niliongea kwa kujiamini.

"Tunamshukuru Mwenyezi Mungu kama umepona, na kama itakuwa bado sasa njia itakuwa nyepesi, in shaa Allah tunaomba upate tahfifu" aliongea Sheikh kwa sauti yake nzito ile ya ki mwinyi mwinyi.

Nikampa hela kidogo akakataa akasema kaninunulie ubani, mtama na juzuu kwa ajili ya watoto. Basi nikakimbia dukani eneo la Gongoni na kununua vitabu na mahitaji aliyoniagoza kisha nikarudi na kumkabidhi.

Akanishika kichwa akaniombea dua...

"... (Tafsiri) Mwenyezi Mungu akuzidishie elimu na akuruzuku riziki yenye wasaa... "

Nikamshukuru pale, tukaagana kisha nikaeleka kwa mzee Zahiri.

Nikamkuta yupo katikati ya maombezi yake ya vingoma na wakina mama wakicheza na kutoa milio ya ajabu

Lakini nilivyoingia uwanjani tu pale wote wakatulia, kisha wakajipanga mstari na kuinamisha vichwa na kunisalimia " Assalaam aleikum yaa Shariff"

Tabibu Zahiri akawa anashangaa, mie nikajifanya sioni na kuendelea kuitikia salaam.

" Wa aleikum salaam yaaa ahl... " Nikasita kidogo.

Nikamgeukia Tabibu Zahiri na kumsalimia kwa unyenuekevu naye akaitikia.

Zoezi lake likawa kama limezimika hivi kwa muda, wale wamama wote walikaa kwa kutulia na kuinamisha vichwa.

Nikamshukuru kwa muongozo na kwamba alisema kweli mimi si wa upande ule bali wa kitabu, na Sheikh Mohamed amenisaidia...

Nilampa ujira wake akapokea na kuniambia kwa kuniuliza, mbona imekuwa hivi kulikoni?

Aliuliza akioneshea upande ule wa akina mama...

"Nikatoa fimbo yangu na kuwanyooshea wale akina mama na kusema

"Shatitu yaa mahulkatun..." Nikamaanisha tawanyikeni enyi viumbe wa Mwenyezi Mungu...

Mara wote pale wakalala chini kwa sekunde chache kisha wakaamka na kushangaa huku wakijikung'uta na kuuliza nini kimetokea.

Nikamwambia Tabibu Zahiri kuwa hao tayari wameshapona na hawatokuja tena hapa kwa ugonjwa huo wa kusababishwa na majini (mapepo).

Nikaaga nikaondoka huku Mzee Zahiri bado akiwa anajiuliza maswali.

Siku ukaishia hivyo.

Nikaanza kumtafuta Shariff mtoto bila mafanikio, nikaambiwa amenunua gari basi Isuzu hivyo zinamfanya awe bize nayo.

“Siku hizi yupo bize na chite ukae…” alisikia mmoja wa majirani.

Baada ya wiki mbili kuisha, nilimuaga Baba na Mama rasmi kuwa sasa naenda kuitumikia fani yangu mpya ya utabibu.

Wakanipa baraka zote na nikaenda kwa minajiri ya kuanza kufanya tiba kwa watu huku nikiendelea na kazi za baba.

Kituo cha kwanza kilikuwa pale Mkunguni na Livingstone nyumbani kwa ajili ya kuangalia kodi na kuchukuwa vitu vyangu kwa ajili ya makazi mapya nitakayo tafuta.

Nikakuta chumba kimeshapangishwa na nikapewa kodi yangu na vitu vyangu viliwekwa stoo.

Kwa hali niliyoikuta stoo sikupenda, nikamwambia yule mpangaji kiongozi kuwa pia vitu hivyo aviuze anitunzie hela yangu.

"Hivi basi nitavinunua mimi, nitajie ni kiasi gani.." alidakia haraka haraka.

Ok, hatuwezi kushindwana, nitarudi baada ya wiki moja unipatie kiasi fulani (nikamtajia pale)

Hakubisha, maana kilikuwa ni kiasi kidogo cha kawaida. Nikaondoka na kwenda lodge ya jirani.

Usiku ule niliazimia kwenda Pangani kwa yule Mganga kwenda kumshukuru kwa muongozo. Hivyo ilivyofika saa nane na nusu usiku nikafungua mlango wa lodge kisha nikaushindika (kuurudishia) na kuacha funguo mlangoni mimi nikiwa humo humo ndani ya lodge, Nikazima taa nikafanya yangu fyuuuu nikawa hewani, baada ya kutalii sehemu mbalimbali ilipokatibia saa kumi na moja nikatua jiurani na dispensary ya Kikokwe, nikawa kawaida nikaanza kutembea kwa miguu kuelekea nyumbani kwa Shariff.

Nyumba ya Shariff ilikuwa imejitenga kidogo na ilikuwa mwendo wa kama mwendo wa robo saa hivi kutoka pale zahanati.
**********

Itaendelea…

Ikiendelea nitag nimeipenda sana
 
2. MALARIA NA TIBA

Tulivyo anza kuona nchi kavu kwa mbali, nahodha aliamuru kibendera kipandishwe ili ile kama ishara ya maandalizi makubwa yanahitajika, wakati huo hatukuwa na simu, 'rediokol' wala vifaa vya kutuongoza zaidi ya ujuzi wa nahodha na mabaharia wengine kwa kutumia elimu ya nyota angani na uzoefu maeneo na miamba bahari.

Tulifika majira ya saa moja hivi asubuhi, maana muda mwingi tulitumia upepo kama nishati ya kutusafirisha kwa sehemu kubwa ya bahari tukiweka akiba petroli kwa dharura.

Mwinyi Mkila akiwa na wafanyakazi wake wengine walikuja kutupokea, wakiwemo 'bwana samaki' (afisa wa Serikali anayehusika na mali bahari), watu wengine wengi wakiwemo watoto wa rika tofauti maana ilikuwa ni siku ya Jumamosi.

Kwa mazingira ya pwani, ni kawaida ya watu kujaa wakati chombo kikiingia kutoka uvuvini, wengine kutafuta kitoweo, wengine kuchuuza na wengine kuburudisha macho tu.

Kwakuwa uvuvi ule ulikuwa ni maalumu, watu wa nje wigo wa Mwinyi Mkila walibaki kushuhudia tu kilichoendelea.

Kamba na kaji walipimwa kwenye mizani ili kupata idadi ya kilo zilizopatikana. Kaji huhifadhiwa peke yake na kamba peke yake kwenye matenga makubwa ambapo nyumbani tena hufungwa upya na kuwekewa barafu mpya tayari kwa safari ya kwenda Dar es Salaam alfajiri kwa kutumia mabasi ya SIKINDE na CHAMPSI MULJI.

Wale samaki wengine pia Mwinyi Mkila alipatana na wavuvi na kujuwa bei.

Baadhi ya wachuuzi waliomba wauziwe wale Jodari na Sehewa kwa ajili ya vitoweo, na ilifanyika hivyo.

Injini ilibebwa kwa toroli kurudishwa nyumbani, matenga ya samaki nayo vivyo hivyo. Mashua alikabidhiwa kijana mwingine ambaye hakwenda dagoni kwa ajili ya ukaguzi na kuiweka sehemu salama.

Wavuvi wote pamoja nami tulifika nyumbani salama na zoezi la kupewa ujira likaendelea.

Baada ya hilo zoezi wavuvi wote wakiwa na tabasamu walielekea kupumzika majumbani kwao, mimi nikabaki na baba huku akinidadisi uzoefu nilioupata huko dagoni.
****

Siku ilienda vyema na muda mwingi niliutumia kupumzika, lakini jua lilivyoanza kuzama tu nikaanza kusikia (kuhisi) baridi isiyo ya kawaida. Nilihisi homa maana tulivyokuwa dagoni tuliumwa na mbu pamoja na usubi ingawaje nyavu (mosquito net) za kuzuia mbu tulikuwa nazo.

Nilipewa panadol ili kujaribu kutuliza homa lakini kadri muda ukivyokuwa unakwenda ndivyo homa ikawa inazidi.

Baba aliamuru kaka yangu mkubwa anipeleke hospitali, hapakuwa mbali sana maana ni mwendo wa kutembea kiasi cha robo saa tu.

Nilifika hospitali giza likiwa limeshaingia nikiwa natetemeka sana, nikapelekwa kuonana na daktari wa zamu, akaniandikia kwenda kupima damu kwa ajili ya malaria na homa ya matumbo.
*****

Nilipata matibabu sawia na vipimo vilivyoonesha, sikuwa na malaira kali, ilionekana kwa mbaali tu (scanty) na sikuwa na homa ya matumbo wala maradhi mengine kwa mujibu wa vipimo.

Nilipewa dawa za kushusha homa pamoja na kuanzishiwa dozi ya klorokwini (chloroquine) kwa ajili ya kutibu malaria iliyoonekana kidogo.

Baada ya siku 3 nilipata nafuu kiasi, bahati nzuri sikuwa mvivu wa kumeza dawa, hata hizo klorokwini nilizimeza kwa kuweka kidonge kwenye ndizi mbivu ndogo na kupita kooni bila tatu hadi nilipo maliza dozi ya 4-4-2. Wakati mwingine pia nilitumia tonge la ugali kuweka dawa na kumeza.

Siku ya nne nikazidiwa tena, safari hii sikuwa na homa bali nilikuwa napata gumbizi mara kwa mara. Nikapelekwa tena hospitali na kupimwa wingi wa damu lakini nilikuwa na damu ya kutosha (13 na) hivyo daktari alishauri nipelekwe Muhimbili kwa ajili ya vipimo vya magonjwa ya moyo.
*****

Muhimbili walianza upya kunipima vipimo vyote muhimu lakini hawakuona ugonjwa wowote wa kuweza kunipa kuzunguzungu ninachojisikia.

Ikashauriwa nipimwe kipimo cha mionzi kwenye kichwa ili kuangalia kama kuna tofauti yoyote humo.

Vipimo vyote vilionesha nipo kawaida, lakini wakaamua kunitoa damu na kuipeleka maabara kwa ajili ya uchunguzi zaidi nikaambiwa majibu yatapatikana baada ya siku thelathini.
***

Ndani ya siku 30 za kusubiri majibu kutoka maabara nilikuwa napitia nyakati ngumu na za ajabu ajabu mara kizunguzungu, mara homa lakini havidumu sana kwa maana inakuwa kama homa ya vipindi.

Majibu yalikuja kuwa sina tatizo lolote, na ndipo daktari mmoja wakati wa 'clinic' akatushauri tujaribu dawa za mitishamba.

"Jaribuni kienyeji inawezekana huu siyo ugonjwa wa hospitalini" alisikika yule daktari mtu mzima hivi.

Pilika zikaanza sasa, baada ya kikao vya kifamilia Bagamoyo.

Katika kile kikao ndio nikaelezea kuwa wakati nipo dagoni nilipatwa na gumbizi na kuanguka na kupoteza fahamu.

Ikaamuliwa tuende kwa Zahiri aliyekuwa akiishi Mangesani.

Baada ya kuelezewa hali ilivyonitokea, atatuambia tuende siku ya alhamisi ambapo pia kuna wagonjwa wengine wengi watakuja siku hiyo ili kufanya tiba ya pamoja.

Zahiri (R.I.P) ni tabibu aliyekuwa akitibu maradhi yahusianayo na 'mashetani' ya kijini.

(Alikuwa maarufu sana Bagamoyo na alikuwa shabiki (mwanachama) wa Simba sports club. Mara nyingi Simba wakienda Bagamoyo lazima wafike kwake).

Siku ya alhamisi ilipowadia nilienda kwa Zahiri nikisindikizwa na kaka yangu mkubwa, wagonjwa tukatengwa peke yetu eneo la uani (kwenye uzio wa nyumba) uliozungushiwa kwa makuti, na wasindikizaji waliamriwa wakae pembeni lakini ndani ya uzio huo huo.

Maandalizi ya utabibu yakawa tayari nikaona vigoma (vyapuo) vikipigwa kwa mdundo wa aina yake mara wagonjwa ambao wengi wao walikuwa akina mama walianza kutikisa vichwa, mie nilikuwa dhahiri bila kupata athari za midundo hiyo.

Hali ya ngoma na kucheza iliendelea hadi wengine walianza kugalagala na wengine kuanza kuzungumza maneno yasiyoeleweka, kiarabu si kiarabu, kihindi si kihindi ilimradi vurugu ya mchanganyiko wa lugha, mie nikishuhudia yoye kwa macho.

Nashangaa siku hiyo sikupatwa na homa wa gumbizi badala yake nilikuwa nipo kawaida tu nikishuhudia yote yaliyokuwa yakiendelea.

Baada ya muda fulani kupita, Zahiri alimfuata mgojwa mmoja mmoja na kumshika sikio na kuzungumza sikioni mwa mgonjwa huyo kwa kiswahili na kiarabu.

Wagonjwa wengine walijibu, wengine walipiga kelele tu, wengine walikaa kimya, na alipofika kwangu akanishika sikio nikasisimka lakini nikarudi kawaida.

Alizungumza maneno mengi ya kiarabu na kiswahili lakini mie nilikiwa namuangalia tu.

Mwishowe akamuambia kaka kuwa turudi jumamosi kwa ajili ya tiba zaidi.

Hatukupewa dawa yoyote wala kuombwa pesa.
****

Jumamosi tulifika pale wagonjwa wachache maana wengi siku ya alhamisi walipatiwa dawa za kutumia.

Tukakuta kumeandaliwa sinia zenye vyakula vitamu vitamu vya aina mbalimbali ikiwemo tende, halua, peremende, ndizi mbivu (kisukari), sharubati nk.

"Leo ni siku ya 'chanu' maalum" alisema tabibu Zahiri.

Akashika kitabu na kusoma meneno ambayo sikuyaelewa na vigoma vidogo viaanza kupigwa huku yeye akiendelea kusoma maeno katika lugha isiyokuwa kiswahili wa kiarabu.

Wale wagonjwa wengine mara nikaona wanajongea kwa mitindo tofauti kwenye sinia za vyakula na kuanza kula, lakini mimi nilikuwa nimekaa tu kwenye jamvi pale chini huku nikiziangalia zile ndizi maana napendaGa sana ndizi.

Hali ile iliendelea na mara wale wagonjwa wakawa kawaida, wakapewa dawa zao za kutumia majumbani mwao ikiwemo dawa kama karatasi nyeupe iliyoandikwa maneno na namba za ajabu ajabu kwa wino kama wa rangi ya machungwa hivi (zafarani?) Kwa ajili ya kuloweka kwenye maji kwa ajili ya kunywa na mengine kuogea.

Wakaondoka wagonjwa wote nikabakia mimi na kaka.

Tabibu Zahiri akanisogelea, akaniangalia usoni kwa kunikazia macho na kuzungumza lugha mbalimbali lakini nilikuwa nimetulia tu.

Akachukuwa karatasi nyeupe na peni nyekundu akaanza kuandika andika kwenye karatasi mfano wa kuchora chora kisha akawa kama anakatakata aliyoyaandika na hatimaye akaja na kauli kwamba nipelekwe kwenye kitabu.

"Huyu si wa hapa, mpelekeni kwa Sheikh Mohamed"

Sheikh Mohamed (Allah amwie radhi) wakati huo alikuwa ni kiongozi mkubwa wa dini hapo Bagamoyo na alikuwa ana wanafunzi kutoka sehemu mbalimbali kwa ajili ya kuwafundisha elimu ya dini ya kiislamu.

Ilikuwa ni kawaida ya Sheikh Mohamed kukaa nje ya baraza yake kila siku asubuhi baada ya kuswali na kuendea kufanya ibada mbalimbali ikiwemo kupokea salamu za wapita njia.

Hivyo haikuwa vigumu kumpata Sheikh Mohamed kama alivyokusudia tabibu Zahiri.

Jumapili asubuhi mimi na kaka yangu tulifika nyumbani kwa Sheikh Mohamed si mbali sana kutoka kwa tabibu Zahiri ambapo ni umbali wa kuvuka barabara moja ya lami tu.

"Assalaam aleikum" tulimsalimia kwa pamoja

"Wa aleikum salaam, karibuni" alijibu kwa sauti yake nzito huku akituonyeaha sehemu ya kukaa kwenye kibaraza kando ya 'kiambaza' cha nyumba yake, maana dalili zote tulikuwa tunaonesha sisi siyo wa kusalimia na kupita.

"Sheikh tumekuja tuna shida, ndugu yangu huyu anasumbuliwa na maradhi tusiyoyajuwa..." Kaka alieleza historia nzima.

"Haya karibuni ndani" Sheikh alijibu huku akiinuka na kuelekea sebuleni ambapo kulikuwa na busati.

Wakati huo wote mimi nipo kawaida kabisa, sina dalili zozote za maradhi.

Baada ya utangulizi wa kaka, Sheikh akasema "al faat'ha"

Tukaanza kusoma sura ya ufunguzi kutoka kitabu cha Qur’an.

Hii sura waumini wote wa kiislam wanaijuwa maana ndiyo hutumika katika ibada ya swala mara kwa mara.

Baada ya kumaliza kusoma sura ya ufunguzi, akaanza kusoma yeye sura mbalimbali kwa ufupi ufupi na kwa haraka haraka sana, kisha akaagiza yaletwe maji kwenye bilauli akayasomea kisha akaniamuru niyanywe palepale.

Baada ya kunywa akasema turudi Jumatatu baada ya swala ya alasiri kwa ajili ya kisomo maalum.

Siku hazikuganda, Jumatatu ikafika na muda ukawadia tukaenda kwa Sheikh.

Tulivyofika alitukaribisha na kutuambia kuwa amefanya dua kisha akasema:-

“Maradhi haya ni ya bara huko, inabidi tiba aanzie huko”

Neno Bara kwa wakazi wa Pwani hulitumia kama vile kusema ‘mikoani’

Tukaangaliana na kaka pale kisha tukaaga na kuondoka.
***********

Inaendelea
Hongera Sana Ndugu JBourne, hakika unayoyaandika ndio uhalisia mtupu wa watu wa Bwagamoyo na ahughuli zao. Mkuu tafadhali endelea huu ni moja wa nyuzi ambao umenivuta kwa karibu sana. Ahsante
 
13. RASMI NAANZA UTABIBU

Tuliongea sana na Sheikh Shariff na kunisihi nizidishe ibada, maana nikijitakasa nafsi na kunyenyekea kwa Mwenyezi Mungu basi nitakuwa mtu mwenye karama nyingi. Hakufafanua zaidi lakini nilielewa kuwa sasa ni muda wa kuanza kufanya ibada mbali mbali maana hata kuswali tu nilikuwa mvivu yaani Ijumaa hadi Ijumaa na mwezi wa Ramadhani hadi mwezi wa Ramadhani na siku kuu za idi.

Akanikumbusha kuwa aliniandikia kikaratasi ili niwe nakisoma mara kwa mara…

“Niseme ukweli tu, baada ya kukariri yale maneno sikuwahi kuyasoma tena…” nilimjibu
Akasema, basi kuanzia sasa inabidi uwe unasema maneo yale kila baada ya swala ya asubuhi, kila baada ya al’asir na kila baada ya swala ya isha (usiku) pia usiku wa manane ukiweza kuamka. Baba, huyu pia sikumweleza kuhusu habari za ujinini, niliishia tu pale kwa mbirikimo.

Baada ya mazungumzo marefu na kupata nasaha mbalimbali nilimpa zawadi kulingana na mazingira yake, maana huwa hapendi hela. Kisha nikaaga na kuondoka ili nivuke upande wa pili wa mji ambako ndio kulikuwa kumechangamka zaidi. Nikachukuwa lodge ili ikifika usiku wa manane iwe flying point yangu huku nikiacha mlango wa lodge bila kufunga na funguo.

Nilijitafakari sana kuhusu uhusiano wangu na Mwenyezi Mungu na hali yangu ya nusu mtu nusu jinni na nadhiri ya mama kuwa nitumtumikie Mwenyezi Mungu, hatimaye nikadhamiria sasa nirudi Dar na kufanya kazi ya kumtumikia Mungu kwa kutibu watu.

Asubuhi nilishukia maeneo ya Ilala jirani na Msikiti wa Arusha, nikajikuta hamu ya kwenda kufanya ibada mle msikitini inanijia, nikaingia nikafanya ibada zangu za awali na humo ndani niliwakuta watu wawili wapo na ibada zao kadhaa maana muda wa swala ya pamoja ulikuwa bado. Baada ya swala ya pamoja tulipeana mikono karibia waumini wote mle ndani na kuanza kutawanyika muda ambao tayari miale ya jua lilikuwa imeanza kuchomoza.

Nikawa nazunguka kwa miguu mtaani huku nifanya ibada ya tasbihi (kama rozali wa wakristo) lakini bila kuwa na hiyo tasbihi, na mara nikakumbuka kuhusu yale maneno kutoka kwa Shariff wa Kikokwe…, sehemu ya maneno hayo (dua) ilikuwa inasema “…Rabbi zidni ilman wa ruzqkni fahma…” yani “Ewe Mola wangu unizidishie elimu na uniruzuku...”, nikawa naendelea kusema maneno hayo hatimaye nikaona sehemu kuna gari aina ya Isuzu canter inapakia mizigo, nikasogea pale huku nikiwa na begi langu dogo la begani na kumuuliza dereva ambaye alikuwa kwenye gari…

“… anahama huyu anaenda mkoa, hivyo namkusanyia vitu vyake napeleka Mgulani kuna lori la kumsafirisha, ni mjeshi…” alisema yule dereva.

Mara moja nikabisha hodi na kuingia na kumuuliza anayehama kama upande mzima aliokuwa anakaa kumepata mpangaji.

“…nadhani bado, maana order nilipokea usiku na leo kuna usafiri wa bure basi imenibidi usiku mzima nifanye kazi ya kufungasha na kumuaga mwenye nyumba, sidhani kama tayari ameshapata mtu wa kuingia…” alijibu yule mpangaji huku akiendelea kusaidiana na waliokuja kumsaidia, nadhani ni kutoka kwenye hiyo kenta.

Nikajikuta nimepata vyumba (sehemu ya kuanzia maisha ya uganga).

Usafi ulifanyika baada ya kukabidhiwa vyumba kwa kushirikiana na vijana hapo mtaani, nikaomba pia vyumba vyangu vyote vipakwe rangi na pia nikabadilisha vitasa, nikaweka nyavu mpya madirishani nk vyote hivyo kwa gaharama zangu.

Kuna kitu sijakwambia baba (alisema Pazi), ni kwamba kila nikiwa na shida ya dharura basi nikiingiza mkono kwenye ile rasketi (ambayo sasa ipo ndani ya mkoba) nakuta kibunda cha hela kulingana na mahitaji, kama itazidi basi ni kidogo sana. Hata shangazi siku ile nilivyomwambia kuwa wasihofie kuhusu hela kwisha, tayari niliona jambo hili la ajabu likinitokea, kwa mara ya kwanza wakati namrudishia hela zilizobaki yule Ustadhi wa Kabwe.

Baada ya siku tatu nilihamia pale Ilala kwenye nyumba niliyopanaga (upande mzima, chumba sebule chumba na chumba kingine kikijitegemea). Niliweka ndani Kitanda na godoro kutoka Keko, kochi moja la chumbani, sebuleni palikuwa na zuria la kijana tupu na mito ya kuegemea, chumba kingine niliweka godoro pana la futi sita kwa sita wakati chumba ambacho nilidhamiria kulala niliweka la futi nne na nusu. Kile chumba cha peke yake nikaweka kapeti laini la plastiki, nikaweka na kiti cha mbao cha kawaida. Niliazimia hiki chumba ndio kiwe cha kutibia wateja.

Nikawataarifu nyumbani Bagamoyo kuwa nipo salama na nimepanga Ilala hivyo naweza kuendelea kumsaidia mzee kazi zake za feri baada ya kipindi kirefu cha matibabu.

Niliendelea kumsaidia baba kwa zaidi ya mwezi bila kupata mgonjwa wa kumtibu, huku ratiba yangu ikiwa imekabiliwa na vipindi vya ibada za pamoja misikitini.

Siku moja jioni nyumba hiyo hiyo ninayokaa ambapo mwenye nyumba na familia yake wanakaa upande mmoja na wapangaji wengine kadhaa wanakaa ‘mabanda ya uani’ (vilikuwa vyumba vizuri tu na siyo mabanda kama ilivyozoeleka kuitwa) kuna dada mmoja alipandisha mashetani (alipagawa, alipatwa na mapepo) akwa anagalagala huku wapangaji wakimzunguka wasijue la kufanya zaidi ya kumsitiri kwa kumfunika khanga…

“Kamwiteni Maalim Juma aje kumuombea…” alisikika baba mwenye nyumba akimwambia mtoto wake mmoja wa kiume…

Baada ya dakika mbili tatu hivi yule mtoto akarudi na kumjibu baba yake kuwa “…hayupo, ametoka…”

“Kwani anasumbuliwa na nini…” niliuliza maana nami nikawa mmoja wa washuhudiaji…

“…huyu huwa ana maruhani, yanamsumbua kama nini, mara kwa mara yanamgalagaza…” alijibu mmoja wa wapangaji ambaye alionekana akimuonea huruma.

Wakati huo yule dada aliyeanguka pale chini alikuwa ametulia kimyaaa kama vile amezimia, wakati tukiendelea kushangaa pale mara ghafla akaingia mtu ambaye ndio nikajuwa kuwa ni maalim Juma na akaanza kumsomea rukiya

(Ruqia ni maombezi maalumu ya kimatibabu, ni mchanganyiko wa aya mbali mbali za qur’an katika mpangilio maalum kwa ajili hiyo)

Baada ya dakika kadhaa yule dada akaamka na kukaa na kushangaa jinsi umati ulivyo mzunguka na kuuliza… “…imenitokea tena!!!?...”

Baada ya yule dada kuwa sawa na watu wakawa wanaendelea na shughuli zao nikamfuata yule baba mwenye nyumba na kumwambia, mimi naweza kumtibu huyo dada na yasirudie tena maruhani yake.

“Mimi tangia siku ya kwanza nakuona nilidhania wewe ni mganga kutokana muonekano wako lakini cha ajabu zaidi ya mwezi sikuoni ukifanya uganga wako ama wateja wakija au kuna ofisi sehemu unafanyia uganga huo? Maana naona tu unatoka na kurudi…” alisema yule mwenye nyumba

“Hapana baba, nikitoka huwa naenda feri kufanya kazi za samaki, baba yangu ni mchuuzi hivyo huleta samaki feri nami humsaidia katika kuuza…” niliweka koma kisha nikaendelea…

“Ni kweli mimi ni mganga, lakini sijaanza rasmi kazi, nafikiri kwa huyu dada itakuwa ndio naanza sasa” Nikamaliza

“Basi ngoja nikamwite…” alisema na kuondoka.

Punde si punde wakaja wadada wawili na mzee pale sebuleni kwangu…

“Hodi…” alibisha mwenye nyumba
“Karibuni…” nilijibu kwa maana tayari nilijuwa kuwa hayupo peke yake.

Mwenye nyumba akatoa historia fupi ya yule dada…

“… ana zaidi ya mika miwili hapa huyu na karibu kila mwezi hali hii inamtokea mara moja au mara mbili….” Alisema.

Nikawaambia basi tuingie chumba hicho cha peke yake ili nimsikilize…, tukanyanyuka wote pale na kuingia chumba chenye kapeti laini ya plastiki.

“Enhe, nielezee ilikuwaje….” Nilimuuliza yule dada mbele ya mpangaji mwenzie na baba mwenye nyumba.

Akasema kuna siku alichelewa kutoka matembezini akarudi usiku mwingi maeneo ya Boma (Ilala) akapigwa na kama upepo wa baridi kali kisha akapata kizunguzungu lakini alieweza kutembea akiwa na marafiki zake hadi walipoachana jirani na hapa nyumbani maana walikuwa wanakaa mitaa ya jirani.

“…Tangia siku hiyo ikawa inanitokea hali ya ubaridi na kuanguka na kutojuwa kinachoendelea kwa muda kadhaa…” alisema yule dada.

“Nimehangaika sana kwa waganga hadi sasa nimechoka, angalau nikisomewa na yule Maalim ndio kidogo napata unafuu lakini haipiti mwezi lazima itanitokea tena…” alisema.

“Kaka msaidie huyu, anapata tabu kweli…” alidakia yule dada mwingine.

Wakati naendelea kutafakari jinsi ya kwenda chumbani kuchukuwa fimbo yangu, ikaja kama video hivi ikionesha jinsi tukio zima lilivyomtokea miezi ishirini na saba iliyopita.

Niliona kweli alikuwa na marafiki zake wane, wote wakiwa wana hali ya ulevi, wote wakiwa na hali ya kuwa na janaba walimtukana kijana mmoja aliyewasalimia pale jirani na Boma lakini wao wakamporomoshea matusi kwamba hana kitu aachane na wao…

Janaba tafsiri isiyo pana ni ile hali inayompata mtu mwanamume akitokwa na manii (mbegu za kiume) au mtu mwanamke akifika mshido kwa kufanya tendo la ndoa ama kuota tu akiwa amelala, ama kwa kujichua mwenyewe ama kuchuliwa ama tupu zao zikigusana na tupu za jinsia moja ama tofauti.


Nikainuka fasta na kwenda chumbani kuchukuwa fimbo na kurudi. Niliwakuta wote watatu wakiwa wametulia kimyaa wakisubira nini kitaendelea.

Nilivyoingia na ile fimbo tu yule dada mgonjwa ghafla akainamisha kichwa, akanyoosha miguu kwa mbele na kuibana, yule dada aliyekuja naye akamfunika khanga kichwani maana alikuwa amejifunga kilemba tu cha kawaida.

“inataka kumtokea tena…” alisikika yule dada akisema

Nikanyoosha ile fimbo kumuelekezea na kusema…

“…Atrukuha washanuha ayuha al makhluq al maloon…” nikimaanisha kwa tafsiri isiyo ya moja kwa moja “toka awe pepo uliye laaniwa...!!!”

Yule dada mgonjwa alianguka akatulia tuli…

Baba mwenye nyumba akawa ananiangalia na yule dada akamfunika vizuri yule mgonjwa.

Kabla sijasema neno lingine yule mgonjwa aliamka na kukaa na kuanza kujinyoosha.

“Huyu mwenzako…(nilianza kusema huku nikimuelekea yule dada msindikizaji) alipatwa na upepo mbaya siku hiyo aliyosema kuwa alikuwa anatoka matembezini. Walikuwa wapo wane, lakini wewe hukuwepo (nilimwambia yule dada), wote walikuwa wamelewa na walitoka kufanya zinaa. Lakini pia walimtukana mtu wasiye mjua, yule waliye mtukana alikuwa ni Jinni, Jinni miongoni mwa majini waasi naye alikuwa katika matembezi yake. Hivyo aliona amkomeshe huyu dada kwa kuwa yeye ndiye aliye poromosha matuzi wakati wenzake waliishia tu kusema maneno ya kawaida.” Nikatulia.

Kisha nikamgeukia mwenye nyumba na kumwambia, tayari huyu amepona, haitorudia tena hali inayompataga. Halafu nikamwangalia yule mgonjwa ambaye sasa alikuwa na sura ya kawaida, nikamwambia kuwa, “Dada umepona, lakini acha maasi unayofanyaga karibu kila siku, badala yake tafuta jambo lingine litakalo kuingizia kipato…, sasa mnaweza kwenda” Nilimaliza.

“Shilingi ngapi kaka gharama za matibabu? “aliuliza yule msindikizaji

Nikawaza, sijui niwaagize walete kuku nami nilipize yaliyonikuta ya kulishwa vimiguu na virigisi… lakini sauti nyingine ikaniambi acha ujinga, kama hela mbona unapata…

“Nendeni tu, toeni sadaka huko mnapofanyia ibada” nilijibu huku wakiwa hawaamini macho yao.

Yule mwenye nyumba akasema…

“Nikiona hayajamrudia hadi miezi mitatu, ndio nitajuwa kweli amepona, na nitakuletea watu wengi wanaosumbuliwa na matatizo kama haya.

“Sawa baba” nilijibu huku nami nikitoka na kufunga ule mlango na kuingia sebuleni kwangu.

Usiku ule nikaota nipo tena kule Ujinini, nikaambiwa kuwa nimefanya vizuri kuanza kazi rasmi, lakini kwa kuwa mimi siyo 100% jinni, basi nikapewa pete mbili moja ina kito chekundu na nyingine ni ya kawaida ila ina maandishi yaliyoandikwa ibn Shariff ambapo nilielekezwa yenye kito nivae kwenye kidole cha upande wa mkono wa kulia kitakachotosha na nyingine kidole cha upande wa mkono wa kushoto ili niweze kufanya matibabu kirahisi na mawasiliano ya moja kwa moja kutokea ujinini kwa ajili ya rufaa.

Alfajiri nilipoamka kweli nikakuta pete kwenye kochi kama nilivyoota. Nikajuwa hii haikuwa ndoto bali nilichukuliwa hadi huko ujinini. Nikazivaana zote zilifiti vidole vya katikati. Nilipo fungua begi langu nikakuta kuna kanzu nyingine tatu nimeletewa na ile ya awali haipo, zilikuwa za rangi tofauti, nyeupe, bluu na khaki hivi zote zikiwa zimekamilika kwa suruali zake na kofia zake ambazo ni nadra sana kuziona madukani , zilikuwa kofia kama za kumimina hivi, hazina maungio ama mshono.

Baada ya miezi mitatu wagonjwa wakaanza kuja, nikawa nawatibia bure hadi baada ya miezi mitatu mingine kuisha ndipo nikaambiwa na sauti za usiku kuwa nianze kutoza hela lakini kwa kila mgonjwa atakavyoguswa (yaani nisitaje kiwango)

Wateja wakawa wananipatia hela nyingi sana kiasi kwamba hazikufaa tena kuzihifadhi ndani ya nyumba, nikafungua akaunti benki ya posta.

Niliendelea kutibu watu wengi, nikawa maarufu, sehemu ikawa haitoshi, nikahamia Mbezi beach ambako nilipanga na hatimaye nikapata kiwanja hapa nilipojenga.

Muda huo tayari alfajiri ilishaingia hivyo tukaswali pamoja kisha tukajipumzisha hadi nilivyokuja kuamshwa kwa kugongewa mlango ikiwa tayari saa tatu kasoro asubuhi. Nikapiga simu nyumbani kuwajulia hali, Hamida mke wangu alikuwa amenuna lakini nikamwambia nitaenda kumuhadithia kilichonifanya nisiende nyumbani, lakini nilimgusia kuwa niko nyumbani kwa Pazi mtoto wa mzee Mwinyi Mkila.

“Assalaam aleikum baba, pole sana kwa uchovu, haya jiandae tuje tupate kifungua kinywa…” alisema Pazi akiwa nje ya mlango.

Baada ya kifungua kinywa alimwita mke wake na watoto wake maana ilikuwa siku ya Jumamosi.

“Huyu ndiye mke wangu aitwaye Behati binti Mdigo, na hawa ni watoto wangu huyu anaitwa Suleyha na mdogo wake anaitwa Abuubakar pia kuna mdogo wao amabye bado ni mchanga amelala, yeye anaitwa Subira.” Alinitambulisha familia yake pale kisha wakaondoka sisi tukarudi sebuleni na kuendelea kupata kisa…

Basi bwana, nilitibu kule Mbezi beach, watu aina tofauti tofauti, wenye mia tano, wenye elfu moja, wasio na hela wenye hela , na wengine walirudi kutoa shukrani kwa kunipatia hela nyingi sana na ndizo zikanifanya niweze kujenga nyumba nzuri hii ambayo nilitaka uione.

Tiba yangu iliegemea kwenye watu wenye matatizo yahusishayo uchawi na mambo ya majini, wateja wengine ambao hawakuwa wa kada hiyo nilikuwa nawaambia wazi kuwa fani hiyo sina wajaribu kwingine, jambo lililoniongezea sana wateja kwani waliniona ni mkweli na wala sikuwa wa gharama maana walikuwa ‘wanajinyonga wenyewe’, yaani wanajikadiria malipo wenyewe kulingana na uzito wa ugonjwa na namna walivyoteseka katika kujitibu kabla ya kufika kwangu.

Katika harakati za kutibu wagonjwa ndipo siku moja alikuja binti wa miaka kumi na nane hivi naye akisumbuliwa ugonjwa wa kuanguka.

Kwa historia aliyoeleza mama yake ambaye alimtela kutoka kwao Kiwalani Dar es Salaam, alisema…

“Alianza kupata kuzunguzungu mara tu alivyovunja ungo miaka kama mine iliyopita, basi tukajuwa huyu ukubwa wake umemjia kwa namna hii, lakini hali ilivyozidi ndio tukaanza kuhangaika kwa walimu mbali mbali kwa ajili ya tiba…”

“Kasomemewa huyu, kafushwa huyu, kanywa makombe kadha wa kadha, kachanjwa huyu hadi tumekata tamaa…” alilalamika yule mama Behat.

“Hebu mlete chumba hiki…” nilisimama na kumuambia yule mama amlete binti yake chumba kingine ambacho kilikuwa kitanda na bafu.

“Kamuogeshe mwanao kisha subiri hadi maji yakauke yenyewe ndipo umfunge khanga hizi” nilisema na kuwaonesha khanga kisha nikashindika mlango na kutoka kuwahudumia wateja wengine, wao nikawaacha humo.

Siku hiyo ilikuwa ya Alhamisi nakumbuka, wateja walikuwa si wengi hivyo niliwamaliza mapema.

Nikarudi kule chumbani nilipowaacha mama na bintiye na kubisha hodi…

“Karibu, fungua mlango umeshindikwa tu huo…” alijibu yule mama.

Nikamwambia mama, “…sasa saa ya tiba imefika, mpakate mwanao…” nikachukuwa fimbo yangu na kumnyooshea na kutamka maneno ya kumfukuza pepo…”

Yule binti alipiga kelele na sauti ikasikika akisema “…hatutoki, tupo wengi... hatutoki…”

Nikamnyooshea tena fimbo mara kadhaa na hatimaye alitulia, lakini roho ikaniambia kuwa huyu bado, sijaweza vizuri ngoja niombe msaada kutoka ujinini.
**********

Itaendelea…
 
7. KUVUKA ZIWA TANGANYIKA

Alfajiri tulikisia vishindo vishindo vya mtu kurudi, lakini hatukuamka hadi palivyokucha kabisa. Tulivyopata staftahi tuliendelea na mazungumzo ya kawaida na mke wa Ustadhi wakati tukisubiri Ustadhi mwenyewe aamke maana alikesha safarini.

Majira ya saa tano na nusu hivi asubuhi Ustadhi alitoka nje na kuja kutusabahi.

“Assalaam aleikum, habari za huko mtokako, poleni kwa safari na karibuni sana Kabwe” alitusalimia salamu ndefu.

Tuliitikia kwa pamoja na kisha akaomba aletewe chai pale nje huku akianza sasa kuongeza na sisi kwa kutusikiliza.

Kama kawaida Shangali alianza kumuelezea sababu ya safari yetu kwake, kwamba atusaidie ili tuweze kufika huko upande wa pili na wala hatupajui wapi hasa tunapotakiwa kwenda. Alimpa salamu kutoka kwa mzee Njembi…

“Alituambia tukikuona wewe basi safari yetu itakuwa salama na tutafika tuendako” alimalizia Shangazi.

“Sawa karibuni, wa aleikum salaam wa rahmatullah wa barakatu” aliitikia salam ya kutoka kwa mzee Njembi.

“Aaah ni kweli mimi nina chombo changu ambacho nakiendesha mwenyewe, na kazi yangu kubwa ni kupeleka matufa ya wateja wangu upande wa pili. Napeleka petroli, dizeli na wakati mwingine mafuta ya kula na ya kujipaka”

“Ni kazi ambayo nimeifanya kwa muda mrefu tangia kijana mdogo nilipokuja huku kutafuta maisha kutokea Irangi Kondoa”

“Kwa uzoefu nilionao ndiyo maana mzee Njembi ameniamini sana hata katika kumsaidia katika mambo yake mengine binafsi. Nilifahamiana na mzee Njembi siku chache tu baada ya kukabidhiwa chombo niwe nahodha kamili”

“kabla ya hapo nilikuwa nahodha msaidizi lakini kwa bahati nzuri tajiri mwenye chombo alinunua boti nyingine ya kisasa hivyo yule nahodha akapewa chombo kipya nami nikapewa chombo cha zamani”

“Sasa kumbe nisijuwe kuna baadhi ya watu wenyeji wa hapa hawakupenda mimi nipewe kile chombo badala yake wapewe watoto wao. Kwa sababu hiyo nilisumbuliwa sana na mauzauza ya kienyeji hapa, japokuwa nami niliaga kwetu Kondoa lakini haikufua dafu, ikabidi nianze kutafuta msaada”

“Katika kuhangaika kwangu ndipo nikakutana na Mzee Njembi kule Ujiji, hakika alinisaidia sana kiasi kwamba nilivyorudi nilifanya kazi vizuri tena kwa ufanisi na bila bughuza zozote kama za mwanzo licha ya majaribio yao kadhaa ambapo matokeo yalikuwa yanarudi kwao”

“Watu wakaanza kuniita ustadhi ustadhi, kumbe walisemezana wao kwa wao kuwa wamemchezea ustadhi sasa mambo yao hayaendi, na uaslama wao ukawa baada ya kuacha kunisumbua” Alisema kwa kirefu Ustadhi.

“Jina langu halisi ni Muharami bin Said ibn Kassim Chavai, lakini ukiulizia Muharami mji huu huwezi kunipata, we sema ustadhi tu, kila mtu hapa ananijuwa”

“Hebu fikiria, usiku mnalala asubuhi mnajikuta mpo nje barazani mmelala! Siku nyingine mnajikuta ufukweni kabisa mwa ziwa miguu ikiwa inagusa maji kidogo! Siku nyingine wote mkiamka mnakuta mmechanjwa mchirizi mmoja mgongni au kifuani, mchirizi mrefu lazima uuone au mwenzako auone! Siku nyingine unapotea tu ziwani hufika bandarini hadi unaishiwa mafuta uliyopanga kutumia! Siku nyingine unakutana na dhoruba isiyo na kichwa wala miguu yani unashangaa ghafla tu wimbi hili hapa tena mengine yanakuja dadodabo (double double)” Alituambia na kuendelea…

“Hebu niambie, wewe ungefanyeje!” aliuliza. Sisi hatukujibu kitu.

“Nilijaribu kutumia njia ninazozijuwa weee lakini haikuwezekana, nimezunguka Rukwa ya Mpanda, Rukwa ya Upimbwe, Rukwa ya Sumbawanga, Rukwa ya Unyika (siyo Unyiha), Rukwa ya Laela hadi sehemu iitwayo Mkutano jirani na Kijiji cha wachawi sikufanikiwa, maana ilikuwa inaoneka kama wote ni timu moja tu ndipo nikaanza kuhangaika kutafuta msaada nje ya mkoa huu wa Rukwa.” Alimalizizia chai yake kisha akaendelea…; wakatu huo sisi tupo kimya tu tunasikiliza na kujifunza kumbe siye Pazi tu anayehangaika kutafuta kwa tabu.

“Nikaenda Kusini Mtwara jirani na Msumbiji, kule yule bibi akaniambia nimepata tabu bure kwenda huko, nigeuze niende Kigoma Ujiji pale wanapawezea Rukwa” Alisema.

Hapa sasa nikaendelea kujifunza kumbe mambo haya ya nguvu za giza zina madaraja, mipaka, mamlaka na utimu. Ama kweli unaweza ukaishi duniani na usijuwe chochote kinachoendelea katika mambo ya nguvu za giza. Vitu vinatisha sana. Nikakumbuka jinsi nilivyo pelekwa mzimuni kule Handeni na kuzungumza na viumbe visivyoonekana lakini kwa kupitia vinywa wa watoto! Sita kaa nisahau.

“Kwa mzee Njembi nilipikwa kwenye chungu cha maji moto yasiyounguza na kutengenezewa ulinzi kwa kadri mahitaji yangu yalivyokuwa na kushida majaribu ya kutisha kutoka kwa ulinzi huo, hatimaye nikawa salama na hadi leo wananiita ustadhi, siyo kwa mazuri bali kwa shughuli waipatayo pindi wakiazimia kunifanyia ubaya.” Alisema.

“Kazi zangu zilienda vizuri hadi miaka michache iliyopita nikanunua chombo changu binafsi na ndipo mzee Njembi akaanza kunitumia kumchukulia miti shamba (dawa) kutoka Zaire. Bahati mbaya ng’ambo huko kuna hatari sana ya usalama, hakuna usalama kabisa, ukienda ukirudi unamshukuru Mungu, maana unaweza kutekwa njiani na waasi wa jeshi lao huko, unaweza kutekwa na maharamia tu humuhumu na kudhulumu mali yote ili mradi usalama siyo wa uhakika huko hata njiani (ziwani)” alisema.

“Kuna siku wakati nafanya kazi zangu za usaidizi wa nahodha, niliwahi kupakia abiria kutoka ng’ambo na kuwapeleka Kigoma, walikuwa wageni kabisa, nikawafanyia ukarimu wa kuwasaidia katika mambo waliyoijia na kuhakikishia usalama wa mizigo yao njiani ziwani, baada ya kufika na wakati wa kurudi na sikuwadai ujira wowote wa ziada kwa usaidizi niliowafanyia.”

“Kumbe wale jamaa walikuwa wanajeshi waasi huko ng’ambo, mimi sikujuwa hadi siku moja chombo chetu kilipotekwa njiani na kupelekwa ng’ambo, wakachukuwa mali zote, mimi na nahodhwa wangu tukapelekwa kambini”

“Sasa alipokuja yule mkubwa wapo pale akaniangaliaaa, kisha akasema tupelekwe ofisini kwake, nikashangaa tunahudumiwa chakula kizuri na kupewa sehemu ya kulala pazuri. Pazuri kwa maana ya kwamba kuna hema na blangeti lililotandikwa kama kitanda. Katikati ya usiku akaja yule mkubwa wako bado akiwa amevalia magwanda yao ya jeshi na minyota nyota yake iliyo kaa vibaya, akaniita na kuniambia…”

“Mmesalimika kwa kuwa nimekutambua, wewe ni kijana mwema sana, kuna siku ulinisaidi sana. Akajitambulisha vizuri nikamkumbuka. Akaniambia atakuja kunitorosha, ameshawatuma wafuasi wake wakaniwekee pipa moja la dizeli kwenye boti na magunia, alituambia ikifika usiku wa manane atatuma askari aje atuongoze hadi kwenye boti yetu”

“Kweli usiku ule ule alikuja askari akatupa ishara ya kuwa tumfuate, tulitembea kwa kunyata hadi tulipofika ilipoegeshwa boti, akayaloweka yale magunia na kufunika injini ya boti ili isitoe mlio mkubwa ili tutoroke. Pia alituambia tupitie njia nyingine maana ile ya kawaida bado wanajeshi wanafanya doria zao za kuteka mali ili wapate kuishi huko msituni”

“Tuliwasha boti na kuondoka kwa kuelekea kaskazini kwa muda kadhaa kisha ndio tukafuata njia ya kenda uelekeo wa bandari ya Kigoma. Lakini kwa kuwa ilikuwa usiku wa giza totolo na pasipo mwezi wala nyota maana ilikuwa msimu ya mvua tukajikuta tumepotea palipo pambazuka na kuona tupo uelekeo wa hifadhi ya Jeshi letu (JW).”

“Mara tukasikia milio ya risasi na sauti kwenye spika ikituamuru tusalimu amri, tulizima injini na kusimama na kunyoosha mikono juu, kuna boti mbizi za jeshi za doria (fibre boats) zilituzingira wakiwa na silaha nzito huku mwanjeshi mmoja akiongea na simu ya upepo.”

“Sauti ya amri ikatoka kwenye boti moja” “Jitambulisheni, ninyi ni akina nani na mnatoka wapi na mnaelekea wapi?!”

“Sisi ni watanzania, sisi ni watanzania…” tulijitetea,

“Watanzania! Mbona mna boti ya waasi!” alisikika mmoja wa wale wanajeshi. Kuangalia hivi kwenye jina la boti yetu nikaona kumeandikwa BANA SUDI KIVU kwa maandishi mekundu. Kumbe tayari kule wale waasi walishajimilikisha, isingekuwa yule mkuu wao, sijui tungekuwa na hali gani”

“Sisi ni watanzania, mimi ni mfipa na mwenzangu ni mrangi” alijitetea nahodha wangu.

“Bahati nzuri kule kwenye boti ya JW kulikuwa na Msandawe, hivyo alikuwa anakijuwa kwa kubabaisha kirangi na pia alikuwepo Mpimbwe ambaye pia alikuwa anaelewa kifipa”

“Abari ja mutondo!” alisema yule mjeshi huku akituangalia, haraka haraka nikajibu “jaboa”,

“Akasema tena ikiana!”

Nikajibu fasta “anga!” hii ilikuwa kisandawe.

Urangi na Usandawe ni jirani hivyo kwa kiasi fulani unaweza kujuwa baadhi ya maneno ya lugha nyingine. Mara akadakia mjeshi mwingine “Mwalalauli” yule mwenzangu akajibu “Eenditaa!”, japo alichapia lakini ilieleweka kuwa kweli kwa hatua ya kwanza inawezekana kuwa sisi ni watanzania.”

“Tukaelekezwa kuongoza hadi nchi kavu ambako kila tulivyokuwa tunakaribia tukawa tunawaona wanajeshi wakiwa wamekaa tayari kwa mashambulizi kutushambulia”

“Tukafika nchi kavu, tukapelekwa msobe msobe hadi sehemu kavu na kuamriwa kukaa chini”

“Baada ya mahojiano pale kweli wakathibitisha kuwa sisi ni watanzania na tulitekwa, tukapewa usindikizwaji hadi tulivyotoka nje ya eneo leo, lakini walifuta yale maadishi kwa rangi nyeusi”

“Tulifika Kabwe tukiwa hatuamini macho yetu”

“Sasa katika safari zetu zilizofuata za kawaida, kuna siku tukakuta na yule mkuu wa waasi akiwa kiraia pale bandarini ng’ambo kwao, akaifuata boti yetu na kuja kutusalimia kirafiki. Akaniambia, siku nyingine nikienda niseme maneno (ambayo alinitajia) kwa mtu yoyote anayeonekana kama askari nitakuwa salama na nitafikishwa kwake”

“Kwa kupitia huyo mkuu wa waasi, nikapata uchochoro sasa wa kufanya niashara kwa uhuru maeneo hayo na kuanza kupata mafanikio hadi bosi wetu akanunua boti nyingine mpya nami nikaachiwa ya zamani hadi nikanunua boti yangu ambayo ninayo hadi leo”

“Ni boti yangu tu inaweza kutembea mwambao wote wa ng’ambo bila matatizo, ndiyo maana Mzee Njembi alikuambieni mnitafute mimi. Na hata huko msituni kwa mbirikimo nitakupelekeni maana huko ndiyo safari ya huyu kijana ilipo” akaniangalia kisha akawaangalia wenzangu.

“Lakini nasikitika, ninyi safari yetu itaishia hapa, hamuwezi kwenda kule, mtakaa hapa hadi nirudi nije nikupeni habari za ndugu yenu” alimaliza na kutulia.

Tukabaki tunatizamana pale kwa mshangao!

“Sasa ikakuwaje huyo kwenda peke yake wakati hali yake inabadilika badilika, nani atamsaidia?” mama alihoji.

“Mama wala usiwe na wasiwasi, kule mambo ni mengi, mkienda wote kutakuwa na uzito sana wa safari, niaminini mimi, muaminini mzee Njembi” alimaliza na kuingia ndani akatuacha kujidaliana.

Tulijadiliana weee na tukakubaliana akija tumwambie kaka anisindikize, Shangazi na Mama wanisubiri. Basi baada ya muda kupita alirudi na kutuuliza tumefikia muafaka gani.

Ustadhi alikuwa ni mtu wa makamo, ni mmoja wa wale warangi wenye ngozi nyeusi, mwembamba mrefu na mchapa kazi. Baadaye nilikuja kujuwa kuwa alianza shughuli za uvuvi katika bonde la Rukwa kwenye Ziwa Rukwa na hali ya mavuno ilipokuwa ngumu ndipo akaenda Ziwa Tanganyika na kuanza kazi za ubaharia, unahodha usaidizi hadi sasa amekuwa nahodha mahiri.

“Tumeamua kaka yake amsindikize” alijibu shangazi.

“Hapana, haitowezekana, najuwa kwanza hapo ninyi hayupo mwenye makarasi ya kuvukia (passport) wala kadi ya homa ya manjano, sasa huyu atasumbuliwa sana na askari wa kule na wanapenda rushwa balaa, wenyewe wanaita ‘makuta’, chukueni ushauri wangu, huyu kijana niachieni mimi, atarudi salama in shaa Allah” alisema.

Wote pale tukaangaliana, na kisha kaka akasema, “duu tulisahau kuwa tunataka kwenda nchi nyingine, maana pia kuna ishu ya visa na kulipia kwa dola (dollar), vyote hivyo hatuna”

“Kuhusu viza (visa) kama ungekuwa na passport hata ile ya karatasi tungeweza kugonga wakati wa kuingia, lakini ni vyema ninyi mkabaki hapa nami nitarudi na mwanenu salama.” Alijibu Ustadhi.

Siku ikaishia hivyo na tukapanga kesho yake usiku safari ianze. Boti ilipakiwa mapika ya dizeli na petrol kutoka kwa wateja tayari kwa safari. Kwa kuwa sikuwa mgeni wa safri za kwenye maji sikuwa na hofu.

Baada ya chakula cha jioni, nikachukuwa rasket (kibegi kidogo kilaini cha kufaa mgongoni au begani) yangu, na suruali yangu moja tu ya savco jeans, na nilivaa mtumba wa jeans ya levi’s straus na tshirt ya mtumba ya rangirangi, kwenye rasket kulikuwa na tshirts mbili za ziada, hivyo sikuwa na mzigo mzito, tukaenda kwenye boti na nikapanda, nikakaa jirani na anapokaa nahodha.

Tulikuwa watu watano tu kwenye boti ambapo wawili walikuwa ni wateja wenye mafuta na mmoja ni msaidizi wa Ustadhi. Safari ikaanza kwa msaidizi wa nahodha kuongoza chombo.

“Tuna safari ya kilomita mia moja na ishirini hivi hadi tufike tutakapoanzia safari ya nchi kavu mimi na wewe” alisema Ustadhi.

Safari iliendelea kwa kupiga stori za hapa na pale hadi hali ya ziwa ilipobadilika na kuwa na upepo mkali na mawimbi makubwa, Ustadhi akachukuwa unahodha. Safari iliendelea, kukiwa kimya na nahodha aliyakata mawimbi kwa kuyafuata, hali iliyofanya tutumia muda mwingi kutembea umbali mfupi. Hali ilitulia baada ya kama saa moja hivi ya dhoruba. Nilishangaa sana kuona kumbe hata ziwani kuna mawimbi makubwa sana. Stori zikaanza tena na nahodha msaidizi akachukuwa unahodha kuongoza chombo.

“Unajuwa Pazi, tunapoenda sasa kushusha mzigo ni kama kilonita hamisitu kutoka kule Kabwe, lakini, siyo hapo tutakapoanzia safari, itabidi mimi na wewe tuelekee kwingine, lakini tutatembea kando kando ya mwambao hadi tutakapofika hapo tutakapo anzia safari…” aliniambia, mie nikawa naitikia tu maana naona napelekwa kama taahira, sijui hata hatma yangu itakuwa nini maana kila sehemu naambiwa uende huku, mara uende huku ili mradi sipati suluhu ya maradhi yangu. Hata hivyo nilijipa moja kwa historia ya Ustadhi aliyotuhadithia.

“Tutashusha mizigo sehemu panapoitwa Zongwe, kisha tutaelekea bandari ya Moba…” alisema.

Safari ya kufika bandari ya kushusha mizigo ilituchukuwa kama saa sita hivi na mizigo yote ikashushwa hapo na saa kumi na moja tukaanza safari ya kwenda huko Kaskazini kwenye hiyo bandari ya Moba ambapo napo ilituchukuwa masaa manne hivi maana chombo kilikuwa chepesi licha ya ka umbali kidogo.

“Sasa dogo!” alisema Ustadhi huku akimuelekea yule msaidizi wake

“Leo ndio mtihani wako wako wa mwisho kufudhu unahodha, itabidi urudi kule Zongwe, upakie mapipa tupu na abiria utakao wapata urudi Kabwe, na uchukuwe mizigo ya Kabwe ulete huku” aliendelea.

“Uendelee kufanya hivyo hadi siku utakaponiona bandari ya Zongwe, haya, kila la heri” alimaliza na kumuamuru aondoshe chombo kuwahi Zongwe.

**********

Itaendelea
Nilipoishia kwa leo
 
14. MWANZO WA MWISHO

“Mama mvalishe nguo zake huyo mgonjwa kisha mrudi keshokutwa ili kesho nikatafute dawa zake za kutumia…” nilimuaga yule mama huku akitaka kunipatia ujira lakini nilikataa maana kabisa niliona sijamaliza kazi.

Tangia nilivyoruhusiwa kuchukuwa hela kwa wateja, zile hela za miujiza sikupata tena, hata wakati wa dharura lakini nadhani kwa sababu nilikuwa na hela ndani na benki.

Kwenye rufaa niliambiwa kuwa binti ana maruhani kutoka falme nyingine za kijini ambao ni wakali na wakorofi na wanamtumia katika kufanikisha baadhi mambo yao huku duniani. Nikaambiwa niende msitu wa Mbirikimo ili kuchukuwa mizizi na majani ambayo mchanganyiko wake utawakera sana hao maruhani hadi kuondoka wenyewe.

Majini ni viumbe ambao nao wamegawanyika katika utaifa mbalimbali na makabila mbalimbali. Jinni siyo Malaika, na Malaika siyo Majini, hawa ni viumbe tofauti ingawaje waliwahi kufika hapa duniani kabla ya mwandamu kuja na kupewa utawala wa hii dunia.

Kama nilivyoandika awali kwamba Mwenyezi Mungu aliumba viumbe vya aina nyingi, tunavyovijuwa na tusivyo vijuwa, vinavyoonekana kwa macho ya kawaida na visivyoonekana kwa macho ya kawaida…

Katika simulizi za kale, tunaambiwa kuwa baada ya ulimwengu kuumbwa na viumbe wote kuumbwa kulikuwa na Amani na utulivu. Malaika walikuwepo na Majini walikuwepo. Ikatokea sababu kukawa na ugomvi kati ya majini na Malaika (hapa kabla ya binadamu kuubwa), vita ile ilipiganwa na Malaika walishinda, lakini katika vita hivyo Malaika mkuu akamuokota mtoto mdogo wa kijini na kumchukuwa na kuishi naye katika tawala za kimalaika.

Jinni yule mtoto alikuwa akiitwa Ibilisi. Na akajifunza mengi katika elimu kutoka kwa Malaika, akawa kama ni mmoja wao.

Siku ambayo Mwenyezi Mungu alipwaamrisha Malaika watii kwa salamu ule mwili wa Adam ambao ulikuwa umefinywangwa kwa udogo, Malaika walitii isipokuwa Ibilisi ambaye alijivuna na kujisivu kwamba yeye hawezi kumtiii kiumbe aliyeumbwa kwa udongo kwani yeye ni bora maana aliumbwa kwa nuru ya moto…

Ndipo Ibilisi akalaaniwa na kutupwa hewani (nje ya falme ya Malaika…). Lakini kabla ya kufukuzwa aliomba aishi muda mrefu hadi aone hao wanadamu watakavyokuwa…

Inasemekana Mungu alimkubalia lakini si kwa urefu atakao yeye bali kadri Mwenyezi Mungu atakavyoona inafaa…

Basi Ibilisi (aka, Lucifer) akaahidi kuwapotosha wanadamu wote ili waje waadhibiwe pamoja naye, maana Ibilisi anajuwa uwepo wa paradiso na uwepo wa jehanamu…

Inasemekana Mwenyezi Mungu akamwambia kuwa 'hutoweza kuwapotosha watu wangu isipokuwa wale ambao ni wa motoni tu…'

Kazi ya kwanza ya kupotosha Ibilisi aliianza kwa mke wa Adamu kama maandiko yanavyosema.

Kuna baadhi ya maandiko ya habari za kale huwezi kuyapata katika Biblia ama Qur’an ama vitabu vingine vya falsafa dini za kale, lakini maandiko ya namna hii yapo. ingawaje naheshimu imaani ya mapokeo ya wengine.
***********

Ipo specie ya Majini ambao huishi miaka mingi sana kiasi cha kushuhudia kizazi kirefu cha binadamu, yaani zaidi ya miaka elfu moja…

Ipo spicie ya Majini ambayo ikifikisha uzee wanarudi tena kuwa watoto na kurudia rudia kwa karne kadhaa kabla ya mwisho wa maisha yao…

Ipo spicie ya Majini ambao miaka nenda miaka rudi wao umri wao wanakuwa watoto tuu…

Ili mradi kuna spicies nyingi za majini.

Majini ikiwa ni sehemu ya Ibilisi na ndugu zake baada ya kutimuliwa Mbinguni na kuletwa duniani waliamua kuwa na makazi yao sehemu mbalimbali za ardhi ikiwemo mapangoni, chini ya maji, kwenye miti ama majabali makubwa na kazi yao kubwa ni kuwapotosha wanadamu ili wasimtii Mwenyezi Mungu kama ilivyo kwake.

Majini yamepewa uwezo mkubwa kama nilivyo eleza awali lakini hawakupewa umbo kama la binadamu na wanatamani sana wawe kama binadamu na kufanya mambo ya kibinadamu ndiyo maana huwaingia kwa namna isiyoelezeka kirasisi wanadamu na kuwatumikisha katika kufanikisha mambo yao.

Mwanadamu akiingiwa na Jini siyo lazima apige kelele, au aanguke kama tulivyo zoea, bali anaweza kutoa kauli ambazo kwa akili ya kibinadamu unajuwa huyu si binadamu kama vile kubashiri na kupatia, ama kutoa historia ya yaliyopita kwa kupatia hii yote ni kutokana na wao kuwa na umri mrefu hivyo kushuhudia mambo na kwa kuwa hawaonekani kwa macho ya kibinadamu basi pia hupeana habari juu ya yale yatakayoenda kutendeka “kwa kusikia” kutoka kwa vinywa vya binadamu ama kwa uwezo waliopewa…

Kwakuwa binadamu tulipewa utawala juu ya viumbe wote, basi kuna elimu ya kuwatawala majini ambapo wenye nayo wakiitumia vizuri inakuwa yenye manufaa na ambao watakaotumia vibaya ina kuwa na madhara makubwa.

Mfano wa wazi ni ujenzi wa mapiramidi kule Misri ni Dhahiri kuwa haikuwa kazi ya wanadamu pekee, mapango ya kule mashariki ya kati kule na hata machimbo ya mfalme Suleiman…nk.

Jini mtumwa anakuwa mtiifu kwa bwana wake na kufanya kama anvyoagizwa. Pia kuna majini wa kutengeneza kwa kanuni, yaani ukiunganisha hiki na hiki basi hupatikana jinni, si kwa maana ya kuumba bali kwa maana ya kumuita kutoka huko aliko kwa kanuni hiyo na kuja kuwa mtumwa kwa makubaliano kadha wa kadha na bwana wake…

Katika makubaliano hayo ukiyachunguza hatimaye ni kumuasi Mwenyezi Mungu kwa kukiuka maamrisho au makatazo yake ikiwemo kula ama kunywa najisi, kuacha kufanya ibada, kuua nk.

Majini wanapenda kuishi kama wanadamu, ingawaje nao wamepewa uhuru wa maamuzi kama sisi, vivyo hivyo ikatokea Malaika fulani wawili na walitamani kuishi kama binadamu ili waone ugumu uliopo wa kuwa mwandamu na kushinda majaribu ili hatimaye kupata daraja la juu katika paradiso ya Mwenyezi Mungu kuliko Malaika kama ambavyo Mwenyezi Mungu aliwaambia Malaika kuwa ninyi sikukuumbeni kwa matamanio kama binadamu ndio maana hao watakaoshida mitihani ya duniani basi watapata ujira ulio mkubwa Paradiso pengine kuliko ninyi…

Ndipo wakajitokeza hao Malaika wawili walioomba waletwe duniani ili wapewe hayo matamanio na waishi kama wanadamu na wakaadhidi watashinda…

Inasemekana Mwenyezi Mungu akawaahidi wakishida watapata daraja la juu na wakifeli wataadhibiwa. Basi nao wakapewa hiyari kama wandamu na wakashushwa maeneo ya Iraq (kwa sasa) ambako kulikuwa na mji na watu.

Hawa malaika wawili walipewa elimu ya utabibu, wakaanza kutibia watu duniani (walikuwa na maumbile ya kibinadamu baada ya kushusha Iraq), na kwa kuwa walikuwa waadilifu na elimu nyingi basi wakapata kazi ya kusuluhisha watu pale ambapo kunatokea kuto kuelewana.

Elimu ya utabibu waliyokuja nayo ndiyo hii iliyosambaa hadi leo, ingawaje elimu nyingi iliondolewa na nyingi ikakatazwa kutumika.

Walifundisha wanadamu waliopenda kujifunza utabibu na hata baadhi ya majini walihudhuria kujifunza elimu hiyo na kuihifadhi vyema huko ujinini.

Lakini kama nilivyosema Majini wapo speices nyingi na makabila mengi, hivyo kuna makabila mengine ni wakorofi tu muda wote na specie ambayo ni comedy sana na hawana madhara sana kwa binadamu ni vibwengo (tofauti na jinsi vibwengo wanavyochukuliwa hivi sana)

Jinni Ibilisi na kundi lake wakaanza kuitumia elimu ile ya utabibu kinyume nyume ili kuwadhuru watu…

Kwa mfano, ikitokea mtu amegombana na mwenzake, basi Ibilisi humfuata na kumwambia, kwa mfano, “…Wewe fulani si amekuudhi, basi mpe klorokwini 10 zote kwa mara moja, atadhurika…” ambapo elimu ya utabibu ilisema mgonjwa wa malaria yafaa apewe vidonge 10 lakini siyo kwa mara moja bali ameze labda vinne kwa siku mbili kisha siku ya tatu ameze vidonge viwili au ameze vinne leo kesho viwili na siku mbili zitakazofuata viwili viwili jumla vidonge kumi.

Hapo tiba ikageuka na kuanza kuwa na madhara, elimu ya kinyume ikaanza kusambaa dhidi ya majini na kuanza kuwafundisha wanadamu kwa ajili ya kudhuriana hatimaye lengo la Ibilisi likawa linatimia la kuwapotosha wanadamu.

Kombozi mbali mbali zikaja kwa ajili ya kuwaokoa wanadamu na kurejea njia iliyo sahihi na miongozo ya vitabu ikaletwa hadi ikafika nyakati za Mtume Muhammad (rehema na Amani zimwendee)alipo pewa kitabu kiitwacho Qur’an.

Baadhi ya Majini walivyosikia, walirejea kwa Mwenyezi Mungu, wakawa wanyeyekevu lakini baadhi walibaki kwa Ibilisi na kuendeleza lengo lao la kupotosha wanadamu. Hapa ndipo kukawa na neno SHETANI.

Shetani ni kiumbe yeyote aliyemuasi Mwenyezi Mungu kwa kudhihirisha uasi wake, hivyo kuna mashetani ya kijini na mashetani ya kibinadamu na ya viumbe wengine tusio wajuwa.

Hivyo Shetani siyo lazima awe jinni, na wala si kila jinni ni shetani, wapo majini ambao ni wacha Mungu.

Wale malaika wawili waliofanywa waishi kama binadamu walifeli mtihani kwa kutofanya uadilifu kwa hukumu fulani ambapo walimpendelea mtu aliye na makossa kwa sababu ya mahaba maana walipewa matamanio, hivyo Mwenyezi Mungu amewaadhibu kama ambayo walipenda iwe, baada ya kupewa uhuru wa kuchaguwa waadhibiwe hapa Duniani hadi siku ya mwisho wa maisha yao au waachwe waendelee kuishi hadi siku ya hukumu nao wahukumiwe kama binadamu wengine.
***


Basi baba, usiku ule ikabidi nifanye safari ya kwenda Umbirikimoni kwa mara nyingine kwa ajili ya kuchukuwa miti shamba ambayo ingemtibu yule binti. Ni kwamba kuna harufu ambazo majini kwa jinsi walivyoumbwa hawazipendi, moja majani ambayo hawajapendi ni mmea uitwao “mlangajini”, hii mimea ipo upo kwa wingi maeneo ya pwani, majini pia hawapendi harufu mbaya ingawaje kuna specie ya majini wanaokula vinyesi na makazi yao ni chooni na sehemu zenye uvundo uvundo. Majini walioasi ni waongo waongo sana, anaweza kujifanya ametoka na kumwachia huru mwanadamu kumbe yupo, wengine hujifanya wapo wengi kumbe yupo peke yake ili mradi tu alete usumbufu, wengine mabubu, huwa hawataki kusema bali huandika kwa kalamu, yani unaweza kukuta mtoto mdogo wa darasa la nne kwa mfano akiwa amepandisha mashetani ataomba kalamu na karatasi na kuanza kuorodhesha vitu ama kuandika vitu, tena wakati mwingine kwa lugha fasaha ambayo akiwa kawaida hawezi kuiongea wala kuaiandika, na majini wengine ni mabubu kweli. (Pazi alizidi kunifafanulia)

Nilirudi alfajiri ya Ijumaa nikiwa nimepewa ile mizizi na majani maalum kwa ajili ya kuwakera majini na maneno mengine (spells) ambayo nilifundishwa.

Jumamosi mapema walikuwa yule mama na bintiye na wateja wengine pia, basi baada ya kuwahudumia wateja wengine wa mwisho nikaanza kumuandalia dawa yule binti. Yule mama tayari nilishamwambia kuwa matibabu yake yataendelea kwa siku saba ili yakamilike.

Hapo mbezi nilishakuwa maarufu na nikawa na wasaidizi wangu watatu, mmoja ni wa kiume na wawili ni wanawake ambao ambao niliwaajiri kwa madhumuni ya usafi na kusaidia kazi ndogo ndogo hapo nyumbani. Usafiri haikuwa kipaumbele kwangu maana niliweza kwenda nitakapo bila kipingamizi.

Baada ya siku saba yule binti alipona kabisa, wakatoa shukrani zao na ujira kadri walivyojaaliawa (maana nilikuwa nimeweka ndoo ya lita 18 ambapo walikuwa hela wanaweka humo bila ya hata mimi kujuwa wameweka kiasi gani ama nini) kisha wakaaga…

“Kwakuwa amepona, baada ya mwezi mmoja anaweza kuja hata peke yake ili nione maendeleo yake…” niliwaambia.

Hadi wakati huo mimi sikuwa na simu wala kuona umuhimu wake, maana nikihitaji kuongea na nimtakaye, namfuata kwa njia yangu mapema asubuhi na kuongea naye kisha narejea kwenye kazi yangu ya utabibu.

Kazi ya baba niliacha baada ya kuhamia Mbezi beach maana nilizidiwa na wateja, baba alinielewa na mama alifurahi kuwa nadhiri yake inatimia.

Kipindi chote tangia nipo kule Ilala, sikujihusisha na uhusiano kimapenzi na wanawake, badala yake nilitumia muda mwingi kufanya ibada na kuwa bize na wagonjwa, wito wa yule binti safari hii (baada ya ule mwezi mmoja) haukuwa wa kimatibabu ya matatizo yake bali ilikuwa mahaba yameniingia.

Katika kuendelea kutibia kwangu nilikuwa Napata wateja wenye majini feki wengi ambao kumbe nia zao ilikuwa kuwachuna (kuwaibia kiaina) waume zao ama mabwana zao au kwa tamaa tu za kibinadamu. Hawa nilikuwa nawakataa moja kwa moja kwa kuwaambia dawa zenu hazipo kwenye fani yangu. Kuna baadhi ya wagonjwa walikuja wakilazimishwa ili wawe waganga kama ilivyokuwa kwangu, wengine kwa sababu ya bahati mbaya tu ya kuwa sehemu isostahili kwa wakati usiostahili, wengine kwa sababu ya kurogwa ma kutupiwa, wengine kwa sababu ya kimahaba baada ya kupendwa na specie ya majini wapenda ngono.

Hii specie ya majini (wanawake na majini wanaume) wakimpenda mtu basi humuandama kwa kufanya naye ngono bila ridhaa ya huyo mwanadamu kwa muda na wakati ambapo jinni huyu ataamua. Yani unaweza kuwa kwenye daladala kwa kwa mfano, ghafla jinni linamvaa binti wa watu na kuanza kufanya naye ngono, binadamu wa kawaida hawatoona lakini wataona vitendo vya huyu mgonjwa.

Wengine huingiliwa usiku wakiwa wamelala, na kuna ambao hujijuwa na kuna ambao hawajijui. Mara nyingi kwa binadamu wanawake ambao wana majini mahaba basi huzuiliwa kupata waume, na akipata hakutakuwa na amani ndani, mara mumewe asiweze kumuingilia mkewe, au akiweza basi asirudie ili mradi tu kuwe na nafasi kuwa ya jinni kufaidi ngono na huyo mtu mwanamke. Wengine huzuiliwa kupata watoto, ama akipata wanakufa ama kupotea kwa mazingira ya kutatanisha. Na kwa jinsi hii kuna watoto ambao huzaliwa na kuwa nusu jinni nusu mtu yaani mwanamke anabeba mimba ya jini. Mmoja wapo ni mimi ingawaje kesi yangu ni tofauti kidogo.

Kwa wanaume ambao hupatwa na majini mahaba nao huzuiliwa wapenzi, yaani kijana rijali anakuwa haoi, na akioa basi hafanyi sana ndani. Wengine hudiriki hata kuoa jinni kabisa na kushirikiana nao kwa mambo mbalimbali lakini watoto wanaozaliwa na majini wanawake kutoka kwa wanaume binadamu huishia kupotea kuonekana duniani ila wale wa waliokaa kwenye matumbo ya wanadamu wanawake basi huishi duniani.

Katika kuwahudumia wagonjwa, nikajifunza kumbe kuna Sehemu Rufiji kuna mcha Mungu ambaye naye anawaombea watu na mambo yao yanaenda vizuri. Nikatamani sana nifike huko lakini sijui ni kusahau ama kuzidiwa na wateja, sikupata kwenda kutembea huko hadi mwaka mmoja uliopita.

**********

Inaendelea...
 
15. NGUVU ZA TIBA KUONDOLEWA

Baada ya siku thelathini na kitu hivi nilipata ugeni wa yule binti kutoka Kiwalani, ambaye kwa jina anaitwa Behat. Lakini mimi nilianza kumuita Bahati maana niliona ni bahati sana kukutana naye, na yeye alipata bahati sana kufika kwangu akiwa na mama yake baada ya mihangaiko mingi ya kitiba.

“Karibu Bahati…” nilisema huku nikimuonesha sehemu ya kukaa kusubiri maana nilikuwa nachukuwa maelezo ya mteja mwingine. Baada ya kuwahudumia wateja wote na kuondoka, tulibaki mimi na wasaidizi wangu na Bahati ambaye hakuja kama mgonjwa kwa siku ya leo ingawaje yeye alijuwa amekuja kwa kuangaliwa anaendeleaje.

“…Mama hajambo? Anaendeleaje na miguu yake?” niliuliza maana mama yake alipataga shida ya miguu kwenye magoti na alitibiwa kwa tiba za kimagharibi (western medicine)

“Anaendelea vizuri, anakusalimia…” alijibu Bahati.

Behat alikuwa ni mtoto wa mwisho kwa baba na kwa mama na ndio kwanza alikuwa amemaliza kidato cha nne miezi michache iliyopita. Nilianza kumchambua na kumvua nguo kwa macho na kuona uzuri uliojificha katika nguo alizovaa za kujihifadhi vyema.

Nilimuambia kuwa atabaki kwa siku tatu kisha arudi kwao halafu arudi tena baada ya miezi miwili. Basi nikamwacha achanganyike na wale wasaidizi wangu nami nikawa na shughuli zangu zingine.

Usiku kama saa tatu baada ya chakula, nikamwelekeza kile chumba ambacho ndicho alichoogeshewa ile siku ya kwanza, alipoingia nikamfuata na kumwambia…

“Jisikie upo nyumbani, ukichoka utajipumzisha…” nilimwambia.

Baadaya kama dakika arobaini hivi wakati nimehakikisha wasaidizi wangu wameingia kupumzika nilienda chumba alicholala Behat ambacho kilikuwa mkabala na master bedroom yangu mbali kabisa na upande wa vyumba vya wale wasaidizi wangu.

“Ngo ngo ngo….” Kwa ubisho wa sauti ya chini niligonga mlango na kujaribu kuufungua kumbe ulikuwa wazi…

Behat alikuwa bado anajisomea kitabu alichokuja nacho…

“Kumbe bado upo macho…?” niliuliza.

“Eee bado namalizia sehemu hii ndio nilale…” alijibu.

Nikasogea na kukaa pembeni ya kitanda maana chumba kile hakukuwa na kiti.

“Samahani, ujio wangu ni tofauti leo, sikuja kwa ajili ya tiba, bali kwa ajili ya mazungumzo mimi na wewe.

Behat alibaki ananiangalia tu, sijui alikuwa anawaza nini…

“Behat..!” aliitika “Abee”

“Nakupenda sana, nilikupenda tangia macho yako yalivyo gongana na macho yangu siku ya kwanza…”

Pakawa na ukimya….

Kiumri Behat nilimzidi miaka isiyozidi sita, hivyo tulikuwa tunaendana na yeye alikuwa ameshapevuka. Niliendelea kumpa maneno matamu pale na kumuahidi kuwa nataka nimuoe. Alishangaa maana alidhani mmoja wa wale wasaidizi wangu ni mke wangu.

“Kumbe bao hujaona..!” alisema huku bado akiwa ameshika kitabu chake, akiwa ameegemea ukuta juu ya kitanda.

“Ndiyo sijao lakini tayari mimeshapata mchumba ambae ni wewe” nilijibu na pakawa na ukimya.

Baada ya machombezo ya muda mrefu hatimaye tukajikuta sote tupo kama tulivyo zaliwa…

“Mie sijawahi kufanya…” alisema Behat wakati nikiendelea kumtomasa kwa minajiri ya kumuandaa akionesha ushirkiano usio na ujuzi.

Usiku huo nikajikuta nimefanya ngono baada ya muda mrefu, ngono ambayo hata sikufaidi maana Behat alikuwa ni mgeni na kwa kuwa nilikuwa na hamu ya muda mrefu nilijikuta sijafungua njia sawasawa.

Siku ya pili nikashangaa hapakuwa na wateja kabisa pale nyumbani. Nikatumia muda mwingi kuongea na Behat mtoto wa Kidigo. Na usiku wake tukarudia tena mchezo wetu na safari hii nilifungua njia vizuri na kurudia mara moja.

Tukaoga na nikamwacha alale nami nikarudi chumbani kwangu.

Saa sita za usiku chumba changu kikajaa mwanga mkali na sauti yenye mitetemo ikasikika…

“Umefanya nini sasa mwanangu!...”

“Umeharibu kila kitu…”

“Hukupaswa kulala na huyo binti…”

Nikapigwa na butwaa huku nikisikiliza…

“Huyo binti ni nusu jinni kama wewe, lakini yeye amezaliwa na jinni mwanamke, huyo aliyemleta kuja kutibiwa siyo mama yake, mama yake mzazi alifariki binti akiwa mdogo, Mama Behat alibadilishiwa mtoto akiwa hospitalini Ilala, mtoto wake halisi aliugua ghafla na kufariki lakini kabla manesi hawajatambua ndipo aliwekewa Behat na jopo la Majini waliotumwa kwa kazi hiyo…”

“Umeharibu kila kitu…”

“Tulikuandalia mke mzuri ambaye ni jinni kamili uli uzao wenu uweze kuishi huku moja kwa moja, lakini kwa kuwa umetembea na nusu jinni mwenzako umefunga milango yote ya ninyi kurudi ujinini!...”

Sauti ile iliendelea kutoa risala pale kwa masikitiko sana na mwisho akasema…

“Kuanzia sasa wewe si mwanangu tena na nguvu zako zote zimetoka tangia ulipoweka mbegu zako za uzazi ndani ya mfuko tumbo wa huyo Maif bint Shariff wa Kaskanini….”

Mwanga ulipotea na sauti sikuisikia tena, nikapitiwa na usingizi mzito hadi niliposhtuka ilikuwa saa moja kasorobo asubuhi.

Nikaenda kwenye chumba cha matibabu nikakuta hakuna chochote, nikajiangalia mikononi sikuona hata pete moja, nikatafuta ile fimbo bila mafanikio, nikatafuta unyoya na usinga wala sikuviona. Moja kwa moja nikajuwa hapa nguvu zangu za utabibu zimeisha.
***********

Nikaitisha kikao cha dharura na kuwapatia ujira wao wale wasaidizi wangu na kuwapa likizo hadi nitakapowatafuta tena, maana majumbani kwa ndugu zao napajuwa.

Nikaenda chumbani kwa Behati na kukuta ameshaamka na kuniambia aliona mwanga mkali sana usiku lakini ukapotea.

“Bahati…” nilimwita kama ninavyomwitaga, akaitika

“Mimi na wewe asili yetu ni moja…”

“Wewe ni wa Kaskazini na mimi ni wa Magharibi…” nikasema

Nikamshika mkono wake na kuanza kumchunguza, ndipo nikaona pattern ya ngozi yake ipo kama yangu na si kama ya binadamu wengine.

“Inabidi tuoane haraka” nilisema.
*********

Baada ya kumuelezea kwa kirefu ndio akaelewa na yeye akaanza kufunguka kuhusu maono yake. Basi moja kwa moja nikaamua arudi kwao kwanza kisha mimi nifanye utaratibu kwa kufikisha posa kwao.

Nikaenda Bagamoyo na kufanya kikao na wazazi wetu kisha nikafanya kikao na mama, kilikuwa kikao kirefu sana maana ilibidi nifunguke kuhusu mwanzo wa ujauzito wangu na kwamba mzee Mwinyi hakuwa baba yangu wa kunizaa bali nilikuwa mtoto wa Shariff kutoka Magharibi na nikaelezea kisa chote mwanzo mwisho kitu kilicho wafanya Baba na mama kupigwa na butwaa,Mama akaanza kulia huku Baba akiwa amejiinamia.

“Kama nguvu ndio zilikuwa za hivyo mwanangu, basi nadhiri yangu bado sijaitimiza, mimi nilitaka umtumikie Mwenyezi Mungu na wala siyo kumtumikia ama kuwatumikia majini…” ilikuwa kauli ya mama yangu wakati akilia

“Kwa hakika mama, mimi sikujuwa, nilidhani ndio namtumikia Mwenyezi Mungu…” tuliendelea kulia sote pale lakini mwisho wa siku tukatulia na vikao vya ‘kujenga’ vikaanza.
*********

Tarabibu za posa zikakamilika, na ndoa ikapangwa haraka haraka ndani ya miezi miwili tukafunga ndoa mimi na Behat ambaye ndiyo huyo niliye kutambulisha asubuhi na wale ndio watoto wetu.

Baada ya ndoa mimi na Behat tukafanya safari ya kwenda Utete Rufuji kwa mcha Mungu ambaye nilihadithiwa habari zake siku za nyuma.
**********

Itaendelea…
 
16. MAISHA MAPYA na UHURU - Ω

“Nakuusieni na kuihusia nafsi yangu juu ya kumcha Mwenyezi Mungu, amesema Mwenyezi Mungu (aliye takasika), … hiki (Qur’an) ni kitabu kisichokuwa na shaka ndani yake na muongozo kwa wale wamchao …”

“Sisi waislamu, tuna miongozo miwili, Qur’an na Sunna. Qur’an ni maneo ya Mwenyezi Mungu na Sunna ni matendo na mafundisho ya Mtume Muhammad (Rehema na Amani zimwendee).”

“Tukishikamana na Kitabu cha Mwenyezi Mungu na Hadithi za Mtume, hatuwezi kupotea.”

Hayo yalikuwa maneno ya Walii (kipenzi) wa Mwenyezi Mungu wa Utete Rufiji (kama wenyeji walivyokuwa wakimwita) wakati akinukuu aya kutoka Qur’an akiwa anatujenga kiimani.

“Katika hii Qur’an Mwenyezi Mungu ameweka elimu ya toka watu wa mwanzo mpaka watu wa mwisho, elimu zote zimo ndani ya Qur’an, historia imo, mawaidha yamo, mifano imo, visa vimo, hesabu zimo, utaratibu wa kuendesha Dunia umo ndani ya Qur’an na hiki kitabu huhifadhi waumini kwa fitina iliyomo humu duniani…” aliendelea

“Ndani ya Qur’an kuna habari za watu waliokuwepo kabla yetu, kuna habari za watu baada ya sisi kuondoka, ni hakimu baina yetu na ni upambanuzi juu ya mambo mbalimbali. Haifai kuiacha.”

“Hii Qur’an ajabu zake hazimaliziki, wana zuoni hawashibi, kila siku wanatoa faida na hata majini walipoisikia Qur’an inasomwa, wakasema hakika sisi tumesikia Qur’an ya ajabu, … inaongoza kwenye uongofu kwa hiyo tumeiamini na wala hatutofanya ushirikina…, na kwa hakika utukufu wa Mola wetu mlezi umetukuka kabisa,… hana mke wa mwana…, … na kwa hakika wapumbavu miongoni mwetu walikuwa wakisema uongo uliopindukia juu ya Mwenyezi Mungu… nasi tulidhani kuwa watu na majini hawamsingizii uongo Mwenyezi Mungu…,”

Aliendelea yule mcha Mungu tutupatia mawaidha kupitia kitabu kitukufu Qur’an na kutusimulia habari za majini jinsi baadhi walivyo mrejea Mwenyezi Mungu na wengine waliendelea kukengeuka.

“Eee umesema mmetoka Bagamoyo!” aliuliza yule Walii,

“Rudini huko, kuna Sheikh Mkubwa Zawiani, utapata muongozo na elimu kadha wa kadha, kikubwa shikamaneni na hiki kitabu wala msikiache.” Alimaliza yule Walii na tukaagana na kuanza safari ya kurudi.

Nilikuwa mimi na mke wangu Behat, tulilala Rujiji Ikwiriri na siku ya pili tulifika Dar na moja kwa moja kwenda Bagamoyo.

Bagamoyo pale Zawian tukaambiwa tuende Lushoto kumtafuta Shariff Badowo ili atufanyie maombezi makubwa kabla ya kurudi Zawiani kwa ajili ya kumalizia elimu nasihi.

Tulienda Tanga, tukafika nyumbani kwake lakini tukaambiwa amesafiri kwenda Mombasa, tukaambiwa tumtafute kijana mmoja pale Horohoro atatusaidia kufika kwake.

Yule kijana alikuwa ni mfanyakazi wa mabasi ya Modern (Mombasa – Tz – Zambia nk), alikuwa anaitwa Sarojo, alitusaidia sana hadi tukafika kwa Shariff Badowo na kufanya dua kubwa kubwa sijapata kuona na tulivyorudi Zawiani tulikuwa na utulivu mkubwa.
*********

Tukiwa Zawiani – Bagamoyo

“Tatizo lenu mlivyokuja mara ya kwanza hamkutaka kunisikiliza kwa kituo, wewe na kaka yako wote mlikuwa na haraka haraka kiasi cha kutopata yote ambyo nilitaka kuwaambieni.” Alikuwa anaongea Sheikh Mohamed kwa sauti yake nzito iliyojaa umwinyi mwinyi hivi kwa kutulaumu kiaina…

“Sasa ulivyorudi na kuniambia kuwa umepona, nikadhani labda umejuwa asili ya shida yako na kutatuliwa ipasavyo…” aliendelea…

“Kumbe bado kwa maoni yangu, ulikuwa kwenye safari ya kujijuwa na kujitambua… na sasa kwa vile umefikia hatua hii basi ukae kitako nikuelimishe…” alisema.

“Mwenyezi Mungu alituumba ili tumuabudu yeye, tena yeye tu na wala tusimshirikishe na miungu mingine, hayo ndiyo malengo hasa ya sisi kuumbwa, hata maumbile yetu yamewekwa kurahisisha zoezi hilo la kumuabudu yeye”

“Tukimuabudu yeye hatumuongezei chochote, na tusipomwabudu hatumpunguzii chochote, YEYE ambaye hakuna Mola apasaye kuabudiwa kwa haki ile YEYE, Yu hai na ni wa kudumu, halali wala kupatwa na usingizi. NDIYE Mola wa Mbingu na Ardhi na vilivyomo baina yake…”

“Anajuwa yaliyochificha mbele na nyuma, na katika sisi viumbe hatuna tujuwalo ama hatuwezi kujifunza (kupata elimu) ila kwa kuridhia kwake, na utukufu wake umeenea Mbinguni na ardhini na wala hawezi kushindwa kuvilinda viumbe vyake maana yeye ametukuka (aliye juu) na NDIYE MKUU.” Alisema Sheikh kisha akasoma aya katika mpangilio wake.

Alivyoanza kusoma nami nikakumbuka kile kikaratasi nilichopewa Kikokwe niwe nasoma mara kwa mara, maneno hayo yalikuwa sehemu ya dua ile niliyopewa huko.

Sheikh aliendelea na risala…

“Katika uumbaji wake (Mwenyezi Mungu) aliumba viumbe mbalimbali, na kila kiumbe kina mamlaka yake na mipaka yake katika kuyaendea mambo…”

Akatoa mifano mbali mbali jinsi viumbe wengi wanavyoishi humu duniani ikiwemo wadudu, hayawani na hatimaye majini na binadamu.

“Binadamu ndio tumepewa uhalifa (uongozi) katika dunia hii, yani tunatakiwa tuweze kuitawala dunia ipasavyo…”

“Majini nao wana tawala zao, wana mataifa yao, wana makabila yao, wana koo zao, wana mila zao na desturi zao, na wamepewa uwezo mbalimbali lakini pia wamewekewa mipaka…”

“Haifai kwa Majini kuingia kwenye tawala za kibinadamu na kuwasumbua watu kwa kuwapagawisha, kuwatia maradhi ama eti kujifanya wanawalinda…”

“Wao wana ‘ulimwengu’ wao na sisi binadamu tuna ‘ulimwengu’ wetu…”

“Hivyo ni makossa makubwa kwa Jinni kumuingia mwanadamu kwa namna yoyote ile kwa visingizio mbalimbali…”

“Idadi ya majini ni kubwa mara nyingi sana kuliko wanadamu, na kwa kuzingatia kuwa wao wanaishi muda mrefu kuliko wanadamu basi wingi wao huongezeka mara kwa mara kiasi cha kutapakaa duniani kote… kwa wingi wao huo hata kila mwanadamu aliye hai muda huu akikusanya majini sabini kila mmoja, basi binadamu wote watakusanya na wengi sana bado watabaki hawajakusanywa”

“Kuna elimu mbalimbali za kuweza kuwamiliki hawa majini, lakini ni moja ya elimu zilizokatazwa kwa kuwa hatimaye huleta hasara badala ya faida…”

“Lakini kwa kuwa Duniani humu kuna fitina mbalimbali ikiwemo fitna ya afya, mali, wake, waume, watoto nk basi baadhi ya watu hupatwa na husda, chuki na vijicho ambavyo huwadhuru wenzao, na kazi zote hizo hufanywa na hao majini ambao wameasi kwa kushirikiana na binadamu kwa namna mbalimbali za elimu ya kichawi”

“Elimu ya kukabiliana na matatizo hayo pia ipo, ipo kwa njia nyeusi na kwa njia nyeupe…”

“Hivyo tiba zipo, lakini kuna tiba kwa njia sahihi na zipo tiba za kwa njia ya kishirikina”

“Kufanya ushirikina ni moja ya dhambi ambayo kama ikitokea umekufa bila ya kutubu basi ni dhambi isiyo sameheka labda kwa rehma zake Mola wetu maana yeye ndiye mjuzi zaidi”

“Hivyo basi ushirikina HAUFAI mbele za Mwenyezi Mungu”

“Kwakuwa tiba sahihi zipo, basi yatupasa kufuata tiba kwa njia zilizoelekezwa kwa miongozo ya dini yetu”

“Tiba isiyo sahihi utaijuwa kwa masharti yake ambayo hatimaye yanakupelekea katika kumuasi Mwenyezi Mungu kwa namna zote nne, kuwaza, kunena, kutenda na kutotimiza wajibu…”

“Sasa kwa kuwa ninyi mliamua kuishi kama binadamu…”

Tukawa tunaangaliana na Behat…

“…yafaa muendelee kuishi hivyo na kufuata maamrisho na makatazo yote ambayo yapo katika muongozo wa Qur’an na Sunna…”

“Pazi…!” aliniita Sheikh

“Mwenzako ana kiumbe tumboni…”

Nikawa manuangalia Behat tumboni sioni kitu zaidi ya ‘flat screen’ (hakuwa na hata kijitambi kidogo)

“Atazaliwa kiumbe ambaye sasa atakuwa mwanadamu kamili, wanenu hawatokuwa na passport ya kuingia Ujinini kama ilivyo kwenu hivi sasa ingawaje bado mpo nusu jinni.., wewe Pazi ni nusu binadamu nusu jinni na huyo mwenzako ni nusu jinni na nusu binadamu…”

Moja kwa moja nikaelewa tofauti yake kwa mmoja wetu alilala kwenye tumbo la uzazi binadamu ilhali mwingine alila kwenye tumbo la uzazi jinni.

Aliendelea kutupa risala pale weeee mwisho akasema…

“Tafuteni njia halali za kupata rizki zenu, hata kama itakuwa ni kutibu watu basi uifanye tiba iliyo sahihi kwa njia za kisunna (yaani kwa njia ya mafundisho ya Mtume Muhammad, Rehema na Amani zimwendee)

“Kitu kingine muhimu sana ni kwamba haifai kubeza dini nyingine, mfano hawa wenzetu wakristo tunaishi nao humu mjini, majumbani na kupeana heshima za kibinadamu, Kuna Kanisa kubwa kule Mantep (Sikuhizi wanaita ADEM), kuna Kanisa dogo kule miembe safa (jirani na kushukia MSALABANI) na kuna Kanisa kule Mwanakalenge. Hawa ni binadamu wenzetu na wana Imani yao thabiti katika kumwabungu Mungu wao kwa mujibu wa mafundisho yao, ukumbuke kuwa hawa pia kiongozi wao alipewa Kitabu kama ilivyo Qur’an kwa sisi. Usiwabeze wala kudharau Imani zao maana kuna wengine huenda wakawa bora mbele ya mwenyezi Mungu kuliko baadhi yetu, lakini haikatazwi kuwalingania ili waje katika uislam, tena kwa lugha iliyo nzuri na staha.”

“Kumbuka hata Nabii Mussa (Rehema na Amani zimfikie) alipoambiwa akamlinganie Firauni (Farao) aliambiwa akazungumze naye kwa upole licha ya kufuru kubwa aliyokuwa akiifanya. Kazi yetu ni kufikisha ujumbe lakini kumuongoa mja siyo kazi yetu, Allah mwingi wa Rehema sisi sote ni viumbe vyake, tusijitie ukiburi, YEYE Allah huamua atakavyo.”

Aliendelea…

“Vitabu cha elimu hiyo ya tiba zipo, vitafute ujifunze kwa walimu ukihitimu uendelee na tiba halali, kama hutoweza basi rejea kwenye kazi ya baba yako, ameshazeeka sasa afaa kusaidiwa sana…”

Alimalizia risala yake kwa kutusihi kuwa sisi bado ni nusu watu nusu majini, hivyo kiasili tuna nguvu za kijinni basi tuwe makini na maneno tuyasemayo na kujitahidi kujizuia hasira zetu maana huenda zikawa na athari kwa binadamu wa kawaida.

Tulirudi nyumbani na kumkuta mama akitusubiri kwa hamu.

“Enhe, mmeambiwaje huko?...” Mama aliuliza kwa shauku

Tukamwelezea yote na hatimaye mimi na mke wangu tukaamua kumtumikia Mwenyezi Mungu kwa kuwalingania watu katika dini huku nikiendeleza kazi ya Baba.

“Nadhiri yako sasa Mama inaenda kutimia…” nilisema.

Baada ya siku tatu, tuliaga kurudi Dar es Salaam kuendelea na maisha.

Leo hii tuna watoto watatu, tunaendeleza kazi ya uvuvi na uchuuzi kwa njia za kisasa, Baba na mama walishafariki, mama mkubwa pia alishafariki.

Tukapata Chakula cha mchana pamoja, kisha akanisindikiza nami nikachukuwa njia ya kurudi kwangu Upanga.

Jumamosi ile ilikuwa tulivu lakini nyumbani kwangu hapakuwa hivyo, nilikuta mke wangu amenuna, lakini nikamwambia hebu baada ya kula uje chumbani nimsimulie kisa chote nilichosimuliwa….
*******

Hakutaka nilale bali nimmalizie kisa chote maana muda tayari ulikuwa umeshaenda sana na siku Jumapili ilikuwa ndio inaingia (kwa mujibu was aa za na kalenda ya Gregori)…

Nilimkidhia haja yake baada ya kuona amevutiwa pia na kushangazwa japo kwa kuifupisha.

Mwishowe tuliendeleza ‘libeneke’ la mume na mke.

**************** MWISHO*************


Update!

Sheikh Mohamed alishafariki, Mzee Zahiri naye, Mwalimu Mwaloki, Mzee wa tiba Mlingotini, Mzee Njembi, Mcha Mungu wa Rufiji, Shariff Badowo, Shariff wa Kikokwe wote wametangulia mbele za haki.

Watu wengine ambao wametajwa katika simulizi hii sina update zao.

Imenibidi nifupishe ili niende na muda-huru niliokuwa nao maana ni mchache.



Niliamua kushea nanyi kisa hiki kama kumbukumbu ya kukumbuka uwepo wa Pazi na familia yake hapa Duniani kwa maana ya kwamba ile familia yote ilifariki kwa kuzama baharini miaka kumi na moja na siku arobaini na nane hivi ziliyopita walipokuwa wakitokea Unguja kuelekea matembezini Pemba kwenye MV. Spice Islander.

**********



Hakika sisi sote ni wa Mwenyezi Mungu na kwa hakika kwake tutarejea.



 
16. MAISHA MAPYA na UHURU - Ω

“Nakuusieni na kuihusia nafsi yangu juu ya kumcha Mwenyezi Mungu, amesema Mwenyezi Mungu (aliye takasika), … hiki (Qur’an) ni kitabu kisichokuwa na shaka ndani yake na muongozo kwa wale wamchao …”

“Sisi waislamu, tuna miongozo miwili, Qur’an na Sunna. Qur’an ni maneo ya Mwenyezi Mungu na Sunna ni matendo na mafundisho ya Mtume Muhammad (Rehema na Amani zimwendee).”

“Tushikamana na Kitabu cha Mwenyezi Mungu na Hadithi za Mtume, hatuwezi kupotea.”

Hayo yalikuwa maneno ya Walii (kipenzi) wa Mwenyezi Mungu wa Utete Rufiji (kama wenyeji walivyokuwa wakimwita) wakati akinukuu aya kutoka Qur’an akiwa anatujenga kiimani.

“Katika hii Qur’an Mwenyezi Mungu ameweka elimu ya toka watu wa mwanzo mpaka watu wa mwisho, elimu zote zimo ndani ya Qur’an, historia imo, mawaidha yamo, mifano imo, visa vimo, hesabu zimo, utaratibu wa kuendesha Dunia umo ndani ya Qur’an na hiki kitabu huhifadhi waumini kwa fitina iliyomo humu duniani…” aliendelea

“Ndani ya Qur’an kuna habari za watu waliokuwepo kabla yetu, kuna habari za watu baada ya sisi kuondoka, ni hakimu baina yetu na ni upambanuzi juu ya mambo mbalimbali. Haifai kuiacha.”

“Hii Qur’an ajabu zake hazimaliziki, wana zuoni hawashibi, kila siku wanatoa faida na hata majini walipoisikia Qur’an inasomwa, wakasema hakika sisi tumesikia Qur’an ya ajabu, … inaongoza kwenye uongofu kwa hiyo tumeiamini na wala hatutofanya ushirikina…, na kwa hakika utukufu wa Mola wetu mlezi umetukuka kabisa,… hana mke wa mwana…, … na kwa hakika wapumbavu miongoni mwetu walikuwa wakisema uongo uliopindukia juu ya Mwenyezi Mungu… nasi tulidhani kuwa watu na majini hawamsingizii uongo Mwenyezi Mungu…,”

Aliendelea yule mcha Mungu tutupatia mawaidha kupitia kitabu kitukufu Qur’an na kutusimulia habari za majini jinsi baadhi walivyo mrejea Mwenyezi Mungu na wengine waliendelea kukengeuka.

“Eee umesema mmetoka Bagamoyo!” aliuliza yule Walii,

“Rudini huko, kuna Sheikh Mkubwa Zawiani, utapata muongozo na elimu kadha wa kadha, kikubwa shikamaneni na hiki kitabu wala msikiache.” Alimaliza yule Walii na tukaagana na kuanza safari ya kurudi.

Nilikuwa mimi na mke wangu Behat, tulilala Rujiji Ikwiriri na siku ya pili tulifika Dar na moja kwa moja kwenda Bagamoyo.

Bagamoyo pale Zawian tukaambiwa tuende Lushoto kumtafuta Shariff Badowo ili atufanyia maombezi makubwa kabla ya kurudi Zawiani kwa ajili ya kumalizia elimu nasihi.

Tulienda Tanga, tukafika nymbani kwake lakini tukaambiwa amesafiri kwenda Mombasa, tukaambiwa tumtafute kijana mmoja pale Horohoro atatusaidia kufika kwake.

Yule kijana alikuwa ni mfanyakazi wa mabasi ya Modern (Mombasa – Tz – Zambia nk), alikuwa anaitwa Sarojo, alitusaidia sana hadi tukafika kwa Shariff Badowo na kufanya dua kubwa kubwa sijapata kuona na tulivyorudi Zawiani tulikuwa na utulivu mkubwa.
*********

Tukiwa Zawiani – Bagamoyo

“Tatizo lenu mlivyokuja mara ya kwanza hamkutaka kunisikiliza kwa kituo, wewe na kaka yako wote mlikuwa na haraka haraka kiasi cha kutopata yote ambyo nilitaka kuwaambieni.” Alikuwa anaongea Sheikh Mohamed kwa sauti yake nzito iliyojaa umwinyi mwinyi hivi kwa kutulaumu kiaina…

“Sasa ulivyorudi na kuniambia kuwa umepona, nikadhani labda umejuwa asili ya shida yako na kutatuliwa ipasavyo…” aliendelea…

“Kumbe bado kwa maoni yangu, ulikuwa kwenye safari ya kujijuwa na kujitambua… na sasa kwa vile umefikia hatua hii basi ukae kitako nikuelimishe…” alisema.

“Mwenyezi Mungu alituumba ili tumuabudu yeye, tena yeye tu na wala tusimshirikishe na miungu mingine, hayo ndiyo malengo hasa ya sisi kuumbwa, hata maumbile yetu yamewekwa kurahisisha zoezi hilo la kumuabudu yeye”

“Tukimuabudu yeye hatumuongezei chochote, na tusipomwabudu hatumpunguzii chochote, YEYE ambaye hakuna Mola apasaye kuabudiwa kwa haki ile YEYE, Yu hai na ni wa kudumu, halali wala kupatwa na usingizi. NDIYE Mola wa Mbingu na Ardhi na vilivyomo baina yake…”

“Anajuwa yaliyochificha mbele na nyuma, na katika sisi viumbe hatuna tujuwalo ama hatuwezi kujifunza (kupata elimu) ila kwa kuridhia kwake, na utukufu wake umeenea Mbinguni na ardhini na wala hawezi kushindwa kuvilinda viumbe vyake maana yeye ametukuka (aliye juu) na NDIYE MKUU.” Alisema Sheikh kisha akasoma aya katika mpangilio wake.

Alivyoanza kusoma nami nikakumbuka kile kikaratasi nilichopewa Kikokwe niwe nasoma mara kwa mara, maneno hayo yalikuwa sehemu ya dua ile niliyopewa huko.

Sheikh aliendelea na risala…

“Katika uumbaji wake (Mwenyezi Mungu) aliumba viumbe mbalimbali, na kila kiumbe kina mamlaka yake na mipaka yake katika kuyaendea mambo…”

Akatoa mifano mbali mbali jinsi viumbe wengi wanavyoishi humu duniani ikiwemo wadudu, hayawani na hatimaye majini na binadamu.

“Binadamu ndio tumepewa uhalifa (uongozi) katika dunia hii, yani tunatakiwa tuweze kuitawala dunia ipasavyo…”

“Majini nao wana tawala zao, wana mataifa yao, wana makabila yao, wana koo zao, wana mila zao na desturi zao, na wamepewa uwezo mbalimbali lakini pia wamewekewa mipaka…”

“Haifai kwa Majini kuingia kwenye tawala za kibinadamu na kuwasumbua watu kwa kuwapagawisha, kuwatia maradhi ama eti kujifanya wanawalinda…”

“Wao wana ‘ulimwengu’ wao na sisi binadamu tuna ‘ulimwengu’ wetu…”

“Hivyo ni makossa makubwa kwa Jinni kumuingia mwanadamu kwa namna yoyote ile kwa visingizio mbalimbali…”

“Idadi ya majini ni kubwa mara nyingi sana kuliko wanadamu, na kwa kuzingatia kuwa wao wanaishi muda mrefu kuliko wanadamu basi wingi wao huongezeka mara kwa mara kiasi cha kutapakaa duniani kote… kwa wingi wao huo hata kila mwanadamu aliye hai muda huu akikusanya majini sabini kila mmoja, basi binadamu wote watakusanya na wengi sana bado watabaki hawajakusanywa”

“Kuna elimu mbalimbali za kuweza kuwamiliki hawa majini, lakini ni moja ya elimu zilizokatazwa kwa kuwa hatimaye huleta hasara badala ya faida…”

“Lakini kwa kuwa Duniani humu kuna fitina mbalimbali ikiwemo fitna ya afya, mali, wake, waume, watoto nk basi baadhi ya watu hupatwa na husda, chuki na vijicho ambavyo huwadhuru wenzao, na kazi zote hizo hufanywa na hao majini ambao wameasi kwa kushirikiana na binadamu kwa namna mbalimbali za elimu ya kichawi”

“Elimu ya kukabiliana na matatizo hayo pia ipo, ipo kwa njia nyeusi na kwa njia nyeupe…”

“Hivyo tiba zipo, lakini kuna tiba kwa njia sahihi na zipo tiba za kwa njia ya kishirikina”

“Kufanya ushirikina na moja ya dhambi ambayo kama ikitokea umekufa bila ya kutubu basi ni dhambi isiyo sameheka labda kwa rehma zake Mola wetu maana yeye ndiye mjuzi zaidi”

“Hivyo basi ushirikina HAUFAI mbele za Mwenyezi Mungu”

“Kwakuwa tiba sahihi zipo, basi yatupasa kufuata tiba kwa njia zilizoelekezwa kwa miongozo ya dini yetu”

“Tiba isiyo sahihi utaijuwa kwa masharti yake ambayo hatimaye yanakupelekea katika kumuasi Mwenyezi Mungu kwa namna zote nne, kuwaza, kunena, kutenda na kutotimiza wajibu…”

“Sasa kwa kuwa ninyi mliamua kuishi kama binadamu…”

Tukawa tunaangaliana na Behat…

“…yafaa muendelee kuishi hivyo na kufuata maamrisho na makatazo yote ambayo yapo katika muongozo wa Qur’an na Sunna…”

“Pazi…!” aliniita Sheikh

“Mwenzako ana kiumbe tumboni…”

Nikawa manuangalia Behat tumboni sioni kitu zaidi ya ‘flat screen’ (hakuwa na hata kijitambi kidogo)

“Atazaliwa kiumbe ambaye sasa atakuwa mwanadamu kamili, wanenu hawatokuwa na passport ya kuingia Ujinini kama ilivyo kwenu hivi sasa ingawaje bado mpo nusu jinni.., wewe Pazi ni nusu binadamu nusu jinni na huyo mwenzako ni nusu jinni na nusu binadamu…”

Moja kwa moja nikaelewa tofauti yake kwa mmoja wetu alilala kwenye tumbo la uzazi binadamu ilhali mwingine alila kwenye tumbo la uzazi jinni.

Aliendelea kutupa risala pale weeee mwisho akasema…

“Tafuteni njia halali za kupata rizki zenu, hata kama itakuwa ni kutibu watu basi uifanye tiba iliyo sahihi kwa njia za kisunna (yaani kwa njia ya mafundisho ya Mtume Muhammad, Rehema na Amani zimwendee)

“Kitu kingine muhimu sana ni kwamba haifai kubeza dini nyingine, mfano hawa wenzetu wakristo tunaishi nao humu mjini, majumbani na kupeana heshima za kibinadamu, Kuna Kanisa kubwa kule Mantep (Sikuhizi wanaita ADEM), kuna Kanisa dogo kule miembe safa (jirani na kushukia MSALABANI) na kuna Kanisa kule Mwanakalenge. Hawa ni binadamu wenzetu na wana Imani yao thabiti katika kumwabungu Mungu wao kwa mujibu wa mafundisho yao, ukumbuke kuwa hawa pia kiongozi wao alipewa Kitabu kama ilivyo Qur’an kwa sisi. Usiwabeze wala kudharau Imani zao maana kuna wengine huenda wakawa bora mbele ya mwenyezi Mungu kuliko baadhi yetu, lakini haikatazwi kuwalingania ili waje katika uislam, tena kwa lugha iliyo nzuri na staha.”

“Kumbuka hata Nabii Mussa (Rehema na Amani zimfikie) alipoambiwa akamlinganie Firauni (Farao) aliambiwa akazungumze naye kwa upole licha ya kufuru kubwa aliyokuwa akiifanya. Kazi yetu ni kufikisha ujumbe lakini kumuongoa mja siyo kazi yetu, Allah mwingi wa Rehema sisi sote ni viumbe vyake, tusijitie ukiburi, YEYE Allah huamua atakavyo.”

Aliendelea…

“Vitabu cha elimu hiyo ya tiba zipo, vitafute ujifunze kwa walimu ukihitimu uendelee na tiba halali, kama hutoweza basi rejea kwenye kazi ya baba yako, ameshazeeka sasa afaa kusaidiwa sana…”

Alimalizia risala yake kwa kutusihi kuwa sisi bado ni nusu watu nusu majini, hivyo kiasili tuna nguvu za kijinni basi tuwe makini na maneno tuyasemayo na kujitahidi kujizuia hasira zetu maana huenda zikawa na athari kwa binadamu wa kawaida.

Tulirudi nyumbani na kumkuta mama akitusubiri kwa hamu.

“Enhe, mmeambiwaje huko?...” Mama aliuliza kwa shauku

Tukamwelezea yote na hatimaye mimi na mke wangu tukaamua kumtumikia Mwenyezi Mungu kwa kuwalingania watu katika dini huku nikiendeleza kazi ya Baba.

“Nadhiri yako sasa Mama inaenda kutimia…” nilisema.

Baada ya siku tatu, tuliaga kurudi Dar es Salaam kuendelea na maisha.

Leo hii tuna watoto watatu, tunaendeleza kazi ya uvuvi na uchuuzi kwa njia za kisasa, Baba na mama walishafariki, mama mkubwa pia alishafariki.

Tukapata Chakula cha mchana pamoja, kisha akanisindikiza nami nikachukuwa njia ya kurudi kwangu Upanga.

Jumamosi ile ilikuwa tulivu lakini nyumbani kwangu hapakuwa hivyo, nilikuta mke wangu amenuna, lakini nikamwambia hebu baada ya kula uje chumbani nimsimulie kisa chote nilichosimuliwa….
*******

Hakutaka nilale bali nimmalizie kisa chote maana muda tayari ulikuwa umeshaenda sana na siku Jumapili ilikuwa ndio inaingia (kwa mujibu was aa za na kalenda ya Gregori)…

Nilimkidhia haja yake baada ya kuona amevutiwa pia na kushangazwa japo kwa kuifupisha.

Mwishowe tuliendeleza ‘libeneke’ la mume na mke.

**************** MWISHO*************


Update!

Sheikh Mohamed alishafariki, Mzee Zahiri naye, Mwalimu Mwaloki, Mzee wa tiba Mlingotini, Mzee Njembi, Mcha Mungu wa Rufiji, Shariff Badowo, Shariff wa Kikokwe wote wametangulia mbele za haki.

Watu wengine ambao wametajwa katika simulizi hii sina update zao.

Imenibidi nifupishe ili niende na muda-huru niliokuwa nao maana ni mchache.



Niliamua kushea nanyi kisa hiki kama kumbukumbu ya kukumbuka uwepo wa Pazi na familia yake hapa Duniani kwa maana ya kwamba ile familia yote ilifariki kwa kuzama baharini miaka kumi na moja na siku arobaini na nane hivi ziliyopita walipokuwa wakitokea Unguja kuelekea matembezini Pemba kwenye MV. Spice Islander.

**********



Hakika sisi sote ni wa Mwenyezi Mungu na kwa hakika kwake tutarejea.



Shukrani sana kaka ,ALLAH awapunguzie adhabu ya kaburi wote waliotangulia katika hii simulizu yako

Sent using Jamii Forums mobile app
 
16. MAISHA MAPYA na UHURU - Ω

“Nakuusieni na kuihusia nafsi yangu juu ya kumcha Mwenyezi Mungu, amesema Mwenyezi Mungu (aliye takasika), … hiki (Qur’an) ni kitabu kisichokuwa na shaka ndani yake na muongozo kwa wale wamchao …”

“Sisi waislamu, tuna miongozo miwili, Qur’an na Sunna. Qur’an ni maneo ya Mwenyezi Mungu na Sunna ni matendo na mafundisho ya Mtume Muhammad (Rehema na Amani zimwendee).”

“Tushikamana na Kitabu cha Mwenyezi Mungu na Hadithi za Mtume, hatuwezi kupotea.”

Hayo yalikuwa maneno ya Walii (kipenzi) wa Mwenyezi Mungu wa Utete Rufiji (kama wenyeji walivyokuwa wakimwita) wakati akinukuu aya kutoka Qur’an akiwa anatujenga kiimani.

“Katika hii Qur’an Mwenyezi Mungu ameweka elimu ya toka watu wa mwanzo mpaka watu wa mwisho, elimu zote zimo ndani ya Qur’an, historia imo, mawaidha yamo, mifano imo, visa vimo, hesabu zimo, utaratibu wa kuendesha Dunia umo ndani ya Qur’an na hiki kitabu huhifadhi waumini kwa fitina iliyomo humu duniani…” aliendelea

“Ndani ya Qur’an kuna habari za watu waliokuwepo kabla yetu, kuna habari za watu baada ya sisi kuondoka, ni hakimu baina yetu na ni upambanuzi juu ya mambo mbalimbali. Haifai kuiacha.”

“Hii Qur’an ajabu zake hazimaliziki, wana zuoni hawashibi, kila siku wanatoa faida na hata majini walipoisikia Qur’an inasomwa, wakasema hakika sisi tumesikia Qur’an ya ajabu, … inaongoza kwenye uongofu kwa hiyo tumeiamini na wala hatutofanya ushirikina…, na kwa hakika utukufu wa Mola wetu mlezi umetukuka kabisa,… hana mke wa mwana…, … na kwa hakika wapumbavu miongoni mwetu walikuwa wakisema uongo uliopindukia juu ya Mwenyezi Mungu… nasi tulidhani kuwa watu na majini hawamsingizii uongo Mwenyezi Mungu…,”

Aliendelea yule mcha Mungu tutupatia mawaidha kupitia kitabu kitukufu Qur’an na kutusimulia habari za majini jinsi baadhi walivyo mrejea Mwenyezi Mungu na wengine waliendelea kukengeuka.

“Eee umesema mmetoka Bagamoyo!” aliuliza yule Walii,

“Rudini huko, kuna Sheikh Mkubwa Zawiani, utapata muongozo na elimu kadha wa kadha, kikubwa shikamaneni na hiki kitabu wala msikiache.” Alimaliza yule Walii na tukaagana na kuanza safari ya kurudi.

Nilikuwa mimi na mke wangu Behat, tulilala Rujiji Ikwiriri na siku ya pili tulifika Dar na moja kwa moja kwenda Bagamoyo.

Bagamoyo pale Zawian tukaambiwa tuende Lushoto kumtafuta Shariff Badowo ili atufanyia maombezi makubwa kabla ya kurudi Zawiani kwa ajili ya kumalizia elimu nasihi.

Tulienda Tanga, tukafika nymbani kwake lakini tukaambiwa amesafiri kwenda Mombasa, tukaambiwa tumtafute kijana mmoja pale Horohoro atatusaidia kufika kwake.

Yule kijana alikuwa ni mfanyakazi wa mabasi ya Modern (Mombasa – Tz – Zambia nk), alikuwa anaitwa Sarojo, alitusaidia sana hadi tukafika kwa Shariff Badowo na kufanya dua kubwa kubwa sijapata kuona na tulivyorudi Zawiani tulikuwa na utulivu mkubwa.
*********

Tukiwa Zawiani – Bagamoyo

“Tatizo lenu mlivyokuja mara ya kwanza hamkutaka kunisikiliza kwa kituo, wewe na kaka yako wote mlikuwa na haraka haraka kiasi cha kutopata yote ambyo nilitaka kuwaambieni.” Alikuwa anaongea Sheikh Mohamed kwa sauti yake nzito iliyojaa umwinyi mwinyi hivi kwa kutulaumu kiaina…

“Sasa ulivyorudi na kuniambia kuwa umepona, nikadhani labda umejuwa asili ya shida yako na kutatuliwa ipasavyo…” aliendelea…

“Kumbe bado kwa maoni yangu, ulikuwa kwenye safari ya kujijuwa na kujitambua… na sasa kwa vile umefikia hatua hii basi ukae kitako nikuelimishe…” alisema.

“Mwenyezi Mungu alituumba ili tumuabudu yeye, tena yeye tu na wala tusimshirikishe na miungu mingine, hayo ndiyo malengo hasa ya sisi kuumbwa, hata maumbile yetu yamewekwa kurahisisha zoezi hilo la kumuabudu yeye”

“Tukimuabudu yeye hatumuongezei chochote, na tusipomwabudu hatumpunguzii chochote, YEYE ambaye hakuna Mola apasaye kuabudiwa kwa haki ile YEYE, Yu hai na ni wa kudumu, halali wala kupatwa na usingizi. NDIYE Mola wa Mbingu na Ardhi na vilivyomo baina yake…”

“Anajuwa yaliyochificha mbele na nyuma, na katika sisi viumbe hatuna tujuwalo ama hatuwezi kujifunza (kupata elimu) ila kwa kuridhia kwake, na utukufu wake umeenea Mbinguni na ardhini na wala hawezi kushindwa kuvilinda viumbe vyake maana yeye ametukuka (aliye juu) na NDIYE MKUU.” Alisema Sheikh kisha akasoma aya katika mpangilio wake.

Alivyoanza kusoma nami nikakumbuka kile kikaratasi nilichopewa Kikokwe niwe nasoma mara kwa mara, maneno hayo yalikuwa sehemu ya dua ile niliyopewa huko.

Sheikh aliendelea na risala…

“Katika uumbaji wake (Mwenyezi Mungu) aliumba viumbe mbalimbali, na kila kiumbe kina mamlaka yake na mipaka yake katika kuyaendea mambo…”

Akatoa mifano mbali mbali jinsi viumbe wengi wanavyoishi humu duniani ikiwemo wadudu, hayawani na hatimaye majini na binadamu.

“Binadamu ndio tumepewa uhalifa (uongozi) katika dunia hii, yani tunatakiwa tuweze kuitawala dunia ipasavyo…”

“Majini nao wana tawala zao, wana mataifa yao, wana makabila yao, wana koo zao, wana mila zao na desturi zao, na wamepewa uwezo mbalimbali lakini pia wamewekewa mipaka…”

“Haifai kwa Majini kuingia kwenye tawala za kibinadamu na kuwasumbua watu kwa kuwapagawisha, kuwatia maradhi ama eti kujifanya wanawalinda…”

“Wao wana ‘ulimwengu’ wao na sisi binadamu tuna ‘ulimwengu’ wetu…”

“Hivyo ni makossa makubwa kwa Jinni kumuingia mwanadamu kwa namna yoyote ile kwa visingizio mbalimbali…”

“Idadi ya majini ni kubwa mara nyingi sana kuliko wanadamu, na kwa kuzingatia kuwa wao wanaishi muda mrefu kuliko wanadamu basi wingi wao huongezeka mara kwa mara kiasi cha kutapakaa duniani kote… kwa wingi wao huo hata kila mwanadamu aliye hai muda huu akikusanya majini sabini kila mmoja, basi binadamu wote watakusanya na wengi sana bado watabaki hawajakusanywa”

“Kuna elimu mbalimbali za kuweza kuwamiliki hawa majini, lakini ni moja ya elimu zilizokatazwa kwa kuwa hatimaye huleta hasara badala ya faida…”

“Lakini kwa kuwa Duniani humu kuna fitina mbalimbali ikiwemo fitna ya afya, mali, wake, waume, watoto nk basi baadhi ya watu hupatwa na husda, chuki na vijicho ambavyo huwadhuru wenzao, na kazi zote hizo hufanywa na hao majini ambao wameasi kwa kushirikiana na binadamu kwa namna mbalimbali za elimu ya kichawi”

“Elimu ya kukabiliana na matatizo hayo pia ipo, ipo kwa njia nyeusi na kwa njia nyeupe…”

“Hivyo tiba zipo, lakini kuna tiba kwa njia sahihi na zipo tiba za kwa njia ya kishirikina”

“Kufanya ushirikina na moja ya dhambi ambayo kama ikitokea umekufa bila ya kutubu basi ni dhambi isiyo sameheka labda kwa rehma zake Mola wetu maana yeye ndiye mjuzi zaidi”

“Hivyo basi ushirikina HAUFAI mbele za Mwenyezi Mungu”

“Kwakuwa tiba sahihi zipo, basi yatupasa kufuata tiba kwa njia zilizoelekezwa kwa miongozo ya dini yetu”

“Tiba isiyo sahihi utaijuwa kwa masharti yake ambayo hatimaye yanakupelekea katika kumuasi Mwenyezi Mungu kwa namna zote nne, kuwaza, kunena, kutenda na kutotimiza wajibu…”

“Sasa kwa kuwa ninyi mliamua kuishi kama binadamu…”

Tukawa tunaangaliana na Behat…

“…yafaa muendelee kuishi hivyo na kufuata maamrisho na makatazo yote ambayo yapo katika muongozo wa Qur’an na Sunna…”

“Pazi…!” aliniita Sheikh

“Mwenzako ana kiumbe tumboni…”

Nikawa manuangalia Behat tumboni sioni kitu zaidi ya ‘flat screen’ (hakuwa na hata kijitambi kidogo)

“Atazaliwa kiumbe ambaye sasa atakuwa mwanadamu kamili, wanenu hawatokuwa na passport ya kuingia Ujinini kama ilivyo kwenu hivi sasa ingawaje bado mpo nusu jinni.., wewe Pazi ni nusu binadamu nusu jinni na huyo mwenzako ni nusu jinni na nusu binadamu…”

Moja kwa moja nikaelewa tofauti yake kwa mmoja wetu alilala kwenye tumbo la uzazi binadamu ilhali mwingine alila kwenye tumbo la uzazi jinni.

Aliendelea kutupa risala pale weeee mwisho akasema…

“Tafuteni njia halali za kupata rizki zenu, hata kama itakuwa ni kutibu watu basi uifanye tiba iliyo sahihi kwa njia za kisunna (yaani kwa njia ya mafundisho ya Mtume Muhammad, Rehema na Amani zimwendee)

“Kitu kingine muhimu sana ni kwamba haifai kubeza dini nyingine, mfano hawa wenzetu wakristo tunaishi nao humu mjini, majumbani na kupeana heshima za kibinadamu, Kuna Kanisa kubwa kule Mantep (Sikuhizi wanaita ADEM), kuna Kanisa dogo kule miembe safa (jirani na kushukia MSALABANI) na kuna Kanisa kule Mwanakalenge. Hawa ni binadamu wenzetu na wana Imani yao thabiti katika kumwabungu Mungu wao kwa mujibu wa mafundisho yao, ukumbuke kuwa hawa pia kiongozi wao alipewa Kitabu kama ilivyo Qur’an kwa sisi. Usiwabeze wala kudharau Imani zao maana kuna wengine huenda wakawa bora mbele ya mwenyezi Mungu kuliko baadhi yetu, lakini haikatazwi kuwalingania ili waje katika uislam, tena kwa lugha iliyo nzuri na staha.”

“Kumbuka hata Nabii Mussa (Rehema na Amani zimfikie) alipoambiwa akamlinganie Firauni (Farao) aliambiwa akazungumze naye kwa upole licha ya kufuru kubwa aliyokuwa akiifanya. Kazi yetu ni kufikisha ujumbe lakini kumuongoa mja siyo kazi yetu, Allah mwingi wa Rehema sisi sote ni viumbe vyake, tusijitie ukiburi, YEYE Allah huamua atakavyo.”

Aliendelea…

“Vitabu cha elimu hiyo ya tiba zipo, vitafute ujifunze kwa walimu ukihitimu uendelee na tiba halali, kama hutoweza basi rejea kwenye kazi ya baba yako, ameshazeeka sasa afaa kusaidiwa sana…”

Alimalizia risala yake kwa kutusihi kuwa sisi bado ni nusu watu nusu majini, hivyo kiasili tuna nguvu za kijinni basi tuwe makini na maneno tuyasemayo na kujitahidi kujizuia hasira zetu maana huenda zikawa na athari kwa binadamu wa kawaida.

Tulirudi nyumbani na kumkuta mama akitusubiri kwa hamu.

“Enhe, mmeambiwaje huko?...” Mama aliuliza kwa shauku

Tukamwelezea yote na hatimaye mimi na mke wangu tukaamua kumtumikia Mwenyezi Mungu kwa kuwalingania watu katika dini huku nikiendeleza kazi ya Baba.

“Nadhiri yako sasa Mama inaenda kutimia…” nilisema.

Baada ya siku tatu, tuliaga kurudi Dar es Salaam kuendelea na maisha.

Leo hii tuna watoto watatu, tunaendeleza kazi ya uvuvi na uchuuzi kwa njia za kisasa, Baba na mama walishafariki, mama mkubwa pia alishafariki.

Tukapata Chakula cha mchana pamoja, kisha akanisindikiza nami nikachukuwa njia ya kurudi kwangu Upanga.

Jumamosi ile ilikuwa tulivu lakini nyumbani kwangu hapakuwa hivyo, nilikuta mke wangu amenuna, lakini nikamwambia hebu baada ya kula uje chumbani nimsimulie kisa chote nilichosimuliwa….
*******

Hakutaka nilale bali nimmalizie kisa chote maana muda tayari ulikuwa umeshaenda sana na siku Jumapili ilikuwa ndio inaingia (kwa mujibu was aa za na kalenda ya Gregori)…

Nilimkidhia haja yake baada ya kuona amevutiwa pia na kushangazwa japo kwa kuifupisha.

Mwishowe tuliendeleza ‘libeneke’ la mume na mke.

**************** MWISHO*************


Update!

Sheikh Mohamed alishafariki, Mzee Zahiri naye, Mwalimu Mwaloki, Mzee wa tiba Mlingotini, Mzee Njembi, Mcha Mungu wa Rufiji, Shariff Badowo, Shariff wa Kikokwe wote wametangulia mbele za haki.

Watu wengine ambao wametajwa katika simulizi hii sina update zao.

Imenibidi nifupishe ili niende na muda-huru niliokuwa nao maana ni mchache.



Niliamua kushea nanyi kisa hiki kama kumbukumbu ya kukumbuka uwepo wa Pazi na familia yake hapa Duniani kwa maana ya kwamba ile familia yote ilifariki kwa kuzama baharini miaka kumi na moja na siku arobaini na nane hivi ziliyopita walipokuwa wakitokea Unguja kuelekea matembezini Pemba kwenye MV. Spice Islander.

**********



Hakika sisi sote ni wa Mwenyezi Mungu na kwa hakika kwake tutarejea.



Shukran mkuu kwa kutujuza

Ila swali langu ni kua Pazi alikupa kisa hiki kma siri? Na je aliruhusu kisimuliwe kama mafundisho kwa wengine?
 
Shukran mkuu kwa kutujuza

Ila swali langu ni kua Pazi alikupa kisa hiki kma siri? Na je aliruhusu kisimuliwe kama mafundisho kwa wengine?
Yes, ilikuwa ni siri kwa miaka 10

Kwa kuwa hawapo tena Duniani nimeamua kuelimisha watu kiasi nilivyokumbuka

Alifunguka mengi, lakini mengine bado siyo sawa kuyazungumza
 
Yes, ilikuwa ni siri kwa miaka 10

Kwa kuwa hawapo tena Duniani nimeamua kuelimisha watu kiasi nilivyokumbuka

Alifunguka mengi, lakini mengine bado siyo sawa kuyazungumza
M naona kuna watu wana mazito zaidi ya haya uloyasimulia ila wamekaa kimya tatizo labda uandishi inakua kazi nzito sana

Ila mimi kma mimi nikikupa siri yangu bora ufe nayo na si rahisi kutoa siri
 
M naona kuna watu wana mazito zaidi ya haya uloyasimulia ila wamekaa kimya tatizo labda uandishi inakua kazi nzito sana

Ila mimi kma mimi nikikupa siri yangu bora ufe nayo na si rahisi kutoa siri
Mwenyewe alisema nikae nayo miaka 10 baada ya yeye kufariki dunia.

Lakini mengine hakuniruhusu kuyasema na sijayaandika wala sinto yaandika.

Nimezidisha mwaka 1 katika kutunza yale aliyoniruhusu kuyasimulia.

Bila shaka alijuwa ukomo wa umri wake, na huenda ikawa hawakufa majini maana maiti hazikupatikana...

Niishie hapo.
 
Back
Top Bottom