Taarifa za kibenki tulizonazo zinaonyesha kwamba tarehe 1 Mei 2004, Deep Green Finance ilifungua Akaunti Na. 011103024840 katika tawi la Corporate la Benki ya Taifa ya Biashara (NBC), Dar es Salaam. Kitu cha kwanza cha kushangaza ni kwamba siku hiyo ilikuwa ni Sikukuu ya Wafanyakazi (Mei Mosi) na ilikuwa siku ya mapumziko. Kitu cha pili cha kushangaza ni kwamba kampuni hii iliruhusiwa kufungua na kuendesha akaunti hiyo bila ya kuingiza wala kutoa fedha yoyote kwa zaidi ya mwaka mmoja kuanzia tarehe 1 Mei 2004 hadi tarehe 31 Julai 2005. Kitu cha tatu cha kushangaza ni kwamba pamoja jina la Deep Green Finance kuashiria kwamba kampuni hii ni taasisi ya kifedha, orodha ya taasisi za kifedha iliyotolewa na BOT tarehe 21 Agosti 2007 haionyeshi kwamba kampuni hii imewahi kusajiliwa na BOT kama taasisi ya kifedha!
Hata hivyo, kwa kipindi kifupi cha miezi minne kati ya Agosti 1 na Desemba 1, 2005 kampuni hii ilipokea jumla ya shilingi 10,484,005,815.39 kutoka Wizara ya Fedha na/au BOT. Fedha hizo zilitolewa kwa utaratibu ufuatao:
(a) Tarehe 1 Agosti 2005 BOT, kwa kutumia hundi Na. 241740, ilihamisha dola za Marekani 1,354,167.26 au shilingi za Tanzania 1,546,778,770.92 kwenda kwenye akaunti ya Deep Green Finance. Siku hiyo hiyo fedha hizo zote zilichukuliwa kutoka kwenye akaunti ya Deep Green Finance kwa utaratibu maalum wa haraka (special clearance) na kupelekwa mahali kusikojulikana na kwa madhumuni yasiyofahamika;
(b) Tarehe 1 Septemba 2005 BOT, kwa kutumia hundi Na. 015558, ilihamisha dola za Marekani 1,827,137.44 au shilingi za Tanzania 2,083,255,881.60 kwenda kwenye akaunti ya Deep Green Finance. Siku hiyo hiyo jumla ya shilingi 2,083,333,333.33 zilichukuliwa kwa mara nyingine tena kwa kutumia utaratibu huo huo maalum wa haraka na kupelekwa kusikojulikana;
(c) Tarehe 8 Septemba 2005 Tangold Ltd. ilihamisha dola za Marekani 100,256.62 au shilingi za Tanzania 114,611,746.80 kwenda kwenye akaunti ya Deep Green Finance. Itakumbukwa kwamba Tangold Ltd. ni kampuni ya kigeni iliyoandikishwa nchini Mauritius tarehe 5 Aprili 2005 na kupewa Cheti cha Kutimiza masharti ya Tanzania tarehe 20 Februari 2006. Hata hivyo, mawaziri kadhaa wa Serikali ya Rais Jakaya Kikwete wameendelea kudai kuwa kampuni hiyo inamilikiwa kwa asilimia mia moja na Serikali ya Tanzania. Wakurugenzi wa Tangold Ltd. ni Gavana Daudi Balali, Waziri wa Miundombinu Andrew Chenge, Katibu Mkuu (Fedha) Gray Mgonja, Katibu Mkuu (Maji) Patrick Rutabanzibwa na Katibu Mkuu (Ofisi ya Waziri Mkuu) Vincent Mrisho. Kufuatana na barua ya Mkaguzi na Mdhibiti Mkuu wa Hesabu za Serikali kwa BOT ya tarehe 21 Desemba 2006, Tangold Ltd. ililipwa na BOT dola za Marekani 13,736,628.73 kwa kupitia akaunti isiyojulikana ya Nedbank Ltd. ya Afrika Kusini na kwa madhumuni yasiyojulikana;
(d) Tarehe 16 Septemba 2005 jumla ya shilingi 129,000,000.00 zilitolewa kutoka kwenye akaunti ya Deep Green Finance na kuwekwa kwenye akaunti ya muda maalum (FDR);
(e) Tarehe 3 Oktoba 2005 jumla ya shilingi 2,083,333,333.33 za Wizara ya Fedha zililipwa kwa utaratibu maalum wa haraka kutoka kwenye akaunti ya Deep Green Finance. Inaelekea fedha hizo zililipwa kabla BOT haijaingiza fedha yoyote kwenye akaunti ya Deep Green Finance kwa vile tarehe 4 Oktoba 2005 BOT ilihamisha dola za Marekani 1,789,075.89 au shilingi 2,083,891,765.35 kwenda kwenye akaunti hiyo;
(f) Tarehe 8 Oktoba 2005 jumla ya shilingi 39,761,397.98 zilihamishwa kutoka kwenye akaunti ya Deep Green Finance kwenda Tangold Ltd.;
(g) Tarehe 31 Oktoba 2005 jumla ya shilingi za Tanzania 2,083,333,333.33 fedha za Wizara ya Fedha zilihamishiwa kwenye akaunti ya Deep Green Finance;
(h) Tarehe 2 Novemba 2005 dola za Marekani 1,821,095.57 au shilingi za Tanzania 2,083,653,279.68 zilihamishwa kutoka kwenye akaunti ya Deep Green Finance kwenda kusikojulikana;
(i) Tarehe 30 Novemba 2005 BOT ilihamisha shilingi za Tanzania 2,083,333,333.33 zikiwa fedha za Wizara ya Fedha kwenda kwenye akaunti ya Deep Green Finance. Siku moja baadaye, dola za Marekani 1,817,199.52 au shilingi za Tanzania 2,184,610,383.04 zilihamishwa kutoka kwenye akaunti ya Deep Green Finance kwenda kusikojulikana;
(j) Tarehe 10 Desemba 2005 shilingi 100,940,489.71 zilihamishwa kutoka Tangold Ltd. kwenda kwenye akaunti ya Deep Green Finance. Hii ilikuwa ni siku nne tu kabla ya Uchaguzi Mkuu wa Desemba 14, 2005 kufanyika nchini kote;
(k) Tarehe 19 Desemba 2005, siku tano baada ya Uchaguzi Mkuu kufanyika, dola za Marekani 88,722.17 au shilingi za Tanzania 104,755,554.09 zilihamishwa kutoka kwenye akaunti ya Deep Green Finance kwenda kusikojulikana;
(l) Tarehe 9 Februari 2006 shilingi 3,836,800.00 zilihamishwa kwenda akaunti ya mawakili wa Deep Green Finance, IMMMA Advocates, iliyoko benki ya Standard Chartered. Haijulikani kama fedha hizi zilikuwa ni kwa ajili ya malipo ya mawakili hao au la;
(m) Malipo ya mwisho kutoka kwenye akaunti ya Deep Green Finance yalifanywa tarehe 22 Novemba 2006 ambapo jumla ya shilingi 14,465,000.00 zilihamishiwa katika akaunti isiyojulikana ya benki ya Standard Chartered na kwa matumizi yasiyojulikana;