SFO watoa tuhuma tisa dhidi ya Chenge
2009-02-09 10:07:58
Na Mwandishi Wetu
Makachero wa Uchunguzi wa Makosa Makubwa ya Jinai (SFO) wa Uingereza waliokuwa wanachunguza tuhuma za mlungula uliotolewa kwa aliyekuwa Waziri na Mwanasheria Mkuu wa Serikali ya Tanzania, Andrew Chenge, ili kuruhusu ununuzi wa rada ya bei mbaya, wamejenga tuhuma kuu tisa ambazo zinaweza kumfikisha mwanasiasa huyo kizimbani.
Tuhuma hizo zimo kwenye ripoti ya SFO ambayo vyombo vya kisheria vya serikali ya Tanzania vilikabidhiwa tangu Machi mwaka jana, lakini hakuna hatua zozote zilizochukuliwa dhidi ya Chenge na mshirika wake wa karibu katika sakata hili, Mkurugenzi Mkuu wa Shirika la Umeme nchini (Tanesco), Dk Idriss Rashidi.
Tuhuma ambazo zimetajwa na SFO dhidi ya watuhumiwa hao wawili, wakiwa ni miongoni mwa watuhumiwa 10 wanaochunguzwa katika kashfa ya rada iliyoigharimu Tanzania Dola za Marekani milioni 40, ni kwamba Chenge na Dk Rashidi walikuwa ni watu muhimu katika kufikiwa kwa mkataba wa ununuzi wa rada hiyo iliyouzwa kwa serikali na shirika la kuuza vifaa vya kijeshi la Uingereza, BAE System.
Mbili, Chenge anatajwa kuwa karibu na wakala wa kampuni ya Siemens Plessey System (SPS) iliyokuwa ikisukuma mpango huo, Sailesh Vithlani na kwamba ukaribu wao ulijitokeza wazi wakati wa kumalizia makubaliano ya mkataba wa ununuzi wa rada hiyo.
Tatu, SFO wanadai kwamba uhusiano wa karibu kati ya Chenge na Vithlani ulikuja katika kipindi ambacho wakala huyo, (Vithlani) anadaiwa kuwaeleza wafanyakazi wa SPS kuwa alikuwa na makubaliano ya zamani na mapya, makubaliano hayo katika mawasiliano yao yalimaanisha rushwa.
Nne, makachero hao wanamtuhumu Chenge kuwa alifanya maamnuzi mengi ya kisheria ambayo yalionekana wazi kwa jinsi mkataba wa malipo ulivyofikiwa katika ununuzi wa rada hiyo.
Tano, SFO pia wanatuhumu kwamba maamuzi hayo kwa vyovyote vile yanaonyesha kwamba hayakuzingatia maslahi ya Tanzania katika ununuzi wa rada hiyo.
Kwa maana hiyo kulikuwa na kitu kilichomfanya Chenge asiweke maslahi ya taifa mbele katika kutoa maoni hayo ya kisheria ambayo yalichukuliwa katika kufikia maamuzi ya mkataba wa kununua rada.
Sita, makachero hao wanaunganisha matukio hayo hapo juu na mmiminiko wa ghafla wa fedha kwenye akaunti ya Chenge kisiwani Jersey zikitokea Frankfurt.
Saba, Chenge anatuhumiwa na makachero hao kwamba ili kuficha kujulikana kwa fedha hizo, alianzisha kampuni ya Franton ambayo inamiliki akaunti hiyo, lakini pia akaibua anwani mjini London ambayo ilitumika kwa mawasiliano, kuficha kuonekana kwake moja kwa moja katika miliki ya fedha hizo.
Nane, SFO wanamtuhumu Chenge kwamba kutokana na ujanjaujanja wa kuficha vyanzo vya fedha hizo, benki hiyo iliamua kuvunja mahusiano naye kama mteja kwa kuwa hakuwa tayari kutoa maelezo ya kina juu ya fedha hizo.
Tisa, makachero wanatuhumu kwamba malipo ya Dola za Marekani 600,000 kwa Rashidi yanaonyesha kwamba hakuwa mpokeaji pekee wa rushwa kutoka kwa BAE System, ila ni mtu muhimu katika kuisambaza kwa kuwa watuhumiwa hao wawili (Chenge na Rashidi) walikuwa watu muhimu katika ununuzi wa rada hiyo.
Tuhuma hizi dhidi ya Chenge zinajulikana kwa vyombo vya kisheria vya nchi, lakini hadi sasa hakuna hata chombo kimoja cha kiserikali kimefungua kinywa kueleza hatma ya uchunguzi wa mwanasiasa huyo.
Chenge mara kadhaa amekanusha kuchukua rushwa ya rada, na alisema fedha alizojiwekea benki kisiwani Jersey ni vijisenti, lakini mara mbili ametoa kauli za kutatanisha juu ya vyanzo wa Dola za Marekani milioni 1.5 katika akaunti yake akieleza ni malipo yake halali kwa kazi za uanasheria lakini mara nyingine akasema ni urithi na akiba ya familia.
Katika fedha hizo alidai mkewe anamiliki asilimia 25.
SFO wamekuwa wanachunguza sakata la rada kwa miaka mitatu sasa, na kuna kila dalili imekuwa ikipewa ushirikiano na serikali tofauti na Kenya ambako walitangaza wiki iliyopita kufunga uchunguzi wa wizi wa Aglo Leaseing kutokana na kutokuwapo kwa dalili za kufungua mashitaka dhidi ya watuhumiwa wa kashfa hiyo.
Hadi sasa ni Vithlani pekee amefunguliwa mashitaka rasmi mahakamani kutokana na kashfa ya rada, lakini wakati mashitaka hayo yanawasilishwa katika Mahakama ya Hakimu Mkazi Kisutu, mshitakiwa hakuwapo na tangu wakati huo anasakwa kuja kujibu mashitaka yake.
SOURCE: Nipashe