Baraza la Mawaziri latupa muswada wa...
2006-12-29 10:02:24
Na Mwinyi Sadallah, Zanzibar
Baraza la Mapinduzi Zanzibar (BLM), limekataa kupitisha rasimu ya muswada wa sheria ya kuanzisha mamlaka ya kupambana na rushwa na maadili ya viongozi.
Rasimu hiyo iliwasilishwa katika Baraza hilo na Katibu Mkuu katika Wizara ya Nchi Ofisi ya Rais Katiba na Utawala Bora Zanzibar, Bw. Mahadhi Juma Maalim.
Naibu Mwanasheria Mkuu wa Zanzibar, Bw. Omar Makungu, alisema awali muswada huo ulikuwa uwasilishwe katika kikao cha Baraza la Wawakilishi cha Oktoba mwaka huu.
Alisema sababu kubwa iliyotolewa na Baraza la Mawaziri ni kwamba waandaaji wa muswada huo, lazima kwanza wakachukue uzoefu wa sheria kama hizo zinavyotumika katika nchi za Jumuiya ya Madola.
Hata hivyo, Naibu Mwanasheria Mkuu huyo alisema muswada huo uliandikwa kwa kutumia uzoefu wa sheria zinazotumika katika nchi za Jumuiya ya Afrika Mshariki, ikiwemo Uganda, Tanzania Bara na Kenya.
Bw. Makungu alisema kwa mara ya mwisho mwaka 2005, walishindwa kuwasilisha muswada huo kutokana na harakati za uchaguzi mkuu.
Sheria hii ya kupambana na rushwa na kuweka maadili ya viongozi haitakwenda tena Januari, kwa vile Baraza la Mawaziri wametutaka tuchukue uzoefu katika nchi za Jumuiya ya Madola,, alisema Naibu Mwanasheria Mkuu.
Hata hivyo, alisema mswada huo umekusanya mambo mbalimbali ikiwemo viongozi kutangaza mali zao katika kipindi cha mwezi mmoja tangu kuteuliwa katika nyadhifa zao.
Alisema pia sheria hiyo inapiga marufuku wanasiasa kutoa sadaka au takrima katika harakati za uchaguzi na itakuwa ni kosa kwa kiongozi atakayethibitishwa kufanya hivyo.
Kwa mujibu wa Ibara ya 68 (1) ya rasimu ya muswada huo, itakuwa ni makosa kwa mtu kutoa fedha, chakula viburudisho na huduma za malazi katika kipindi cha uchaguzi.
Katika rasimu ya muswada huo, Ibara ya 35 (1) inasema kila kiongozi wa serikali atatangaza mali yake, mke na watoto wake baada ya kupata wadhifa.
Kwa mujibu wa rasimu hiyo, mtu yeyote atakayekwenda kinyume na sheria hizo, ikiwemo kujihusisha na rushwa adhabu yake ni faini ya Sh. zisizozidi milioni 10 au kutumikia adhabu ya miaka isiyozidi 10 jela, au adhabu zote kwa pamoja.
Naibu Mwanasheria Mkuu huyo alisema kazi ya kuuboresha mswada huo imekwishakamilika ikiwemo kukusanya maoni ya wanasheria na Wajumbe wa Baraza la Wawakilishi kufanyiwa semina na kuijadili rasimu hiyo.
Alieleza kuwa mpango wa kuanzishwa sheria hiyo unafadhiliwa na Shirika la Mpango wa Maendeleo la Umoja wa Mataifa (UNDP).
Hatufahamu ni lini muswada huu utakwenda na sasa tunazingatia kupata uzoefu wa kutosha kwa nchi za Jumuiya ya Madola, alisema Bw. Makungu.
Walipokuwa wakijadili rasimu ya muswada huo katika semina waliyoandaliwa Wajumbe wa Baraza la Wawakilishi baadhi ya wajumbe kutoka CCM walisema kutokana na mazingira ya kisiasa ya Zanzibar wana wasiwasi sheria hiyo itatumika vibaya kwa kukomoana.
Kikao cha Baraza la Wawakilishi kinatarajiwa kuendelea tena mwezi ujao kujadili miswada mbalimbali ya sheria.
* SOURCE: Nipashe 29/12/2006