Hili ni swali la msingi na jibu langu ni ndiyo. Yafuatayo ni maoni yangu ya jinsi gani tukidhamiria kwa kweli tutaweza kupunguza rushwa ndogondogo.
http://h1.ripway.com/Mwanakijiji/Maoni/kubadilishamfumo.pdf
Niliandika hoja hiyo hapo juu kabla ya kusoma habari hii hapa toka gazeti la "Mwananchi"
Dawa ya mishahara ya walimu yapatikana
Na Mwandishi Wetu
KERO ya kuchelewa kwa mishahara ya walimu wa shule za msingi inahitimishwa mwezi huu baada ya serikali kujitia kitanzi cha kuhakikisha walimu wote wanalipwa mishahara yao tarehe 23 ya kila mwezi.
Vile vile serikali imeingia mkataba wa kibashara na benki ya NMB ili kuiwezesha kulipa mishahara ya walimu na watumishi wengine wa halmashauri ifikapo kila tarehe 23, hata kama haijapata fedha kutoka serikalini.
Walimu wa shule za msingi ni kada ambayo licha ya kuchelewa kwa mishahara yao, pia wamekuwa wakisumbuka kulipwa, wanapokwenda benki huelezwa kuwa mishahara haijaingia kwenye akaunti zao.
Akitangaza uamuzi huo jana, Waziri wa Fedha, Zakia Meghji, alisema baada ya kukutana na wakurugenzi wa halmashauri zote nchini, uongozi wa Wizara ya Elimu na Mafunzo ya Ufundi, Tawala za Mikoa na Serikali za Mitaa, Menejimenti ya Utumishi na Benki ya Microfinance (NMB), wameamua mishahara ya watumishi wa halmashauri iwe inalipwa tarehe 23 kila mwezi.
Meghji alisema mshahara ni haki ya mtumishi, pia mi mkataba kati ya mwajiri na mwajiriwa na kuongeza kuwa ni haki ya mwajiriwa kulipwa kwa wakati.
Rais mstaafu, Benjamin Mkapa aliwahi kutoa agizo la mishahara ya watumishi kulipwa tarehe 25 ya kila mwezi, lakini limekuwa likitekelezwa kwa watumishi wa serikali kuu tu, huku watumishi wa halmashauri wakiteseka hadi mwezi mwingine.
Waziri Meghji, alisema katika kuondoa vikwazo na visingizio vya kuchelewesha mishahara, Hazina Makao Makuu watalazimika kufanya kazi hata siku za mwisho wa wiki na kwamba atakayesababisha mishahara kuchelewa atawajibishwa.
"Kuchukua payroll (orodha ya malipo) Hazina Makao Makuu na Hazina ndogo mikoani kutafanyika hata kama ni siku za mwisho wa wiki au sikukuu," alisema.
Alisema atakayesababisha kuchelewa kwa mishahara hiyo atawajibishwa hata kama serikali italazimika kulipa riba kwa NMB kwa sababu wana mkataba wa biashara.
Alisema utaratibu huo utaanza kwa watumishi wanaolipwa kupitia halmashauri za wilaya ambao wengi ni walimu wa shule za msingi na watumishi wa kada ya afya, lakini baadaye utahusisha walimu wa sekondari.
Waziri Meghji alibainisha sababu za kuchelewa kulipwa kwa wakati kuwa ni kuchelewa kuchukua orodha ya malipo (payroll) kutoka hazina, dhana ambayo imepitwa na wakati na kwamba serikali imeamua kutafuta njia muafaka kuondoa tatizo hilo.
Katika kufanikisha ulipaji mishahara mapema, serikali imekubaliana na NMB kuboresha huduma za malipo ya mishahara kwa kufungua vituo vya malipo ya mishahara nje ya makao makuu ya wilaya.
Meghji alisema NMB itasaidia kufungua akaunti benki hata kama mtumishi hana fedha za kufungulia na benki hiyo itaanzisha mfumo wa kutoa taarifa za mishahara kwenye akauti ya mtumishi kupitia ujumbe wa maandishi katika simu.
Alisema kuanzia sasa, orodha ya malipo itakuwa inaandaliwa Hazina tarehe 12 ya kila mwezi, kutumia huduma ya usambazaji vifurushi (courier) kupeleka kwenye hazina ndogo zilizoko kila mkoa na msambazaji anatakiwa kuchukua orodha hiyo bila kukosa saa 2.00 asubuhi tarehe 13 ya kila mwezi.
Meghji alisema hatua nyingine ni msambazaji kuwajibika kuwasilisha orodha hiyo hazina ndogo ya kila mkoa kabla ya saa 2.00 asubuhi ya tarehe 15 kila mwezi, wakurugenzi watendaji wanawajibika kuzichukua saa 2.00 terehe 15 ya kila mwezi na watatakiwa kuziwasilisha pamoja na hundi za malipo ya mishahara kwenye benki ifikapo tarehe 22 ya kila mwezi.
Katika kukabiliana na mabadiliko hayo, wakurgenzi wametakiwa kupunguza idadi ya siku za kushughulikia malipo ya mishahara kwa nia ya kuleta tija, kusimamia kwa karibu suala la mishahara, kuchukua orodha ya malipo kutoka Hazina ndogo kwa tarehe iliyopangwa na kuhakikisha wanawasilisha benki orodha pamoja na hundi ya malipo kabla ya tarehe 22 ya kila mwezi.