MAKALA
Nakala chapishi
Mtumie mwenzio
Jiandikishe utaarifiwe
Tunajenga jamii ya kiharamia
Paul Mabuga Machi 19, 2008
WIKI iliyopita nilikuwa katika mji mdogo wa Maganzo ambao ni maarufu Tanzania na nje, hususani katika soko la vito la Ubelgiji, kutokana na biashara ya almasi. Niliona kipande cha chuma chenye maandishi ya kuwekwa kwa jiwe la msingi la ujenzi wa barabara ya lami, kimengolewa.
Barabara hii ni ile ya kutoka Mpakani mwa Mkoa wa Mwanza na Shinyanga eneo la Nyasamba hadi Tinde na nyingine ya kutoka Nzega kupitia Tinde hadi Isaka. Zote hizi zilijengwa kwa msaada wa jumuia ya Ulaya na jiwe lake la msingi liliwekwa na rais mstaafu Benjamin Mkapa.
Niliozungumza nao juu ya kitendo hicho wanaona ni jambo la kawaida, na kufikia hatua ya kusema, kuna jamaa alihamisha kuganga njaa. Lakini kingine cha ajabu, wanasema, Maganzo ni mji wa matanuzi na kila siku ni Jumapili, ukikosa ngana (almasi), tafuta cha kuuza uishi.
Pengine huu nao ni ufisadi katika ngazi fulani, hata hivyo, kuwalaumu wananchi hawa kwa hujuma hii bila kwenda mbali zaidi inaweza kuwa ni haraka mno maana hii ni dalili ya mambo mengi yaliyofichika, juu ya suala na dhana ya uzalendo inayosistiza, pamoja na mambo mengine, kujali zaidi maslahi ya umma kabla ya ya binafsi. Nani katufikisha hapa ndiyo mjadala wa haki.
Jambo muhimu zaidi katika barabara hii, ni kwamba imejengwa kama hatua muhimu ya kuunganisha ukanda wa kati, kwa maana ya njia ya kutoka Bandari ya Dar es Salaam, kupitia Dodoma hadi mpakani na nchi ya Burundi. Balozi wa Rwanda nchini Zeno Mutimura aliwahi kusema ukanda huu ni muhimu sana kwao kutokana na unafuu wake ikilinganishwa na ukanda wa kaskazini.
Wakati barabara ya ukanda wa kati zimeharibiwa na mvua mwaka jana, wafanyabishara wa Rwanda walilazimika kusafirisha bidhaa zao kupitia ukanda wa kaskazini, kutoka bandari ya Mombasa, Kenya kupitia Uganda hadi Kigali umbali wa kilometa 1792. Njia ambayo ni aghali ikilinganishwa na ukanda wa kati, bandari ya Dar es Salaam, kupitia Isaka hadi Kigali ambao una mrefu wa kilometa 1620.
SIETCO wakitengeneza barabara Manyoni
Watanzania kwa wakati huo walipiga kelele baada ya maelezo ya Serikali kuwa, mkandarasi aliyepewa zabuni ya kujengwa barabara ya ukanda huo kipande cha kati ya Manyoni na Singida, Sietco, ana uwezo mdogo na ndiyo maana alikuwa nyuma ya ratiba ya utekelezaji kwa miezi mingi.
Hapa swali la kujiuliza ni kwamba kwa nini unampa kazi mkandarasi ambaye uwezo wake ni mdogo na kwa nini usifanye tathmini ya kina ya uwezo wake kabla ya kutoa zabuni? Ama kuna kishawishi? Ni kitu gani hasa kinaonekana kama kishawishi na kuna tofauti gani katika vigezo vya uzalendo kati ya hali hii na wale jamaa wa Maganzo?
Ukweli ni kwamba Sietco, wana rekodi mbaya linapokuja suala la ujenzi wa barabara katika eneo la Afrika ya Mashariki, hasa baada ya kuwa wametimuliwa katika kazi ya upanuzi wa mradi wa Umeme wa Owen nchini Uganda mwaka 1996.
Katika kumbukumbu za Bunge la Uganda, kikao cha Aprili 12, 2000, inaelezwa kuwa kampuni hiyo ilishindwa kufanya kandarasi hiyo nchini Uganda kutokana na mpango duni wa kazi, udhibiti na mawasiliano duni na kukosekana mamlaka na uwajibikaji miongoni mwa watendaji wake na uwezo mdogo .
Sietco walishinda kazi hiyo nchini baada ya kuonekana kuwa gharama zao zipo chini ikilinganishwa na wakandarasi wengine 43 waliokuwa wamejitokeza kufanya kazi hiyo, mnamo mwaka 1993. Hata juhudi za kumaliza suala hili halikufanikiwa hadi pale serikali ya Uganda ilipovunja mkataba na kampuni hiyo Septemba, 2006. Hapa tuwasifu Waganda.
Kingine cha kushtua kidogo, ni kwamba taarifa ya mapendekezo ya mpango wa kuimarisha mapambano dhidi ya rushwa nchini Uganda ya Mwaka 1998, ulinukuu vyombo vya habari juu ya madai ya watendaji wa Sietco kwamba walitumia asilimia 30 ya gharama ya mradi kuwahonga maafisa wa Bodi ya Umeme nchini humo.
Kauli iliwahi kutolewa na serikali kuwa mkandarasi huyu alipewa kazi hii, eti kwa sababu gharama zake zilikuwa chini ikilinganishwa na wengine.Pia iliwahi kukiri kuwa kushindwa kukamilika kwa zabuni ya kampuni hiyo ndani ya muda ni ushahidi kuwa uwezo wa mkandarasi huyu mdogo na serikali imejifunza.
Katika mazingira kama haya, kwa nini kusiwe na hofu kuwa katika kutoa kazi kwa mkandarasi ambaye hana uwezo kuna mazingira yanayotia shaka, uzalendo ulikuwa wapi ama uliharibiwa na nini hadi tathmini ya kina isiwepo. Ni kwa nini kazi itolewe kwa kampuni ambayo inadaiwa kulalamika kuwa iliwahi kutoa rushwa watoa zabuni serikalini na tena si mbali, ni hapo nchi jirani ya Uganda.
Linapokuja suala la kutoa zabuni, na katika mazingira kama haya, kuna dalili kuwa wasomi wetu wanawachuuza wananchi. Wanasahau yale maneno tuliyokuwa tukikakarishwa shuleni, kwamba, aliyepata bahati ya kupata elimu ni sawa na aliyetumwa mbali kwenda kutafuta chakula na jamii yake yenye njaa na kinachotarajiwa ni yeye kurudi na nafaka na kuwakomboa ndugu zake.
Wao badala yake wanashiba na kuvimbiwa huko ugenini na wanatangaza kimya kimya kutorudi kwa waliowatuma. Tunaona kwa dalili nyingi, hawa jamaa waliotumwa na jamii yenye njaa, wana mali zisizo na maelezo, na bahati yao hakuna mwenye ubavu wa kuwauliza kwa dhati kuwa wamezipata wapi. Inanikumbusha habari moja ya skari polisi wa cheo cha chini mwenye kitambi na hoja kuwa atamkimbizaje mwizi.
Tanzania imefikia pahala, wasomi na hususani viongozi wamewasaliti wananchi, hawatendi tena yale ambayo wanyonge wanayatarajia, haya yote yanatokana na kukosekana kwa maadili ya kitaifa. Mhadhiri mmoja wa chuo kikuu aliwahi kuonya kuwa ni hatari sana kuwa na msomi asiyekuwa na maadili. Lakini wananchi nao wanaona, kusoma ma kusikia juu ya jinsi wanavyosalitiwa na wasomi na viongozi wa nchi yao.
Wasiwasi wangu ni kwamba kuna siku ambayo wananchi watachoka, baada ya kutotimia kwa matarajio yao. Watageuka na kuwa kama Watanzania wa Maganzo, na nchi haitakalika.
Source Raia Mwema