Mimi naamini rushwa itaisha Tanzania kama Watanzania tukiamua kupambana nayo bila woga au kificho katika kila kona ya nchi yetu.
Angalia hili swala la mafisadi, tuliwahi kuambiwa hadharani na Waziri Mkuu Pinda, Mwanasheria Mkuu Mwanyika na Mkuu wa polisi nchi kwamba mafisadi ni watu ambao wana utajiri mkubwa hivyo haiwezekani kuwafikisha mahakamani maana kufanya hivyo nchi itawaka moto na kushindwa kuiongoza. Lakini hadi hii leo tumeshaona vigogo mbali mbali waliowahi kuwa na nyadhifa za juu ndani ya serikali wamefikishwa mahakamani na nchi bado haijawaka moto na kuna habari wengine zaidi watafikishwa mahakamani.
Angalia swala la Mkapa, ambapo JK aliwahi kutwambia kwamba, "Mwacheni Mzee wetu apumzike kwa amani." lakini juzi tumesikia kauli ya Waziri Mkuu Pinda akisema kwamba Serikali haimugopi Mkapa na hakuna aliye juu ya sheria Tanzania kama kuna dalili za kujitajirisha kwa njia za haramu.
Pale mambo ya nje kulikuwa na rushwa ya hali ya juu katika utoajia wa Passport. Membe alipowekwa pale kama Waziri wa mambo ya nje akapambana nayo na kwa muda mfupi sana passport zikawa zinatoka haraka mno tena bila kutoa hongo. Na wakati huo huo nchi ilikuwa imegubikwa na giza nene kutokana na kukosekana umeme. Aliamrisha inunuliwe jenereta ili kuwawezesha wafanyakazi wachape kazi, aliamrisha zipangwe shift 3 za wafanyakazi wote wanaohusika na utoaji wa passport kutokana na maombi mengi ya passport za Watanzania ndani na nje ya nchi. Na alihakikisha anapambana na wote wale ambao walitumia nyadhifa zao pale katika ofisi ya utoaji wa passport kujitajirisha.
Kama Watanzania tutaendelea kutoa rushwa ili tupate huduma haraka na yale tunayotaka ndani ya serikali au taasisi mbali mbali za umma halafu kulalamika pembeni kwamba, "Nchi hii rushwa imezidi" basi kamwe rushwa haitaisha lakini tukiamua kupambana nao wanaodai rushwa ili watuhudumie pamoja na kuwa ni haki yetu kupata huduma hizo basi hakuna kitakachoshindikana.
Kama serikali ikiamua kutoa somo kali kupitia TV, Redio na magazeti kuhusu haki za Watanzania kupata huduma bila kutoa rushwa na kuweka sheria kali dhidi ya watoaji na wapokeaji rushwa ikiwamo kifungo cha miaka 10 au zaidi, kazi ngumu na kufukuzwa kazi basi ushindi dhidi ya rushwa unaweza kabisa kupatikana.
RUSHWA NI ADUI WA HAKI, SITAPOKEA WALA KUTOA RUSHWA.