SIMULIZI: Mkufu wa Malkia wa Goshen

Nazipataje dadake, Fanya kunitafunia nimeze mie



 
Shunnie naifananisha Roho yako na ya malkia Sandarus, Asante Sana dada ake , hizi zinasaidia Sana ktk ma traffic jams
 
MKUFU WA MALKIA WA GOSHEN -- 003

Simulizi za series



“Nyie binadamu mnafanya nini Tanashe?” Malkia akatahamaki zaidi kwani lilikuwa ni swali lilelile aliloulizwa akiwa ndotoni. Na sasa hapo ndipo akajua ya kwamba yale aliyoyaona ndotoni yalikuwa ni yale yatakayotukia mbele yake.

Sasa afanyaje?

Hakuwa na muda wa kumueleza Zura juu ya yale aliyopata kuyashuhudia ndotoni. Waliongozana na bibi wale kama ilivyokuwa kwa mujibu wa ndoto mpaka pale walipofika kwenye nyumba kubwa nyeusi ambamo waliingia na mjadala kuhusu mkufu ukazuka baada ya muda mfupi, bibi wale wakiwa wanataka kuuona na kuugusa.

Hii ndiyo nafasi! Akaamini Malkia Sandarus. Kama kweli alikuwa anataka kuokoka dhidi ya wale vigagula basi ilimbidi atumie mwanya huu vema. Aliuvua mkufu wake akiwa anajua fika ya kwamba utawaunguza wale viumbe.

Alipomkabidhi bibi mmojawao, ulimuunguza akaudondodha chini. Malkia akauwahi mkufu wake na kuwanyooshea kana kwamba silaha.

“Kaa mbali!” Alifoka. Bibi wale walisogea mbali na walihofia. Walikumbatiana kwa woga na ni wazi nyuso zao za kizee zilizojikunja zilionyesha hofu. Malkia alimtazama Zura akamtaka anyanyuke kitini waondoke upesi. Zura akatii.

Walisogelea mlango, bado Malkia akinyooshea mkufu wake kwa wale bibi, wakaondoka kumfuata farasi waliyemkwea na kumuamrisha aondoke haraka! Farasi alikimbia upesi na ndani ya muda mfupi alikuwa amemezwa na giza asionekane hata mahali alipoelekea.

“Umeruhusuje akaondoka?” Alilalama bibi mmoja kana kwamba hakuwepo wakati tukio linatokea.

“Ila hawezi akafika mbali,” Mwingine naye akasema.

“Ndio, hawezi akafika mbali. Ila tumeshakosa ule mkufu. Vipi kama wakiupata wachawi wengine?” Aliuliza mmoja kwa jazba. Ilikuwa ni ngumu kweli kuwatofautisha tangu kila mmoja alikuwa na jicho moja tu.

“Endapo wakiupata wachawi wengine basi itakuwa mbaya sana kwetu.” Aliendelea kuongea.

“Sasa tutafanyaje?” Akauliza mwingine.

“Inabidi tuwafuatilie mpaka pale tutakapoupata mkufu huo. Hatuwezi tukaipoteza hii nafasi!” Alilonga mmoja kwa shari. Haraka bibi hao watatu waliungana wakatengeneza mtu mmoja mkubwa mno mwenye macho matatu.

Mikono yake ilikuwa imejaza kimraba na miguu yake ilikuwa mipana kama shina la gogo. Kabla hajaondoka kwenda kuwafuatilia Malkia na Zura, alinguruma kama simba. Kunguru wote waliokuwa wanazunguka hilo eneo wakakimbia wakitawanyikia kila pande.

Mtu huyo mkubwa, ama tunaweza kumuita jitu, alikimbia upesi akitupa miguu yake chini na kusababisha kishindo kikubwa, kishindo ambacho hata kama ungelikua maili moja mbali basi ungelipata kukisikia.

Kichwa chake kilichokuwa juu kilimuwezesha kutazama kila pande na basi akawa anabashiri wapi anaowatafuta wameelekea. Kila alipopita miti ilitikisika na viumbe wakakimbia kuokoa maisha yao.

Baada ya kukimbia kwa muda wa dakika nne tu, sauti yake ya kishindo ikawafikia Malkia na Zura ambao bado walikuwa juu ya mgongo wa farasi.

“Malkia, wanakuja!” Zura alisema kwa hofu. Malkia hakutia neno, zaidi alimwamrisha farasi wake aongeze mwendo.

Haikujalisha ni kwa namna gani farasi alivyokimbia, jitu lilizidi kuwakaribia zaidi na zaidi. Hata kwa mtoto angeliweza kubashiri ndani ya muda finyu Malkia na Zura watakamatwa.

“Malkia, anazidi kutukaribia!”

Malkia aligeuza uso wake kutazama. Hapo farasi akajikwaa. Alidondoka akawamwagia Malkia na Zura mbali! Malkia alibiringita mara tatu wakati Zura akibiringita mara tano kabla hajatulia tuli.

Malkia alinyanyua uso wake akamtazama Zura, hakuonekana kama ana fahamu. Alimtazama na farasi wake akamuona anagugumia kwa maumivu.

Kwa muda kidogo hakujali kama anakimbizwa bali kutazama usalama wa wenziwe. Alipokuja kutazama anayewakimbiza, alishangaa kumuona tayari amemfikia mguuni! Alijaribu kunyanyuka, akakandikwa kofi zito akazirai.


Jitu lilimbeba Zura na Malkia likaondoka nao. .
.
.
.
.
* HAKUNA ZAIDI … ZAIDI YA MKUFU WA MALKIA WA GOSHEN! *
.
.
.
.
.
Jitu lilifika nyumbani kwake akawatua mateka wake. Punde akaparanganyika na kuwa wale bibi watatu.

“Tunawaua?” Mmoja aliuliza.

“Hapana!” Mwingine akajibu. “Tunamuhitaji zaidi akiwa hai.”

“Kwanini?”

“Huyu ni Malkia!” Alifoka. “Tukimtumia huyu Goshen itakuwa chini yetu.”

“Tukimtumiaje?”

“Tukimtumiaje! – Kwani hujui? Mbona akili yako imelala sana wewe?”

Kukawa kimya kidogo.

“Tukikamata kichwa cha Malkia, tutapata yale yote tunayoyataka toka Goshen!” Alisema mmojawao. Walifurahi wakionyesha vinywa vyao vyenye uhaba wa meno.

Ulikuwa ni wasaa mzuri sasa kurudi kwenye ardhi ya Goshen baada ya kufukuzwa huko kwa muda mrefu tangu pale walipogundulikana ni wachawi.

Ilikuwa ni desturi. Tanashe ni tawala ya wachawi ambao wamerundikwa hapo toka kwenye tawala mbalimbali baada ya kuvumbuliwa toka kwenye jamii zao ya kwamba ni wachawi.

Kwa mtu yeyote pale anapogundulikana kuwa na sifa zozote za kilozi, basi adhabu yake huwa ni kumtupia kwenye ardhi hiyo ya Tanashe – ardhi iliyolaaniwa.

Ardhi isiyo na maji wala chakula. Na kama mtu ni kweli alikuwa mlozi, akishaingizwa Tanashe huo unakuwa mwisho wake kwani hawezi toka tena humo kurudi tawala aliyotokea.

Mipaka yake imetiwa dawa madhubuti ambayo hakuna mchawi yeyote anayeweza kuvuka na kwenda kwenye tawala yoyote za karibu. Huko ndani ya Tanashe atajua anakula ama kunywa nini. Atajua anaishije muda uzidi kusonga.

Wachawi wengi walipoteza familia zao. Hawakuweza tena kuona aidha watoto, wake ama waume zao baada ya kupelekwa Tanashe.

Si tu kwamba kwasababu hawakuweza kutoka humo, bali pia binadamu wa kawaida wasio wachawi hawakusogelea tawala hiyo. Watu kadhaa ambao walijaribu kuingia humo waliishia kuwa vitoweo na isijulikane hata walipoelekea.

Sifa kubwa ya tawala hiyo ya Tanashe ilikuwa ni kutokuwa na alama yoyote ya binadamu pale jua linapochomoza. Kama ungelikuwa karibu na mpaka ukatazama ndani ya tawala hiyo muda wa mchana, usingeona chochote bali mithili ya jangwa.

Lakini ifikapo usiku, mji unakua na unaweza ukawaona watu wanakatiza katiza. Na kama basi upo karibu, si ajabu kuona mtu anakutazama huku akikulaghai kwa kukuita.

“Usisogelee karibu na Tanashe!” Lilikuwa ni mojawapo ya onyo maarufu walilokuwa wanapewa watoto na aidha wazazi wao ama watu wazima.

Hakuna mtoto aliyepotea kwa kuingia humo alafu akapatikana. Inasemekana wakiingia humo nao wanawakuwa walozi.

Kuelekea upande wa kaskazini wa tawala ya Tanashe ndipo kulipokuwa kunapatikana tawala ya Devonship chini ya katili Jayit. Tofauti ndogo zilizokuwepo kati ya tawala hizi ni swala la uongozi na pia mawio na machweo ya jua.

Tanashe haikuwa na kiongozi, bali tu kila eneo lina mchawi anayelitawala. Lakini pia vilevile jua lilikuwa linachomoza na kuzama kwenye tawala hiyo. Kinyume na Devonship, mtawala alikuwa mmoja tu tawala nzima: Jayit, na ndani ya tawala hiyo jua halikuwahi kamwe kuonekana!

Mkufu wa Malkia uliviringishwa ndani ya kikaratasi cheusi na mmoja wa wale bibi. Alipomaliza kuufungasha vema mkufu huo, aliwatazama wenzake wakaanza kujadili ni namna gani ya kuufanya mkufu huo.

Ila wakiwa wanajadili wakagundua kuna umuhimu wa kujua ni wapi mkufu huo ulipotokea kwa minajili kwamba ndipo itakuwa rahisi kwao kuuongoza lakini hata kuuamrisha kutokana na matakwa yao.

“Tunaweza kutawala Tanashe na mkufu huu!”

“Sio tu Tanashe. Tunaweza tukarejea Goshen kwenye familia zetu na kutawala huko!”

Walienda uwani mwa nyumba yao kubwa, huko waliteka kioo cha saizi ya kati na fuvu mbili za vichwa vya binadamu. Waliviweka pamoja juu ya meza.

Meza hiyo pia ilikuwa imeshikiliwa na mifupa ya miguu ya binadamu. Walifungua kile kikaratasi kilichofichama mkufu kwa malengo kwamba wautoe mkufu huo na kuutazamisha kwenye kioo ili wapate kuona kwa kupitia kioo chao, wapi haswa chimbuko la mkufu huo.

Mmojawao akiwa ameushikilia huo mkufu kwa kile kikaratasi ili asipate kuungua, aliutupia huo mkufu juu ya kioo, na kisha kwa pamoja wakasema maneno yasiyoeleweka.

Punde macho ya fuvu zile mbili za binadamu yakaanza kufuka moshi wa kijani. Moshi huo ulitanda karibia eneo lote. Bibi wale walitabasamu wakijua sasa pale moshi utakapokoma wataweza kuona yale wanayoyataka ndani ya kioo chao cha ajabu.

Moshi ukakoma.

Walitazama kwenye kioo upesi wakiwa na nyuso za hamu. Ajabu hawakuona chochote!

“Unaona kitu?” Mmoja aliuliza.

“Hapana, sioni. Najiona mwenyewe na nyie.”

Punde kioo kikaanza kupiga ufa kana kwamba ukuta. Kklaakk! Kakkaakakakk! Kakaaakkak! Kufumba kufumbua kikapasuka kwanguvu. Vipande vyake viliruka juu na vikawaingia machoni mwa wale bibi wakaishia kulalama kwa maumivu wakishikilia nyuso zao.

Haikupita punde, wakasikia sauti za fisi mbele ya nyumba yao. Kila mmoja alinyofoa jicho lake akalipangusa dhidi ya vioo na kuyarudisha tena usoni.

“Nani huyo?” Mmoja aliuliza.
“Si mwingine bali ni Faki!” Mwingine akajibu.
“Atakuwa anataka nini?”

Swali hilo lilikosa majibu. Waliuchukua mkufu kwa kutumia kile kitambaa mmojawao akauficha sehemu za siri na kisha wakaenenda huko nje waliposikia sauti ya fisi akibweka.

Walikuta fisi wakubwa karibia mia moja na hakukuwa na alama yoyote ya binadamu.

“Unahitaji nini Faki?” Bibi mmoja aliuliza. Wote walikuwa wamekunja mikono yao wakiiweka kifuani.

Fisi walikaa kitako, kutoka nyuma yao akasogea fisi mkubwa kuliko wote. Alipojongea mbele aligeuka na kuwa binadamu mrefu mwenye misuli ya kutosha.

Alikuwa mweusi mwenye ndevu nyingi. Uso wake ulifanana na fisi kabisa. Hakuwa amevalia kitu chochote, hivyo alikuwa uchi mnyama. Alisogea karibu na bibi wale watatu akapandisha nyusi moja juu.

“Nahitaji mlichokichukua kwangu,” Alisema Faki kwa kujiamini.

“Kipi tumechukua kwako?” Bibi mmoja aliuliza. Faki akatabasamu kwa kejeli.

“Hamjaingia kwenye himaya yangu leo hii?” Aliuliza. Bibi wakatazamana na kisha mmoja akajibu:
“Tumeingia lakini tulikuwa tunafuata kitu chetu.”

Faki akatabasamu.

“Hamuwezi mkafuata kitu chenu kwangu. Kitu kikiwa kwenye himaya yangu, ni changu. Naomba mnipatie sasa hivi!”

“Faki, hatuwezi tukakupa kisicho chako,” alisema bibi mmoja.

“Ila mliweza kuingia kwenye eneo langu, si ndio?” Akauliza Faki. Kukawa na kaukimya kafupi.

“Sina muda wa kupoteza hapa na nyie vikongwe. Naombeni kilicho changu niende.”

“Unakijua hata hicho unachodai ni chako?” Aliuliza bibi.

“Najua ndio,” akajibu Faki. “Ni binadamu – wawili!”

“Tutakupa mmoja.”
“Nataka wote!”
“Tutakupa mmoja tukagawane.”
“Nimesema nataka wote!”
“Basi hautopata kitu!” Alisema bibi mmoja kwa kujiamini akimtazama Faki machoni.

Faki alirudi nyuma kuungana na fisi wenzake. Ndani ya muda mfupi aligeuka mwili akawa fisi mkubwa kama alivyokuwa hapo awali. Pasipo kupoteza muda, bibi nao wakajikusanya na kuwa mtu mkubwa mno mwenye macho matatu.

Alinguruma kama simba akielekeza mdomo wake angani. Faki alibweka naye kwanguvu kisha akaamrisha fisi mia moja aliokuja nao wamshambulie yule mtu mkubwa – jitu!

Kufumba na kufumbua ikawa vita!


Fisi wakamrukia yule jitu wakamrarua na kumng’ata. Lakini naye jitu asiwe nyuma alikuwa anawakamata na mkono wake mkubwa akawavunja vunja ama kuwatupia mbali.

Makelele ya fisi na ya jitu yalitapakaa. Malkia Sandarus na Zura waligutuka toka kwenye usingizi mzito wa kutokuwa fahamuni. Walikuwa wamefungiwa kwenye kichumba kidogo cheusi chenye dirisha dogo juu.

Kwa mujibu wa dirisha hilo, anga lilikuwa linaanza kung’aa kuelekea asubuhi ya mapema zaidi.

“Zura, mkufu upo wapi?” Aliuliza Malkia. Alikuwa anaogopa, kama ungelimuona tu uso wake basi ungeling’amua hilo.

“Sijui Malkia wangu,” Zura alijibu. Malkia alipapasapapasa shingo yake lakini hakuona kitu, mkufu haukuwepo! Aliendea mlango wa chumba hicho akajaribu kuufungua, akashindwa.

Zura alimtengea Malkia wake mkono kama ngazi, Malkia akaupanda na kuchungulia nje kwa kupitia ka mwanya ka dirisha. Huko nje akaona pambano kubwa kati ya fisi na lile jitu kubwa. Aliperuzi huku na kule kutafuta lakini hakuona mkufu wake.

Ndani ya muda mfupi wakasikia mlango unafunguliwa. Haraka walifuata mlango huo, wakamkuta farasi wa Malkia! Ilikuwa ni ajabu. Kwa kutumia mdomo wake, farasi huyo alipindua kitasa akijua fika ndaniye mulikuwa na dereva wake, malkia wake: Sandarus.

Ilikuwa ni bahati kwa farasi huyo kuachwa peke yake pale Zura na Malkia walipotwaliwa. Yule jitu, ama wale bibi, hawakuona umuhimu wa kumchukua farasi huyo. Walimuacha wakitumai hatodumu muda mrefu kabla hajaliwa na viumbe vingine ndani ya Tanashe.

Hawakufahamu kwanini farasi huyo alikuwa ni wa Malkia. Hawakujua kwamba kiumbe huyo ana uwezo wa kumtafuta Malkia wake popote pale ndani ya maili tano. Mnyama pekee ndani ya Goshen anayemjua bwana wake na hayupo radhi kumtumikia mtu mwingine yeyote zaidi ya huyo.

“Roob!” Aliita Malkia akimkumbatia farasi wake. Alimkwea yeye pamoja na Zura akamuamuru kuzunguka ndani ya nyumba ile kubwa wakitafuta mkufu wake.

Walizunguka kote lakini hawakuuona. Walizunguka uani wakawa wanachungulia mpambano ambao bado ulikuwa unaendelea – kati ya fisi na jitu. Lengo lao lilikuwa ni kutafuta mkufu wa Malkia. Jitu alikuwa amejeruhiwa vibaya mno akivuja damu, na hata fisi nao hawakuwa wengi – kama arobaini tu ndio bado walikuwa hai.

Kitendo cha Malkia kuchungulia, mkufu ulianza kuhangaika ndani ya sehemu za siri za jitu.

Ulijinyongorota ukaenda huku na kule kwa nguvu ukitaka kuchoropoka. Ulimsumbua jitu huyo kiasi kwamba akapoteza kabisa atensheni kwenye mpambano. Fisi walimshambulia vibaya mno. Walimdondosha chini na kuendelea kumng’ata. Mkufu ulitoka ndani ya vazi lake ukaenda upesi kwenye mkono wa Malkia. Haraka Malkia akamruhusu farasi wake akimbie!

Sauti ya farasi akikimbia ikakamata masikio ya fisi. Faki – fisi mkubwa kiongozi – akaamuru fisi wote kumkimbiza farasi yule aliyebebelea binadamu. Fisi wote walio hai wakaanza kumfukuza farasi huyo kwa kasi. .

.
.
.* HAKUNA ZAIDI … ZAIDI YA MKUFU WA MALKIA WA GOSHEN! * .
.
.
.
.
Farasi wa Malkia alikimbia upesi. Mbio zake hazikuweza kumithilika na zile za fisi wanaomkimbiza. Japokuwa fisi walikuwa wanakimbia taratibu ukilinganisha na farasi wa Malkia, hawakuonekana kuchoka ama dalili za kukata tamaa!

Kama ingelikuwa muda ulikuwa upande wao basi wangelihakikisha wanawapata binadamu wale juu ya mgongo wa farasi, ila jua la asubuhi lililokuwa linachomoza likawakatisha hamu, tena wakiwa wamekaribia kumkamata farasi huyo aliyetupa miguu yake kuvuka mpaka na kuingia ardhi ya Goshen.

Fisi hao waligeuka na kuanza kukimbia kurejea kwenye makazi yao. Kadiri walivyokuwa wanakimbia, na jua lilivyokuwa linachomoza, walikuwa wanageuka kuwa binadamu.
.
.
.
.
MKUFU WA MALKIA WA GOSHEN!
.
.
.
Lako jicho!
Ndo naanza kushuka nayo
 
MKUFU WA MALKIA WA GOSHEN -- 04

Simulizi za series


ILIPOISHIA

Fisi hao waligeuka na kuanza kukimbia kurejea kwenye makazi yao. Kadiri walivyokuwa wanakimbia, na jua lilivyokuwa linachomoza, ndivyo walivyokuwa wanageuka kuwa binadamu.

ENDELEA

Mwishowe walipotea isijulikane wapi wameelekea. Malkia na Zura waliwatazama wakiyoyoma huku mioyo yao ikidunda kwa mjazo wa hofu na mashaka.

Ilibaki kidogo tu wangekuwa habari nyingine, waliamini hivyo. Walimeza mate wakiwa wanahema kabla hawajageuza kwenda kwenye makazi ya Zura.

Jambo hilo lilifanyika kwa siri mno, Malkia hakuhitajika kuonekana. Zura alihakikisha hilo linatimia mpaka wanafika nyumbani kwake alipokuta mzoga wa mumewe ukiwa umelazwa chumbani.

Zura aliumizwa sana na hilo tukio, akalia sana. Kwa kusaidiana na Malkia walifukua kaburi na kumzika mwanaume huyo ndani ya nyumba ili wasipate kuonekana, kisha wakajipumzisha.

Walikuwa wamechoka mno. Karibia usiku wote hawakuwa wamelala, lakini pia walitumikisha viungo vyao haswa kurandaranda huku na kule hivyo walivyojilaza tu kitandani usingizi haukuwaonea huruma, ukawakomba.

Walikoroma kwa usingizi baada tu ya muda mfupi.
.
.
.
.
.
.
***
.
.
.
.
.
Jua lilisimama, na kama ingelikuwa ni nyakati za sasa za kutumia saa basi bila shaka kwa muda huo ilikuwa ni saa nne ya asubuhi.

Siku ilikuwa nzito haswa. Uwanja mkubwa wa tawala ya Goshen ulikuwa umefurika mno, na kabla haujaingia ndani basi ungekutana na rundo kubwa la rafasi waliowaleta wageni toka tawala mbalimbali waje kushuhudia kusimikwa kwa kiongozi mpya wa ardhi hiyo, Bwana Fursa.

Nyimbo zilizosindikizwa na vifaa vitamu kama vinubi na firimbi, ziliita kwenye kila kona ya uwanja. Watalaamu wa kucheza walijimwaya uwanjani wakisogeza muda taratibu, huku wasiwe peke yao wakasindikizwa na vinywaji na vyakula vya kumwaga.

Katikati ya uwanja bendera ya kila tawala ilisimikwa ikawa inapeperuka kwa madaha. Kulikuwa kuna tawala tano uwanjani kwa kujibu wa idadi ya bendera; bendera nyekundu yenye jua jeupe katikati ikiwakilisha tawala ya Maam; bendera nyeusi yenye matone meupe kumi na saba ikiwakilisha tawala ya Kusi; bendera nyeupe yenye mikuki miwili meusi iliyokinzana ikiwakilisha Goshen; bendera ya bluu yenye mchoro mkubwa wa samaki ikiwakilisha Theon; na bendera ya mwisho ikiwa na rangi nyeusi, nyekundu na nyeupe bila ya mchoro wala picha yoyote ikiwakilisha tawala ya Bhotu.

Karibia waanchi wote wa Goshen walikuwepo hapo. Wachache ambao hawakuwepo walikuwa aidha vilabuni wanakunywa pombe zao ama wapo mashambani wanawajibika.

Lakini kila mtu alikuwa na ratiba ya kuja eneo hilo, kilichowatofautisha ni ratiba tu. Miongoni mwao wengi walikuwa wanangojea jua likikaribia kufika katikati ya anga ndipo waanze safari kujisogeza.

Kwa mujibu wa desturi ya Goshen, mfalme husimikwa pale jua linapokuwa katikati ya anga. Hiyo ni ishara ya kuonyesha utawala wake utakuwa wa haki usio na pendeleo na pande yoyote. Unapofika muda huo tu, watu hufurahia wakimtazama mfalme akivekwa taji la kifalme.

Matarumbeta hupigwa, vigelegele vinapigwa na jeshi linasalimu amri mbele yake.

Watu wote uwanjani wakiwa wanangoja muda huo adhimu, Fursa akiwa katikati ya wapambe wake watatu, aliitwa kando na mwanamke mnene ila mwenye umbo lisilojificha. Alikuwa ni malkia, mke mkubwa wa mfalme aliyefariki. Aliinama akamng’ata Fursa sikio kabla mwanaume huyo hajanyanyuka upesi na kusogea mbali kidogo na umati.

“Naona unanisahau, Fursa.” Alisema malkia huyo akiwa amekaza sura.

“Sijakusahau Veda.” Akajitetea Fursa.

“Kumbuka bila mimi usingelikuwa hapa.”

“Najua, Veda. Tutaongelea tu haya mambo, usijali.”

“Lini na leo ndio unaapishwa kuwa mfalme?”

“We jua tutaongea kwani kuna haraka gani? Endapo tukifanya haraka tutawapa watu mashaka!”

“Sawa. Ila kaa ukijua kwamba, ukimwaga mboga mie n’tamwaga ugali. Ukianza mie n’tamaliza!”

Baada ya Veda kutoa tisho hilo, alitimka. Fursa aliminya mdomo wake kisha naye akarejea kule alipokuwa awali. Nyuma yake alikuwa anaongozana na mababa watatu waliobebelea mikuki ya chuma.

Ila huyu baba ana siri gani na Veda, mke mkubwa wa mfalme?

Turudi nyuma.

Kabla mfalme hajafa, Veda alikuwa ana mahusiano ya siri na Fursa. Nyuma ya mgongo wa Mfalme watu hawa walikuwa wanafanya mapenzi na huku wakipeana ahadi motomoto za kuja kutawala Goshen siku za usoni.

Ilifikia kipindi Veda, mke mkubwa wa mfalme, akashika ujauzito lakini kuepusha shari alikunywa madawa na kutoa mimba hiyo, lakini bado penzi lao halikukoma, Veda akiwa amechochewa kuingia kwenye mahusiano hayo kutokana na uwezo mbovu wa Mfalme kumpa huduma kitandani.

Mwishowe, Veda alimtilia sumu mumewe kwenye kikombe cha kahawa. Tokea hapo, Mfalme akawa dhoofu lihali. Hakuweza kutembea wala kuongea vema. Macho yake yaliingia ndani akawa haoni.

Mdomo wake ulikuwa mkavu muda wote na mapigo yake ya moyo yakawa ya kusuasua ama kupiga kwa mfululizo. Alikuwa hivyo mpaka kufa kwake. Japokuwa kuna muda alishuhudia mke wake, Veda, akiwa anazini na Fursa, alishindwa kufanya chochote wala kumwambia yoyote. Hata machozi hakuwa nayo!

Sasa Veda alikuwa anamkumbushia Fursa miadi waliyowekeana: ya kwamba kiti cha umalkia ni chake pekee. Hakuna atakayekikaimu, na tena wakishakuwa mume na mke, Fursa hatokuwa na mwanamke mwingine yoyote isipokuwa yeye.

Fursa alikuwa ameshasahau miadi hiyo. Madaraka matamu bwana! Akili yake yote ilikuwa ni kutazama namna gani atakuwa anajisikia akiwa kwenye kiti cha kifalme kinachoogopwa na kuheshimiwa na wote baada tu ya miungu yao.

Muda ulisonga kwenye ardhi ya Goshen na sasa ulibakia muda mchache sana kwa jua kuwasili katikati ya anga. Shamrashamra zikawa kubwa zaidi na watu, wale waliokuwa mbali na hilo eneo, wakanyoosha miguu yao kuja eneoni maana kitovu cha shughuli kilikuwa kimekaribia kuwadia.

Fursa alinyanyuka akajongea katikati ya uwanja. Hapo aliketi akakutana na wazee watatu wa baraza ambao mmojawao alikuwa amebebelea mto mwekundu wenye taji la dhahabu na vito vya thamani.

Taji hilo ndilo lilikuwa lakaribia kupachikwa kwenye kichwa cha Fursa ambaye macho yake ya tamaa yaligoma kubanduka kwenye taji hilo lililokuwa linametameta na kuita.

Alijikuta anameza mate kana kwamba anangojea chakula kitamu kilichokuwa kinamtesa na harufu yake nzuri.

Ikiwa imebakia sasa sekunde, na Fursa akiwa amesimama tayari kwa ajili ya kupachikwa kofia na watu wote wamesimama kushuhudia hilo, ghafla mawingu yasijulikane yametoka wapi yalijikusanya kwa kasi na kubana anga. Jua halikuonekana tena na kukawa giza.

Hali hiyo ilitengeneza hofu.
.
.
.
.
.
. * HAKUNA ZAIDI … ZAIDI YA MKUFU WA MALKIA WA GOSHEN! *
.
.
.
.

Farasi wa Malkia Sandarus alisimama ghafla akapandisha miguu yake ya mbele juu. Mgongoni mwake alikuwa amembelea Malkia lakini pia Zura. Wanawake hao walikuwa njiani kwenda uwanjani kutengua ama kupinga kusimikwa kwa Fursa kama mfalme.

Ila kabla hawajafika huko, walistaajabu hali ya hewa inabadilika ghafla mbele ya macho yao kiasi kwamba hata farasi pia alihofia!

Walitahayuri, na bado wakiwa hapo wakasikia sauti kubwa ya kishindo inakuja. Haraka Zura alikamata bega la Malkia akapayuka:

“Malkia, ni Jayit anakuja!”

Malkia alikuwa mgumu kuelewa, ila baada ya muda mfupi alielewa kile alichokuwa anakinena Zura: Jayit anakuja! Hakuna mahali Jayit anakanyaga pakawa na mwanga wa jua. Kila mtu anajua kwenye utawala wa Devonship hakuna kitu kinaitwa jua wala mwanga wake.

Ina maana sasa Jayit anakuja!

Ilikuwa ni taharuki. Malkia hakutaka kuacha tawala yake akimbie. Alitaka kuhakikisha anamuona Jayit lakini pia kumzuia asidhuru watu wake. Akiwa humo tahamuni, akakumbuka jambo, ila kwa muda alikuwa amekawia kufanya lolote.

Wakati akiwa amelala kuna muda alihisi kifua chake kikiwa cha moto. Ilikuwa ni mkufu wake ukiwa unampasha habari juu ya yale ambayo yangetokea muda si mrefu mbele. Ulionyesha ujio wa Jayit, lakini pia ukionyesha yale ambayo angeyafanya mwanaume huyo kwenye tawala ya Goshen.

Masikini Malkia hakuweza kusikia wala kuona yote hayo. Usingizi mzito mno aliokuwa nao ulimnyima hiyo fursa. Alikuwa amechoka mno na mwili wake ulikuwa unahitaji sana kupumzika.

“Malkia, tuondoke!” Alisisitiza Zura. “Huu sio muda wa kubakia tena hapa. Kama kweli unaipenda Goshen, ni bora tukaondoka sasa. La sivyo utauwawa na hautopata tena fursa ya kuwa nao wala kuwasaidia.”

Huo ulikuwa ukweli mchungu kwa Malkia. Machozi yalimtiririka. Alimgeuza farasi wake akamkimbiza kuelekea upande karibu zaidi wa mpaka wa Goshen.

Waliridhia kuelekea utawala wa Maam, huko wakafanye kuyachimbua mengi juu ya mkufu ule alionao Malkia. Waliamini kwasababu mkufu huo umetoka huko basi ni lazima kutakuwa kuna mabaki ya historia juu yake. Historia ambayo inaweza ikawapa muelekeo wa kipi cha kufanya na namna gani ya kufanya.

Kutokana na giza lililokuwepo, baada ya muda hatukuwaona walipoelekea. Hata rangi nyeupe ya farasi ilikuwa imemezwa.
.
.
.
.
.
***
.
.
.
Farasi wengi weusi walisimama mbele ya uwanja mkubwa wa Goshen. Watu wegine walikuwa wamekimbia kwa kuogopa, ila wengi wao walibakia eneo hilo wakiamini ya kwamba ndipo ni salama kuliko pengine.

Wanajeshi walikuwa wamejaa, hivyo walitumai endapo litakapotokea lolote basi wanajeshi hao watalinda pumzi zao.

Wanaume waliokuwa wamebebelewa kwenye farasi hao weusi walikuwa ni watu wenye miili mikubwa. Walikuwa na nywele nyingi na mikononi mwao walikuwa wamebebelea mapanga marefu yaliyokuwa yanametameta kwa ukali.

Toka katikati ya farasi hao ambao walikuwa wamajipanga kwa nidhamu kubwa, alitokea mwanaume mrefu mwembamba. Nywele zake zilikuwa ndefu mno zilizogota kwenye mabega. Macho yake yalikuwa mekundu kama amevuta marijuana. Mdomo wake ulikuwa mweusi kama wa kunguru. Alitisha kumtazama. Alitisha akikutazama.

Alikuwa ni Jayit!

Mkononi mwake alikuwa na panga jembamba zaidi ya walinzi wake, ila lilikuwa refu na kishikizi chake kilikuwa na fuvu dogo la kichwa cha binadamu.

Uwanja mzima ulikuwa kimya. Japokuwa wengine hawakuwa wanamuona Jayit, walikuwa wanahisi uwepo wake. Kitendo cha jua kuzizima ilikuwa ni alama tosha.

Jayit alitembea kumfuata Fursa. Alipofika hata salamu hakutoa, akasema:

“Nahitaji makaburi.”

Sauti yake ilikuwa ya chini lakini nzito mno. Fursa kabla hajajibu alitazama kwanza uwanja mzima, akaona jinsi watu wanavyomtazama. Hakutaka kuwaangusha, tena akiwa ni kiongozi ambaye muda si mrefu kuna uwezekano wa kuwa mfalme.

Alikataa kumpa Jayit uwanja wa makaburi, lakini pia akamtaka mwanaume huyo aondoke kwenye ardhi ya Goshen upesi!

Jayit alitabasamu tabasamu la upande mmoja kisha akaguna. Alimtazama Fursa kwa macho yake makali. Fursa alitetemeka mwili mzima. Jayit alitabasamu tena kisha akaliza vidole vyake … pat!

Mara giza likaongezeka maradufu. Sasa hakukuwa na uwezekano wa kuonana na yeyote yule!

Jua lilikuja kurejea baada ya dakika tano ama zaidi. Si Jayit wala watumishi wake walioonekana mahala popote pale! Fursa, akiwa ameongozana na walinzi wake kadhaa, alielekea upesi kwenye eneo la makaburi. Huko alikuta makaburi mawili yamefukuliwa na mifupa haipo. Makaburi hayo yalikuwa ya babu na bibi wa Jayit.

Sasa Jayit alikuwa amepata kile alichokuwa anakitaka kwa muda mrefu. Hakuna aliyekuwa anajua ataenda kufanyia nini hayo mabaki, na ilimuogofya kila mtu.

Hakuna aliyedhani mtu kama Jayit anaweza akawa na dhamira safi. Hakuna! Na hakuna pia aliyekuwa na uthubutu wa kwenda kwenye tawala yake kumuuliza ilhali sasa alikuwa tayari ameshatimka.

Ilikuwa tumbo joto.

Zoezi la kumsimika mfalme lilisitishwa maana jua lilikuwa tayari limeshatoka katikati ya anga, na watu pia hawakuwa kwenye munkari wa hilo zoezi tena bali uwoga. Fursa alighafirishwa mno na hilo. Uso wake ulikuwa mwekundu na kwake kesho ilikuwa mbali mno.

.
.
.
.
.
***
.
.
.
Lako jicho!
Shoo
 
MKUFU WA MALKIA WA GOSHEN --- 006
Simulizi za series


ILIPOISHIA

“Usijali.” Akasema bibi mwingine. “Tutakupa njia rahisi ya kumpata.”
“Ila…” Akadakia bibi mwingine. “Kaa ukijua ukitutoroka, tutajua na hautodumu zaidi ya masaa manne kabla hujafa!”

ENDELEA

Tisho hilo lilifunga mjadala kabla bibi hawajampatia Veda jicho moja kubwa walilomtaka atumie kama dira ya kumpatia Malkia. Walimueleza namna ya kutumia dira hiyo kwa ufanisi.

Pale kiini chake cheusi kitakapogeuka na kuelekea kwenye upande wowote basi huko ndipo alipo wanayemtafuta. Veda akaelewa, ila kabla hajaenda akapatiwa na usafiri.

Usafiri huu ulikuwa ni wa ajabu na uliomshangaza Veda. Walikuwa kunguru wengi mno. Alistaajabu ni kwa namna gani atatumia kunguru hao kwenye usafiri. Bibi walimtoa hofu na kumwelekeza maneno kadhaa tu, Veda akawa mtaalamu. Ni kupiga tu mluzi kunguru wote wanamzunguka wakiwa wanapaa, na akiwa katikati humo basi atanyanyuka toka ardhini na atapata kuwaelekeza ndege hao wapi aelekee. Watatii!

Lengo ni moja tu, kuupata mkufu wa Malkia. Na hata kama itamlazimu kumuua Malkia basi afanye hivyo. Hata kama itamlazimu kuusukuma mlima, basi afanye vivyo.

Hakuna chochote kinachopasa kumzuia. Mkufu ni lazima uje kwenye mikono ya bibi wale kwa gharama yoyote ile, aidha ya mali ama damu!

Basi kunguru wakamzunguka Veda na kumnyanyua, wakamtoa eneo lile.
.
.
.
.
.
***
.
. .
.
.
.
Ulikuwa ni muda wa asubuhi ya kuelekea mchana Malkia na Zura wakiwa mgongoni mwa farasi kukata mbuga kuitafuta Osheni – tawala ya masonara.

Walikuwa wamebebelea chakula na maji waliyopewa na bibi yake Malkia vipate kuwasaidia njiani. Chakula kilikuwa ni mikate migumu na nyama kavu, viliwekwa kwenye kimfuko cha ngozi, wakati maji yakiwa yamefungashwa kwenye kibuyu kilichozibwa na mdomo mweusi.

Tangu walipoanza safari hiyo, hawakupumzika hata mara moja. Safari ilikuwa ndefu hivyo hawakutaka kuirefusha zaidi kwa kupumzika pasipo na mahitaji.

Lakini jua lilipokuja kutuama katikati ya anga, iliwalazimu kupumzika. Walikula kidogo na kunywa kukanda makoo yao makavu, kisha safari ikaendelea. Walitembea kwa muda wa kama lisaa ama zaidi, wakafikia milima ya Wawetu. Huko wakaona mito yenye maji safi, ambapo walichota maji na kuongezea yale yaliyokuwa kwenye kibuyu chao.

Wakatembea ndani ya milima hiyo ya Wawetu kwa takribani masaa sita. Hata jioni iliwakuta wakiwa katika safu hiyo ya milima yenye baridi kali hivyo wakalazimika kupumzika wakiwa wamejikunyata na kukumbatiana ili wapeane joto.

Lakini wakiwa hapo, hawakujua, kulikuwa kuna mtu anawatazama. Mtu huyo kwa siri sana aliwakata jicho. Nyayo zake zilizokanyaga chini hazikutoa sauti yoyote na macho yake makubwa kama bundi yalikuwa yanang’aa.

Hatukumjua ni nani huyu na anataka nini.

Kwa usiku wote hakufanya kitu. Malkia na Zura walidamka mapema ya asubuhi wakaendelea na safari yao. Walitembea kwa takribani masaa matatu wakaingia ndani ya jangwa kavu.

Humo wakakumbana na joto kali ukiambatana na mvuke wa joto uendao juu. Farasi alipunguza mwendo akawa anatembea.

Punde waliwaona watu watatu wanakuja tokea mbali. Mwanzoni waliwaona kama watu wadogo lakini kadiri walivyokuwa wanajongea wakawa wanapata maumbo yao kamili.

Walikuwa ni wanaume watatu waliojifunika vichwa na nyuso kwa vitambaa wakiwa wamevalia kanzu za kahawia, zikitofautiana kwa kukoza tu.

Walitupa salama zao kwa Malkia na Zura, wakiwa na sura zenye ukarimu na matabasamu ya bashasha. Walikuwa ni wazuri kwa uso wakiwa wametinda vema ndevu zao. Rangi yao ilikuwa nyeupe lakini nywele zao zilikuwa nyeusi ti.

Zura na Malkia walipuuzia salamu hizo wakaendelea na safari. Walikumbuka kile ambacho bibi aliwaambia ya kwamba wasiongee na yeyote njiani.

Waliwatazama tu wanaume hao pasipo kuwaongelesha. Na mara wanaume wale walipopishana na farasi wa Malkia, wakapotea kama upepo!

Malkia na Zura walishtushwa sana na hilo. Iliwafanya wajione hawapo wenyewe eneo lile. Kwa namna moja ama nyingine walijiuliza ingekuwaje kama wangeliitikia salamu ile.

Walichoka kutembea wakapumzika. Miguu ilikuwa inawauma na miili yao iliyokong’otwa na jua ilikuwa imevuja jasho na kuchoka. Waliketi chini ya mtende wakapata kula na kunywa kidogo.

Kutokana na kuchoka, walipitiwa na usingizi mwepesi. Ila baada ya muda mfupi walisikia sauti ya watu ikiwajongea. Waliamka upesi wakatazama. Walimuona mama mmoja mweusi akiwa ameambatana na watoto wawili waliovalia kimasikini.

Walikuwa wamechoka mno wakitembea kwa kuburuza miguu yao. Midomo ilikuwa mikavu na yenye kiu. Macho yalikuwa meupe kama watu wakosefu wa damu. Walikuwa wanatia huruma na imani vilevile.

Walisimama mbele ya Malkia na Zura wakaomba maji maana wana kiu, na chakula maana wana njaa. Malkia na Zura walitazamana kwanza kabla ya kuchukua maamuzi yoyote. Walihofia inaweza ikawa mtego.

Japokuwa kweli watu wale walikuwa wanatia huruma, je ni kweli ni binadamu ama majini? Hata kuwauliza wametokea wapi hawakuweza, waliogopa, hivyo walibakia wakiwatazama watu hao mpaka pale walipoondoka.

Japokuwa watu wale walibembeleza wajibiwe kama watapewa chakula na maji au lah, Malkia na Zura walinyamaza kimya. Ilihitaji moyo mkubwa kufanya hilo kwani waombaji walikuwa wanalia na nyuso zao kweli zilionyesha mahitaji.

Ajabu watu hao walipoondoka, baada ya kouona hawasikiliwi, walipotea kufumba na kufumbua! Haikuonekana wala kujulikana wapi wameelekea. Hapo ndio Malkia na Zura wakafahamu kwamba watu wale hawakuwa binadamu wa kawaida.

“Tuondoke!” Alisema Malkia. Walinyanyuka wakatembea wakimvuta farasi.

Walitembea mpaka pale jua lilipozama na kuwa usiku, wakapumzika.

Maajabu ya jangwa ni kwamba, mchana huwa ni joto kali mno wakati usiku kukiwa ni baridi kali. Malkia na Zura walijikuta wanajikunyata wakitetemeka kwa baridi hiyo katili.

Katikati ya usiku huo uliorandana na pepo kali zilizotimua vumbi, Malkia alishituka usingizini baada ya kusikia joto kifuani. Ulikuwa ni mkufu wake unawaka. Aliutazama ndani ya kidani akaona tukio lililokamata akili yake.

Kulikuwa kuna rundo kubwa la kunguru wakipaa angani. Hakuona mtu yeyote kati ya kunguru hao, na hakujua hao kunguru wametokea wapi na wanataka nini.

Ilikuwa ni fumbo gumu kwake.

Kunguru hao walikuwa wakubwa wenye mbawa pana. Walikuwa wanaruka kwa kuzunguka kitu ambacho Malkia hakuwa anakiona. Kasi yao ilikuwa kubwa sana na ingemtaka mtu kuwa makini ili apate kugundua kuwa hao ni kunguru, la sivyo ungeweza sema ni ukuta mweusi!

Ghafla kidani cha mkufu kilizima na kumwachia Malkia kwenye dimbwi la mawazo. Aliwaza na kuwazua ni nini kile. Mwishowe aliishia kwa kuweka tahadhari ya kwamba anatakiwa kuwa makini atakapoona ndege hao kwani mara zote mkufu humwonyesha ya mbele.

Asubuhi na mapema waliamka, Malkia akamwambia Zura yale aliyoyaona. Waliweka nadharia ya kuwa makini kisha wakaendelea na safari yao, ila kwa sasa wakiongeza kasi ili kunguru hao wasiwakute wakiwa jangwani pasipo na msaada.

Farasi alikimbia na kukimbia. Walitazama nyuma mara kwa mara kama wanafuatwa lakini hawakuona chochote. Wakiwa wanakaribia kumaliza jangwa wakamuona mwanamke mmoja amelala chini kama mtu asiyejitambua.

Alikuwa amevalia gauni refu jeusi akiwa peku. Nywele zake ndefu zilikuwa zinadeki ardhi wakati mdomo wake ukiwa umeachama kama mtu aliyepitiwa na usingizi wa pono.

“Ebu ngoja!” Aliamuru Malkia.

Macho yake yaliyoganda kwa mwanamke yule yaligundua jambo ambalo hakutaka kuliamini. Yule mwanamke alikuwa ni mke mwenzake. Tena mke mkubwa. Yaani alikuwa Veda!

Amefikaje pale? Aliwaza. Kwa namna moja ama akadhani Fursa atakuwa amemtimua mwanamke huyo. Fursa ana roho mbaya sana, aliamini. Lakini pia kwa namna nyingine akadhani aidha alikuwa amefananisha.

Hata kama amefukuzwa na Fursa, amefikaje pale?

Labda kwa muda wote ambao hawajaonana, mwanamke huyo alikuwa yu njiani ama amefika huko. Kichwa chake kilimpa mawazo hayo. Kabla hajamshika bega na kumvuta, Zura alimtahadharisha aachane naye lakini Malkia akasita.

Hakuweza kumuacha mtu wa himaya yake, tena mtu aliyeshea naye nyumba moja. Alimgeuza Veda akimuita jina. Mara Veda akafungua macho yake na kumtazama Malkia.

Kufumba na kufumbua nguo ya Veda ikageuka kuwa kunguru lukuki. Kunguru hao walimzingira Malkia na Veda wakawanyanyua juu. Baada ya muda mfupi, Malkia alidondoshwa chini, kunguru wakakimbia!

Malkia alijitazama kifuani, hakuona kitu. Mkufu ulikuwa umeenda. Alikwea farasi akawakimbiza kunguru hao lakini hakufanikiwa. Walimuacha asijue la kufanya.

Alibubujikwa na machozi ya kujaza beseni. Zura alimbembeleza akimtaka aache kulia.

“Sasa tutafanyaje?” Aliuliza Malkia.

“Tuendelee na safari yetu,” akajibu Zura.

Hekima na busara yake ilifikia maamuzi hayo. Aliona hakuna tija nyingine zaidi ya kuendelea kutembea kukamilisha safari yao. Washamla ng’ombe mzima, basi mkia wasiusaze.

“Tunaenda kufanya nini kama hatuna mkufu?” Aliuliza Malkia.

“Mkufu wako tutaupata tu. Lakini hatuwezi tukafunga tena safari hii.” Alijibu Zura.

Sauti yake ya kiutuuzima ilimfanya Malkia apate angalau faraja. Alimkumbatia Malkia na kumbembeleza kama mwanae.

Laiti kama kuna watu wangelitaka kummaliza Malkia Sandarus basi ingelikuwa kazi rahisi sana kama wangelianza na Zura. Kwani bila ya mwanamke huyu, Malkia ni mtupu mno; mpweke na asiye na tumaini.
.
.
.
.
.
***
.
.
.
.
.
Uso wa Veda ulijaa furaha baada ya kuupata mkufu. Si tu kwamba alikuwa amekamilisha kazi aliyotumwa, la hasha! Alikuwa amelipiza kisasi kwa Malkia Sandarus kwa kumchukulia bwana wake, marehemu mfalme wa Goshen.

Siku zote Veda hakuwa anawapenda wake wenzake hata kidogo. Aliona wote wamekuja kumnyakua mume wake toka kwenye mikono yake.

Aliwaona kama wezi ambao wamekuja kupokonya tonge ambalo alilipika kwa mkono wake mwenyewe. Aliishi kwa kuwachukia na hata kuwafanyia fitna kwa mumewe ili awachukie.

Leo amepora mkufu wa mmojawao, lilikuwa jambo la fahari kwake. Lakini zaidi ya hapo lilimpa maswali kadhaa.

Ule mkufu una nini? Kwanini bibi wale wanautaka kiasi kile? Kwanini upo kifuani kwa Malkia Sandarus? Kazi yake nini?

Maswali hayo yalimpa hamu ya kutaka kufahamu zaidi na zaidi. Alihairisha safari yake ya kwenda Tanashe akawa anajadili na kichwa chake juu ya mkufu ule. Alipata hamu akauvaa. Macho yake yalibadilika yakawa ya bluu. Alijihisi mwepesi na mwenye nguvu zaidi.

Alijikuta anatabasamu akasema na nafsi yake:

“Huu mkufu kwanzia leo ni wangu!”

Hakujali wale wabibi wanaomngoja Tanashe. Alijua fika hawawezi kumfanya lolote kwakuwa wakimuua hawatopata mkufu ule kwasababu wao wenyewe hawawezi toka Tanashe.

Na hata kama wakimuua, hajali pia, hana tena cha kupoteza maishani. Mtu pekee aliyekuwa anampenda amemsaliti; mume wake amekufa; hana familia. Ya nini aogope kufa?

Alibebwa na kunguru wake akaenda mpaka kwenye himaya ya Goshen. Kwa siri aliingia ndani ya ikulu ya tawala hiyo akimtafuta Fursa, mwanaume aliyejeruhi moyo wake. Kisha akitoka hapo awatafute na wapambe wote wa mwanaume huyo.

Wote hao alikuwa amepanga kuwazawadia kifo.

Ilichukua dakika tatu tu, wote hao waliokuwa kwenye orodha ya Veda wakawa wananing’inia shingo zao zikikabwa na vitanzi! Kuanzia Fursa mpaka na wapambe wake. Bila kusahau mwanajeshi yule aliyemchoma kisu mwanamama huyo.

Zilipita siku mbili za msiba Fursa akiwa mfalme aliyedumu kwa muda mfupi zaidi madarakani, siku mbili tu! Baada ya msiba kukoma, Veda alijitangaza kuwa malkia wa tawala hiyo.

Kila mtu akamwogopa kwa maajabu yake ya kubebwa na ndege na macho yake ya bluu lakini pia kwa namna alivyoua wanaume watano ndani ya muda mfupi vile. Watu wote wa Goshen pamoja na jeshi wakainamisha vichwa vyao chini kumpokea kiongozi wao huyo mpya, malkia Vedas Alturo!
.
.
.
.
.
* HAKUNA ZAIDI … ZAIDI YA MKUFU WA MALKIA WA GOSHEN! *
.
.
.
.
.
Kama ulidhani bibi wale watatu wa Tanashe walikuwa wametulia wakati hayo ya Veda yakitokea, basi umekosea.

Kwa muda wote huo bibi hawakuwa na furaha kwa namna walivyosalitiwa, ama kupokwa tonge mdomoni. Walijaribu kumuua Veda kama vile walivyomuahidi endapo akikiuka, lakini hawakufanikiwa.

Mkufu ulimlinda mwanamke huyo dhidi yao. Kama angelikuwa hajauvaa basi kazi ingelikuwa rahisi, ila haikuwa hivyo.

Wakajuta kwanini hawakuwaza tokea hapo mwanzoni ya kwamba mwanamke huyo anaweza kuuvaa huo mkufu. Walijiona wajinga na wasio wataalamu wa mambo ya kiulozi. Walibakia kulaumiana na kutupiana shutuma ambazo hazikuwasaidia kwa muda huo.

Wakati huo upande wao wa kaskazini ya mbali, kwenye tawala ya Devonship chini ya Jayit, kulikuwa kuna tafrija nzito muda huo. Jayit alikuwa amechinja ng’ombe thelathini na tisa kwa ajili ya damu, huku akiwafukia wengine tisa wakiwa hai.

Vitambaa vyeusi na vyekundu vilikuwa vimetandazwa kwenye ikulu yake yenye rangi nyeusi. Wanaume tisa wenye mvi nyeupe walikuwa wameketi kwenye viti vyeusi wakimtazama mfalme wao aliyekuwa anatazama mafuvu ya vichwa mawili aliyoyaweka mezani.

Jayit alikuwa amevalia gauni jekundu mkononi akishikilia panga lake refu jembamba. Alisugua mafuvu yale mawili kwa panga lake mpaka pale alipopata unga mweupe. Aliuchota unga huo akauweka kwenye karatasi nyeusi aliyoikunjama.

Mafuvu hayo mawili yalikuwa ni ya babu na bibi yake waliokufa miaka kadhaa huko nyuma. Bibi na babu yake hao walikuwa ndio wachawi pekee waliobakia Goshen wakati wengine wote wakitupiwa Tanashe.

Uchawi wao ulikuwa ni mkubwa kiasi kwamba hakuna aliyethubutu kuwagusa, wala kuwahisi kama ni walozi. Nusu ya idadi ya watu wa Goshen walikuwa wameuliwa na watu hao na hakuna aliyegundua.

Kwa miaka nenda rudi, bibi na babu yake Jayit walitawala tawala zote pasipo wafalme wa tawala hizo kujua. Wakati wafalme wakitawala tawala zao mchana, bibi na babu wa Jayit walikuwa wanazitawala usiku.

Hakuna aliyeweza kuwazuia, hata kifo chenyewe kilishindwa. Ni pale tu walipofuja ulozi wao na kujidhuru wenyewe ndipo walipokufa, la sivyo wangeishi milele! Uchawi wao haukuwa wa kujifunza, bali wa damuni.

Sasa Jayit alikuwa anataka nguvu hiyo; nguvu ya kizazi chao; nguvu ya babu na bibi yake. Ingawa alikuwa ana nguvu zake binafsi lakini bado kwake haikuwa inatosha kabisa. Alitaka nyongeza. Alitaka zaidi!

Alitaka kutawala tawala zote wakati wa usiku!
.
.
.
.
Lako jicho!
Mzigoo wa 2017 ila wamoto
 
MKUFU WA MALKIA WA GOSHEN -- 009

Simulizi za series


“Tafadhali, usiogope,” alisisitiza Sultan, ama Mfalme Mansoor. Alikuwa amejawa na tabasamu. Uso wake ulikuwa mweupe na ungeliona furaha ndani yake.


“Sina huo mkufu, kiongozi,” alisema Malkia Sandarus. Uso wake ulikuwa unamaanisha alichokisema japokuwa ilimuwia vigumu Sultan kuamini.


“Nitakupatia utajiri mkubwa mno,” alisema Sultan. “Sio kwamba ni ahadi. Punde tu utakaponipa mkufu huo nitakupatia utajiri wako papo hapo.”

“Naelewa Sultan,” Malkia alidakia. “Ila nasikitika kukwambia sina hicho unachokitaka.”


Uso wa Sultan ukanywea. Alimtazama mjumbe wake aliyempasha hizo habari za mkufu, mjumbe naye akatia rupia kubembeleza. Bahati mbaya kwao bado jibu likawa ni lilelile, sina mkufu!

“Mkufu umekwapuliwa na mtu nisiyemjua wakati nikiwa njiani kuja huku,” alisema Malkia Sandarus. Alielezea hali ilivyokuwa na mwishowe yeye na Zura wakatoka ndani ya kitoroli cha farasi kurudi kwa msonara mdogo.


Sultan hakuamini kile Malkia alichosema. Aliamini hiyo itakuwa ni janja tu ya mwanamke huyo kuuficha mkufu huo. Alimtazama mjumbe wake na macho meusi, akamwagiza:

“Wafuatilie popote watakapokuwepo. Hakikisha unaupata mkufu na kuuleta kwangu.”


Mjumbe alitikisa kichwa kukubali kisha akatoka ndani ya toroli tayari kwa ajili ya kutimiza agizo.


Alitembea haraka mpaka pale alipowatia machoni Malkia na Zura ndipo akapunguza mwendo. Kila wanawake hao walipogeuka nyuma, alijificha asionekane. Alifanya hivyo mara kwa mara mpaka Malkia na Zura wanazama ndani ya nyumba ya msonara mdogo.
Alisimama hapo kwa sekunde kadhaa. Alitafakari cha kufanya akaona kuendea nyumba jirani na itunzayo wahusika wake ndilo jambo muhimu. Afike hapo na kuomba makazi ya muda mfupi, hata kama yatamgharimu mali. Alijua ya kwamba watu wanaoishi mtaa ule ni watu hohehahe, masonara wadogo wanaobangaiza, hivyo basi hawawezi wakakaba tamaa zao ipasavyo.


Kwahiyo aliujongelea mlango wa jirani akagonga na kuongea na mwenyeji. Alimweleza haja yake na akakubaliwa baada ya kutumia ushawishi wa pesa. Mjumbe huo wa Sultan alitaka chumba kilicho karibu na dirisha kwasababu ya malengo yake.


Mwenyeji wake pasi na kinyongo akampatia. Hakujua bwana huyo ana nini kichwani, hakutaka hata kuwaza tangu yeye ataingiza pesa za kutosha, basi.


Lakini kwenye ulimwengu huu haupo mwenyewe. Wakati mtumishi huyo wa Sultan akiwa kwenye harakati zake hizo, naye alikuwa anachorwa pasipo kutambua.


Mwanaume mrefu mwembamba alikuwa anamtazama tokea wakiwa ndani ya kitoroli cha farasi. Alimfuatilia wakati anawafuatilia Malkia na Zura, mpaka pale alipojihifadhi eneo jirani ndipo akang’amuka na kuondoka.


Alitembea upesi na kwa uangalifu kutazama na kuhakiki kama yu mwenyewe. Alitembea na kutembea akakomea kwenye geti la jengo la msonara mkubwa.


Alinong’onezana na walinzi kisha akaingia ndani. Moja kwa moja alionana na Msonara mkubwa ambaye alikuwa anamsubiria kwa hamu kubwa. Alikuwa ameketi sebuleni akikuna ndevu zake.


Kitendo cha kutomuona Sultan ndani ya jengo lake akiwa ameondoka pasipo kumuaga kilimpa shaka na kumfanya atake kujua, ndipo akamtuma wakala wake upesi akatazame, huenda labda akawa amepokonywa tonge mdomoni na wasonara wengine.
Bahati nzuri akagundua hakuwa amepokonywa tonge, ila bahati mbaya zaidi alikuwa yu njiani kupokonywa sahani kabisa!


“Unasema ukweli?” Aliuliza Msonara mkubwa akitumbua macho.

“Ni kweli kabisa,” akajibu wakala wake.

“Nimemuona mtumishi wa Sultan anawafuatilia wale wanawake na amechukua makazi mahala pa karibu.”


Msonara mkubwa akashika kichwa chake akiachama. Ilikuwa wazi sasa Sultan Mansoor atakuwa ameshajua habari za mkufu. Hii haikuwa habari nzuri kwake hata kidogo. Alighafirika na aliomba aachwe mwenyewe apate kutafakari.


Alikaa hapo sebuleni mpaka pale Sultan aliporudi. Walihudumiwa chakula na vinywaji wakiwa wanateta mambo kadhaa ya biashara. Msonara mkubwa hakutaka kuvamia lile swala lake kwa pupa kwa kuhofia kumshitua Sultan, hivyo alifanya jambo hilo kwa ustadi; aliliweka kando kwanza kisha kadiri muda ulivyosonga akafungua kucha zake.


“Nimeshangazwa ulitoka pasipo kuniaga. Kuna jambo ulienda kulifuatilia?” Aliuliza Msonara akinywa chai yenye kila vikorombwezo. Macho yake yalikuwa yalikuwa yanamtazama Sultan na fika yalimuona mwanaume huyo akiwa ameguswa na hilo swali.


“Nilienda tu kutembea,” alijibu Sultan kiwepesi.

“Tu?”

“Ndio, kwani kuna shida yoyote?”

“Hapana. Ni kama tu nilivyosema, nilishangazwa.”

Kukawa kinywa kwa dakika mbili wakinywa na kula. Kila mtu alikuwa anawaza yake kichwani. Ni kama vile walikuwa wanategeana nani aanze kuongea. Walikuwa wanatazamana kwa kuibiaibia.

“Kuna lolote umeliona au umeligundua huko nje?” Msonara mkubwa alikuwa wa kwanza kufungua mdomo wake.
“Ndio,” Sultan akajibu. Msonara mkubwa akakabwa na kiu ya kutaka kusikia. “Nimeona tawala yenu inazidi kutanuka,” alimalizia Sultan. Taarifa hiyo ikamkwaza Msonara, si hiyo aliyokuwa anaitaka. Aliishia kuguna akabadili mada.


“Naweza nikafahamu ni lini unaondoka kiongozi?”

Sultan akamtazama na jicho lenye ng’eng’e.
“Muda si mrefu, usijali,” alijibu kwa sauti nzito. Hawakutia tena neno, lakini vichwa vyao vyote vilikuwa vinachambua, kukeketa na kung’amua.
.
.
.
.
.
.
***
.
.
.
.
.
.
Wakati wa mchana Rhoda anaendea nyumba moja ya wastani, ndaniye anaishi mmoja wa wazee wa baraza la uongozi wa tawala ya Goshen. Ni mmojawapo wa watu wale waliokuwa wananasibu tungo zao juu ya kumpindua malkia Vedas.

Rhoda alipiga hodi akasimama mlangoni hapo. Alikuwa amevalia kinadhifu akificha utupu wake na gauni refu la kijivu lenye ngozi mabegani. Nywele zake alikuwa amezikusanya vema na kuzibana hivyo kuupa uso wake nafasi nzuri ya kuonekana. Alivutia kutazama na harufu yake ya uwaridi ilikuwa inamvutisha mtu kuwa naye kando.

“Naweza nikakusaidia?” Aliuliza Mzee wa baraza. Uso wake haukuwa rafiki. Alikumbuka kabisa uso wa mgeni wake ni wa mwanamke aliyewahi kuwa na mahusiano ya kisiri na Fursa. Na kwa namna moja ama nyingine akadhani mwanamke huyo atakuwa amekuja kumpapatikia maana hana pa kujishikiza kwa sasa.


“Samahani kwa usumbufu,” alichombeza Rhoda. “Nina maongezi na wewe.”

“Sema, nakusikia,” akasema mzee huyo akiwa ameushikilia mlango wake. Kiwiliwili kilikuwa ndani nje akichomoza kichwa tu.
“Najua mlichopanga kufanya,” alisema Rhoda. “Nataka na mimi nishirikishwe.”

Mzee wa baraza akatoka ndani vizuri. Aliufunga mlango akimtazama Rhoda kwa macho ya mkazo.

“Unasemaje we mwanamke?”

Rhoda alieleza kila kitu ya kwamba alisikia kile wazee hao wamepanga kufanya, hivyo basi anaomba naye apewe nafasi la sivyo ataenda kumpasha habari malkia.

Mzee wa baraza alicheka kinafki, akauliza:
“Unadhani nani atakuamini malaya wewe?”
“Hata kama asiponiamini, kuna kitu ataweka kichwani juu yenu,” alijibu Rhoda. “Na maana yake ni kwamba hamtofanikiwa maana jicho lake litakuwa nanyi muda wote.”

Uzuri mwanamke huyo alikuwa amekaa mahali ambapo mzee huyo hakuweza kumdhuru. Palikuwa ni karibu na njia pana ipitishayo watu mara kwa mara. Isingekuwa hivyo pengine mzee yule angechukua hatua mkononi kwa namna alivyokuwa anamtazama Rhoda.
Rhoda alishika njia kuondoka, lakini mzee huyo akamwita.

“Unataka nini?” Aliuliza.

“Nataka mali kuficha siri yenu,” akajibu Rhoda.

Mzee wa baraza alimtazama Rhoda kwa macho ya kishetani. Ingawa alimkubalia mwanamke huyo yale anataka, ni dhahiri shayiri uso wake ulionyesha atapanga ya kidhalimu.

“Hili ni kati yangu mimi na wewe tu, usije ukathubutu kufanya lolote la kijinga,” alionya Rhoda. “Utakapofanya chochote jua n’takuwa nimetangulia hatua mbele yako.”

Alikomea hapo akaondoka zake. Mzee wa baraza aliingia ndani akiwa amefura. Alijiandaa kwa kujiveka mavazi kisha akatoka kwenda kukutana na wenzake apate kuwapasha habari, hii ilikuwa kinyume na makubaliano aliyoyaweka na Rhoda.
Lakini mzee huyo wa baraza pasipo kujua, Rhoda alikuwa anamfuatilia. Kwa mbali kabisa Rhoda alimtazama mzee huyo akitembea kwenda nyumba moja baada ya nyingine.
Rhoda alijikuta anasonya akatikisa kichwa chake.

“Punda!” Alilaani. “Huwezi kumlazimisha kunywa maji mtoni.”

Sasa alikuwa amebakiza chaguo moja tu; kwenda kwa malkia Vedas. Chaguo hili hakuwa analipenda, ila sasa ndilo pekee lilikuwa limebakia mkononi mwake. Hakuwa na namna.
.
.
.
.
.
.
.
***
.
.
.
.
.
.
.
Jua lilizama na hivyo usiku ukawasili. Huu ndio ulikuwa wasaa wa Jayit kuamka.

Japokuwa kwenye himaya yake ya Devonship jua halijawahi kuonekana, kitendo cha himaya zingine kuwa giza humpa faraja na kuona sasa ulimwengu wote upo mikononi mwake; hujihisi hana mipaka; hujihisi mwenye nguvu zaidi.

Alimuita jemedari wake wa vita, Tititat. Mwanaume huyo mzito wa kushiba akafika mbele yake ndani ya muda mfupi. Alikuwa tayari amejiandaa kwa vita akiwa amebebelea panga lake lenye kiu ya damu. Macho yake makubwa yalikuwa yamechomoza akiwa anahema kwanguvu.

Jayit aliwagiza aite jeshi lote mbele ya hekalu kwani ana neno la kuwapa. Tititat akafanya kama alivyoagizwa. Jeshi lote lilijaa mbele ya hekalu la kiongozi wao wakisubiria agizo.
“Leo ndio siku!” Sauti ya Jayit ilinguruma kama radi. Kila kitu kilikuwa kimya kikimsikiliza.

“Leo ndio siku ya kuonyesha utawala wetu maana hakuna wakutuzuia pale jua linapozama!”

“Woi! Woi! Woi!” Jeshi likaitikia kwanguvu.

“Leo tunaenda kuonyesha nguvu zetu!”

“Woi! Woi! Woi!”

“Ni leoo!”

“Woi! Woi! Woi!”

“Na leo ni zamu ya Maam! Kachukueni vyote vilivyomo huko. Katekeni vyote vya thamani na mvilete nyumbani! Msiache chochote cha dhahabu wala shaba!”
“Woi! Woi! Woi!”

Jeshi likapotea kuelekea kule lilipoagizwa, Tititat akiliongoza. Ndani ya muda mfupi tu halikuonekana. Ni vumbi tu ndilo lilibakia!
Jayit alirudi ndani ya hekalu lake akaketi kitini. Kwa kutumia ramli yake ya kichawi aliona jeshi lake likiyoyoma, likitenda na hata likirejea.

Huko Maam kuliachwa patupu vitu vyote vya thamani vikikombwa. Sio tu hivyo, bali hata watu waliuawa damu ipatikane. Damu kwa ajili ya wanajeshi hao wa Devonship kama kiburudisho kazini.

Ilikuwa ni ajabu mno, wanajeshi wa Devoship hawakuonekana pale walipokatiza ama kufanya matendo yao. Ni vishindo tu ndivyo vilikuwa vinasikika! Ungeshangaa tu kuona mtu anadondoka chini akipapatika, ama vitu vikibebwa na kupotea!

Jayit alishindwa kuzuia tabasamu lake la mamba usoni kwa kuona mafanikio hayo. Wakati sasa jeshi lake larejea, alichezesha ramli yake na kutazama himaya ya Goshen.

Alitazama himaya hiyo kila mahali akakomea mahali aishipo mtawala. Alitazama eneo hilo kwa makini, akamwona malkia Vedas akiwa kitandani anafanya mapenzi.

Alijaribu kumtazama mwanaume huyo aliyekuwa anafanya tendo hilo na malkia, akashindwa kabisa kumng’amua, hakuwa anamjua. Alibakiwa na maswali kede kichwani, lakini mwishowe aliamua kuyapuuzia na kumtafuta malkia mwingine amjuaye, Malkia Sandarus.

Ni kwa muda Jayit hakuwa amepekuwa wala kuifuatilia tawala hiyo. Hakuwa hata anajua kama kwa sasa ipo chini ya mwanamke Vedas Alturo.

Alimtafuta Malkia Sandarus nyumba nzima hakumwona. Staajabu alikuja kumpata akiwa ndani ya himaya ya masonara, tena ndani ya nyumba ndogo ya msonara akiwa amelala chini pembeni ya mwanamke ambaye hakumfahamu.
Hakubanduka hapo upesi, akatazama kwa makini na mazingira ya eneo hilo. Ndani ya muda mfupi akagundua kuna wanaume wawili walio karibu na hilo eneo. Wanaume hao walikuwa hawajalala, bali wapo macho kwenye hali ya ulinzi. Mmoja alikuwa akichungulia kupitia dirishani, wakati mwingine akiwa ameketi mbali kidogo lakini akitazama nyumba aliyomo Malkia Sandarus.

Jayit alipata hamu ya kujua zaidi. Kwa namna moja ama nyingine hisia zake zilimtuma ya kwamba pale kutakuwa kuna kitu cha thamani kinachowindwa, na basi tamaa ikamkaba. Jeshi lake lilipowasili, alimwita Tititat kando na kumtaka aende Osheni – tawala ya masonara haraka iwezekanavyo. Aende huko akapeleleze. Aende huko akawinde hicho kinachowindwa.

Pasipo kukawia, Tititat akamkwea farasi wake na kuanza safari ya kwenda Osheni.
.
.
.
***
.
.
.
Usiku ulienda upesi kukakucha ndani ya himaya ya Osheni. Watu waliamka wakashika kazi za kurepea na kuandaa vito vya dhahabu ama vito vingine vya thamani kama vile almasi na kadhalika. Kila mtu aliwajibika, na kama ungelikuwa hapo ukaona basi ungelisema ala! Huu ndio mji wa wachapakazi.


Malkia Sandarus na Zura nao wasiwe nyuma, walikuwa wanafanya usafi ndani ya makazi waliyokuwa wanaishi. Ilifikia pahala wakagawana kazi hizo ili wafanye ufanisi kwahiyo basi Zura alibakia nyumbani wakati Malkia Sandarus akienda kuchota maji.


Alienda safari nne na chungu chake kichwani, akayamiminia maji hayo kwenye bilauri fulani kubwa. Lakini baada ya hapo, hakuonekana tena akileta maji. Ilichukua muda mrefu, na sasa Zura anapata shaka.
Alitoka ndani akaangazaangaza kila kona pasipo kumuona Malkia. Aliamua kufunga safari kwenda huko kisimani yapatikanapo maji. Akiwa njiani, anaona watu kadhaa wakiwa wamejizonga na wanateta kitu.

Alipata shaka na miguu yake ilichanganyia upesi kwenda eneo la tukio.

Alifika akasogeza watu kando apate kuona. La haula! Akaona kitu cha kushangaza; akaona kitu kilichompokonya nguvu.

Alikuwa ni malkia! Akiwa chini amekobekwa kisu kifuani. Hakuwa na dalili yoyote ya uhai. Na tayari mwili wake ulikuwa wa baridi.

Zura alimtikisa malkia wake pasipo mafanikio. Alimpiga makofi aamke lakini napo alijichosha tu kwani Malkia Sandarus alikuwa amekufa!
Mwanaume aliyemuua alikuwa hatua kadhaa mbali na eneo hilo. Alikuwa ni mwanaume yule aliyetumwa na malkia Vedas Alturo; alikuwa ni mwanaume yule aitwaye Nedal!

Lakini wakati akifanya mauaji hayo, wanaume wawili: wakala wa Msonara mkubwa na mtumishi wa Sultan Mansoor, walishuhudia tukio zima. Hawakuwa na la kufanya zaidi ya kutazama, kwani wao hawakuwa na lingine linalowahusu zaidi ya mkufu! .
.
.
.
.
.
*****
.
.
.
.
LAKO JICHO
 

Similar Discussions

Back
Top Bottom