SIMULIZI: Mkufu wa Malkia wa Goshen

SIMULIZI: Mkufu wa Malkia wa Goshen

Riwaya nzuri ..jaribu kuwa unatoa japo ndefu kidogo au weka 2 kwa siku..otherwise kusubiria mpaka iishe ndio nisome.
Ebu angalia huwa natoa ngapi kwa siku au unalaumu tu kama huwezi kusoma subiri iishe kama unavyotaka
 
*MKUFU WA MALKIA WA GOSHEN --- 006*
*Simulizi za series*


ILIPOISHIA

“Usijali.” Akasema bibi mwingine. “Tutakupa njia rahisi ya kumpata.”
“Ila…” Akadakia bibi mwingine. “Kaa ukijua ukitutoroka, tutajua na hautodumu zaidi ya masaa manne kabla hujafa!”

ENDELEA

Tisho hilo lilifunga mjadala kabla bibi hawajampatia Veda jicho moja kubwa walilomtaka atumie kama dira ya kumpatia Malkia. Walimueleza namna ya kutumia dira hiyo kwa ufanisi.

Pale kiini chake cheusi kitakapogeuka na kuelekea kwenye upande wowote basi huko ndipo alipo wanayemtafuta. Veda akaelewa, ila kabla hajaenda akapatiwa na usafiri.

Usafiri huu ulikuwa ni wa ajabu na uliomshangaza Veda. Walikuwa kunguru wengi mno. Alistaajabu ni kwa namna gani atatumia kunguru hao kwenye usafiri. Bibi walimtoa hofu na kumwelekeza maneno kadhaa tu, Veda akawa mtaalamu. Ni kupiga tu mluzi kunguru wote wanamzunguka wakiwa wanapaa, na akiwa katikati humo basi atanyanyuka toka ardhini na atapata kuwaelekeza ndege hao wapi aelekee. Watatii!

Lengo ni moja tu, kuupata mkufu wa Malkia. Na hata kama itamlazimu kumuua Malkia basi afanye hivyo. Hata kama itamlazimu kuusukuma mlima, basi afanye vivyo.

Hakuna chochote kinachopasa kumzuia. Mkufu ni lazima uje kwenye mikono ya bibi wale kwa gharama yoyote ile, aidha ya mali ama damu!

Basi kunguru wakamzunguka Veda na kumnyanyua, wakamtoa eneo lile.
.
.
.
.
.
***
.
. .
.
.
.
Ulikuwa ni muda wa asubuhi ya kuelekea mchana Malkia na Zura wakiwa mgongoni mwa farasi kukata mbuga kuitafuta Osheni – tawala ya masonara.

Walikuwa wamebebelea chakula na maji waliyopewa na bibi yake Malkia vipate kuwasaidia njiani. Chakula kilikuwa ni mikate migumu na nyama kavu, viliwekwa kwenye kimfuko cha ngozi, wakati maji yakiwa yamefungashwa kwenye kibuyu kilichozibwa na mdomo mweusi.

Tangu walipoanza safari hiyo, hawakupumzika hata mara moja. Safari ilikuwa ndefu hivyo hawakutaka kuirefusha zaidi kwa kupumzika pasipo na mahitaji.

Lakini jua lilipokuja kutuama katikati ya anga, iliwalazimu kupumzika. Walikula kidogo na kunywa kukanda makoo yao makavu, kisha safari ikaendelea. Walitembea kwa muda wa kama lisaa ama zaidi, wakafikia milima ya Wawetu. Huko wakaona mito yenye maji safi, ambapo walichota maji na kuongezea yale yaliyokuwa kwenye kibuyu chao.

Wakatembea ndani ya milima hiyo ya Wawetu kwa takribani masaa sita. Hata jioni iliwakuta wakiwa katika safu hiyo ya milima yenye baridi kali hivyo wakalazimika kupumzika wakiwa wamejikunyata na kukumbatiana ili wapeane joto.

Lakini wakiwa hapo, hawakujua, kulikuwa kuna mtu anawatazama. Mtu huyo kwa siri sana aliwakata jicho. Nyayo zake zilizokanyaga chini hazikutoa sauti yoyote na macho yake makubwa kama bundi yalikuwa yanang’aa.

Hatukumjua ni nani huyu na anataka nini.

Kwa usiku wote hakufanya kitu. Malkia na Zura walidamka mapema ya asubuhi wakaendelea na safari yao. Walitembea kwa takribani masaa matatu wakaingia ndani ya jangwa kavu.

Humo wakakumbana na joto kali ukiambatana na mvuke wa joto uendao juu. Farasi alipunguza mwendo akawa anatembea.

Punde waliwaona watu watatu wanakuja tokea mbali. Mwanzoni waliwaona kama watu wadogo lakini kadiri walivyokuwa wanajongea wakawa wanapata maumbo yao kamili.

Walikuwa ni wanaume watatu waliojifunika vichwa na nyuso kwa vitambaa wakiwa wamevalia kanzu za kahawia, zikitofautiana kwa kukoza tu.

Walitupa salama zao kwa Malkia na Zura, wakiwa na sura zenye ukarimu na matabasamu ya bashasha. Walikuwa ni wazuri kwa uso wakiwa wametinda vema ndevu zao. Rangi yao ilikuwa nyeupe lakini nywele zao zilikuwa nyeusi ti.

Zura na Malkia walipuuzia salamu hizo wakaendelea na safari. Walikumbuka kile ambacho bibi aliwaambia ya kwamba wasiongee na yeyote njiani.

Waliwatazama tu wanaume hao pasipo kuwaongelesha. Na mara wanaume wale walipopishana na farasi wa Malkia, wakapotea kama upepo!

Malkia na Zura walishtushwa sana na hilo. Iliwafanya wajione hawapo wenyewe eneo lile. Kwa namna moja ama nyingine walijiuliza ingekuwaje kama wangeliitikia salamu ile.

Walichoka kutembea wakapumzika. Miguu ilikuwa inawauma na miili yao iliyokong’otwa na jua ilikuwa imevuja jasho na kuchoka. Waliketi chini ya mtende wakapata kula na kunywa kidogo.

Kutokana na kuchoka, walipitiwa na usingizi mwepesi. Ila baada ya muda mfupi walisikia sauti ya watu ikiwajongea. Waliamka upesi wakatazama. Walimuona mama mmoja mweusi akiwa ameambatana na watoto wawili waliovalia kimasikini.

Walikuwa wamechoka mno wakitembea kwa kuburuza miguu yao. Midomo ilikuwa mikavu na yenye kiu. Macho yalikuwa meupe kama watu wakosefu wa damu. Walikuwa wanatia huruma na imani vilevile.

Walisimama mbele ya Malkia na Zura wakaomba maji maana wana kiu, na chakula maana wana njaa. Malkia na Zura walitazamana kwanza kabla ya kuchukua maamuzi yoyote. Walihofia inaweza ikawa mtego.

Japokuwa kweli watu wale walikuwa wanatia huruma, je ni kweli ni binadamu ama majini? Hata kuwauliza wametokea wapi hawakuweza, waliogopa, hivyo walibakia wakiwatazama watu hao mpaka pale walipoondoka.

Japokuwa watu wale walibembeleza wajibiwe kama watapewa chakula na maji au lah, Malkia na Zura walinyamaza kimya. Ilihitaji moyo mkubwa kufanya hilo kwani waombaji walikuwa wanalia na nyuso zao kweli zilionyesha mahitaji.

Ajabu watu hao walipoondoka, baada ya kouona hawasikiliwi, walipotea kufumba na kufumbua! Haikuonekana wala kujulikana wapi wameelekea. Hapo ndio Malkia na Zura wakafahamu kwamba watu wale hawakuwa binadamu wa kawaida.

“Tuondoke!” Alisema Malkia. Walinyanyuka wakatembea wakimvuta farasi.

Walitembea mpaka pale jua lilipozama na kuwa usiku, wakapumzika.

Maajabu ya jangwa ni kwamba, mchana huwa ni joto kali mno wakati usiku kukiwa ni baridi kali. Malkia na Zura walijikuta wanajikunyata wakitetemeka kwa baridi hiyo katili.

Katikati ya usiku huo uliorandana na pepo kali zilizotimua vumbi, Malkia alishituka usingizini baada ya kusikia joto kifuani. Ulikuwa ni mkufu wake unawaka. Aliutazama ndani ya kidani akaona tukio lililokamata akili yake.

Kulikuwa kuna rundo kubwa la kunguru wakipaa angani. Hakuona mtu yeyote kati ya kunguru hao, na hakujua hao kunguru wametokea wapi na wanataka nini.

Ilikuwa ni fumbo gumu kwake.

Kunguru hao walikuwa wakubwa wenye mbawa pana. Walikuwa wanaruka kwa kuzunguka kitu ambacho Malkia hakuwa anakiona. Kasi yao ilikuwa kubwa sana na ingemtaka mtu kuwa makini ili apate kugundua kuwa hao ni kunguru, la sivyo ungeweza sema ni ukuta mweusi!

Ghafla kidani cha mkufu kilizima na kumwachia Malkia kwenye dimbwi la mawazo. Aliwaza na kuwazua ni nini kile. Mwishowe aliishia kwa kuweka tahadhari ya kwamba anatakiwa kuwa makini atakapoona ndege hao kwani mara zote mkufu humwonyesha ya mbele.

Asubuhi na mapema waliamka, Malkia akamwambia Zura yale aliyoyaona. Waliweka nadharia ya kuwa makini kisha wakaendelea na safari yao, ila kwa sasa wakiongeza kasi ili kunguru hao wasiwakute wakiwa jangwani pasipo na msaada.

Farasi alikimbia na kukimbia. Walitazama nyuma mara kwa mara kama wanafuatwa lakini hawakuona chochote. Wakiwa wanakaribia kumaliza jangwa wakamuona mwanamke mmoja amelala chini kama mtu asiyejitambua.

Alikuwa amevalia gauni refu jeusi akiwa peku. Nywele zake ndefu zilikuwa zinadeki ardhi wakati mdomo wake ukiwa umeachama kama mtu aliyepitiwa na usingizi wa pono.

“Ebu ngoja!” Aliamuru Malkia.

Macho yake yaliyoganda kwa mwanamke yule yaligundua jambo ambalo hakutaka kuliamini. Yule mwanamke alikuwa ni mke mwenzake. Tena mke mkubwa. Yaani alikuwa Veda!

Amefikaje pale? Aliwaza. Kwa namna moja ama akadhani Fursa atakuwa amemtimua mwanamke huyo. Fursa ana roho mbaya sana, aliamini. Lakini pia kwa namna nyingine akadhani aidha alikuwa amefananisha.

Hata kama amefukuzwa na Fursa, amefikaje pale?

Labda kwa muda wote ambao hawajaonana, mwanamke huyo alikuwa yu njiani ama amefika huko. Kichwa chake kilimpa mawazo hayo. Kabla hajamshika bega na kumvuta, Zura alimtahadharisha aachane naye lakini Malkia akasita.

Hakuweza kumuacha mtu wa himaya yake, tena mtu aliyeshea naye nyumba moja. Alimgeuza Veda akimuita jina. Mara Veda akafungua macho yake na kumtazama Malkia.

Kufumba na kufumbua nguo ya Veda ikageuka kuwa kunguru lukuki. Kunguru hao walimzingira Malkia na Veda wakawanyanyua juu. Baada ya muda mfupi, Malkia alidondoshwa chini, kunguru wakakimbia!

Malkia alijitazama kifuani, hakuona kitu. Mkufu ulikuwa umeenda. Alikwea farasi akawakimbiza kunguru hao lakini hakufanikiwa. Walimuacha asijue la kufanya.

Alibubujikwa na machozi ya kujaza beseni. Zura alimbembeleza akimtaka aache kulia.

“Sasa tutafanyaje?” Aliuliza Malkia.

“Tuendelee na safari yetu,” akajibu Zura.

Hekima na busara yake ilifikia maamuzi hayo. Aliona hakuna tija nyingine zaidi ya kuendelea kutembea kukamilisha safari yao. Washamla ng’ombe mzima, basi mkia wasiusaze.

“Tunaenda kufanya nini kama hatuna mkufu?” Aliuliza Malkia.

“Mkufu wako tutaupata tu. Lakini hatuwezi tukafunga tena safari hii.” Alijibu Zura.

Sauti yake ya kiutuuzima ilimfanya Malkia apate angalau faraja. Alimkumbatia Malkia na kumbembeleza kama mwanae.

Laiti kama kuna watu wangelitaka kummaliza Malkia Sandarus basi ingelikuwa kazi rahisi sana kama wangelianza na Zura. Kwani bila ya mwanamke huyu, Malkia ni mtupu mno; mpweke na asiye na tumaini.
.
.
.
.
.
***
.
.
.
.
.
Uso wa Veda ulijaa furaha baada ya kuupata mkufu. Si tu kwamba alikuwa amekamilisha kazi aliyotumwa, la hasha! Alikuwa amelipiza kisasi kwa Malkia Sandarus kwa kumchukulia bwana wake, marehemu mfalme wa Goshen.

Siku zote Veda hakuwa anawapenda wake wenzake hata kidogo. Aliona wote wamekuja kumnyakua mume wake toka kwenye mikono yake.

Aliwaona kama wezi ambao wamekuja kupokonya tonge ambalo alilipika kwa mkono wake mwenyewe. Aliishi kwa kuwachukia na hata kuwafanyia fitna kwa mumewe ili awachukie.

Leo amepora mkufu wa mmojawao, lilikuwa jambo la fahari kwake. Lakini zaidi ya hapo lilimpa maswali kadhaa.

Ule mkufu una nini? Kwanini bibi wale wanautaka kiasi kile? Kwanini upo kifuani kwa Malkia Sandarus? Kazi yake nini?

Maswali hayo yalimpa hamu ya kutaka kufahamu zaidi na zaidi. Alihairisha safari yake ya kwenda Tanashe akawa anajadili na kichwa chake juu ya mkufu ule. Alipata hamu akauvaa. Macho yake yalibadilika yakawa ya bluu. Alijihisi mwepesi na mwenye nguvu zaidi.

Alijikuta anatabasamu akasema na nafsi yake:

“Huu mkufu kwanzia leo ni wangu!”

Hakujali wale wabibi wanaomngoja Tanashe. Alijua fika hawawezi kumfanya lolote kwakuwa wakimuua hawatopata mkufu ule kwasababu wao wenyewe hawawezi toka Tanashe.

Na hata kama wakimuua, hajali pia, hana tena cha kupoteza maishani. Mtu pekee aliyekuwa anampenda amemsaliti; mume wake amekufa; hana familia. Ya nini aogope kufa?

Alibebwa na kunguru wake akaenda mpaka kwenye himaya ya Goshen. Kwa siri aliingia ndani ya ikulu ya tawala hiyo akimtafuta Fursa, mwanaume aliyejeruhi moyo wake. Kisha akitoka hapo awatafute na wapambe wote wa mwanaume huyo.

Wote hao alikuwa amepanga kuwazawadia kifo.

Ilichukua dakika tatu tu, wote hao waliokuwa kwenye orodha ya Veda wakawa wananing’inia shingo zao zikikabwa na vitanzi! Kuanzia Fursa mpaka na wapambe wake. Bila kusahau mwanajeshi yule aliyemchoma kisu mwanamama huyo.

Zilipita siku mbili za msiba Fursa akiwa mfalme aliyedumu kwa muda mfupi zaidi madarakani, siku mbili tu! Baada ya msiba kukoma, Veda alijitangaza kuwa malkia wa tawala hiyo.

Kila mtu akamwogopa kwa maajabu yake ya kubebwa na ndege na macho yake ya bluu lakini pia kwa namna alivyoua wanaume watano ndani ya muda mfupi vile. Watu wote wa Goshen pamoja na jeshi wakainamisha vichwa vyao chini kumpokea kiongozi wao huyo mpya, malkia Vedas Alturo!
.
.
.
.
.
*** HAKUNA ZAIDI … ZAIDI YA MKUFU WA MALKIA WA GOSHEN! ***
.
.
.
.
.
Kama ulidhani bibi wale watatu wa Tanashe walikuwa wametulia wakati hayo ya Veda yakitokea, basi umekosea.

Kwa muda wote huo bibi hawakuwa na furaha kwa namna walivyosalitiwa, ama kupokwa tonge mdomoni. Walijaribu kumuua Veda kama vile walivyomuahidi endapo akikiuka, lakini hawakufanikiwa.

Mkufu ulimlinda mwanamke huyo dhidi yao. Kama angelikuwa hajauvaa basi kazi ingelikuwa rahisi, ila haikuwa hivyo.

Wakajuta kwanini hawakuwaza tokea hapo mwanzoni ya kwamba mwanamke huyo anaweza kuuvaa huo mkufu. Walijiona wajinga na wasio wataalamu wa mambo ya kiulozi. Walibakia kulaumiana na kutupiana shutuma ambazo hazikuwasaidia kwa muda huo.

Wakati huo upande wao wa kaskazini ya mbali, kwenye tawala ya Devonship chini ya Jayit, kulikuwa kuna tafrija nzito muda huo. Jayit alikuwa amechinja ng’ombe thelathini na tisa kwa ajili ya damu, huku akiwafukia wengine tisa wakiwa hai.

Vitambaa vyeusi na vyekundu vilikuwa vimetandazwa kwenye ikulu yake yenye rangi nyeusi. Wanaume tisa wenye mvi nyeupe walikuwa wameketi kwenye viti vyeusi wakimtazama mfalme wao aliyekuwa anatazama mafuvu ya vichwa mawili aliyoyaweka mezani.

Jayit alikuwa amevalia gauni jekundu mkononi akishikilia panga lake refu jembamba. Alisugua mafuvu yale mawili kwa panga lake mpaka pale alipopata unga mweupe. Aliuchota unga huo akauweka kwenye karatasi nyeusi aliyoikunjama.

Mafuvu hayo mawili yalikuwa ni ya babu na bibi yake waliokufa miaka kadhaa huko nyuma. Bibi na babu yake hao walikuwa ndio wachawi pekee waliobakia Goshen wakati wengine wote wakitupiwa Tanashe.

Uchawi wao ulikuwa ni mkubwa kiasi kwamba hakuna aliyethubutu kuwagusa, wala kuwahisi kama ni walozi. Nusu ya idadi ya watu wa Goshen walikuwa wameuliwa na watu hao na hakuna aliyegundua.

Kwa miaka nenda rudi, bibi na babu yake Jayit walitawala tawala zote pasipo wafalme wa tawala hizo kujua. Wakati wafalme wakitawala tawala zao mchana, bibi na babu wa Jayit walikuwa wanazitawala usiku.

Hakuna aliyeweza kuwazuia, hata kifo chenyewe kilishindwa. Ni pale tu walipofuja ulozi wao na kujidhuru wenyewe ndipo walipokufa, la sivyo wangeishi milele! Uchawi wao haukuwa wa kujifunza, bali wa damuni.

Sasa Jayit alikuwa anataka nguvu hiyo; nguvu ya kizazi chao; nguvu ya babu na bibi yake. Ingawa alikuwa ana nguvu zake binafsi lakini bado kwake haikuwa inatosha kabisa. Alitaka nyongeza. Alitaka zaidi!

Alitaka kutawala tawala zote wakati wa usiku!
.
.
.
.
Lako jicho!
 

Similar Discussions

Back
Top Bottom