SIMULIZI: Mkufu wa Malkia wa Goshen

SIMULIZI: Mkufu wa Malkia wa Goshen

Bibie kitu hiki kimesimamia kucha nimeona unajua kuvaa viatu vya Baba vizuri na majirani wasijue kuwa Baba hayupo Big up sana mkuu [HASHTAG]#Steve[/HASHTAG] kwa kulea Bibie [HASHTAG]#shunie[/HASHTAG]
[emoji120] [emoji120]
 
*MKUFU WA MALKIA WA GOSHEN -- 04*

*Simulizi za series*


ILIPOISHIA

Fisi hao waligeuka na kuanza kukimbia kurejea kwenye makazi yao. Kadiri walivyokuwa wanakimbia, na jua lilivyokuwa linachomoza, ndivyo walivyokuwa wanageuka kuwa binadamu.

ENDELEA

Mwishowe walipotea isijulikane wapi wameelekea. Malkia na Zura waliwatazama wakiyoyoma huku mioyo yao ikidunda kwa mjazo wa hofu na mashaka.

Ilibaki kidogo tu wangekuwa habari nyingine, waliamini hivyo. Walimeza mate wakiwa wanahema kabla hawajageuza kwenda kwenye makazi ya Zura.

Jambo hilo lilifanyika kwa siri mno, Malkia hakuhitajika kuonekana. Zura alihakikisha hilo linatimia mpaka wanafika nyumbani kwake alipokuta mzoga wa mumewe ukiwa umelazwa chumbani.

Zura aliumizwa sana na hilo tukio, akalia sana. Kwa kusaidiana na Malkia walifukua kaburi na kumzika mwanaume huyo ndani ya nyumba ili wasipate kuonekana, kisha wakajipumzisha.

Walikuwa wamechoka mno. Karibia usiku wote hawakuwa wamelala, lakini pia walitumikisha viungo vyao haswa kurandaranda huku na kule hivyo walivyojilaza tu kitandani usingizi haukuwaonea huruma, ukawakomba.

Walikoroma kwa usingizi baada tu ya muda mfupi.
.
.
.
.
.
.
***
.
.
.
.
.
Jua lilisimama, na kama ingelikuwa ni nyakati za sasa za kutumia saa basi bila shaka kwa muda huo ilikuwa ni saa nne ya asubuhi.

Siku ilikuwa nzito haswa. Uwanja mkubwa wa tawala ya Goshen ulikuwa umefurika mno, na kabla haujaingia ndani basi ungekutana na rundo kubwa la rafasi waliowaleta wageni toka tawala mbalimbali waje kushuhudia kusimikwa kwa kiongozi mpya wa ardhi hiyo, Bwana Fursa.

Nyimbo zilizosindikizwa na vifaa vitamu kama vinubi na firimbi, ziliita kwenye kila kona ya uwanja. Watalaamu wa kucheza walijimwaya uwanjani wakisogeza muda taratibu, huku wasiwe peke yao wakasindikizwa na vinywaji na vyakula vya kumwaga.

Katikati ya uwanja bendera ya kila tawala ilisimikwa ikawa inapeperuka kwa madaha. Kulikuwa kuna tawala tano uwanjani kwa kujibu wa idadi ya bendera; bendera nyekundu yenye jua jeupe katikati ikiwakilisha tawala ya Maam; bendera nyeusi yenye matone meupe kumi na saba ikiwakilisha tawala ya Kusi; bendera nyeupe yenye mikuki miwili meusi iliyokinzana ikiwakilisha Goshen; bendera ya bluu yenye mchoro mkubwa wa samaki ikiwakilisha Theon; na bendera ya mwisho ikiwa na rangi nyeusi, nyekundu na nyeupe bila ya mchoro wala picha yoyote ikiwakilisha tawala ya Bhotu.

Karibia waanchi wote wa Goshen walikuwepo hapo. Wachache ambao hawakuwepo walikuwa aidha vilabuni wanakunywa pombe zao ama wapo mashambani wanawajibika.

Lakini kila mtu alikuwa na ratiba ya kuja eneo hilo, kilichowatofautisha ni ratiba tu. Miongoni mwao wengi walikuwa wanangojea jua likikaribia kufika katikati ya anga ndipo waanze safari kujisogeza.

Kwa mujibu wa desturi ya Goshen, mfalme husimikwa pale jua linapokuwa katikati ya anga. Hiyo ni ishara ya kuonyesha utawala wake utakuwa wa haki usio na pendeleo na pande yoyote. Unapofika muda huo tu, watu hufurahia wakimtazama mfalme akivekwa taji la kifalme.

Matarumbeta hupigwa, vigelegele vinapigwa na jeshi linasalimu amri mbele yake.

Watu wote uwanjani wakiwa wanangoja muda huo adhimu, Fursa akiwa katikati ya wapambe wake watatu, aliitwa kando na mwanamke mnene ila mwenye umbo lisilojificha. Alikuwa ni malkia, mke mkubwa wa mfalme aliyefariki. Aliinama akamng’ata Fursa sikio kabla mwanaume huyo hajanyanyuka upesi na kusogea mbali kidogo na umati.

“Naona unanisahau, Fursa.” Alisema malkia huyo akiwa amekaza sura.

“Sijakusahau Veda.” Akajitetea Fursa.

“Kumbuka bila mimi usingelikuwa hapa.”

“Najua, Veda. Tutaongelea tu haya mambo, usijali.”

“Lini na leo ndio unaapishwa kuwa mfalme?”

“We jua tutaongea kwani kuna haraka gani? Endapo tukifanya haraka tutawapa watu mashaka!”

“Sawa. Ila kaa ukijua kwamba, ukimwaga mboga mie n’tamwaga ugali. Ukianza mie n’tamaliza!”

Baada ya Veda kutoa tisho hilo, alitimka. Fursa aliminya mdomo wake kisha naye akarejea kule alipokuwa awali. Nyuma yake alikuwa anaongozana na mababa watatu waliobebelea mikuki ya chuma.

Ila huyu baba ana siri gani na Veda, mke mkubwa wa mfalme?

Turudi nyuma.

Kabla mfalme hajafa, Veda alikuwa ana mahusiano ya siri na Fursa. Nyuma ya mgongo wa Mfalme watu hawa walikuwa wanafanya mapenzi na huku wakipeana ahadi motomoto za kuja kutawala Goshen siku za usoni.

Ilifikia kipindi Veda, mke mkubwa wa mfalme, akashika ujauzito lakini kuepusha shari alikunywa madawa na kutoa mimba hiyo, lakini bado penzi lao halikukoma, Veda akiwa amechochewa kuingia kwenye mahusiano hayo kutokana na uwezo mbovu wa Mfalme kumpa huduma kitandani.

Mwishowe, Veda alimtilia sumu mumewe kwenye kikombe cha kahawa. Tokea hapo, Mfalme akawa dhoofu lihali. Hakuweza kutembea wala kuongea vema. Macho yake yaliingia ndani akawa haoni.

Mdomo wake ulikuwa mkavu muda wote na mapigo yake ya moyo yakawa ya kusuasua ama kupiga kwa mfululizo. Alikuwa hivyo mpaka kufa kwake. Japokuwa kuna muda alishuhudia mke wake, Veda, akiwa anazini na Fursa, alishindwa kufanya chochote wala kumwambia yoyote. Hata machozi hakuwa nayo!

Sasa Veda alikuwa anamkumbushia Fursa miadi waliyowekeana: ya kwamba kiti cha umalkia ni chake pekee. Hakuna atakayekikaimu, na tena wakishakuwa mume na mke, Fursa hatokuwa na mwanamke mwingine yoyote isipokuwa yeye.

Fursa alikuwa ameshasahau miadi hiyo. Madaraka matamu bwana! Akili yake yote ilikuwa ni kutazama namna gani atakuwa anajisikia akiwa kwenye kiti cha kifalme kinachoogopwa na kuheshimiwa na wote baada tu ya miungu yao.

Muda ulisonga kwenye ardhi ya Goshen na sasa ulibakia muda mchache sana kwa jua kuwasili katikati ya anga. Shamrashamra zikawa kubwa zaidi na watu, wale waliokuwa mbali na hilo eneo, wakanyoosha miguu yao kuja eneoni maana kitovu cha shughuli kilikuwa kimekaribia kuwadia.

Fursa alinyanyuka akajongea katikati ya uwanja. Hapo aliketi akakutana na wazee watatu wa baraza ambao mmojawao alikuwa amebebelea mto mwekundu wenye taji la dhahabu na vito vya thamani.

Taji hilo ndilo lilikuwa lakaribia kupachikwa kwenye kichwa cha Fursa ambaye macho yake ya tamaa yaligoma kubanduka kwenye taji hilo lililokuwa linametameta na kuita.

Alijikuta anameza mate kana kwamba anangojea chakula kitamu kilichokuwa kinamtesa na harufu yake nzuri.

Ikiwa imebakia sasa sekunde, na Fursa akiwa amesimama tayari kwa ajili ya kupachikwa kofia na watu wote wamesimama kushuhudia hilo, ghafla mawingu yasijulikane yametoka wapi yalijikusanya kwa kasi na kubana anga. Jua halikuonekana tena na kukawa giza.

Hali hiyo ilitengeneza hofu.
.
.
.
.
.
. *** HAKUNA ZAIDI … ZAIDI YA MKUFU WA MALKIA WA GOSHEN! ***
.
.
.
.

Farasi wa Malkia Sandarus alisimama ghafla akapandisha miguu yake ya mbele juu. Mgongoni mwake alikuwa amembelea Malkia lakini pia Zura. Wanawake hao walikuwa njiani kwenda uwanjani kutengua ama kupinga kusimikwa kwa Fursa kama mfalme.

Ila kabla hawajafika huko, walistaajabu hali ya hewa inabadilika ghafla mbele ya macho yao kiasi kwamba hata farasi pia alihofia!

Walitahayuri, na bado wakiwa hapo wakasikia sauti kubwa ya kishindo inakuja. Haraka Zura alikamata bega la Malkia akapayuka:

“Malkia, ni Jayit anakuja!”

Malkia alikuwa mgumu kuelewa, ila baada ya muda mfupi alielewa kile alichokuwa anakinena Zura: Jayit anakuja! Hakuna mahali Jayit anakanyaga pakawa na mwanga wa jua. Kila mtu anajua kwenye utawala wa Devonship hakuna kitu kinaitwa jua wala mwanga wake.

Ina maana sasa Jayit anakuja!

Ilikuwa ni taharuki. Malkia hakutaka kuacha tawala yake akimbie. Alitaka kuhakikisha anamuona Jayit lakini pia kumzuia asidhuru watu wake. Akiwa humo tahamuni, akakumbuka jambo, ila kwa muda alikuwa amekawia kufanya lolote.

Wakati akiwa amelala kuna muda alihisi kifua chake kikiwa cha moto. Ilikuwa ni mkufu wake ukiwa unampasha habari juu ya yale ambayo yangetokea muda si mrefu mbele. Ulionyesha ujio wa Jayit, lakini pia ukionyesha yale ambayo angeyafanya mwanaume huyo kwenye tawala ya Goshen.

Masikini Malkia hakuweza kusikia wala kuona yote hayo. Usingizi mzito mno aliokuwa nao ulimnyima hiyo fursa. Alikuwa amechoka mno na mwili wake ulikuwa unahitaji sana kupumzika.

“Malkia, tuondoke!” Alisisitiza Zura. “Huu sio muda wa kubakia tena hapa. Kama kweli unaipenda Goshen, ni bora tukaondoka sasa. La sivyo utauwawa na hautopata tena fursa ya kuwa nao wala kuwasaidia.”

Huo ulikuwa ukweli mchungu kwa Malkia. Machozi yalimtiririka. Alimgeuza farasi wake akamkimbiza kuelekea upande karibu zaidi wa mpaka wa Goshen.

Waliridhia kuelekea utawala wa Maam, huko wakafanye kuyachimbua mengi juu ya mkufu ule alionao Malkia. Waliamini kwasababu mkufu huo umetoka huko basi ni lazima kutakuwa kuna mabaki ya historia juu yake. Historia ambayo inaweza ikawapa muelekeo wa kipi cha kufanya na namna gani ya kufanya.

Kutokana na giza lililokuwepo, baada ya muda hatukuwaona walipoelekea. Hata rangi nyeupe ya farasi ilikuwa imemezwa.
.
.
.
.
.
***
.
.
.
Farasi wengi weusi walisimama mbele ya uwanja mkubwa wa Goshen. Watu wegine walikuwa wamekimbia kwa kuogopa, ila wengi wao walibakia eneo hilo wakiamini ya kwamba ndipo ni salama kuliko pengine.

Wanajeshi walikuwa wamejaa, hivyo walitumai endapo litakapotokea lolote basi wanajeshi hao watalinda pumzi zao.

Wanaume waliokuwa wamebebelewa kwenye farasi hao weusi walikuwa ni watu wenye miili mikubwa. Walikuwa na nywele nyingi na mikononi mwao walikuwa wamebebelea mapanga marefu yaliyokuwa yanametameta kwa ukali.

Toka katikati ya farasi hao ambao walikuwa wamajipanga kwa nidhamu kubwa, alitokea mwanaume mrefu mwembamba. Nywele zake zilikuwa ndefu mno zilizogota kwenye mabega. Macho yake yalikuwa mekundu kama amevuta marijuana. Mdomo wake ulikuwa mweusi kama wa kunguru. Alitisha kumtazama. Alitisha akikutazama.

Alikuwa ni Jayit!

Mkononi mwake alikuwa na panga jembamba zaidi ya walinzi wake, ila lilikuwa refu na kishikizi chake kilikuwa na fuvu dogo la kichwa cha binadamu.

Uwanja mzima ulikuwa kimya. Japokuwa wengine hawakuwa wanamuona Jayit, walikuwa wanahisi uwepo wake. Kitendo cha jua kuzizima ilikuwa ni alama tosha.

Jayit alitembea kumfuata Fursa. Alipofika hata salamu hakutoa, akasema:

“Nahitaji makaburi.”

Sauti yake ilikuwa ya chini lakini nzito mno. Fursa kabla hajajibu alitazama kwanza uwanja mzima, akaona jinsi watu wanavyomtazama. Hakutaka kuwaangusha, tena akiwa ni kiongozi ambaye muda si mrefu kuna uwezekano wa kuwa mfalme.

Alikataa kumpa Jayit uwanja wa makaburi, lakini pia akamtaka mwanaume huyo aondoke kwenye ardhi ya Goshen upesi!

Jayit alitabasamu tabasamu la upande mmoja kisha akaguna. Alimtazama Fursa kwa macho yake makali. Fursa alitetemeka mwili mzima. Jayit alitabasamu tena kisha akaliza vidole vyake … pat!

Mara giza likaongezeka maradufu. Sasa hakukuwa na uwezekano wa kuonana na yeyote yule!

Jua lilikuja kurejea baada ya dakika tano ama zaidi. Si Jayit wala watumishi wake walioonekana mahala popote pale! Fursa, akiwa ameongozana na walinzi wake kadhaa, alielekea upesi kwenye eneo la makaburi. Huko alikuta makaburi mawili yamefukuliwa na mifupa haipo. Makaburi hayo yalikuwa ya babu na bibi wa Jayit.

Sasa Jayit alikuwa amepata kile alichokuwa anakitaka kwa muda mrefu. Hakuna aliyekuwa anajua ataenda kufanyia nini hayo mabaki, na ilimuogofya kila mtu.

Hakuna aliyedhani mtu kama Jayit anaweza akawa na dhamira safi. Hakuna! Na hakuna pia aliyekuwa na uthubutu wa kwenda kwenye tawala yake kumuuliza ilhali sasa alikuwa tayari ameshatimka.

Ilikuwa tumbo joto.

Zoezi la kumsimika mfalme lilisitishwa maana jua lilikuwa tayari limeshatoka katikati ya anga, na watu pia hawakuwa kwenye munkari wa hilo zoezi tena bali uwoga. Fursa alighafirishwa mno na hilo. Uso wake ulikuwa mwekundu na kwake kesho ilikuwa mbali mno.

.
.
.
.
.
***
.
.
.
Lako jicho!
 

Similar Discussions

Back
Top Bottom