mkumbwa junior
JF-Expert Member
- Oct 22, 2014
- 814
- 1,545
Twende kaziMKUFU WA MALKIA WA GOSHEN 011
Simulizi za series
Upepo ulipuliza kando, Tititat akabadili mwelekeo. Hii ilikuwa kheri tena ya haja kwani kwa sasa shari ya kukumbana na aidha Nedal au Zura ilikuwa finyu ya mraba. Na ikawa hivyo Tititat asimwone yeyote isipokuwa miili ya wale wafu – wajumbe waliouwawa na Nedal.
Aliona eneo hilo akiwa umbali wa hatua kama hamsini. Sauti ya fisi ilibeba hisia zake na kumfanya atazame eneo hilo. Roho yake ilimtuma ajongee papo na mwili wake ukatii, basi akasogea.
Alituama eneoni hapo kwa muda akiperuzi na macho yake. Hakuona cha maana basi akaendelea na safari yake. Lakini kichwa chake hakikutaka kubanduka kwenye tukio hilo. Aliendelea kuwaza miili ile kiasi kwamba alijiona mwehu. Watakuwa tu ni masikini waliofia njiani! Alijipa ahueni. Lakini makazi ya watu yana umbali kiasi gani cha kuwafanya wafie jangwani? Basi watakuwa wameuawa! Akahitimisha na wazo hilo jepesi japokuwa bado lilinanga kichwa chake.
Dhamira yake kuja kule ilikuwa ni kumtafuta tu yule aliyeagizwa amtafute – Malkia Sandarus, maana ana kitu cha thamani ambacho mfalme wake, Jayit, amekibashiri. Kitu ambacho kinawindwa. Kitu ambacho hakijulikani ni kipi. Ajabu hili! Uwezo hulevya.
Ni kwa wakati huo, Zura, mwanamke pekee aliyekuwa ndani ya jangwa, alikuwa amejilaza juu ya mchanga wa jangwa akiwa amejifunika shuka dhoofu. Baridi lilikuwa kali na likamtenda akajikunyata. Farasi wake aliketi kando ila bado yeye macho yake yakiwa wazi, akiyatupa huku na kule.
Kwa muda huo kulikuwa tulivu na si ajabu hata wewe ukadhani ndio muda mwema wa kujipumzisha.
Si kwamba Zura alikuwa amesahau yale aliyoyaona ya miili ya wafu, la hasha! Macho yake yaligoma kufumba kwa kuhofia usalama wake. Mkono wake wa kuume ulikuwa umeshikilia kisu chake kidogo alichokiweka kiunoni ya kwamba kwa lolote litakalojiri basi atajitutumua kujiokoa.
Alitenda vivyo kwa masaa kama manne, macho yaangaza. Lakini Mungu hakuwa mjinga kuweka usingizi uambatane na kufunga macho, kwani nayo yahitaji kupumzika. Basi taratibu Zura akawa anashindwa kuyaokoa macho yake na usingizi, akalala! ‘kajoto’ alikojitengenezea kwa kujikumbatia mwenyewe na kujitandaza shuka kakampa ahueni, hakujua hata ni muda gani mkono wake uliacha kisu.
Aliufaidi huo usingizi kwa lisaa limoja tu kabla hajashtushwa kwa kukosa hewa! Kabla ya tukio hilo, farasi alilia lakini Zura hakusikia. Shingo yake ilikabwa vilivyo kiasi cha kutoa macho akipapatika kutaka kujikomboa. Uso wake uliunda huruma na mbashara aliona uso wa mtoa roho.
“Shhh! Nyamazaa!” Sauti ya kiume ilinong’oneza masikio ya Zura. Alikuwa ni Nedal akimtenda mwanamke huyo. Usiniulize alifika hapo muda gani maana sitakuwa na jibu.
Mikono minene ya mwanaume huyo ilikuwa imeficha shingo ya Zura barabara, uso wa mwanamke huyo ukachomoza mishipa ya damu kana kwamba mito juu ya ramani. Kwa namna alivyokuwa amebanwa, alisahau hata kama ana kisu. Mikono yake yote ilikuwa inang’ang’ana kuivuta mikono ya Nedal, kazi ambayo haikuonyesha dalili yoyote ya kuleta matunda.
Ikiwa imebakia sekunde sasa Zura afariki, twaweza sema hivyo, mara alijikuta akipata ahueni ya ghafla baada ya mikono mizito ya Nedal kubanduka shingoni mwake! Hakuamini kama amepona. Farasi alimtwanga Nedal teke zito la kichwani, Nedal akazirai.
Kabla ya kufanya lolote, Zura akahangaika kwanza kuvuta pumzi kwa nguvu zake zote. Alikohoa na kukohoa. Alishikilia shingo yake iliyokuwa inamdai maumivu makali. Kwa muda wa kama dakika tatu alikuwa anavuta pumzi tu.
Alichomoa kisu chake akamtazama Nedal aliyekuwa amezirai. Alijitahidi kumng’amua mtu huyo lakini hakuwepo kumbukumbuni mwake hivyo akashindwa kuelewa ni sababu gani ilivyomfanya mwanaume huyo atake kumuua. Alitaka kummaliza kwa kumkobeka kisu cha kifua, akashindwa. Roho yake ya huruma ilikuwa kubwa kuliko ya ukatili.
Alinyanyuka akampongeza farasi wake kwa kumbata kabla hajamkwea na kuondoka toka hapo kwa kasi kubwa.
Hakusimama mpaka pale farasi alipochoka, akashuka toka mgongoni mwa mnyama huyo akawa anatembea. Hakutaka kulala kabisa japokuwa mwili ulikuwa unahitaji hiyo huduma. Alihofia, tena maradufu! Aliuona usingizi kama kifo.
Alitembea kwa muda wa lisaa akipambana na pepo kali ya jangwa. Ila ghafla akiwemo metembezini, akajikuta akizama kwenye tego. Alikanyaga eneo fulani ambalo lilimomonyoka upesi na kummeza kana kwamba mdomo wa mamba. Si yeye wala farasi wake aliyebakia kwenye uso wa dunia!
Palikuwa kimya ghafla usiwaze kama kulikuwa kuna viumbe hai hapo sekunde tano nyuma.
.
.
.
.
***
.
.
.
.***
.
.
.
.
.
Masaa mawili tangu pale jua lilipochomoza, Rhoda anaamka toka kwenye usingizi mzito.
Ni ndani ya chumba kikubwa mno chenye samani za gharama ndefu mathalani kitanda kikubwa na kipana, madirisha makubwa, kabati kubwa, vigoda na viti vya kujipumzishia.
Rhoda alitazama huku na kule. Hakuwa anajua pale alipo wala hakujua amefikaje, lakini punde akili yake pevu ilimwambia yu ndani ya hekalu ya mfalme, ndiyo! Hakuna chumba chochote chaweza kuwa vile ndani ya himaya yote ya Goshen. Japokuwa Rhoda hajawahi kutembelea vyumba vyote ndani ya himaya ya Goshen, aliamini hivyo.
Pasipo juhudi tabasamu likachipuka usoni mwake. Hatimaye amefanikiwa! Aliwaza. Kwahiyo malkia Vedas amesadiki yale aliyomwambia? Ndio!
Alifuata dirisha mojawapo akaangaza kutazama nje. Uso wake ulijawa tabasamu. Alijiona yuko juu ya dunia. Alitazama karibia himaya yote ya Goshen asiamini. Niko ndotoni au? Hapana bwana! Alipepesa macho yake ahakikishe kama anaota. Alitabasamu mpaka jino la mwisho.
Mara mlango ulifunguliwa, akaingia mwanaume mmoja jabali akiwa amevalia nguo za watunza usalama. Alikuwa ni mojawapo wa wanaume wale waliomkomboa Rhoda toka kwenye mikono ya wauaji. Alimtazama Rhoda na macho makavu akisema:
“Nifuate!”
Kisha akaondoka. Rhoda alimfuata mwanaume huyo mpaka mahali penye kibaraza kinachotazama kaskazini mwa himaya ya Goshen. Hapo alimkuta Vedas akiwa na mwanaume mmoja mgeni machoni: alikuwa ni mrefu, mwili wa kiume, nywele nyeupe, macho yenye kiini cha kijani na kidevu pacha akiwa amevalia nguo iliyomkaa vema.
Alikuwa ndiye mwanaume yule Jayit aliyemwona kwenye rada zake akifanya mapenzi na Vedas.
Rhoda alitoa heshima yake kwa malkia kabla hajaamriwa aketi chini. “Nimehakiki yale uliyoyasema ni kweli,” alisema malkia Vedas.
“Na kutokana na uzalendo wako basi nimeamua kukutunuku kwa hilo.”
Rhoda aligundua ya kwamba malkia alituma wanajeshi wake wamfuatilie baada ya kutoka pale hekaluni akiamini ya kwamba kama ni kweli yale aliyoyasema basi ni lazima wazee wale dhalimu wa baraza wangechukua hatua na kujiingiza mkenge.
Lakini zaidi ya hapo, Rhoda akajuzwa kuwa wazee hao tayari wameshauawa. Mbaya si wale tu wadhalimu, bali wote. Miili yao ilikuwa nje inaning’inia kwenye vitanzi. Hapo Rhoda akaguswa, lakini pia akashangazwa na roho ya Vedas. “Nimeona nikupe nafasi kubwa sana kwenye usalama,” alisema Vedas. wakati akiongea hayo alikuwa anatazama himaya yake.
“Lakini kabla ya kukupa nafasi hiyo, nataka nihakikishwe zaidi juu ya uwezo wako. Kwahiyo kwa mwezi huu wote utakuwa chini ya uangalizi wangu. Utakuwa ukiishi kwako kama kawaida lakini huduma zako zote zikitokea hapa. Utakuwa unafanya kazi zako kama kawaida lakini lengo lako likiwa ni moja tu – kuwa jicho langu la ndani.
Kuna watu wengi kwenye himaya hii. Si wote wenye nia nzuri na mimi, na si wote wenye nia nzuri na Goshen. Na bahati mbaya sipo kila mahali kuhakikisha hilo.
Nahitaji kuona kila mahali. Nahitaji kumsikia kila mtu. Kutimiza hilo basi nakuhitaji wewe. Kwa kazi yako unayoifanya, upo karibu sana na midomo ya watu. Nataka uniletee kila wanachokiteta.”
Baada ya maelezo hayo, Rhoda aliondoka zake kurudi nyumbani. Alipewa dinari nyingi sana za kumfaya afanye chochote anachotaka maishani. Aliagizwa aboreshe kazi yake ya mama n’tilie na kila baada ya siku mbili awe analeta mrejesho wa yale anayoyasikia na kuyaona. “Una uhakika hili litafanya kazi?” Aliuliza Vedas akimtazama mwanaume aliyekuwa kando yake.
Mwanaume huyo alitabasamu. Hakuwa na papara. Macho yake yalikuwa yanatazama uwanda wa Goshen. Ukimwita Phares, utakuwa hujakosea. Phares, mwanaume wa chupa; Phares, mwanaume aliyeghaniwa na malkia Vedas; Phares, mwanaume asiye na makazi bali kwenye ulozi wa Vedas; mwanaume ambaye Vedas anamwamini kuliko yeyote.
“Pasi na shaka, itafanya kazi,” alijibu Phares. “Na kama isipofanya kazi basi ndiyo itakuwa fursa yako ya kutimiza haja yako ya kummaliza.” Malkia Vedas alitabasamu kwa mbali, ila tabasamu lake hilo halikudumu likajifinya na kuunda uso wa kazi.
Siri ilikuwa sirini.
Malkia Vedas anapata kufahamu mahusiano ya Rhoda na marehemu Fursa. Jambo hili analing’amua baada ya kutonywa na mojawapo wa wanajeshi wake ambaye alikuwa anajua juu ya mahusiano hayo yaliyokuwa ya siri. Malkia anataka kummaliza Vedas akiwa usingizini, lakini Phares anamsihi amwache hai kwani ana matumizi ya faida kabla ya kumalizwa.
.
.
.
. ***
.
.
.
Ilikuwa ni zaidi ya juma moja lakini si zaidi ya mwezi tangu Sultan alipowasili kwenye himaya yake, tawala kubwa Arabuni, akiwa amebebelea vipuri kadha wa kadha vya dhahabu alivyotoka navyo Osheni.
Alikuwa hana furaha na mtingwa wa mawazo. Lakini pia mkimya aliyependa kujitenga mara kwa mara. Mke mkubwa wa Sultan anasumbuliwa sana na hili jambo. Anatamani kujua kinachomsibu mumewe japokuwa zoezi hilo limekuwa gumu kila mara anapojaribu.
Ndani ya siku hiyo, Sultan anashindwa kuendelea kubeba jambo hilo kifuani. Alimwita mkewe mkubwa akamtaka aketi pembezoni. Alimweleza juu ya mkufu wa himaya ya wasioonekana, ambao habarize alizikuta Osheni, na jitihada zake alizofanya kuuweka mkufu huyo kimyani.
Anatatizwa na ukimya wa mjumbe wake, na hajui ni nini shida haswa. Kwa namna kubwa anahisi ameshaupoteza. “Huenda mjumbe wangu akawa ameshauwawa,” alisema Sultan. Uso wake ulikuwa mwekundu, macho yake yakilegea kwa uchovu.
Mke wake alimsogelea karibu zaidi akamwekea mkono begani. “Mbona hukunambia hili jambo mapema mpenzi?” “Na sikutaka hata kulisema. Hili ni jambo la siri, na nyie wanawake hamna vifua.” “Ila si mimi, Sultan.” Alijigamba mke mkubwa. “Ni siri zako ngapi naziweka kwenye uvungu wa kifua changu?” “Najua ni nyingi ila hii ni kubwa zaidi. Hili jambo ni watu wachache sana wanalijua, na kama lingekuwa linajulikana na wengi lingeshazua vita.” Mke akaguna. Alishusha pumzi ndefu na kuivuta. Alikunja sura yake akijaribu kuchekecha jambo alilolikumbuka.
“Mpenzi!” aliita.
Sultan akaitika kwa kumtazama mke wake huyo; mwanamke mtu mzima ila mwenye uzuri kwa kukusisimua moyo; mwanamke aliyekuwa amejiremba itakiwavyo kila kitu kikiwa kwenye kiti chake.
“Lakini unaonaje ukajaribu kwa Al Karim!”
alisema mke.
“Al Karim?” Aliuliza Sultan akitafakari. “Ndio, kwa Al Karim. Hakuna asiyejua habari zake zinazovuma kutokea kaskazini. Mjuvi na mtaalamu wa ramli. Kwanini usiende kumweleza shida yako? Bila shaka atajihisi fahari kumhudumia Sultan.”
Sultan alinyamaza akiwazua. Baada ya dakika mbili alirudisha macho yake kwa mkewe akauliza: “Tunaweza tukamwamini kweli?”
“Bila shaka,” akajibu mke mkubwa. “Ni binamu yangu, mtoto halisi wa mjomba wangu, kaka wa kwanza wa baba yangu. Endapo nikimtaka afunge mdomo, basi atatenda.” Sultan alishawishika kuchukua hiyo njia. Siku iliyofuata, asubuhi na mapema, akadamka pamoja na mkewe mkubwa wakaongozana na msafara wake kuelekea kaskazini mwa himaya yake kubwa.
Alitumia siku moja njiani kabla ya kufika kwenye nyumba kuukuu ya bwana Al Karim. Alipewa mapokezi makubwa sana japokuwa alikuja kwa kush’tukiza. Walichinjwa wanyama kadhaa na mivinyo ikamwagikia vinywani.
Jioni ya siku hiyo, akiwa na Al Karim pekee, Sultan alieleza haja yake ya moyo iliyomleta pale. Haja hiyo ikamshtua Al Karim kwa kina. Macho yalimtoka pima na mdomo wake ukaachama.
“Sultan, ni kweli usemayo?” “Pasi na shaka, Sultan hawezi kuongopa.”
“Ni wangapi wajua kuhusu hili?”
“Wachache mno.”
“Lakini Sultan, wajua ni namna gani mkufu huu waweza leta balaa?”
“Najua, lakini ni vema tukafikiria mema yake kwanza kabla ya mabaya.”
“Sultan wangu,” Al Karim aliita kwa sauti ya upole. “Endapo kama wenye nao wataamka, basi watatuteketeza wote.” Alionya.
“Kivipi?” Sultan akauliza.
“Huu mkufu ni wa himaya ya wasioonekana. Hakuna himaya yoyote inayoweza kuwazuia hawa. Endapo kama wakija kudai chao, himaya yetu itageuka kuwa majivu!”
“Na vipi kwa himaya hizo watakaoumiliki? Huoni watatugeuza sisi majivu kabla ya hao wasioonekana?” Mzozo huu uliishia kwa Sultan kushinda akitumia madaraka yake kama silaha.
Al Karim alipiga ramli akitumia kioo chake cha ajabu, akauona mwili wa mjumbe wa Sultan ukiwa umebakia mifupa sasa. Alijaribu kuutafuta mkufu lakini hakuuona. Sultan akamwagiza amtafute Zura.
Zoezi hilo lilichukua kama dakika tatu, kioo kikawa giza. Al Karim alitikisa kichwa chake, akasema:
“Sultan, hatuwezi kumpata!” “Unamaanisha nini?” “Huyo Zura hayupo duniani!” Sultan akakunja uso.
.
.
.
.
.
****
.
.
.
Kazi kazi! Lako jicho.