Rais Samia amesema amemhamisha Maharage Chande kutoka TCCL ili kuondoa mgongano wa kimaslahi kwa kuwa ana biashara na taasisi hiyo.
"Maharage tumekutoa TANESCO na nikachukulia uzoefu wako wa DSTV nikaona sekta ya TTCL ingekufaa zaidi. Sasa baadae nikagundua una biashara ndani ya TTCL na kwa sababu kampuni ile inafanya vizuri na ndio maana imemuwezesha kijana yule nae kufanya vizuri nikasema hapana, usiende mahali ambapo una biashara, itakuwa conflict of interest. Nikaona sasa nikupe u postamasta mkuu" Amesema Rais Samia.
Aidha, Rais Samia amebainisha kuwa Postamasta wa sasa amekwenda kwenye mafunzo na akirudi atapangiwa kazi nyingine. Amemtaka Maharage kwenda kuikuza sekta hiyo ili iende kidigitali.
Rais Samia amesema taarifa za mambo yanayofanywa na watendaji ziwe zinaandikwa na kutumwa ili aweze kuelewa vyema wakati wa kutoa maamuzi na kuondoa changamoto ya kuondoa watu wanaostahili kuwepo kwenye sehemu husika.
Kuhusu changamoto ya kukatika kwa umeme, Rais Samia ametoa miezi 6 kwa mkurugenzi wa sasa ili aweze kuondoa tatizo hili linalochangiwa na mambo mengi ikiwemo mabadiliko ya hali ya hewa na ukarabati wa mitambo.
"Tatizo la kukatika kwa umeme si la mtu, ni letu kitaifa. Kwa hiyo sasa tumejipanga vizuri, tunafanya ukarabati wa hizo mashine, lakini pia tuna mipango mingine ya kujenga substations, kuunganisha mikoa kwenye gridi ili umeme usikatike. Kwa hiyo, nenda kaanzie pale Maharage alipoishia. Najua utaweza, nakupa miezi 6, nakuangalia pale TANESCO. Kazi yako ya kwanza kusimamia ukarabati wa mitambo, lakini baada ya miezi 6 nisisikie kelele za kukatika kwa umeme"
Maharage hakuona tatizo wakati anapokea uteuzi?