Kama ni kweli basi haya mambo yanazidi kupanuka na mwisho tutapata habari za kusikitisha zaidi. Soma hii kutoka gazeti la Tanzania Daima.
Mallya ni jasusi
na Kulwa Karedia
VIONGOZI watatu kutoka kambi ya upinzani, wameibua madai mengine mazito yanayoonyesha kuwa mtu anayedaiwa kuendesha gari lililokuwa limembeba aliyekuwa Mbunge wa Tarime, marehemu Chacha Wangwe, ni jasusi aliyefuzu mafunzo hayo na ni mtaalamu wa hali ya juu wa kompyuta.
Viongozi hao na vyama vyao kwenye mabano ni Mwenyekiti wa Chama cha Wananchi (CUF), Profesa Ibrahim Lipumba, James Mbatia (NCCR Mageuzi) na Augustine Mrema (TLP).
Waliwaambia waandishi wa habari katika makao makuu ya NCCR- Mageuzi, Dar es Salaam jana kuwa, Mallya ni mmoja wa watu wanaoonekana kupata mafunzo makali ya kijasusi, ambayo yanahatarisha usalama wa taifa.
Aliyeanza kuzungumza katika mkutano huo ni Profesa Lipumba, ambaye alidai kuwa Mallya aliwahi kupata mafunzo hayo nchini Libya, jambo ambalo linapaswa kufanyiwa kazi na vyombo vya usalama ili kubaini ukweli zaidi.
Huyu tunaambiwa alikuwa dereva wa Wangwe, lakini tunaambiwa kwamba ni mtu ambaye alizoeana naye kwa muda mfupi sana, hali ambayo inaibua maswali mengi
lakini tunaambiwa aliwahi kuishi Libya, sasa huku alikuwa anafanya nini? alihoji Profesa Lipumba.
Alisema mbali ya Mallya kuwa na mafunzo hayo, pia katika upekuzi alikuwa na vitambulisho vingi ambavyo vilikuwa na maandishi mbalimbali yakiwamo ya Kiarabu.
Mbali ya kuishi Libya kijana huyo, alikutwa na vitambulisho vingi mno, tena vikiwa katika lugha mbalimbali, vikiwemo vyenye maandishi ya Kiarabu, ndiyo maana tunasema huyu ni jasusi na mtu mwenye mafunzo makali, alisema Profesa Lipumba.
Alisema Mallya anaweza kuwa na maelezo mengi kama akihojiwa vizuri jinsi alivyoweza kumfahamu marehemu Wangwe na mazingira mazima ya ajali ilivyotokea, alisema Profesa Lipumba.
Kuhusu hali ya vurugu iliyotokea wilayani Tarime wakati wa mazishi ya Wangwe, Profesa Lipumba alikiri kuwapo hali hiyo, jambo ambalo alisema liliwatia shaka viongozi wote waliohudhuria mazishi hayo.
Unajua pale Tarime wananchi walionekana kuwa na munkari sana, huku wakionyesha kutoamini kwamba Wangwe kafariki kwa ajali ya gari
lakini baada ya uchunguzi na maelezo yaliyotolewa na kaka yake, Profesa Samwel Wangwe, ulionyesha kuwa alikufa kwa ajali iliyosababisha fuvu la kichwa kupasuka, alisema Profesa Lipumba.
Kwa upande wake Mwenyekiti wa NCCR- Mageuzi, Mbatia, alisema mazingira waliyoyakuta Tarime yalikuwa ya hatari na kumpongeza Kamanda wa Polisi wa Mkoa wa Mara, Lebaratus Lyimo na Mkuu wa mkoa huo, Kanali mstaafu, Issa Machibya, kwa kuhakikisha hali ya utulivu na amani inakuwapo.
Alisema mbali ya hali hiyo, kifo cha Wangwe bado kimewatia mashaka wapinzani, kwani inaonyesha kuna mtandao wa uhalifu unaotishia usalama wa taifa.
Tumegundua kuwa hivi sasa kunaonyesha wazi kwamba kuna mtandao wa uhalifu, uharamia unaotishia usalama wa taifa letu, kwa moyo mweupe nasema lazima tujitolee ili kuhakikisha hali hii haitokei kabisa, alisema Mbatia.
Alisema wamepata taarifa nyeti kwamba Mallya amepata mafunzo makali ya kijasusi, ikiwamo kupindua magari, na kwamba hiyo inawalazimu kukutana na Mkuu wa Jeshi la Polisi, Inspekta Jenerali (IGP), Said Mwema, kwa ajili ya kumweleza ukweli wa mambo hayo.
Kutokana na ukweli wa mambo haya, sasa tunajiandaa kukutana na IGP Mwema kwa ajili ya kumweleza ukweli kuhusu kijana huyu Mallya
tupo hapa kwa masilahi ya taifa letu, alisema Mbatia.
Tunasema uhalifu huu lazima ukomeshwe, taifa haliko salama, niko tayari kumweleza ukweli wa mambo kuhusu suala hili, hatupaswi kuficha, tutatoa ushirikiano wa kila aina kutokomeza uhalifu huu na kwamba tunataka jambo hili liwekwe hadharani, alisema Mbatia.
Naye Mwenyekiti wa TLP, Mrema, alisema kambi ya upinzani imepata pigo kubwa kwa kupoteza kiongozi shupavu na mtetea haki za watu wake.
Kwa mara ya kwanza kambi ya upinzani tumepata pigo kubwa ambalo halijawahi kututokea
tumezoea kuyaona kwa wenzetu, sasa kazi iliyoko mbele yetu ni kupambana na tatizo hili ili kuona nchi yetu inabaki salama, alisema Mrema.
Alisema mtandao wa kijana huyo umesambaa nchini na kuitaka polisi kutopuuzia madai hayo, kwa lengo la kuhakikisha hali ya ulinzi na utulivu inaendelea kuwapo nchini.
Akizungumzia ilivyokuwa Tarime, Mrema alilipongeza Jeshi la Polisi wilayani humo kwa kutotumia nguvu ya kukabiliana na wananchi waliokuwa wamejitokeza kwenye mazishi hayo.
Kama polisi wangetumia nguvu kubwa pale msibani, hali ingekuwa mbaya, lakini walitumia busara iliyowezesha hata sisi kuendelea kubaki pale
hali ya usalama haikuwa nzuri sana, mpaka viongozi wote tulipitishwa kwenye mlango ambao mwili wa marehemu ulikuwa umewekwa, alisema Mrema.
Alisema katika mazishi hayo, baadhi ya T-shirt zilizokuwa zimeandaliwa na bendera zilichomwa moto, kitendo kinachoashiria kuwapo kwa vurugu zilizotokana na ndugu, jamaa, marafiki na wapiga kura wa Wangwe, kutaka kujua sababu ya kifo cha Wangwe.
Alisema hasira ya wananchi wa Tarime haikutokana na ujio wa Mwenyekiti wa CHADEMA, Freeman Mbowe, kama ilivyoripotiwa na baadhi ya vyombo vya habari nchini.
Wakati wapinzani wakitoa tuhuma hizo nzito dhidi ya Mallya (27), tayari kijana huyo amefunguliwa mashitaka katika Mahakama ya Hakimu Mkazi Dodoma, akidawa kuendesha gari bila leseni na kusababisha kifo.
Tangu kutokea kwa ajali hiyo, kumekuwa na maswali mengi kuhusu ni nani hasa alikuwa akiendesha gari lililosababisha kifo cha Wangwe, baada ya maelezo ya watu mbalimbali kuonyesha kuwa Mallya ndiye aliyekuwa dereva, tofauti na maelezo ambayo amekuwa akiyatoa kwa siku kadhaa sasa.
Katika mahojiano ya ana kwa ana aliyofanya na Tanzania Daima kwa nyakati mbili tofauti, Mallya alifikia hatua ya kudai kwamba alikuwa hajawahi kuendesha gari na kwamba alikuwa hana utaalamu wowote wa udereva.
Mimi sijui kuendesha gari na wala sina utaalamu wowote wa kuendesha magari, nimeshangazwa sana na taarifa za watoto wa marehemu zilizopo magazetini kwamba tulipotoka nyumbani nilikuwa namuendesha baba yao.
Ninayaogopa sana magari, lakini niliwahi kujifunza mwaka 2004, nikiwa Nairobi, yupo rafiki yangu mmoja alinishawishi kujifunza, lakini niliacha, wakati najifunza niligonga ukuta, nikaumia vibaya na sikujifunza tena mpaka leo, hivyo sijui kabisa kuendesha, alisema Mallya wakati alipohojiwa na Tanzania Daima siku mbili tu baada ya ajali.
Kauli hiyo ya Mallya ilikuwa ikitofautiana na ile iliyotolewa na watoto wawili wa marehemu Wangwe, Zakayo na Bob, ambao wote walisema wakati wakiondoka nyumbani siku hiyo ya Jumatatu wiki iliyopita, kijana huyo ndiye aliyekuwa akiendesha gari.
Aidha, maelezo yaliyotolewa na mkazi mmoja wa Pandambili aliyekuwa miongoni mwa watu wa kwanza kufika katika eneo la tukio kuhusu nani aliyekuwa akiendesha gari hilo, nayo yanaonyesha picha tofauti na ile iliyokuwa ikielezwa na Mallya.
Katika mahojiano ya ana kwa ana na Tanzania Daima, mkazi huyo wa Pandambili, George Mwigunde, alieleza kuwa, walimkuta marehemu akiwa amekaa katika kiti cha mbele cha abiria cha mkono wa kushoto wakati ajali hiyo ilipotokea.
Mwigunde ambaye alijitambulisha kuwa ni mkulima wa kijiji hicho, alisema kabla ya kumtoa marehemu Wangwe, alilazimika kumfungua mkanda wa gari kutoka katika kiti chake hicho alipokuwa ameketi.
Utata huo kuhusu nini kilitokea hata kumsababishia mauti Wangwe, ulisababisha Chama cha Demokrasia na Maendeleo (CHADEMA), kilazimike kuandika barua kwa Mkuu wa Jeshi la Polisi (IGP), Said Mwema, kikitaka kufanyika kwa uchunguzi wa kina.
CHADEMA katika tamko lake hilo ilisema imefikia uamuzi huo kutokana na kuwapo kwa taarifa zinazoonyesha kuwapo kwa utata katika tukio zima.
Chama hicho kilimtaka IGP kumchunguza Mallya na kubainisha ni mtu wa namna gani, ikiwa pamoja na kufuatilia shughuli zake na uhusiano aliokuwa nao na marehemu Wangwe.
CHADEMA pia ilimtaka IGP kuchunguza ukweli kuhusu maelezo ya Mallya na kujua ni wapi alikuwa amekaa wakati ajali ikitokea na kuchukua hatua zinazopaswa baada ya uchunguzi huo.