•Mbaya wa Wangwe aanikwa
*Lipumba, wenzake wajipanga kumwona IGP
*Wadau wa habari wamjia juu Zitto Kabwe
Na Gladness Mboma
CHAMA cha Demokrasia na Maendeleo (CHADEMA) kimezidi kukabwa koo na baadhi ya wanasiasa kwa kudaiwa kuhusika kwa namna fulani na kifo cha Mbunge wa Tarime, Bw. Chacha Wangwe, kutokana na kumsimamisha umakamu Mwenyekiti.
Akizungumza na mwandishi wa habari hizi Dar es Salaam jana, Mwenyekiti wa Chama cha Siasa cha Sauti ya Umma (SAU), Dkt. Paul Kyara, alisema tangu CHADEMA ilipomsimamisha Bw. Wangwe umakamu alikuwa hatulii bungeni.
"Tunaweza kusema kuwa kifo hicho kimesababishwa na CHADEMA kwa sababu ya kumsimamisha umakamu mwenyekiti Bw. Wangwe
"Ingekuwa si hivyo, Wangwe asingekuwa na pilikapilika za kukimbiakimbia huku na kule, angetulia bungeni na hivyo asingepatwa na ajali kwa kuwa angekuwa na amani, angetulia, CHADEMA wamechangia pamoja na kuwa ni ajali," alisema Dkt. Kyara.
Alisema kwa muda mfupi aliokaa na Bw. Wangwe baada ya kumtembelea ofisini kwake kumwomba ushauri kuhusiana na kusimamishwa umakamu Mwenyekiti wa CHADEMA, simu zake za mkononi zilikuwa zinaingia kutoka sehemu mbalimbali kama vile alikuwa opareta wa simu.
Dkt. Kyara alidai kuwa kaka wa mtuhumiwa wa ajali iliyosababisha kifo cha Bw. Wangwe, mfanyabiashara Bw. Deus Mallya ambaye alikuwa na marehemu Bw. Wangwe ni rafiki mkubwa wa kigogo mmoja ndani ya CHADEMA.
Aliendelea kudai kwamba kigogo huyo wa CHADEMA amekuwa akifanya shughuli za kibiashara na kaka wa Bw. Mallya kwa siku nyingi na kudai kuwapo kwa umuhimu wa kumchunguza.
"Haiwezekani kijana mdogo kama huyo kuwa na urafiki na mtu mkubwa kama marehemu Wangwe, eti amekwenda Dodoma kumwandikia marehemu kitabu cha umaarufu wake, haiwezekani hata kidogo, huyu alikwenda huko kwa lengo fulani," alisisitiza Dkt. Kyara akikariri maelezo ya Bw. Mallya kama alivyokaririwa katika gazeti la Mtanzania la jana.
Alisema mara ya mwisho wakati Bw. Wangwe anakwenda Dodoma alipita ofisini kwake akiongozana na mkewe na watoto wake wawili wakitokea Muhimbili kumwona Naibu Katibu Mkuu wa CHADEMA, Bw. Zitto Kabwe, ambaye alikuwa amelazwa.
"Nilimuuliza hali ya mgonjwa, licha ya kwamba alikuwa akimtukana wakati akiwa Tanga, hapo ndipo nilipojua kuwa Bw. Wangwe alikuwa na moyo ya utu licha ya kutukanwa lakini alikwenda hospitali kumwona," alisema Dkt. Kyara.
Alisema yeye alimkabidhi Bw. Wangwe habari ya kwenda kuchapisha katika vyombo vya habari na kumsihi pia kufikisha suala la kufutiwa uanachama mahakamani, kwani alimweleza kuwa akifukuzwa uanachama 'biashara imekwisha'.
Dkt. Kyara alisema marehemu alimweleza kuwa alikuwa amekwishapata Mwanasheria ambaye alitaka sh. milioni 12 gharama ambayo alimweleza kuwa ni kubwa, na alimshauri atafute wakili mwingine.
Alisema alimshauri marehemu amtafute mwanasheria mwingine licha ya kwamba anasimamia kesi dhidi ya CHADEMA na CCM na aliegemea sana upande wa CCM.
"Nilimwambia ajaribu kwenda kumwona na amweleze kuwa mimi ndiye niliyemtuma na angempa mawazo mazuri na kama akishindwa, nilimwambia amwone Mwanasheria Mathew Kakamba kwa kuwa naye ni Mwanasheria mzuri," alisema Dkt. Kyara.
Alisema marehemu aliishia kwa Bw. Kakamba na kwamba inavyoelekea, walikwishakubaliana na siku ya ajali alikuwa anakwenda Dar es Salaam kusimamia kesi yake kutokana na kuiacha CHADEMA 'uchi' na hivyo kutaka kumfukuza uanachama.
Dkt. Kyara alisema wameshindwa kumwelewa Bw. Kabwe kwa madai yake aliyoyatoa kwamba hakukuwa na fujo wala vurugu katika msiba wa marehemu wangwe.
"Mimi nilikuwa nawasiliana kila baada ya muda na watu wa Tarime, walinieleza kuwa vurugu na fujo kubwa zilizotokea kwenye msiba wa Mbunge wa Tarime, Bw. Wangwe, hazijawahi kutokea kwa msiba wa kiongozi yeyote hapa nchini.
"Na fujo hizo ziliibuka mara baada ya Mwenyekiti wa CHADEMA, Bw. Freeman Mbowe, kuwasili msibani hapo, wanachama wakalazimika kumtoa kwa mlango wa uani, sasa Bw. Zitto anakanusha nini wakati kitu kilikuwa wazi?," alihoji Dkt. Kyara.
Alisema Bw. Kabwe kudai kuwa hakukuwa na fujo wanashindwa kumwelewa alikuwa na maana gani, wakati yeye alikuwa ni mmoja wa viongozi waliokuwa wakituliza fujo.
Mwenyekiti huyo alisema kiongozi anayeaminika kitaifa na katika jamii, hatakiwi kusema uongo hata kidogo.
Alisema kutokana na kifo cha Bw. Wangwe, CHADEMA wasitarajie kupata tena jimbo la Tarime "ni dhahiri kuwa jimbo hilo wamelipoteza ikiwa ni pamoja na ruzuku kupungua na hilo halina mjadala".
Juzi wenyeviti wa CUF, Profesa Ibrahim Lipumba; TLP Bw. Augustino Mrema na Bw. James Mbatia wa NCCR-Mageuzi, walikutana Dar es Salaam na kushangaa kauli ya Bw. Kabwe, kwa wahariri wa vyombo vya habari ikikanusha kuwapo kwa vurugu katika msiba wa Bw. Wangwe kijijini Kemokerere, Tarime.
Naye Said Mwishehe, anaripoti kwamba Mwenyekiti wa CUF, Profesa Ibrahim Lipumba, amesema siku yoyote kuanzia leo watapeleka ushahidi wao kwa Mkuu wa Jeshi la Polisi nchini, IGP Said Mwema ambao utasaidia katika uchunguzi wa ajali ya gari iliyosababisha kifo cha Bw. Wangwe.
Profesa Lipumba alitoa kauli hiyo jana Dar es Salaam wakati Majira lilipotaka kujua ni lini watapeleka ushahidi wao kwa IGP baada ya kusema kwamba kifo cha mbunge huyo kimezua maswali mengi.
Alisema kwa sasa wanaendelea vizuri juu ya suala hilo na watahakikisha wana kila kitu ambacho wanaamini kitalisaidia Jeshi la Polisi kufanya uchunguzi wa kina kuhusu ajali hiyo.
"Tunakwenda vizuri katika hili na nimeacha wenzangu wanaendelea kuweka mambo sawa na siku yoyote kuanzia kesho (leo) tutapeleka kila kitu ambacho kitasaidia Polisi kuchunguza vizuri tukio hilo la kifo," alisema Profesa Lipumba.
Alisema kwa kweli kifo cha Bw. Wangwe bado kimejaa mambo magumu na lazima kitaendelea kujadiliwa na hata familia ya marehemu naamini watalizungumzia hilo.
Alipoulizwa kuhusu kulaumiwa kwa vyombo vya habari na baadhi ya viongozi wa CHADEMA kuhusiana na jinsi waandishi walivyoripoti mazishi ya marehemu Wangwe, alisema suala hilo atalitafutia siku yake kwa kuzungumza na waandishi wa habari.
Naye Naibu Katibu Mkuu CHADEMA, Bw. Kabwe, akizungumzia taarifa zilizotolewa na baadhi ya viongozi wa upinzani kuhusu mazishi ya marehemu Wangwe, alisema hawezi kusema lolote kwa kuwa tayari malalamiko yao yanashughulikiwa na Jukwaa la Wahariri.
"Kwa upande wetu tulishatoa malalamiko yetu kuhusu tukio zima la mazishi ya marehemu Wangwe na jinsi vyombo vya habari vilivyoripoti, hivyo kwa sasa hatuna cha kusema lolote kama kuna kiongozi amekuja na hoja yake, atakuwa shahidi mzuri kwa kulisaidia Jukwaa la Wahariri kufanya kazi yao vizuri," alisema Bw. Kabwe.
Kutoka Shinyanga, Suleiman Abeid, anaripoti kwamba baadhi ya wadau wa habari mjini humo wamemtaka Bw. Kabwe kuwaomba radhi waandishi wa habari kutokana na hatua yake ya kuwatuhumu kuwa waliandika habari za uongo kuhusu kufanyiwa vurugu kwa Bw. Mbowe kwenye mazishi ya marehemu Wangwe.
Hatua hiyo inatokana na kukanushwa kwa madai hayo na viongozi wakuu watatu wa vyama vya upinzani nchini juzi, ambao walithibitisha kuwapo kwa vurugu katika mazishi hayo ambapo pia Bw. Mbowe na wao wenyewe walikabiliana na vurugu hizo.
Wadau hao walisema kutokana na kubainika ukweli wa habari hizo zilizoandikwa na waandishi kuwa viongozi mbalimbali walifanyiwa vurugu ni vizuri sasa Bw. Kabwe akawaomba radhi waandishi hao.
Mmoja wa wadau hao, Bw. Juma Burhani, mkazi wa Lubaga mjini humo, alisema mashambulizi ya Bw. Kabwe dhidi ya waandishi yalivuka kiwango na bahati mbaya madai yake hayakuwa na ukweli.
Alisema ni vizuri kabla ya kukanusha habari hizo za waandishi kufanya utafiti wa kina ili kujua ukweli wake, badala ya kuwapaka matope.
"Wengi tulianza kuingiwa na wasiwasi mkubwa juu ya kitendo hicho, kuona ni vipi waandishi waamue kututangazia habari za uongo tena karibu kila chombo cha habari, lakini tukashangaa kumsikia Bw. Kabwe akikanusha kuwa hapakuwa na tukio hilo, sasa ukweli umebainika, kwa nini asiombe radhi?," alihoji.
Alisema bila ushuhuda uliotolewa na viongozi watatu wa vyama vya upinzani, Bw. Mrema, Bw. Mbatia na Bw. Lipumba, umma wote wa Watanzania ungewadharau kwa kiasi kikubwa waandishi wa habari wa nchini hasa wa mikoani.
Bw. Mohab Dominick mwandishi wa magazeti ya Nipashe, alisema Bw. Kabwe alikurupuka kuwashutumu waandishi na kwamba hakufanya subira kuchunguza ukweli wa habari alizozikanusha.
"Sasa wenzake wameweka mambo hadharani, ni kweli katika mazishi ya Bw. Wangwe kulikuwa na vurugu kubwa, kiasi cha viongozi wa vyama vya upinzani kulazimika kuokolewa na Polisi, lakini Kabwe anadai kuwa hapakuwa na vurugu zozote na amani ilitawala, sijui baada ya maelezo ya wenzake ataueleza nini umma wa Watanzania?," alihoji Bw. Dominick.