[TABLE="class: contentpaneopen"]
[TR]
[TD="class: contentheading"]Malecela azungumzia afya yake
[/TD]
[TD="class: buttonheading, width: 100%, align: right"]
Send to a friend
[/TD]
[/TR]
[/TABLE]
[TABLE="class: contentpaneopen"]
[TR]
[TD="class: createdate"] Wednesday, 22 June 2011 21:40
[/TD]
[/TR]
[TR]
[TD]digg
Boniface Meena
MWANASIASA mkongwe na kada maarufu wa CCM, John Malecela, amezungumzia afya yake kutokea nchini Uingereza, akieleza kuwa inaendelea vizuri baada ya kufanyiwa upasuaji wa moyo katika Hospitali ya Wellington North nchini humo.
Hata hivyo, taarifa za kitaalamu zilizolifikia gazeti hili zinaonyesha kuwa Malecela alipata tatizo la kuvimba kwa mishipa inayotoa damu moyoni kwenda mwilini na kusababisha mtiririko wa damu kuyumba kwa kiasi.
Taarifa zilisema kutokana na hali hiyo, njia pekee ya kuondoa tatizo hilo ilikuwa kumfanyia upasuaji mkubwa wa moyo ambapo madaktari walilazimika pia kuchukua mishipa kutoka katika mguu wake na kuweka kwenye moyo wake.
Lakini jana, Malecela mwenyewe aliyezungumza na Mwananchi kutoka Uingereza alikolazwa baada ya kufanyiwa upasuaji huo, alisema kuwa madaktari wamemshauri afanye mazoezi kwa muda wa wiki tatu hadi sita ili waangalie hali yake na baada ya hapo wataweza kumpa ruhusu ya kurudi nchini.
"Ninaendelea vizuri na madaktari wameniambia nifanye mazoezi kwa muda wa wiki tatu hadi sita kuiangalia hali ikoje ili waweze kunipa certificate (cheti) ya kuweza kurudi nyumbani,"alisema Malecela.
Mwanasiasa huyo aliyewahi kuwa Waziri Mkuu wa Tanzania, amezungumzia hali ya mwenendo wa afya yake baada ya juzi Spika wa Bunge, Anne Makinda, kuwatangazia wabunge taarifa za kutokuwapo bungeni kwa Mbunge wa Same Mashariki, Anne Kilango Malecela kutokana na mumewe kuwa mgonjwa na kufanyiwa upasuaji wa moyo.
Mama Kilango naye azungumzia
afya ya mumewe
Akizungumzia hali ya mumewe, Kilango alisema kuwa walikwenda nchini Uingereza Mei 11 mwaka huu wa ajili ya kumfanyia Malecela uchunguzi wa kawaida wa afya kama ilivyo kwa viongozi wa Serikali na alikuwa hana tatizo lolote.
Alisema kuwa yeye na mumewe wana kawaida ya kufanya mazoezi kila siku na kwamba walipokuwa katika mazoezi ya kawaida nchini Uingereza ambapo Malecela alianza kulalamika kuwa anapumua kwa shida, ndipo walikwenda hospitali ambapo alipimwa na daktari kumweleza kuwa ana matatizo ya moyo.
"Madaktari walimpima wakaona kuna mishipa inayotoa damu moyoni kwenda mwilini ambayo ilikuwa imevimba kutokana na Calcium kujikita kwenye mishipa na kuzuia mtiririko wa damu," alisema Kilango.
Kilango alisema upasuaji huo ulifanyika Mei 31 mwaka huu katika Hospitali ya Wellington North na daktari aitwaye Rakesh Uppal.
"Upasuaji umefanikiwa na yuko nyumbani sasa. Anatakiwa afanye mazoezi mara tatu kwa siku, dakika 20 asubuhi, dakika 20 mchana na dakika 20 jioni. Anafanya mazoezi akiwa na mlinzi wake pamoja na mimi hapa,"alisema Kilango.
Habari za kuumwa kwa mwanasiasa huyo ambaye ameshika nyadhifa mbalimbali serikalini na CCM zilitangazwa juzi na Makinda wakati akiahirisha Kikao cha Bunge.
[/TD]
[/TR]
[/TABLE]