source :
http://www.majira.co.tz/kurasa.php?soma=tanzania&habariNamba=2278
HakiElimu yafurahia kulegezewa kitanzi
Habari Zinazoshabihiana
• Kikwete aiweka kiporo HakiElimu 02.02.2007 [Soma]
• Serikali yake yaisambaratisha HakiElimu 31.01.2007 [Soma]
• Mbunge Cheyo atiwa 'kitanzi' 07.07.2006 [Soma]
*Yampongeza Lowassa kwa kutanguliza busara
Na Mwandishi Wetu
ASASI isiyo ya kiserikali ya HakiElimu, imefurahia kulegezewa kitanzi na Serikali na kuahidi kushirikiana na wananchi na mashirika yasiyo ya kiserikali kuimarisha maendeleo na demokrasia nchini.
Hayo yamo katika taarifa ya asasi hiyo iliyosainiwa na Mwenyekiti wake, Bibi Elieshi Lema na kusambazwa kwa vyombo vya habari jana, siku moja baada ya viongozi wa asasi hiyo kukutana na Serikali chini ya Waziri Mkuu, Bw. Edward Lowassa, Dodoma juzi.
Katika taarifa hiyo, asasi hiyo ilisema ina imani makubaliano yaliyofikiwa juzi, yatafungua ukurasa mpya wa uhusiano baina yake na Serikali na mashirika huru ya kiraia.
Ilimshukuru Bw. Lowassa kwa kuongoza mkutano huo kwa hali ya uwazi na udugu, na kwa kutambua dhima ya mashirika huru ya kiraia na kwa msisitizo wake, kwamba Serikali na HakiElimu wana malengo yanayofanana ya kuleta maisha bora kwa kila Mtanzania.
"HakiElimu inaamini kuwa zuio la Septemba 8, 2005 kwa waraka wa Serikali namba 373 wa Novemba 2005 litaondolewa, ili ifanye kazi kwa uhuru katika ngazi za jamii na shule," ilisema taarifa.
HakiElimu ilieleza kufurahia, kuwa utawala wa sheria na kanuni za kidemokrasia vilisisitizwa wakati wote wa mkutano wake na Waziri Mkuu.
"Pamoja na sheria nyingine, hii inamaanisha kwamba haki ya kikatiba ya uhuru wa habari na wa kujieleza (Ibara ya 18) vitaendelea kuwa msingi wa kazi za HakiElimu na kuongeza uhusiano wetu na Serikali," ilisema taarifa hiyo.
Kwa mujibu wa makubaliano, sasa HakiElimu itafanya utafiti shuleni na kuutangaza, lakini kwa mawasiliano na Wizara ya Elimu na Mafunzo ya Ufundi; itachapisha na kusambaza machapisho yake nchini, lakini kwa yale yatakayopelekwa shuleni, yatatakiwa kupata idhini ya Ofisa Elimu Kiongozi.
Pia HakiElimu itatakiwa kutumia busara kuandaa na kurusha vipindi redioni na katika televisheni, lakini ikizingatia kuwa kilichomo ni cha ukweli na itawakilisha mashirika ya kiraia katika michakato inayofanywa na Serikali bila vikwazo.
Makubaliano mengine ni pia kwamba maofisa wa HakiElimu na wale wa Serikali, watapeana taarifa na kudumisha mawasiliano ya kutosha.