2007-02-01 10:52:42
Na Mwakwaia wa Kuhenga
Mheshimiwa Edward Lowassa, MB.,
Waziri Mkuu, Jamhuri ya Muungano wa Tanzania. Mheshimiwa Waziri Mkuu,
Nadhani tunafahamiana! Kwa kuwa ni hivyo, nina hakika utapenda kusoma waraka huu wa mimi nduguyo, mwananchi mwenzio wa nchi hii.
Nathubutu kukuandikia nikitiwa moyo na ule msemo wa lugha yetu ya Kiswahili: ``Zimwi likujualo halikuli likakuisha!`` Lakini kwa kweli sina sababu ya kuwa na hofu yoyote kuwasiliana nawe kupitia safu hii kwa sababu kwanza wewe siyo zimwi - ni mtu mwenzangu tu - hata kama ni mtawala. Wadhifa ni matokeo tu, siyo msingi wa utu!
Pamoja na hayo, Mheshimiwa Waziri Mkuu, nina hofu kidogo. Nachelea kwamba kadiri mambo yanavyokwenda na hapa tulipofika tusije tukaishia kujenga taifa la mazimwi!
Naona umestuka kidogo PM! Nitakueleza:
Mbele yangu ninayo rasimu ya ule muswada wa Uhuru wa Vyombo vya Habari. Lakini pia ninayo taarifa kutoka ile taasisi isiyo ya kiserikali, HakiElimu. Juzi, Jumanne, taasisi hiyo imeitisha mkutano na waandishi wa habari kufahamisha kuwa Ofisi yako imepiga marufuku matangazo na machapisho yake yote yanayotolewa kwa redio, luninga na vyombo vingine vya habari.
Bahati nzuri au mbaya masuala yote haya mawili ile rasimu ya serikali ya muswada wa Uhuru wa vyombo vya Habari au Uhuru wa kupashana na kutoa habari na kupigwa marufuku matangazo ya HakiElimu yana sura inayofanana na inayogusa Uhuru wa kimsingi wa watu wa nchi hii kwa mujibu wa Katiba yetu.
Waziri Mkuu, kama unavyofahamu, moja ya Uhuru wa kimsingi wa sisi watu wa nchi hii kwa mujibu wa kifungu cha 18 cha Katiba yetu ya Jamhuri inasema hivi:
Kila mtu:
Anao uhuru wa kuwa na maoni na kueleza fikra zake
Anayo haki ya kutafuta, kupokea na kutoa habari bila kujali mipaka ya nchi Anao uhuru wa kufanya mawasiliano na haki ya kutoingiliwa katika mawasiliano yake na
Anayo haki ya kupewa taarifa wakati wote kuhusu matukio mbalimbali muhimu kwa maisha na shughuli za wananchi na pia kuhusu masuala muhimu kwa jamii.
Nina hakika unafuatilia kwa njia moja au nyingine kilio cha wanahabari kama mimi kuhusu rasimu ya muswada unaokuja Bungeni Bill for the Freedom of Information Act 2006.
Mimi ni mmoja wa hao wanaopigia kelele muswada huu kama haupendezi na haufanani hata kidogo na serikali hii ya awamu ya nne ambayo inatokana na ushindi na ridhaa maradufu ya wananchi wa Tanzania waliochagua kwa zaidi ya asimilia 80.
Nilitazamia serikali yangu hii ya CCM ambayo kura yangu ni miongoni mwa kura za mamilioni ya Watanzania kuiweka madarakani, ingekuwa inafikiria mambo makubwa zaidi siyo tu kuimarisha bali kuboresha uhuru wa kusema, uhuru wa kutoa maoni na uhuru wa vyombo huria vya habari na siyo kufikiria kutunga sheria, ambazo ni kinyume cha uhuru wa kimsingi wa mwananchi wa nchi hii katika zama na karne hii.
Kwa mfano muswada unaweka masharti ya mwandishi kuwa na digrii ya taaluma ya Uandishi wa Habari kana kwamba digrii au karatasi yenyewe iliyoandikwa ``degree`` ndiyo inayoandika makala au habari!
Kuweka masharti haya ni mfano wa nchi kama Uingereza kutunga sheria kwamba kiongozi wake wa shughuli za serikali lazima awe na digrii! Wanaojua wanafahamu, kwa mfano kuwa Sir Winston Churchill au John Major hawakuwa na digrii walipokamata nchi kama mawaziri wakuu wa Dola la Uingereza!
Hivi kweli, watu wakisoma makala nzuri ya Mheshimwa Waziri Mohamed Seif Khatib anayotoa katika safu yake ndani ya gazeti MZALENDO au Mudhihir Mudhihir aliyekuwa anaandikia gazeti la Daily News itawajia hata kwa sekunde moja, kuuliza kuwa mabwana hawa wana digrii au lazima wana digrii ili kumudu kuandika makala? Si ni �interest� ya mtu au kipaji chake tu?
Ni mambo ya ajabu sana haya yanayotaka kupenyezwa hapa kwetu!
Itazame tena rasimu hii, PM. Inashangaza kwamba watu wazima wanaweza kujifungia mahala wakaja na dude kama hili na bado wakadiriki kuliita �Freedom of Information Act�!
Ndugu Waziri Mkuu utaniwia radhi kukuita Ndugu, nina hakika wewe si mmoja wa watu wanaonuna ukiitwa Ndugu Lowassa au Ndugu Waziri Mkuu badala ya Mheshimiwa! Pamoja na matatizo yetu yote, kama vile baadhi yetu wanataaluma au baadhi ya vyombo vyetu vya habari kutumika wakati wa kampeni za Uchaguzi na hata baada ya hapo, tulikuwa tumepiga hatua si haba katika uhuru wa kusema na uhuru wa kutoa mawazo.
Hii leo, kipo chombo cha udhibiti wa vyombo vya habari, na mwenendo wa wanahabari wenyewe kilichoundwa na wanahabari wenyewe na wadau wengine yaani Media Council of Tanzania. Ni chombo kinachoheshimiwa na ni chombo huru.
Sasa muswada huu unaokuja utakiua chombo hiki. Kitaanzishwa chombo cha serikali chenye jina la ghiliba, `Media Standards Board`.
Kwa mara ya kwanza taaluma ya uandishi wa habari itakuwa na leseni katika nchi hii, sikumbuki kama ipo nchi yoyote inayotoa leseni kuandika habari.
Sana sana vipo vitambulisho tu kumrahisishia mwandishi kufanya shughuli zake lakini si vinginevyo.
PM: Yote haya ya nini? Hivi kweli serikali yenye ridhaa kubwa namna hii (popular mandate) lipi itaisibu kama uwanja wa uhuru ukipanuka zaidi?
Sasa tuzungumzie jamaa hawa wa HakiElimu. Binafsi nafurahia sana matangazo yao kwenye luninga na redio. Kwa mtazamo wangu na nadhani wa watu wengi, vibwagizo na matangazo yao yanatoa hali halisi au mtazamo mbadala wa mchakato wa maendeleo ya nchi yetu.
Lakini siyo kweli kwamba wapo baadhi ya walimu wanaozikung�unta kangara na konyagi zao barabarani kabla ya kuingia kufundisha darasani na huko kusababisha kizaazaa kwa watoto wanafunzi? Siyo kweli kwamba maisha ya wananchi walio wengi hapa nchini ni duni nyumba za majani, mavazi duni kama vile uvaaji wa kandambili za rangi mbili tofauti au mguu mmoja, au watu wanaoishi karibu na dampo la takataka kama vile pale Vingunguti?
Kuna ubaya gani kutoa ``contrast`` ya taarifa kuwa uchumi wa nchi hii unakua kwa asimilia saba, wakati hali halisi inaonyesha vinginevyo?
Rais wetu, Jakaya, amesema anakasirishwa sana na kupakwa mafuta au kusifiwa kinyume na hali halisi.
Nadhani huu ndiyo ungekuwa mwendo wa serikali yetu na kwa kweli serikali yoyote duniani hujifunza na kufaidika zaidi kusikia wananchi wanasemaje huko mitaani. Je, kupiga marufuku mawazo mbadala kunasaidia? Je, Tutafika?
Edward: Utaniwia radhi kukuita kwa jina lako la kwanza, nadhani ka-rika kangu kananipa ubavu huo! Utakubaliana nami kwamba si rahisi kuyaona mambo kama navyoyaona mimi nikiwa nje ya serikali. Pengine ni vizuri unichukulie very seriously - kwa umakini - na wewe mwenyewe ukiwa mtu makini.
Namalizia kwa kukuuliza: sijui Edward kama huwa unawaangalia hawa vijana wetu wasomi wa vyuo vikuu hasa wanapofanya mikutano yao au maandamano.
Ujumbe mimi naopata ni kwamba kizazi kinachokuja baada yetu sisi kuondoka kitakuwa hakina mchezo na kwa maana zote!
Ni vizuri twende mwendo unaofanana na vijana hawa ambao ndiyo tunaowaachia nchi hii wakati sisi tutakuwa hatupo tena.
Nakushuru. Wasalaam!
Makwaia wa KUHENGA ni Mwandishi Mwandamizi.
E-mail:
makwaia@bol.co.tz