Mkuu,
Rais katoa kauli hii? Tena kwa mtu mwenye kufanya makosa yaliyo wazi? I still do not believe this!
JK abariki kung'olewa Masauni
Thursday, 20 May 2010 04:13
*Asema hakuna fitna, amejimaliza mwenyewe
*Wazanzibari sasa watishia kujitoa UVCCM
Na Waandishi Wetu, Iringa, Dar na Zanzibar
MWENYEKITI wa Chama cha Mapinduzi, Rais Jakaya Kikwete amebariki kung'olewa kwa Mwenyekiti wa Umoja wa Vijana (UV-CCM), Bw. Hamad Yusuf Masauni kuwa amejimaliza mwenyewe.
Akihutubia mkutano Baraza Kuu la Umoja wa Vijana mjini Iringa jana, Rais Kikwete alisema Bw. Masauni alipojaza umri wake kuwa mdogo kuliko uhalisia na ule unaokubalika katika umoja wa vijana, alikuwa anajimaliza mwenyewe na hivyo hakuna fitna dhidi yake.
Hata hivyo alisema kwa kuwa ni kijana mzuri, mchapakazi atapewa kazi nyingine.
Kauli hiyo ya Rais Kikwete imekuja wakati kukiwa na madai ya chini chini kuwa anayeuvuruga umoja huo ni mwanaweza Ridhiwani, jambo ambalo limekanushwa na Ridhiwani mwenyewe pamoja na Katibu Mkuu wa CCM, Bw. Yusuf Makamba.
Akizungumzia uwezekano wa baadhi ya watu kupinga uamuzi huo, Rais Kikwete alisema: "Tulijiandaa kwamba kwa uamuzi huu, kama kuna watu watatunyooshea mabango tutakuwa na cha kuwaeleza."
Rais Kikwete alitumia nafasi hiyo kukemea makundi ndani ya umoja huo akisisitiza kuwa magenge yanawamaliza wenyewe.
Alisema hakuna sababu ya kugombania mambo ambayo wangeweza kuyamaliza ndani ya chama, na hapo hapo akawataka kujipanga kukabiliana na wapinzani wakati wa uchaguzi.
Wakati hayo yajiendelea mjini Iringa, wanachama wa Umoja wa Vijana Zanzibar wamekuja juu na kutishia kurudisha kadi za CCM kwa kile walichodai kujiuzulu kwa Mwenyekiti wa Umoja wa Vijana Taifa (UVCCM), kimesababishwa na majungu.
Wanachama haoa walisema Bw. Masauni amelazimika kujiuzulu kutokana na majungu yaliyopikwa na viongozi wa CCM Zanzibar yaliyotokana na mabadiliko makubwa ndani ya umoja huo ikiwemo kuziba mianya ya upotovu wa fedha.
Akizungumza na Majira Bw. Mohamed Juma aliyejitambulisha kuwa ni mwanachama wa umoja wa vijana katika Jimbo la Kikwajuni, alisema katika kipindi kifupi Bw. Masauni alitengeneza ajira ndani ya umoja huo na kuchunguza vyanzo vya mianya ya upotevu wa mapato ndani ya umoja huo.
"Alianza kwa kasi ikiwemo kujua mapato ya fedha yanayotokana na mali za umoja wa vijana kwa hiyo hilo limeonesha kuwakera baadhi ya viongozi," alisema.
Aidh alisema suala lingine linalojionesha hapo ni kwa baadhi ya viongozi kukerwa na maamuzi ya Bw. Masauni ya kutaka kugombea Ubunge katika Jimbo la Kikwajuni ambalo baadhi ya viongozi walikuwa wakilitolea macho.
Aliongeza kuwa moja ya dalili zinazoonesha kuwa Masauni ameshinikizwa kujiuzulu ni baada ya ziara yake ya kukagua uhai wa umoja wa vijana aliyoifanya hivi karibuni maeneo ya Unguja, ambapo Bw. Masauni alifika katika jimbo hilo na kupandisha bendera, kitu ambacho baadhi ya viongozi walionekana kutokubariki kitendo hicho.
Bw. Masauni tayari alikuwa na nia ya kuwania nafasi ya ubunge katika jimbo hilo ambalo pia Naibu Katibu Mkuu wa CCM, Bw. Saleh Ramadhan Ferouz alikuwa na nia kama hiyo.
Hivi karibuni akizungumza na Majira, Bw. Masauni alisema amefanya mabadiliko kadhaa kwa baadhi ya maeneo ambao alisema lengo lake ni kuimarisha utendaji wa kazi na sio adhabu kwa mtu binafsi na hivyo aliwataka wananchi wasiutafsiri vibaya, hali ambayo pia inaonesha kuwa ni moja ya sababu za kushinikiza majungu ya kumtaka Bw. Masauni ajiuzulu.
Aidha alisema ziara yake katika majimbo mbalimbali ilikuwa na nia ya kuimarisha uhai katika Umoja wa Vijana ambao umekuwa ukiyumba na kudorora kwa kiasi kikubwa.
Baadhi ya viongozi wa umoja wa vijana waliopo Zanzibar na wanachama kwa ujumla wameelezea hofu yao kwamba kitendo cha kujiuzulu Masauni katika wadhifa huo ni sawa na kuipotezea Zanzibar nafasi hiyo na kuchukuliwa kwenda Tanzania Bara.
Source: Majira.