MTOTO wa Rais Jakaya Kikwete, Ridhiwani Kikwete, sasa anatajwa waziwazi na kuhusishwa na mpango wa mapinduzi ndani ya Umoja wa Vijana wa Chama Cha Mapinduzi (UVCCM) Tanzania Daima Jumatano imeelezwa.
Baadhi ya vyanzo vya habari kutoka ndani ya UVCCM vimeliambia gazeti hili kuwa mtoto huyo ndiye anayevuruga umoja huo.
Ridhiwani, ambaye ni mwanasiasa kinda, lakini kwa kuwa mtoto wa rais anakuwa na ushawishi mkubwa ndani ya chama, anatajwa kuwa kinara wa mkakati mchafu unaolenga kumuengua Mwenyekiti wa umoja huo, Hamad Masauni Yusuf.
Mtoto huyo, ambaye ni mjumbe wa Baraza Kuu la UVCCM Taifa, anadaiwa kuwa ndiye msukaji wa mkakati wa kumngoa Masauni katika wadhifa wake.
Taarifa zilizopatikana jijini Dar es Salaam na miongoni mwa viongozi wa ngazi ya juu wa umoja huo waliopo mkoani Iringa, zinaeleza kuwa nyaraka zilizoenea kwenye vyombo vya habari nchini kuhusu kashfa ya Masauni kuhusu tuhuma za kughushi umri wake, zimetokana na kazi ya Ridhiwani.
Uchunguzi wa Tanzania Daima Jumatano umebaini kuwa viongozi hao wanabadilishana taarifa nyeti kuhusu mgogoro wa umoja huo na kumtaja Ridhiwani kama mhusika mkuu wa kuupanga na kuutekeleza.
Ridhiwani mwenyewe anakana kuhusika na mkakati wa kumngoa Masauni, lakini anatajwa kuwa kiongozi wa kundi la viongozi waandamizi wa umoja huo linalopinga mabadiliko yanayolenga kuipeleka jumuiya kwenye maendeleo endelevu.
Habari zaidi zimesema viongozi wa UVCCM wamekuwa wakibadilishana taarifa za ujumbe mfupi wa simu ya mkononi unaodaiwa kumsakama kutokana na mkakati wake dhidi ya viongozi wema wa umoja huo.
Ujumbe huo umekuwa ukisambazwa miongoni mwa wajumbe wa Baraza Kuu la UVCCM ambalo lilikutana jana mjini Iringa.
Ujumbe huo ambao pia umetumwa kwenye simu za baadhi ya waandishi wa gazeti hili, unasomeka:
Ndugu Rizwan (Ridhiwani) Kikwete, tuna taarifa za kutosha juu ya mkakati wenu unaolenga kutaka kuathiri jitihada zetu za kupigania na kuchangia ushindi wa chama chetu na viongozi wake kupitia taasisi yetu iliyotulia ya UVCCM, ikiwemo mipango unayoiongoza kuandaa makala ya gazeti kumchafua Mwenyekiti wa UVCCM taifa, sisi vijana wapenda amani ndani ya jumuiya na chama, kamwe hatutavumilia hali hii, tukiamini kuwa hiyo si haki na wala si njia sahihi ya kujenga jumuiya yetu.
Sababu za kumngoa Masauni
Duru za kisiasa kutoka ndani ya UVCCM, zinasema mkakati wa kumuengua Masauni kwenye nafasi yake ulianza miezi minne iliyopita pale baadhi ya wajumbe wa Kamati ya Utekelezaji wenye ushawishi mkubwa, walikuwa wakifanya vikao vya siri kuibua kashfa hiyo.
Sababu inayoelezwa na duru hizo ni kutokana na msimamo wa Masauni wa kutokubali kuyumbishwa na baadhi ya wajumbe wa kamati hiyo waliopania kuifanya UVCCM taasisi yao binafsi ili wafanye biashara.
Wapo wenzetu waliotaka kumtumia Masauni kufanya biashara ndani ya UVCCM, msimamo wake wa kutetea rasilimali za jumuiya ndio uliomfikisha hapo. Lakini ukiziangalia nyaraka zile unaona zinaweza kuwa na ukweli.
Lakini swali ni kwanini hoja hiyo imeibuliwa leo? alihoji mmoja wa wajumbe wa Baraza Kuu la UVCCM ambaye ameshurutishwa asitajwe gazetini.
Sababu nyingine inayotajwa na duru hizo za siasa ni dhamira ya Masauni kutaka kuwania ubunge katika Jimbo la Kikwajuni, nafasi anayotazamia kuiwania Naibu Katibu Mkuu wa CCM Zanzibar, Saleh Ramadhani Ferouz.
Lakini pia kuna suala la uchaguzi wa UVCCM uliopita. Kilichopo ni kwamba maumivu ya uchaguzi ule bado hayajapona. Kumbuka Masauni alichaguliwa baada ya Rais Kikwete kuamua nafasi ya mwenyekiti iende Zanzibar kama njia ya kutuliza joto la kiuongozi lililokuwa linafukuta katika jumuiya, alisema mmoja wa wajumbe wa Baraza Kuu la UVCCM.
Masauni alichaguliwa Desemba 2008 katika uchaguzi uliokuwa umejaa utata hata kusababisha Mwenyekiti wa CCM, Rais Kikwete, kupendekeza Masauni ambaye alikuwa amegombea nafasi ya makamu mwenyekiti ndiye ateuliwe kugombea uenyekiti.
Waliokuwa wameomba na kugombea uenyekiti wote walitoka Bara, ambao ni Hussein Bashe na Benno Malisa. Hawa waliteuliwa kugombea umakamu.
Kauli ya Masauni
Alipozungumza na Tanzania Daima Jumatano, alisema taarifa za kuwapo kwa nyaraka hizo amezisikia muda mrefu na anajua walioziandaa na kuzisambaza.
Nipo Iringa, baadhi ya wajumbe nimewasikia wakisema wanazo nyaraka hizo, binafsi pia nimezipata lakini ni tuhuma za uongo, zinalenga kunipunguzia kasi yangu ya utendaji katika usimamizi wa rasilimali za umoja, maadili na uwajibikaji, alisema Masauni.
Masauni ambaye kwa kuwa mwenyekiti wa UVCCM anaingia kuwa mjumbe wa Kamati Kuu (CC) ya CCM, - ambaye pia ni mjumbe wa Halmashauri Kuu (NEC) alisema kuna kikundi cha watu kilichodhani kingeweza kumburuza katika maamuzi.
Alisema mbinu za kikundi hicho zimegonga mwamba ndiyo maana wameamua kumchafua kupitia tuhuma za uongo.
Masauni ambaye ni mtoto wa aliyekuwa Mwenyekiti wa Tume ya Uchaguzi ya Zanzibar (ZEC), iliyotuhumiwa kuvuruga uchaguzi kwa nia ya kuipendelea CCM, ametamba kuwa UVCCM ni imara na itaendelea hivyo chini ya uongozi wake.
Nitaendelea kusimamia vema matumizi bora ya rasilimali za umoja na chama kwa ujumla. Nitajitahidi kustawisha uongozi unaozingatia maadili na uwajibikaji bila ya kujali watu wanaotaka kunipunguza kasi, alisema.
Hata hivyo, Masauni hataki kujieleza kwa ufasaha anapoulizwa kuhusu umri wake hasa kwa kujaribu kubadilisha mwelekeo wa mazungumzo.
Nilichaguliwa kwa vikao halali ambavyo kabla ya hapo watu waliangalia rekodi zetu (wagombea wote). Waliangalia mambo ya uadilifu na yote ya msingi... katika mambo yote haya vikao vya chama na hata vyombo vya usalama vilishiriki, sasa sijui watu wanachosema, alijibu.
Alipoulizwa kama haoni ni vema akajiuzulu ili kulinda hadhi yake, Masauni alisema hana mpango huo na badala yake anaelekeza nguvu kuwaunganisha vijana kuleta umoja na kuwajengea uwezo wa kimaendeleo.
Ridhiwani angaka
Kwa upande wake, Ridhiwani ambaye ameingia katika siasa za CCM kwa nguvu kubwa tangu baba yake alipoukwaa urais mwaka 2005, alishangaa kusikia madai ya kuhusika katika mkakati wa kusambaza nyaraka za kashfa dhidi ya Masauni.
Akijibu kwa kifupi tuhuma hizo kwa njia ya ujumbe mfupi wa simu ya mkononi, Ridhiwani, badala ya kujieleza vizuri, aliandika tu: Ahahaha.
Hata alipobanwa na mwakilishi wetu aliyeko mkoani Iringa kabla ya kuingia ukumbini kuanza kikao cha Baraza Kuu, Ridhiwani alisema anatarajia kujibu tuhuma hizo baada ya kikao hicho ambacho kilikuwa kikiendelea hadi usiku jana.
Wajumbe Zanzibar wacharuka
Katika hali inayoonyesha kuwapo mpasuko baada ya kuibuliwa kwa kashfa dhidi ya Masauni, wajumbe wa Baraza Kuu kutoka Zanzibar wamecharuka na kusimama kidete kumtetea.
Zaidi ya wajumbe 50 waliokutwa wakishuka kwenye boti bandarini Dar es Salaam juzi na jana kwa ajili ya kuunganisha safari ya Iringa, walisikika wakiimba nyimbo za kumtetea Masauni na kupania kwenda kumtetea.
Tuachieni Masauni wetu, tumekuja kumchukua kwenda naye Zbar
, kumbe mlimpa kwa shingo upande..., yalikuwa baadhi ya maneno waliyotoa kwenye wimbo wao.
Habari zaidi kutoka mkoani Iringa, zinasema kuwa baadhi ya wajumbe waliozungumza na gazeti hili wametaka iundwe tume kuchunguza nyaraka hizo ili kubaini ukweli.
Wakizungumza bila kutaja majina yao, wajumbe hao walisema endapo itabainika kuwa kweli Masauni alighushi umri wake, lazima awajibike.
Kama anasingiziwa, basi walioandaa mpango huo wawajibishwe hata kama ni Ridhiwani, alisema mmoja wa wajumbe kutoka Pemba.
Masauni anadaiwa kughushi umri wake ili kupata nafasi hiyo nyeti ndani ya umoja huo.
Nyaraka zimeenezwa kwenye vyombo vya habari tangu mwishoni mwa wiki zikidai kuwa Masauni ametaja umri tofauti wa kuzaliwa kutoka kwenye cheti chake cha kuzaliwa na nyaraka za kuombea pasipoti ya kusafiria.
Waraka huo unaonyesha alizaliwa Oktoba 3, 1973, wakati fomu zake za kuomba hati mpya ya kusafiria zinaonyesha alizaliwa Oktoba 3, 1979.
Masauni anatarajiwa kumaliza muda wake wa kikatiba wa uongozi ifikapo mwaka 2012. Akilazimika kujiuzulu au kuondolewa, atakuwa amekosa pia nyadhifa zote za kisiasa.
Wakati huohuo, Rais Kikwete amelazimika kuitisha kikao cha Halmashauri Kuu ya Taifa (NEC) ya dharura kesho, pamoja na mambo mengine, kujadili kashfa na mzozo ulioibuka ndani ya UVCCM
SOURCE: TANZANIA DAIMA