Wapo watakaokulaumu kwa vyovyote utakavyofanya bila ya kujali unalolifanya sasa ni jema au baya, kwa vile mwanzoni ulikosea, utaendelea kuwa mbaya tu siku zote.
Lakini wapo binadamu watakaokulaumu kwa kile ulichofanya wakati huo. Ukifanya vyema, bila ya kujali huko nyuma ulikosea, watakupongeza. Mimi nipo kwenye kundi hili.
Sikupongezi kwa sababu ulienda kuapa kinyume na maamuzi ya chama, sikupongezi kwa sababu umekuwa mbunge wala sikupongezi kwa sababu Ndugai amesema atakulinda. Bali nakupongeza kwa namna unavyokabiliana na tatizo lililopo mbele yako.
Wengi leo walitarajia umseme vibaya Mbowe na CHADEMA. Na hao ndio wanaodhani wamekuwa marafiki zako wapya.
Halima Mdee umeteseka sana kwa sababu ya kupigania haki na demokrasia Tanzania. Umeteseka sana kwa sababu tu umekuwa CHADEMA. Waliokuwa wanakusweka ndani, waliokuwa wanakutengenezea kesi, waliokuvunja mkono, waliokuwa wanakukejeli kwa maneno mengi ya dharau, leo wanajifanya ni marafiki zako.
Kumbuka kuwa mzazi wako hata kama anavaa lubega ni dhahiri ana upendo nawe zaidi kuliko jambazi mwenye jumba la ghorofa hata kama atakutoa kwa baba yako mwenye nyumba ya nyasi akawa anakulaza ghorofani kwenye chumba cha kifahari.
Nakupongeza kwa jinsi ulivyojibu hoja mbalimbali na kuonesha unatambua kuwa ni nani wanaokupenda na nani ni maadui lakini wanasema kuwa ndio walinzi wako. Yaani wauaji na watesaji wako leo wanakuwa walinzi na marafiki zako.
Nakupongeza kwa sababu hukuitusi CHADEMA, hukuitusi Kamati Kuu, hukumtusi Mbowe. Na hapa naipongeza Kamati kuu ya CHADEMA na Mh. Mbowe maana nao hata walipokuwa wakisoma maazimio ya Kamati kuu kuhusiana na Halima Mdee na wenzake, hawakuonesha kejeli wala chuki bali upendo wa dhahiri. Ni kama mzazi anayemchapa mwanae lakini anamchapa kwa sababu anataka abadilike na kuwa mtoto mwema na msikivu zaidi.
Mengine yatabakia katika maamizi ya Chama na ninyi wenyewe, lakini mpaka hapa umevuka kiunzi cha kwanza ambacho maadui wa CHADEMA na Mbowe walikuwa wakikisuburia kwa hamu.
Kwa njia uliyopita, kwa nguvu uliyoiweka, na imani uliyoitengeneza ndani ya CHADEMA, kwa Watanzania na Jamii ya kimataifa, usikubali kuipoteza imani hiyo kwa wepesi kiasi hicho.
Tunafahamu chama kitapitia njia ngumu, viongozi wa CHADEMA watapitia njia ya miiba lakini isiwe sababu ya kujijongesha kwa wadhalimu. Tengenezeni utaratibu, watu wenye mapenzi mema tuchangie kila mwezi ili kukitegemeza chama na watendaji wake. Hakika miongoni mwenu hakuna atakayekufa njaa wala kushindwa kutibiwa alimradi kuwepo utaratibu unaoeleweka.