mambo ya sona hayo!
huwa napenda sana kusoma thread kama hizi,yaani zinazohusu matukio ya kweli yenye hisia.
huko papilon nako kuna nini?? tujuzeni sie wengne "tulikuwa hatupo''
PAPIILON - ‘KIPEPEO’ NDANI YA KISIWA CHA SHETANI:
Kwenye kipindi cha ukoloni, Wafaransa na Waingereza walikuwa na maeneo mahususi waliyokuwa wanayatumia kwa ajili ya kuwatunzia wafungwa kwa kuwaweka mbali kabisa na makazi na mazingira yao ya kila siku (penal colony), ambapo maeneo haya yalikuwa sana sana ni visiwa vyenye malengo ya kuwaadhibu wafungwa na hata kuwarekebisha kwa mujibu wa sheria husika. Sifa yake kubwa maeneo haya yalikuwa yapo mbali na miji, mahali tulivu na hivyo basi kuumba mazingira magumu juu ya uwezekano wa mfungwa kutoroka.
Kipindi hicho waingereza na wafaransa kwa kiasi kikubwa walitumia Amerika ya kaskazini na Australia kama maeneo ya kutunzia wafungwa wao ambapo huko wafungwa walikuwa zaidi ya watumwa wakifanyishwa kazi kama punda wa dobi baada ya kauli ya hakimu kuwaponda hukumu.
Waingereza walimiliki maeneo kama vile: visiwa vya Andaman, kisiwa cha Norfolk, ardhi ya Van Diemen, Queensland na New South Wales. Wafaransa nao wasiwe nyuma walimiliki maeneo hayo mathalan Lousiana, New Caledonia na pia Devil’s Island (kisiwa cha shetani) kilichokuwa kinapatikana huko French Guiana: eneo linalopatikana kwenye ukanda wa kaskazini wa pwani ya Marekani kusini ikiwa ni eneo ambalo lipo chini ya tawala ya ufaransa (oversea region) tangu ukoloni.
Kwanini basi tuongelee Devil’s Island (kisiwa cha shetani) na si maeneo mengine?
‘Kisiwa cha Shetani’ kiliundwa kwenye kisiwa cha ekari 34.5 na serikali ya mtawala Napoleon III mnamo mwaka 1852 baada ya kupata hofu juu ya uongezekaji wa uhalifu nchini Ufaransa, na isichukua muda mrefu ikawa ni makazi ya wahalifu wabaya zaidi kuwahi kutokea ufaransa, wauaji, wafungwa wa kijeshi na wa kisiasa. Simulizi zake za kushtusha zilianza kuteka anga mwanzo mwa karne ya ishirini na baada ya karibia miaka mia moja ya kufanya kazi hatimaye eneo hili likafungwa na wafaransa wenyewe.
Ukiachana na maeneo yote yaliyotengwa na wakoloni kama maeno ya kuwafungia wafungwa (penal colonies), eneo hili ndilo lilikuwa hatari na gumu zaidi kiasi kwamba wafungwa wakalitunuku jina eneo hilo ‘kisiwa cha shetani’ baada ya kuona kisiwa hicho kinastahili kuitwa hilo jina kutokana na yale waliyokuwa wanayapitia kwenye ngome hiyo kata.
Wafungwa walikuwa wanafanya kazi ngumu kwa muda mrefu kwenye camp za mbao au kwenye ujenzi wa barabara. Hali za ufanyaji kazi na wafanyakazi wenyewe ilikuwa mbaya; kiasi cha magonjwa kilikuwa kikubwa mno na njaa pia; wafungwa walioshindwa kufanya kazi vema walinyimwa chakula. Hali hizi zilipurusa wafungwa takribani elfu hamsini huku kisiwa hicho kikipewa jina jingine na wafungwa “Dry Guillotine” kumaanisha mashine kavu inayotumika kukatia vichwa vya binadamu.
Wafungwa wengi walikufa wakijaribu kutoroka. Walitafunwa na wanyama wakali, wakidhoofishwa na magonjwa au kutwaliwa na walinzi wataalamu wa kuwinda wafungwa watorokao, kuzama baharini ama kuliwa na papa.
Kati ya wafungwa 70,000 waliopelekwa kwenye kisiwa hicho, ni wafungwa 2,000 au zaidi kidogo ndio waliokuwa wanafanikiwa kurudi ufaransa. Kati ya wafungwa 5,000 ndio waliokuwa wanastahimili kumaliza hukumu yao, wengi wao wakilazimishwa kubakia huko huko, French Guiana, kutokana na sera iliyoanzishwa miaka miwili tu baada ya gereza hilo kufunguliwa, sera ya kulazimishwa wafungwa kutafuta makazi huko huko wakisaidiwa pesa kidogo na makazi.
Hali ilikuwa mbaya kiasi kwamba ni kati ya asilimia 40 na 80 ya wafungwa walikuwa wanakufa ndani ya mwaka mmoja kabla ya kuuona mwaka mpya gerezani.
Hali hii ya mateso yasiyovumilika, inatufanya tukutane na binadamu aliyewahi kufungwa humo akifanya jitihada za kujikomboa toka kwenye jela hiyo na hatimaye anafanikiwa kwa mbinde nyeusi. Mwanaume huyu si mwingine bali Henri Charriere, ama kwa jina lingine ‘Papillon’.
Henri Charriere a.k.a Papillon
Mfaransa huyu ni mwandishi aliyehukumiwa kwa kesi ya mauaji na mahakama ya nchini ufaransa. Akiwamo jela akapata kuandika riwaya maarufu ya ‘Papillon’ iliyobebelea maelezo yake ndani ya jela na hatimaye safari yake ya kutoroka kwenye ‘kisiwa hicho cha shetani’. Bwana huyu alikataa kuhusika na mauaji japokuwa alikiri kuwa mhalifu wa mambo mengine madogomadogo.
Alijiita jina la ‘Papillon’ ambalo maana yake ni kipepeo kwa lugha ya kifaransa kutokana na kujichora mchoro wa kipepeo kifuani mwake.
Kwa mujibu wa kitabu chake ‘Papillon’, Charriere alikutwa na hatia tarehe 26/10/1931 kwa mauaji ya wakala wa malaya aliyeitwa Roland Le Petit.
Alihukumiwa kifungo cha maisha jela na miaka kumi ya kazi ngumu. Baada ya kutumikia kifungo kwa muda mfupi ndani ya jela ya Beaulieu huko ufaransa, mnamo mwaka 1933 akasafirishwa kwenda French Guiana, kisiwa cha Saint Laurent.
Tokea awali kabisa Papillon alikuwa amenuwia kutoroka jela kwasababu alijiona astahili kuwamo humo akitumika kufanya kazi ngumu kwa mujibu wa hukumu ‘batili’.
Baada tu ya siku arobaini na mbili za kukaa jela ya Saint Laurent, Papillon alitumia mwanya wake wa kufanya kazi kutoroka kwa kuumba boti goigoi iliyofanikiwa kumtoa eneo la jela na kuishia kumwacha msituni alipojiweka kwa muda kadhaa kabla hajakamatwa tena na kuhamishwa jela, akapelekwa kwenye kisiwa cha Shetani.
Aliendelea kufanya majaribio kadha wa kadha ya kutoroka, takribani nane, hatimaye akafanikiwa kutoroka na kuibukia Venezuela. Napo alikamatwa na kufungwa tena, baada ya muda akaachiwa akiwa raia kamili wa Venezuela.
Mochwari ya gereza.
Angalau utakuwa umepata kidogo uelewa kuhusu PAPILLON na Kisiwa cha Shetani.